-
Uvumilivu UnathawabishwaHuduma ya Ufalme—2004 | Agosti
-
-
Uvumilivu Unathawabishwa
1 “Nanyi kwa kuvumilia mtajipatia nafsi zenu.” (Luka 21:19) Maneno hayo, ambayo ni sehemu ya unabii wa Yesu kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo,” yanaonyesha wazi kwamba tunapodumisha ushikamanifu wetu, ni lazima tuwe tayari kukabili majaribu mengi. Lakini kwa nguvu za Yehova, kila mmoja wetu anaweza ‘kuvumilia mpaka mwisho’ na ‘kuokolewa.’—Mt. 24:3, 13; Flp. 4:13.
2 Mateso, matatizo ya afya, magumu ya kiuchumi, na mikazo ya kihisia inaweza kufanya tukabili majaribu kila siku. Hata hivyo, hatupaswi kamwe kusahau kwamba Shetani anajaribu kuvunja utimilifu wetu kwa Yehova. Kila siku ambapo tunabaki washikamanifu kwa Baba yetu, tunachangia kujibu mashtaka ya yule Mdhihaki. Inafurahisha kama nini kujua kwamba “machozi” tunayotoa tunapokabili majaribu hayasahauliki! Hayo ni yenye thamani kwa Yehova, na ushikamanifu wetu huufanya moyo wake ushangilie!—Zab. 56:8; Met. 27:11.
3 Majaribu Huboresha Sifa Zetu: Mateso yanaweza kuonyesha kwamba mtu ana udhaifu wa imani au wa utu, kama vile kiburi au kukosa subira. Badala ya kujaribu kuepuka au kukomesha majaribu kupitia njia zinazovunja kanuni za Maandiko, tunapaswa kutii shauri la Neno la Mungu linalosema “acheni uvumilivu ukamilishe kazi yake.” Kwa nini? Kwa sababu kuvumilia majaribu kwa uaminifu hutuwezesha tuwe “kamili na timamu katika mambo yote.” (Yak. 1:2-4) Uvumilivu unaweza kutusaidia kusitawisha sifa zenye thamani kubwa, kama vile usawaziko, huruma, na rehema.—Rom. 12:15.
4 Imani Iliyojaribiwa: Tunapovumilia majaribu, tunajipatia imani iliyojaribiwa ambayo ina thamani kubwa machoni pa Mungu. (1 Pet. 1:6, 7) Imani hiyo hututayarisha tusimame imara tunapokabili majaribu wakati ujao. Zaidi ya hayo, tunaweza kuona kibali cha Mungu juu yetu, na hilo huimarisha tumaini letu na kulifanya liwe halisi zaidi kwetu.—Rom. 5:3-5.
5 Thawabu kubwa zaidi kwa ajili ya uvumilivu imeonyeshwa katika andiko la Yakobo 1:12 linalosema: “Mwenye furaha ni mtu anayeendelea kuvumilia jaribu, kwa sababu akiisha kukubaliwa atapokea taji la uzima.” Kwa hiyo, na tubaki imara katika ujitoaji wetu kwa Yehova, tukiwa na uhakika kwamba atawathawabisha “wale wanaoendelea kumpenda.”
-
-
Sehemu ya 2: Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye MaendeleoHuduma ya Ufalme—2004 | Agosti
-
-
Sehemu ya 2: Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Kujitayarisha Kuongoza Funzo
1 Kumfundisha mwanafunzi wa Biblia kwa matokeo kunahusisha mengi kuliko tu kuzungumzia habari za funzo na kusoma maandiko yasiyonukuliwa. Tunahitaji kutoa habari hizo kwa njia inayogusa moyo wa mwanafunzi. Ili kufanya hivyo, tunahitaji kujitayarisha vizuri huku tukimfikiria mwanafunzi.—Met. 15:28.
2 Jinsi ya Kujitayarisha: Anza kwa kusali kwa Yehova kumhusu mwanafunzi huyo na mahitaji yake. Mwombe Yehova akusaidie kuufikia moyo wa mwanafunzi. (Kol. 1:9, 10) Ili kuelewa jambo kuu vizuri, tumia muda fulani kufikiria kichwa cha sura au somo, vichwa vidogo, na vitu vingine kama picha. Jiulize hivi, ‘Kusudi kuu la habari hizi ni nini?’ Hilo litakusaidia kukazia mambo makuu unapoongoza funzo.
3 Pitia habari hizo kwa makini fungu kwa fungu. Tambua majibu ya maswali yaliyochapishwa, na utie alama maneno muhimu tu. Changanua jinsi maandiko yasiyonukuliwa yanavyohusiana na jambo kuu katika fungu, na uamue maandiko mtakayosoma wakati wa funzo. Utaona kwamba inasaidia kuandika mambo machache pambizoni mwa kichapo. Mwanafunzi anapaswa kuona waziwazi kwamba yale anayojifunza yanatoka katika Neno la Mungu.—1 The. 2:13.
4 Fikiria Mahitaji ya Mwanafunzi: Kisha, fikiria mahitaji ya mwanafunzi unapopitia somo hilo. Jaribu kufikiria mapema maswali ambayo huenda akauliza na mambo ambayo huenda akaona ni vigumu kuelewa au kukubali. Jiulize hivi: ‘Anahitaji kuelewa au kurekebisha jambo gani ili afanye maendeleo ya kiroho? Ninaweza kuufikiaje moyo wake?’ Kisha rekebisha ufundishaji wako ili upatane na mahitaji hayo. Nyakati nyingine huenda ukahitaji kutayarisha mfano, maelezo, au maswali kadhaa ili kumsaidia mwanafunzi kushika maana ya jambo au andiko fulani. (Neh. 8:8) Lakini epuka kuingiza habari za ziada ambazo hazimsaidii mwanafunzi kuelewa jambo kuu. Pitio fupi mwishoni mwa funzo litamsaidia kukumbuka mambo makuu.
5 Sisi hufurahi sana wakati wanafunzi wanapozaa matunda ya uadilifu ambayo humletea Yehova sifa! (Flp. 1:11) Ili kuwasaidia wafikie mradi huo, jitayarishe vizuri kila wakati unapoongoza funzo la Biblia.
-