Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Jinsi ya Kuanzisha Mafunzo kwa Kutumia Kitabu Biblia Inafundisha
    Huduma ya Ufalme—2006 | Januari
    • Jinsi ya Kuanzisha Mafunzo kwa Kutumia Kitabu Biblia Inafundisha

      Wengi wetu tungefurahia kuongoza funzo la Biblia kama tungefaulu kulianzisha. Kitabu kipya Biblia Inafundisha Nini Hasa? kinaweza kutusaidia. Utangulizi kwenye ukurasa wa 3-7 umekusudiwa kutumiwa kuanzisha mazungumzo ya Biblia yanayotegemea kitabu hicho. Hata wale wasio na uzoefu katika utumishi wataona kwamba ni rahisi kuanzisha mafunzo kwa kutumia utangulizi huo.

      ◼ Jaribu kuanzisha funzo kwa kuzungumzia ukurasa wa 3:

      Baada ya kutaja habari fulani ya karibuni au tatizo linalowasumbua watu katika eneo lenu, mwonyeshe mwenye nyumba maswali yaliyoandikwa kwa herufi nzito kwenye ukurasa wa 3, na umuulize maoni yake. Kisha zungumzia ukurasa wa 4-5.

      ◼ Au huenda ukapenda kuanza kwa kuzungumzia ukurasa wa 4-5:

      Unaweza kuuliza hivi: “Tungefurahi sana kuona mabadiliko haya, sivyo?” Au unaweza kuuliza: “Ungetaka kuona utimizo wa ahadi gani kati ya hizi?” Msikilize kwa makini anapotoa maoni yake.

      Mwenye nyumba akipendezwa na andiko fulani hususa, mwonyeshe kile ambacho Biblia inafundisha kuhusu habari hiyo kwa kuzungumzia mafungu yanayofafanua andiko hilo katika kitabu. (Ona sanduku kwenye ukurasa huu.) Zungumzia habari hiyo jinsi ambavyo ungeizungumzia unapoongoza funzo la Biblia. Unaweza kutumia dakika tano hadi kumi kuzungumzia habari hiyo mlangoni unapomtembelea mtu mara ya kwanza.

      ◼ Unaweza pia kutumia ukurasa wa 6 ili kumchochea mtu atoe maoni yake:

      Mwonyeshe mwenye nyumba maswali yaliyo kwenye ukurasa wa sita, na umuulize hivi: “Je, umewahi kujiuliza maswali haya?” Akipendezwa na swali fulani, zungumzia mafungu ya kitabu yanayojibu swali hilo. (Ona sanduku kwenye ukurasa huu.) Unapozungumzia habari hiyo pamoja na mwenye nyumba unaongoza funzo la Biblia.

      ◼ Unaweza kutumia ukurasa wa 7 kumwonyesha mwenye nyumba jinsi ya kujifunza Biblia:

      Soma sentensi tatu za kwanza kwenye ukurasa huo, kisha ufungue sura ya 3 na umwonyeshe mwenye nyumba jinsi ya kujifunza kwa kutumia fungu la 1-3. Panga kumrudia ili mzungumzie majibu ya maswali yaliyo katika fungu la 3.

      ◼ Jinsi ya kupanga ziara ijayo:

      Unapomalizia mazungumzo katika ziara ya kwanza, fanya mpango ili mwendelee na mazungumzo. Unaweza kusema: “Kwa dakika chache tu tumeona kile ambacho Biblia inafundisha kuhusu habari fulani muhimu. Siku nyingine tunaweza kuzungumzia [taja swali mtakalozungumzia]. Unaonaje nikija wakati kama huu juma lijalo?”

      Tunapokaribia wakati uliowekwa, Yehova anaendelea kututayarisha kwa kazi inayopaswa kufanywa. (Mt. 28:19, 20; 2 Tim. 3:17) Na tutumie kitabu hicho kipya kizuri ili kuanzisha mafunzo ya Biblia.

  • Jinsi ya Kutoa Kitabu Biblia Inafundisha
    Huduma ya Ufalme—2006 | Januari
    • Jinsi ya Kutoa Kitabu Biblia Inafundisha

      Nyongeza hii ina mapendekezo mbalimbali unayoweza kutumia kutoa kitabu Biblia Inafundisha. Ili ufanikiwe, jitahidi kutumia maneno yako mwenyewe, kubadilisha utangulizi upatane na eneo lenu, na kujua mambo hususa yaliyomo katika kitabu ambayo unaweza kutumia kuanzisha mazungumzo. Mapendekezo mengine yanayofaa eneo lenu yanaweza kutumiwa pia.—Ona Huduma Yetu ya Ufalme ya Januari 2005, uku. 8.

      Har–Magedoni

      ◼ “Watu wengi hufikiri kwamba ‘Har–Magedoni’ ni maangamizo makubwa. Je, haishangazi kujua kwamba tunaweza kuitarajia Har–Magedoni kwa hamu? [Mruhusu ajibu, kisha usome Ufunuo 16:14, 16.] Ona maelezo haya kuhusu jinsi maisha yatakavyokuwa baada ya Har–Magedoni.” Fungua ukurasa wa 82-84 na usome fungu la 21.

      Biblia

      ◼ “Watu husema kwamba Biblia ni Neno la Mungu. Je, umewahi kujiuliza kwa nini kitabu hicho kilichoandikwa na wanadamu kinaitwa Neno la Mungu? [Mruhusu ajibu, kisha usome 2 Petro 1:21 na fungu la 5 kwenye ukurasa wa 19-20.] Kitabu hiki kinatoa majibu ya Biblia ya maswali haya.” Mwonyeshe maswali kwenye ukurasa wa 6.

      ◼ “Leo kuna vyanzo vingi sana vya habari kuliko zamani. Lakini unafikiri tunaweza kupata wapi ushauri mzuri utakaotuwezesha kuwa na maisha yenye furaha na mafanikio? [Mruhusu ajibu, kisha usome 2 Timotheo 3:16, 17 na fungu la 12 kwenye ukurasa wa 22-23.] Kitabu hiki kinaonyesha jinsi tunavyoweza kuwa na maisha yanayompendeza Mungu na yanayotunufaisha.” Mwonyeshe chati na picha kwenye ukurasa wa 122-123.

      Kifo/Ufufuo

      ◼ “Watu wengi hawajui inakuwaje mtu anapokufa. Je, unafikiri tunaweza kujua inakuwaje mtu anapokufa? [Mruhusu ajibu, kisha usome Mhubiri 9:5 na fungu la 5-6 kwenye ukurasa wa 58-59.] Kitabu hiki kinaeleza jinsi ahadi ya Mungu ya ufufuo itakavyotimizwa.” Mwonyeshe picha kwenye ukurasa wa 75.

      ◼ “Mpendwa anapokufa, kwa kawaida tunatamani kumwona tena, sivyo? [Mruhusu ajibu.] Watu wengi wamefarijiwa na ahadi ya Biblia ya ufufuo. [Soma Yohana 5:28, 29 na fungu 16-17 kwenye ukurasa wa 71-72.] Sura hii inajibu maswali haya.” Mwonyeshe maswali ya utangulizi kwenye ukurasa wa 66.

      Uzima wa Milele

      ◼ “Watu wengi hutamani kuwa na afya nzuri na maisha marefu. Ikiwa ingewezekana, je, ungetaka kuishi milele? [Mruhusu ajibu, kisha usome Ufunuo 21:3, 4 na fungu la 17 kwenye ukurasa wa 54.] Kitabu hiki kinaeleza jinsi tunavyoweza kupata uzima wa milele, na pia jinsi maisha yatakavyokuwa ahadi ya uzima wa milele itakapotimizwa.”

      Familia

      ◼ “Sote tunataka kuwa na familia yenye furaha, sivyo? [Mruhusu ajibu.] Biblia inaeleza jambo ambalo kila mmoja anapaswa kufanya ili familia iwe na furaha, yaani, kumwiga Mungu kwa kuwapenda wengine.” Soma Waefeso 5:1, 2 na fungu la 4 kwenye ukurasa wa 135.

      Makao

      ◼ “Katika maeneo mengi, ni vigumu sana kwa watu kupata makao mazuri wanayoweza kugharimia. Je, unafikiri kutakuwa na wakati ambapo kila mtu atakuwa na makao mazuri? [Mruhusu ajibu, kisha usome Isaya 65:21, 22 na fungu la 20 kwenye ukurasa wa 34.] Kitabu hiki kinaonyesha jinsi ahadi hiyo ya Mungu itakavyotimizwa.”

      Yehova Mungu

      ◼ “Watu wengi wanaomwamini Mungu wangetaka kumkaribia. Je, unajua kwamba Biblia inatuhimiza tumkaribie Mungu? [Mruhusu ajibu, kisha usome Yakobo 4:8a na fungu la 20 kwenye ukurasa wa 16.] Kitabu hiki kimeandikwa ili kuwasaidia watu wajifunze mengi kumhusu Mungu wakitumia Biblia zao.” Mwonyeshe maswali ya utangulizi kwenye ukurasa wa 8.

      ◼ “Watu wengi huomba jina la Mungu litakaswe au, litukuzwe. Je, umewahi kujiuliza Mungu anaitwa nani? [Mruhusu ajibu, kisha usome Zaburi 83:18 na fungu la 2-3 kwenye ukurasa wa 195.] Kitabu hiki kinazungumzia mafundisho ya kweli ya Biblia kumhusu Yehova Mungu na kusudi lake kwa wanadamu.”

      Yesu Kristo

      ◼ “Duniani pote, watu wamesikia kumhusu Yesu Kristo. Watu fulani wanasema kwamba alikuwa mtu mashuhuri tu. Wengine wanamwabudu wakisema kwamba yeye ni Mungu Mweza-Yote. Je, unafikiri maoni yetu kumhusu Yesu Kristo ni ya muhimu?” Mruhusu ajibu, kisha usome Yohana 17:3 na fungu la 3 kwenye ukurasa wa 37-38. Mwonyeshe maswali ya utangulizi ya sura ya 8.

      Sala

      ◼ “Je, umewahi kujiuliza Mungu anajibu sala kwa njia gani? [Mruhusu ajibu, kisha usome 1 Yohana 5:14, 15 na fungu la 16-18 kwenye ukurasa wa 170-172.] Sura hii inaeleza pia kwa nini tunapaswa kusali kwa Mungu na kile tunachopaswa kufanya ili Mungu asikilize sala zetu.”

      Dini

      ◼ “Siku hizi watu husema kwamba dini hazitatui matatizo ya wanadamu bali zinayasababisha. Je, unafikiri dini zinawaongoza wanadamu ipasavyo? [Mruhusu ajibu, kisha usome Mathayo 7:13, 14 na fungu la 5 kwenye ukurasa wa 145-146.] Sura hii inaonyesha mambo sita yanayoonyesha ni ibada gani inayompendeza Mungu.” Mwonyeshe orodha kwenye ukurasa wa 147.

      Misiba/Kuteseka

      ◼ “Msiba unapotokea, watu wengi hujiuliza kama Mungu kwa kweli anawajali wanadamu na anaona jinsi wanavyoteseka. Je, umewahi kujiuliza swali hilo? [Mruhusu ajibu, kisha usome 1 Petro 5:7 na fungu la 11 kwenye ukurasa wa 11.] Kitabu hiki kinaeleza jinsi Mungu atakavyokomesha kabisa mateso yote yanayowapata wanadamu.” Mwonyeshe maswali yaliyo mwanzoni mwa ukurasa wa 106.

      Vita/Amani

      ◼ “Watu kila mahali wanatamani amani. Je, unafikiri kwamba tumaini la kuwa na amani duniani ni ndoto tu? [Mruhusu ajibu, kisha usome Zaburi 46:8, 9.] Kitabu hiki kinaeleza jinsi Mungu atakavyotimiza kusudi lake na kuleta amani duniani.” Mwonyeshe picha kwenye ukurasa wa 35, na uzungumzie fungu la 17-21 kwenye ukurasa wa 34-36.

      [Sanduku katika ukurasa wa 5]

      Jinsi ya Kueleza Kuhusu Michango

      “Ukitaka kutoa mchango mdogo kwa ajili ya kazi yetu ya ulimwenguni pote, nitafurahi kuupokea.”

      “Ijapokuwa vitabu vyetu hutolewa bila malipo, sisi hukubali michango kwa ajili ya kazi yetu ya ulimwenguni pote.”

      “Huenda unajiuliza tunawezaje kugharimia kazi hii. Kazi yetu ya ulimwenguni pote inategemezwa kwa michango ya hiari. Ukitaka kutoa mchango mdogo sasa, nitafurahi kuupokea.”

  • (1) Swali, (2) Andiko, na (3) Sura
    Huduma ya Ufalme—2006 | Januari
    • (1) Swali, (2) Andiko, na (3) Sura

      Njia rahisi ya kutoa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? ni (1) kumuuliza mwenye nyumba maoni yake kuhusu jambo fulani, (2) kusoma andiko linalohusiana na jambo hilo, kisha (3) kumwonyesha katika kitabu hicho sura inayozungumzia jambo hilo na kusoma maswali ya utangulizi ya sura hiyo. Mwenye nyumba akivutiwa, unaweza kumwonyesha jinsi ya kujifunza Biblia ukitumia mafungu ya kwanza ya sura hiyo. Unaweza kutumia njia hii kuanzisha funzo unapomtembelea mtu mara ya kwanza au unapofanya ziara ya kurudia.

      ◼ “Je, unafikiri wanadamu wanaweza kumjua Muumba mwenye nguvu zote, kama inavyoonyeshwa katika andiko hili?” Soma Matendo 17:26, 27, kisha umruhusu ajibu. Baada ya hapo, zungumzia sura ya 1.

      ◼ “Kwa kuwa tuna matatizo mengi leo, je, unafikiri tunaweza kupata faraja na tumaini kama inavyoonyeshwa katika andiko hili?” Soma Waroma 15:4, kisha umruhusu ajibu. Baada ya hapo, zungumzia sura ya 2.

      ◼ “Ikiwa ungekuwa na uwezo, je, ungekomesha mambo haya?” Soma Ufunuo 21:4, kisha umruhusu ajibu. Baada ya hapo, zungumzia sura ya 3.

      ◼ “Je, unafikiri watoto wetu watakuja kufurahia hali zinazozungumziwa katika wimbo huu wa zamani za kale?” Soma Zaburi 37:10, 11, kisha umruhusu ajibu. Baada ya hapo, zungumzia sura ya 3.

      ◼ “Je, unafikiri maneno haya yatakuja kutimizwa?” Soma Isaya 33:24, kisha umruhusu ajibu. Baada ya hapo, zungumzia sura ya 3.

      ◼ “Umewahi kujiuliza ikiwa wafu wanajua mambo ambayo wale walio hai wanafanya?” Mruhusu ajibu, kisha usome Mhubiri 9:5. Baada ya hapo, zungumzia sura ya 6.

      ◼ “Je, unafikiri kwamba siku moja tutawaona tena wapendwa wetu waliokufa, kama Yesu alivyosema katika mistari hii?” Soma Yohana 5:28, 29, kisha umruhusu ajibu. Baada ya hapo, zungumzia sura ya 7.

      ◼ “Unafikiri ni nini kinachohitajiwa ili mapenzi ya Mungu yatendeke duniani kama mbinguni, kulingana na andiko hili linalojulikana sana?” Soma Mathayo 6:9, 10, kisha umruhusu ajibu. Baada ya hapo, zungumzia sura ya 8.

      ◼ “Je, unafikiri tunaishi katika nyakati zinazotabiriwa katika unabii huu?” Soma 2 Timotheo 3:1-4, kisha umruhusu ajibu. Baada ya hapo, zungumzia sura ya 9.

      ◼ “Watu wengi hawaelewi ni kwa nini matatizo ya wanadamu yanazidi kuwa mabaya. Je, umewahi kujiuliza ikiwa matatizo hayo yanazidi kuwa mabaya kwa sababu inayoonyeshwa katika andiko hili?” Soma Ufunuo 12:9, kisha umruhusu ajibu. Baada ya hapo, zungumzia sura ya 10.

      ◼ “Je, ungependa kupata jibu la swali kama hili?” Soma Ayubu 21:7, kisha umruhusu ajibu. Baada ya hapo, zungumzia sura ya 11.

      ◼ “Je, unafikiri kwamba kufuata shauri hili la Biblia kutawasaidia watu wawe na familia yenye furaha?” Soma Waefeso 5:33, kisha umruhusu ajibu. Baada ya hapo, zungumzia sura ya 14.

      Unaweza kuripoti funzo la Biblia baada ya kuliongoza mara mbili tangu ulipomwonyesha mwenye nyumba jinsi funzo linavyofanywa na ikiwa unafikiri kwamba funzo hilo litaendelea.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki