Uvumilivu Unathawabishwa
1 “Nanyi kwa kuvumilia mtajipatia nafsi zenu.” (Luka 21:19) Maneno hayo, ambayo ni sehemu ya unabii wa Yesu kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo,” yanaonyesha wazi kwamba tunapodumisha ushikamanifu wetu, ni lazima tuwe tayari kukabili majaribu mengi. Lakini kwa nguvu za Yehova, kila mmoja wetu anaweza ‘kuvumilia mpaka mwisho’ na ‘kuokolewa.’—Mt. 24:3, 13; Flp. 4:13.
2 Mateso, matatizo ya afya, magumu ya kiuchumi, na mikazo ya kihisia inaweza kufanya tukabili majaribu kila siku. Hata hivyo, hatupaswi kamwe kusahau kwamba Shetani anajaribu kuvunja utimilifu wetu kwa Yehova. Kila siku ambapo tunabaki washikamanifu kwa Baba yetu, tunachangia kujibu mashtaka ya yule Mdhihaki. Inafurahisha kama nini kujua kwamba “machozi” tunayotoa tunapokabili majaribu hayasahauliki! Hayo ni yenye thamani kwa Yehova, na ushikamanifu wetu huufanya moyo wake ushangilie!—Zab. 56:8; Met. 27:11.
3 Majaribu Huboresha Sifa Zetu: Mateso yanaweza kuonyesha kwamba mtu ana udhaifu wa imani au wa utu, kama vile kiburi au kukosa subira. Badala ya kujaribu kuepuka au kukomesha majaribu kupitia njia zinazovunja kanuni za Maandiko, tunapaswa kutii shauri la Neno la Mungu linalosema “acheni uvumilivu ukamilishe kazi yake.” Kwa nini? Kwa sababu kuvumilia majaribu kwa uaminifu hutuwezesha tuwe “kamili na timamu katika mambo yote.” (Yak. 1:2-4) Uvumilivu unaweza kutusaidia kusitawisha sifa zenye thamani kubwa, kama vile usawaziko, huruma, na rehema.—Rom. 12:15.
4 Imani Iliyojaribiwa: Tunapovumilia majaribu, tunajipatia imani iliyojaribiwa ambayo ina thamani kubwa machoni pa Mungu. (1 Pet. 1:6, 7) Imani hiyo hututayarisha tusimame imara tunapokabili majaribu wakati ujao. Zaidi ya hayo, tunaweza kuona kibali cha Mungu juu yetu, na hilo huimarisha tumaini letu na kulifanya liwe halisi zaidi kwetu.—Rom. 5:3-5.
5 Thawabu kubwa zaidi kwa ajili ya uvumilivu imeonyeshwa katika andiko la Yakobo 1:12 linalosema: “Mwenye furaha ni mtu anayeendelea kuvumilia jaribu, kwa sababu akiisha kukubaliwa atapokea taji la uzima.” Kwa hiyo, na tubaki imara katika ujitoaji wetu kwa Yehova, tukiwa na uhakika kwamba atawathawabisha “wale wanaoendelea kumpenda.”