Moyo Wangu Wafurika kwa Shukrani
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA JOHN WYNN
Nilikinza kwenda mikutano ya Mashahidi wa Yehova mara nyingi kama nini! Nilikuwa nikijifanya kuumwa tumbo au kuumwa kichwa—lolote lile ili niepuke kuhudhuria. Lakini uimara wa mama yangu sikuzote ulifanya magonjwa hayo yatoweke haraka, na nilikuwa najikuta nikitembea pamoja naye kilometa tatu kwenda kwenye Jumba la Ufalme, nikimsikiliza alipokuwa akizungumza Neno la Mungu pamoja na mwandamani mwenye umri mkubwa zaidi.
HILO lilinifundisha somo lenye thamani: Wazazi hawapaswi kuacha kuwa imara, kwa njia yenye upendo, kwa ajili ya lililo sawa machoni pa Mungu. (Mithali 29:15, 17) Hawapaswi kusahau kamwe amri ya kimungu ya ‘kutokuachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe.’ (Waebrania 10:25) Nifikiriapo maisha yangu, ninashukuru kama nini kwamba mama yangu alisisitiza nifanye lililokuwa lenye manufaa zaidi kwangu!
Kushukuru kwa Ajili ya Vielelezo Bora
Ijapokuwa baba yangu alikuwa asiyeamini, alivumilia itikadi za mama alipopata kuwa Mwanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo. Katika 1913 alienda kusikia hotuba “Baada ya Kifo,” iliyotolewa na Charles T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Society. Hata hivyo, alifika akiwa amechelewa, na viti vyote vilikuwa vimekaliwa. Hivyo alialikwa kuketi karibu na jukwaa pamoja na wachelewaji wengine, karibu sana na Pasta Russell. Hotuba hiyo ilimgusa moyo sana. Ilichapishwa siku iliyofuata katika gazeti la habari la mahali hapo, na alitunza nakala moja ya hiyo gazeti na kuisoma tena na tena.
Baada ya huo mkutano, mama alitoa karatasi ikiwa na jina lake, na upesi Mwanafunzi wa Biblia fulani akawasiliana naye. Halafu, akaanza kupelekea watu trakti za Biblia kutoka nyumba hadi nyumba katika mji wa nyumbani kwetu wa Gloucester, Uingereza. Tangu wakati dada zangu wawili na mimi tulipokuwa wachanga sana, tulishirikiana na mama katika kazi ya kuhubiri.
Wakati Harry Francis, Mwanafunzi wa Biblia mwenye bidii, alipohamia Gloucester, mama alimkaribisha kwa uchangamfu. Upesi, alipendezwa na mimi kibinafsi, na kitia-moyo chake kilichangia sana kuwa kwangu painia baadaye, kama wanavyoitwa wahudumu wa wakati wote. Kielelezo cha Ndugu Francis kilinifundisha somo la maana: Wenye umri mkubwa zaidi wapaswa sikuzote kutafuta njia za kuwatia moyo walio wachanga.
Mama yangu alipopata kuwa Mwanafunzi wa Biblia, wengine katika Gloucester walifanya vilevile. Hata hivyo, wazee fulani kutanikoni walianza kujifikiria makuu mno, na washiriki wa darasa—kama kutaniko lilivyoitwa wakati huo—wakaanza kufuata watu. Kwenye mkutano mmoja, washiriki fulani wa kutaniko walifuliza kumdukua mama mgongoni, wakimhimiza ainue mkono wake juu katika kuwaunga mkono wazee fulani. Lakini mama alijua kwamba hawakuwa wakiweka mfano ufaao, na alikataa kutishwa. Wakati huo, katika miaka ya 1920, wengi waliondoka kutanikoni na kutotembea tena katika njia ya kweli. (2 Petro 2:2) Hata hivyo, mama hakukengeuka kamwe katika kuliunga mkono tengenezo kwa uaminifu-mshikaminifu, hivyo akiniwekea kielelezo bora.
Msimamo Wangu kwa Ajili ya Kweli
Hatimaye, katika Juni 1939, nilipokuwa mwenye umri wa miaka 18, nilibatizwa katika Mto Severn. Mwaka huo pia niliwekwa kuwa mtumishi wa vikuza-sauti. Siku hizo tulitumia mashine ya kupigia sahani za santuri iliyovumisha hadharani ujumbe “Dini Ni Mtego na Hila.” Wakati huo mkazo ulitiwa juu ya kufichua unafiki na mafundisho yasiyo ya kweli ya Jumuiya ya Wakristo.
Wakati mmoja nilikuwa mbele ya mwandamano uliokuwa ukibeba beramu yenye kutangaza kwenye upande mmoja “Dini Ni Mtego na Hila” na kwenye ule mwingine “Mtumikie Mungu na Kristo Mfalme.” Kandokando alifuata farasi mdogo ambaye alikuwa na mabango makubwa kwenye pande zote mbili za mgongo wake yaliyotangaza hotuba ya watu wote. Mwandamano huo lazima ulikuwa mwono ulioje katika jiji la kidini sana la Gloucester!
Kujapokuwa magumu ya kifedha nyumbani, mama alinitia moyo niwe painia. Hivyo, katika Septemba 1939, mwanzoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Pili, niliwasili kwenye mgawo wangu wa kwanza wa upainia katika Leamington, mji mdogo katika Warwickshire. Huo mji ulikuwa makao ya makasisi kadhaa waliokuwa wamestaafu.
Katika huduma yetu ya nyumba hadi nyumba tulitumia kinanda cha gramafoni, kucheza hotuba za Joseph F. Rutherford, aliyekuwa wakati huo msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society. Kwa upande mwingine, mashine yetu ya kupigia sahani za santuri (ambayo ilikuwa inaweza kutumiwa kwa wasikilizaji wengi zaidi) ilikuwa nzito zaidi, na tuliibeba katika kigari au gari la kubeba mtoto mchanga. Nyakati nyingine, makasisi walitulazimisha kuondoka kwenye makao yao, kwa kukasirikia ujumbe wenye kufichua dini isiyo ya kweli. Lakini hatukukata tamaa. Yehova alibariki kazi yetu, na leo kutaniko la Mashahidi zaidi ya mia moja linaweza kupatikana katika Leamington.
Katika 1941, Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipokuwa ikiendelea vikali, nilihamia Wales, nilikopainia katika miji ya Haverfordwest, Carmarthen, na Wrexham. Nikiwa mhudumu wa wakati wote, niliachiliwa nisifanye utumishi wa kijeshi, lakini watu hawakupendezwa na msimamo wetu wa kutokuwamo. Hivyo, mwenzangu na mimi tulishutumiwa kuwa wapelelezi au kuwa vibaraka wasaliti. Usiku mmoja, polisi walizingira trela yetu. Mwenzangu, aliyekuwa amerudi tu kutoka kwenye kazi yake ya kupakua makaa ya mawe, alitokeza kichwa chake nje ili aone aliyekuwa pale. Uso wake ulijaa vumbi ya makaa ya mawe, na alionekana kwa wale polisi kana kwamba alikuwa tayari kushiriki katika uvamizi. Jambo hilo lilihitaji kuelezwa!
Tulibarikiwa sana katika migawo yetu. Wakati mmoja, tulipokuwa katika Carmarthen, John Barr aliyetoka kwenye ofisi ya tawi katika London (sasa ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza) alifanya ziara yenye kututia moyo. Wakati huo, kulikuwa na wahubiri wawili tu katika Carmarthen; lakini sasa, kuna zaidi ya wahubiri mia moja. Mji wa Wrexham kwa sasa una makutaniko matatu, na hivi karibuni nilikuwa na pendeleo la kuliweka wakfu Jumba la Ufalme zuri katika Haverfordwest.—1 Wakorintho 3:6.
Kushukuru kwa Ajili ya Huduma Yangu
Tulipokuwa Swansea, South Wales, mwenzangu, Don Rendell, hakuachiliwa asifanye utumishi wa kijeshi. Alitiwa gerezani licha ya kueleza kwamba hangaliweza kwa kudhamiria kupigana dhidi ya Wakristo wenzake katika nchi nyingine. (Isaya 2:2-4; Yohana 13:34, 35) Ili kumtia moyo, na vilevile kuwatolea majirani ushahidi, niliweka ile mashine ya kupigia sahani za santuri karibu na gereza na kucheza hotuba za Biblia.
Hata hivyo, wanawake wa mahali hapo walichukizwa na jambo hilo na walipitisha kofia ya kukusanya pesa ili kuwalipa askari wapige mwandamani wangu na mimi. Tuliondoka, tukikimbia kadiri tulivyoweza—nilikuwa pia nikisukuma kile kigari chenye mashine ya kupigia sahani za santuri—tukitafuta kinga ya Jumba la Ufalme. Lakini tulipofika hapo, lilikuwa limefungwa! Kuingilia kati tu kwa polisi wakati ufaao ndiko kulikotuokoa tusipigwe vikali.
Kwa wazi tukio hilo likaja kujulikana sana. Nilipokuwa nikihubiri katika nchi iliyo karibu na Swansea muda fulani baadaye, mtu fulani aliniambia hivi kwa kibali: “Ukristo ni jambo lile mnalotetea, kama yule mwanamume kijana katika Swansea aliyetangaza kwa ujasiri alichoamini na kulazimika kukimbilia kinga.” Alishangaa kama nini kujua kwamba mimi nilikuwa ndiye yule mwanamume kijana!
Kupainia wakati wa miaka hiyo ya vita hakukuwa rahisi. Hatukuwa na mali nyingi za kilimwengu, lakini zile tulizokuwa nazo, tulizithamini na kuzifurahia. Tulipokea ugavi wa kawaida wa chakula cha kiroho sikuzote, na hatukukosa kamwe mikutano, ila wakati tulipokuwa wagonjwa. Nilinunua baiskeli ya zamani, na tulikuwa na vikapu vikubwa vilivyowekwa juu yake ili kubeba kinanda cha gramafoni na vilevile fasihi za Biblia. Nyakati nyingine nilisafiri umbali wa kilometa 80 juu ya baiskeli! Nilipainia kwa muda wa miaka saba na hukumbuka siku hizo kwa upendo.
Katika 1946, baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili kuwa imemalizika, nilialikwa kufanya kazi Betheli, kama majengo makuu ya Mashahidi wa Yehova yanavyoitwa katika nchi zao. Betheli yetu wakati huo ilikuwa kwenye eneo la 34 Craven Terrace, karibu na London Tabernacle. Nilifurahia ushirika huko pamoja na wale wenye umri mkubwa zaidi, kama vile Alice Hart, ambaye babake, Tom Hart, yaaminika ndiye aliyekuwa Shahidi wa kwanza Uingereza.
Kupata Mwandamani Mwaminifu
Katika 1956, niliondoka Betheli ili kumwoa Etty, painia ambaye tulijuana alipokuja kutoka Uholanzi kumtembelea dadake ambaye wakati huo alikuwa akiishi London. Kuelekea mwisho wa vita, Etty alifundisha kupiga chapa na kuandika hati-mkato kwenye chuo cha biashara katika Tilburg, kusini mwa Uholanzi. Siku moja mwalimu mwingine alijitolea kuendesha baiskeli pamoja naye hadi nyumbani ili kuhakikisha kwamba alifika salama. Alikuwa Mkatoliki wa Kiroma. Walipowasili, mazungumzo pamoja na wazazi wa Etty waliokuwa Waprotestanti yalifuata. Urafiki ulisitawi, na huyo mwalimu akawa mwenye kuzuru mara nyingi nyumbani kwao.
Upesi baada ya vita kumalizika, mwalimu huyo alikuja nyumbani kwa Etty, akipaaza sauti, “Nimeipata kweli!”
“Nilifikiri ulisema ulikuwa na kweli wakati ulipokuwa Mkatoliki wa Kiroma!” babake Etty akaitikia.
“La!” akajibu kwa msisimko. “Ni Mashahidi wa Yehova walio na kweli!”
Walitumia jioni hiyo na nyingine nyingi zilizofuata katika mazungumzo ya Biblia yenye juhudi. Muda mfupi baadaye Etty akawa painia. Katika huduma yake alikabili pia upinzani mkali, ambao katika Uholanzi ulitokana na Kanisa la Katoliki ya Kiroma. Watoto, waliochochewa na makasisi, walikuwa wakivuruga mazungumzo yake alipokuwa akienda nyumba hadi nyumba, na katika pindi moja waliharibu baiskeli yake. Aliipeleka baiskeli yake kwa mtengenezaji ambaye hapo awali alikuwa amekubali kijitabu kutoka kwake. “Angalia walilofanya hao watoto!” akasema akiwa na machozi.
“Sasa, usife moyo,” huyo mwanamume akajibu kwa fadhili. “Unafanya kazi bora. Nitakutengenezea baiskeli yako bila malipo.” Na alifanya hivyo.
Etty aligundua kwamba makasisi hawakuwahangaikia makundi yao hadi tu alipoanza kujifunza nao Biblia. Wakati huo ndipo makasisi na watawa wa kike wangekuja ili kudhoofisha imani ya hao watu katika Biblia na katika Yehova. Licha ya hayo, alifurahia mafunzo ya Biblia mengi yenye kuzaa matunda.
Kushukuru kwa Ajili ya Maisha Yetu Pamoja
Baada ya arusi yetu, Etty na mimi tulipewa mgawo wa kazi ya kusafiri katika Uingereza, na kwa miaka karibu mitano, tulitembelea makutaniko ili kuyatia nguvu kiroho. Kisha mimi nikapokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la 36 la Gileadi, lililofanywa kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York. Mtaala huo wa miezi kumi, uliokamilika Novemba 1961, ulibuniwa hasa ili kuzoeza wanaume kushughulikia kazi katika ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova. Nilipokuwa nimeondoka, Etty alibaki katika Uingereza kwenye Betheli ya London. Nilipohitimu, tulipewa mgawo wa Betheli pamoja.
Kwa miaka 16 iliyofuata, nilifanya kazi kwenye idara ya utumishi, nikishughulikia mambo yenye kuhusiana na utendaji mbalimbali wa kutaniko. Kisha, katika 1978, baada ya mwangalizi wa Makao ya Betheli, Pryce Hughes, kufa, niliwekwa rasmi mahali pake. Daraka la kushughulikia hali njema ya washiriki wa familia yetu ya Betheli yenye kuongezeka, limekuwa mgawo wenye kuthawabisha muda wa miaka hii mingi iliyopita. Sasa tuna washiriki wa familia yetu zaidi ya 260.
Katika 1971 mama yangu mpendwa alikufa akiwa mwenye umri wa miaka 85. Etty na mimi tulirudi Gloucester kwa maziko, ambako ndugu fulani alizungumza vizuri juu ya tumaini la kimbingu ambalo mama alikuwa amelipokea. (Wafilipi 3:14) Ninashukuru kwa utunzaji ambao dada zangu, Doris na Grace, waliandalia mama katika umri wake wa uzee, hivyo wakituwezesha Etty na mimi kuendelea katika utumishi wa wakati wote.
Mara nyingi Etty na mimi huwafikiria wazazi wetu na jinsi walivyotulea katika njia yenye upendo na iliyo imara. Tuna deni kubwa kama nini kwao! Mama yangu hasa alituwekea mimi na dada zangu kielelezo cha ajabu sana, akijenga ndani yetu uthamini kwa Yehova na tengenezo lake.
Kwa kweli, mioyo yetu yafurika kwa shukrani tufikiriapo kwa makini kila siku mpya ya utumishi kwa Baba yetu wa kimbingu, Yehova. Ni Mungu wa ajabu sana, na mwenye upendo kama nini! Mtunga-zaburi wa Biblia alieleza hisia zetu za moyoni alipoandika hivi: “Ee Mungu wangu, Mfalme, nitakutukuza, nitalihimidi jina lako milele na milele. Kila siku nitakuhimidi, nitalisifu jina lako milele na milele.”—Zaburi 145:1, 2.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Nikiwa na mke wangu, Etty