Endeleeni Kuhubiri
1 Siku hizi ni za hatari. Vita vya wenyewe kwa wenyewe na vya kikabila, misiba ya asili, na matukio mengine ya kutisha ni ya kawaida. Wanadamu wanahitaji habari njema zaidi leo kuliko wakati wowote ule. Hata hivyo, watu wengi hawajali mambo ya kiroho. Katika maeneo fulani huenda ni vigumu kuwapata watu nyumbani na ni vigumu hata zaidi kuwapata watu ambao wanataka kutusikiliza au kujifunza Biblia. Licha ya hayo, ni muhimu kuendelea kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu uliosimamishwa.—Mt. 24:14.
2 Kuwapenda Watu: Kazi yetu ya kuhubiri inaonyesha kwamba Yehova anawapenda watu. “Hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Pet. 3:9; Eze. 33:11) Kwa hiyo, ameamuru kwamba “katika mataifa yote lazima habari njema ihubiriwe kwanza,” kama Yesu alivyosema. (Marko 13:10) Mungu anawasihi watu wamtafute ili wasiharibiwe pamoja na ulimwengu wa Shetani utakaoharibiwa hivi karibuni. (Yoe. 2:28, 29, 32; Sef. 2:2, 3) Tunamshukuru sana Yehova kwa sababu ametupa fursa ya kuokoka.—1 Tim. 1:12, 13.
3 Ripoti ya ulimwenguni pote inaonyesha kwamba katika mwaka wa utumishi wa 2004, kwa wastani mafunzo ya Biblia 6,085,387 yaliongozwa kila mwezi, na wanafunzi wapya 5,000 hivi walibatizwa kila juma! Baadhi ya hao waliojiweka wakfu hivi majuzi walipatikana kwa sababu Yehova alibariki jitihada za wahubiri waliojaribu sana kuongea na kila mtu katika maeneo yao. Jambo hili limewaletea ndugu furaha nyingi, na ni pendeleo kubwa sana kuwa wafanyakazi wenzi wa Mungu katika kazi hii ya kuokoa uhai!—1 Kor. 3:5, 6, 9.
4 Kulisifu Jina la Mungu: Tunaendelea kuhubiri ili kumsifu Yehova na kulitakasa jina lake mbele ya wanadamu wote. (Ebr. 13:15) Shetani ‘ameipotosha dunia nzima inayokaliwa,’ na kuwafanya watu wafikiri kwamba Mungu ameshindwa kutatua matatizo ya wanadamu, hajali kuteseka kwa wanadamu, au kwamba hakuna Mungu. (Ufu. 12:9) Tunapohubiri tunatetea kweli kumhusu Baba yetu mtukufu wa mbinguni. Na tuendelee kulitukuza jina lake sasa na hata milele.—Zab. 145:1, 2.