“Mimi Sipendezwi”
1 Hivyo ndivyo watu wengi huitikia ujumbe wetu katika maeneo fulani. Ni nini kitakachotusaidia tusivunjike moyo tunapowakuta watu wasiopendezwa katika eneo? Tunaweza kuwachocheaje watu wapendezwe na habari njema?
2 Dumisha Shangwe: Kukumbuka sababu zinazofanya watu wengi wasipendezwe kutatusaidia kudumisha shangwe. Huenda watu ambao wamefundishwa nadharia ya mageuzi au wale waliolelewa katika jamii ambayo haiamini kwamba kuna Mungu wasijue manufaa ya Biblia. Huenda wengine wamekatishwa tamaa na unafiki ambao wameona katika dini. Kwa wengine, huenda kutopendezwa kukaonyesha hali yao ya kutatanika na kukosa tumaini. (Efe. 2:12) Wengine ‘hawajali’ kwa sababu wamelemewa na mahangaiko ya maisha.—Mt. 24:37-39.
3 Ingawa wengine hawapendezwi, tunaweza kuwa na shangwe katika huduma kwa sababu tunajua kwamba jitihada zetu zinamtukuza Yehova. (1 Pet. 4:11) Isitoshe, kuzungumza kuhusu kweli hata na watu ambao bado hawaithamini, huimarisha imani yetu. Na tujitahidi kuwaona watu katika eneo letu kama Yehova awaonavyo. Aliwaonea huruma watu wa Ninawi ambao ‘hawakujua hata kidogo tofauti kati ya mkono wao wa kuume na wa kushoto.’ (Yona 4:11) Watu katika eneo letu wanahitaji habari njema! Hivyo basi, tusikate tamaa bali tutafute njia za kuwachochea wapendezwe na ujumbe wa Biblia.
4 Zungumzia Mahangaiko Yao: Labda katika utangulizi wako, unaweza kutaja jambo linalowahangaisha watu katika eneo hilo, kisha muulize mwenye nyumba maoni yake. Msikilize anapozungumza, kisha mwonyeshe katika Biblia ujumbe wenye kufariji kuhusu mahangaiko yake. Baada ya msiba kutokea katika eneo fulani, Shahidi mmoja alimpa pole kila mwenye nyumba alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba. Anasema hivi: “Bila kutarajia, watu wakaanza kuzungumza nami. Nikawa na mazungumzo mengi mazuri pamoja nao siku hiyo kwa sababu waliona kuwa ninawajali.”
5 Matatizo yote yanayowakabili wanadamu yataondolewa na Ufalme wa Mungu. Jaribu kutambua ni tatizo gani hasa linalomhangaisha mwenye nyumba. Huenda akakuruhusu umweleze ujumbe wa Biblia wenye tumaini. Akikataa, huenda akakusikiliza “wakati mwingine.”—Mdo. 17:32.