Sehemu ya 2: Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Kujitayarisha Kuongoza Funzo
1 Kumfundisha mwanafunzi wa Biblia kwa matokeo kunahusisha mengi kuliko tu kuzungumzia habari za funzo na kusoma maandiko yasiyonukuliwa. Tunahitaji kutoa habari hizo kwa njia inayogusa moyo wa mwanafunzi. Ili kufanya hivyo, tunahitaji kujitayarisha vizuri huku tukimfikiria mwanafunzi.—Met. 15:28.
2 Jinsi ya Kujitayarisha: Anza kwa kusali kwa Yehova kumhusu mwanafunzi huyo na mahitaji yake. Mwombe Yehova akusaidie kuufikia moyo wa mwanafunzi. (Kol. 1:9, 10) Ili kuelewa jambo kuu vizuri, tumia muda fulani kufikiria kichwa cha sura au somo, vichwa vidogo, na vitu vingine kama picha. Jiulize hivi, ‘Kusudi kuu la habari hizi ni nini?’ Hilo litakusaidia kukazia mambo makuu unapoongoza funzo.
3 Pitia habari hizo kwa makini fungu kwa fungu. Tambua majibu ya maswali yaliyochapishwa, na utie alama maneno muhimu tu. Changanua jinsi maandiko yasiyonukuliwa yanavyohusiana na jambo kuu katika fungu, na uamue maandiko mtakayosoma wakati wa funzo. Utaona kwamba inasaidia kuandika mambo machache pambizoni mwa kichapo. Mwanafunzi anapaswa kuona waziwazi kwamba yale anayojifunza yanatoka katika Neno la Mungu.—1 The. 2:13.
4 Fikiria Mahitaji ya Mwanafunzi: Kisha, fikiria mahitaji ya mwanafunzi unapopitia somo hilo. Jaribu kufikiria mapema maswali ambayo huenda akauliza na mambo ambayo huenda akaona ni vigumu kuelewa au kukubali. Jiulize hivi: ‘Anahitaji kuelewa au kurekebisha jambo gani ili afanye maendeleo ya kiroho? Ninaweza kuufikiaje moyo wake?’ Kisha rekebisha ufundishaji wako ili upatane na mahitaji hayo. Nyakati nyingine huenda ukahitaji kutayarisha mfano, maelezo, au maswali kadhaa ili kumsaidia mwanafunzi kushika maana ya jambo au andiko fulani. (Neh. 8:8) Lakini epuka kuingiza habari za ziada ambazo hazimsaidii mwanafunzi kuelewa jambo kuu. Pitio fupi mwishoni mwa funzo litamsaidia kukumbuka mambo makuu.
5 Sisi hufurahi sana wakati wanafunzi wanapozaa matunda ya uadilifu ambayo humletea Yehova sifa! (Flp. 1:11) Ili kuwasaidia wafikie mradi huo, jitayarishe vizuri kila wakati unapoongoza funzo la Biblia.