Neno la Mungu la Kiunabii Litatimia Lote!
1 Mashahidi wa Yehova sikuzote wamependezwa na unabii wa Biblia. Kwa hiyo, tulisisimuka kujua kwamba kichwa cha mkusanyiko wa wilaya wa mwaka huu kingekuwa “Neno la Mungu la Kiunabii.” Tulikuwa na hamu sana ya kujua kile ambacho Yehova alikuwa ametuandalia kikiwa ‘chakula kwa wakati ufaao.’ (Mt. 24:45) Yeye hakututamausha.
2 Mambo Makuu ya Mkusanyiko: Hotuba ya msingi ya Ijumaa, “Sikiliza Neno la Mungu la Kiunabii,” ilitia ndani mazungumzo yenye kuelimisha ya simulizi la mgeuko-umbo. (Mt. 17:1-9) Ilikazia kwamba hivi sasa tuko ukingoni mwa nyakati nzuri kwa sababu tuko katika wakati wa mwisho kabisa, mfumo mpya ukiwa karibu sana! Njia ya maana tuwezayo kusikiliza Neno la Mungu ni kwa kulisoma kwa ukawaida. Ule mfululizo “Pendezwa na Kusoma Neno la Mungu” uliandaa madokezo yenye kutumika ya kufanya usomaji wetu wa Biblia uwe na faida zaidi na wenye kufurahisha.
3 Jumamosi alasiri tulichunguza sababu ambazo twapasa kusadikishwa kwamba tunaishi katika siku za mwisho. Je, unaweza kukumbuka yote hayo? Jumapili asubuhi, unabii wa Habakuki ulitokezwa kwa njia yenye kupendeza tulipojifunza kwamba siku yetu hufanana sana na siku yake na kwamba hivi karibuni matukio ya maana sana yatatukia wakati Yehova atakapoharibu waovu na kuokoa waadilifu. Je, ulielewa jambo kuu la drama ya Biblia juu ya Yakobo na Esau? Lazima tutafute kwa bidii baraka kutoka kwa Yehova, tukikinza roho ya ubaridi.
4 Kitabu Kipya Chenye Kuvutia Sana: Tulisisimuka kama nini tulipopokea kitabu kipya, Sikiliza Unabii wa Danieli! Bila shaka unasoma kichapo hiki chenye kuvutia sana. Msemaji aliyekitoa alisema: “Isipokuwa mambo machache, unabii wote ulio katika kitabu cha Danieli umetimizwa.” Je, hilo halikazii uharaka wa nyakati zetu?
5 Programu ya mkusanyiko imeimarisha usadikisho wetu kwelikweli kwamba ahadi zote za Mungu ambazo hazijatimizwa zitatimia. Tunachochewa twendelee kuwatangazia wengine neno la Mungu la kiunabii!