Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • be funzo 32 uku. 194-uku. 196 fu. 4
  • Kuzungumza kwa Usadikisho

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuzungumza kwa Usadikisho
  • Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Habari Zinazolingana
  • Kuhubiri Habari Njema kwa Usadikisho Wenye Nguvu
    Huduma Yetu ya Ufalme—2000
  • Kuzungumza kwa Usadikisho
    Boresha Uwezo Wako wa Kusoma na Kufundisha
  • Simameni Mkiwa Kamili kwa Usadikisho Imara
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Wazazi​—Wasaidieni Watoto Wenu Wawe ‘Wenye Hekima kwa Ajili ya Wokovu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
Pata Habari Zaidi
Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
be funzo 32 uku. 194-uku. 196 fu. 4

SOMO LA 32

Kuzungumza kwa Usadikisho

Unahitaji kufanya nini?

Unahitaji kuzungumza kwa njia inayoonyesha unasadiki kabisa kwamba mambo unayosema ni kweli na ni muhimu.

Kwa Nini Ni Muhimu?

Usadikisho utawatia moyo wengine wafikirie kwa uzito mambo unayosema na wayafuate.

MTU anapozungumza kwa usadikisho, wengine huona anaamini kabisa jambo analosema. Mtume Paulo alionyesha usadikisho kama huo katika huduma yake. Aliwaandikia hivi wale waliopata kuwa waamini huko Thesalonike: “Habari njema tuhubiriyo haikutokea miongoni mwenu kwa usemi pekee bali pia kwa . . . usadikisho wenye nguvu.” (1 The. 1:5) Maneno yake na maisha yake yalionyesha usadikisho huo. Sisi pia tunapaswa kutangaza kweli za Biblia kwa usadikisho wenye nguvu.

Kuzungumza kwa usadikisho si kushikilia kauli mno, si kushikilia mambo bila msingi, wala si kuonyesha kiburi. Badala yake, mtu mwenye usadikisho anapozungumzia mambo yaliyo katika Neno la Mungu, yeye huyazungumzia kwa imani yenye nguvu.—Ebr. 11:1.

Pindi za Kuonyesha Usadikisho. Ni muhimu kuzungumza kwa usadikisho unapokuwa katika huduma ya shambani. Mbali na kusikiliza ujumbe wako, kwa kawaida watu hutazama jinsi unavyozungumza. Wanatambua hisia zako kuhusu mambo unayosema. Usadikisho wako unaweza kuonyesha kwamba una jambo muhimu sana la kuwaeleza kuliko maneno tu.

Pia ni vizuri kuwa na usadikisho unapohutubia waamini wenzako. Mtume Petro aliandika barua yake ya kwanza ili “kutoa kitia-moyo na ushahidi wa bidii kwamba hii ndiyo fadhili isiyostahiliwa ya Mungu.” Aliwatia moyo akina ndugu akisema: “Simameni imara.” (1 Pet. 5:12) Mtume Paulo alionyesha usadikisho uliofaidi kutaniko la Roma alipowaandikia. Sisi pia tunaweza kuiga jambo hilo. Aliandika: “Nasadiki kwamba wala kifo wala uhai wala malaika wala serikali wala mambo yaliyo hapa sasa wala mambo yatakayokuja wala nguvu wala kimo wala kina wala kiumbe kingine chochote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.” (Rom. 8:38, 39) Paulo pia aliwaandikia akiwasihi wawatangazie wengine habari njema, na bidii yake mwenyewe katika utumishi ilionyesha wazi kwamba yeye mwenyewe anasadiki umuhimu wa kazi hiyo. (Mdo. 20:18-21; Rom. 10:9, 13-15) Wazee Wakristo wanapaswa kuonyesha wazi usadikisho kama huo wanapofundisha Neno la Mungu.

Wazazi wanapaswa kuwa na usadikisho wanapozungumzia mambo ya kiroho na watoto wao wakati wa funzo na nyakati nyingine. Kwa hiyo, ni lazima wazazi wakuze upendo kwa Mungu na njia zake mioyoni mwao wenyewe. Ndipo wataweza kuzungumza na watoto wao kwa usadikisho wa moyoni ‘kwa maana katika wingi wa moyo kinywa husema.’ (Luka 6:45; Kum. 6:5-7) Usadikisho kama huo pia utachochea wazazi waweke mfano mzuri wa ‘imani isiyo na unafiki.’—2 Tim. 1:5.

Ni muhimu kuzungumza kwa usadikisho hasa imani yako inapopingwa. Mwanafunzi mwenzako, mwalimu, au mfanyakazi mwenzako anaweza kushtuka kwamba hushirikiani nao katika sherehe fulani. Ukimjibu kwa njia thabiti na kumpa sababu nzuri, anaweza kuheshimu msimamo wako unaotegemea Biblia. Namna gani mtu akijaribu kukushawishi ufanye tendo baya kama kukosa uaminifu, kutumia dawa za kulevya, au kufanya uasherati? Ni muhimu kusema wazi kwamba huwezi kamwe kutenda mambo kama hayo na huwezi kuthubutu hata akikujaribu kadiri gani. Zungumza kwa usadikisho unapokataa kishawishi hicho. Yosefu alisema hivi kwa uthabiti alipokataa utongozi wa mke wa Potifa: “Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?” Mke wa Potifa alipoendelea kumtongoza, Yosefu alitoroka.—Mwa. 39:9, 12.

Jinsi ya Kuonyesha Usadikisho. Maneno yako yanaweza kuonyesha usadikisho. Pindi kadhaa Yesu alianzisha mazungumzo yake kwa semi kama hizi: ‘Kwa kweli kabisa nakuambia.’ (Yn. 3:3, 5, 11; 5:19, 24, 25) Paulo alionyesha usadikisho kwa kutumia semi kama “Nasadiki,” “Najua nami nashawishwa katika Bwana Yesu,” na “Ninasema kweli, sisemi uwongo.” (Rom. 8:38; 14:14; 1 Tim. 2:7) Ili kukazia utimizo wa neno lake, nyakati nyingine Yehova aliwapulizia manabii wake watumie semi zenye usadikisho kama, “haina budi kuja.” (Hab. 2:3) Unaporejelea unabii kama huu, unaweza kutumia usemi kama huo. Ukimtumaini Yehova bila kujitumaini na ukizungumza na wengine kwa njia ya heshima, semi zako zenye usadikisho zitaonyesha kwamba una imani yenye nguvu.

Usadikisho unaweza pia kuonyeshwa na nguvu na mkazo wa maneno yako. Ishara za uso na ishara za mwili huchangia kuonyesha usadikisho, hata ingawa kila mtu ana njia tofauti ya kuonyesha ishara hizo. Hata kama wewe ni mwenye haya au kwa kawaida una sauti ya upole, unapoamini kabisa kwamba mambo unayosema ni ya kweli na kwamba wengine wanahitaji kuyasikia, usadikisho wako utaonekana wazi.

Bila shaka, usadikisho wowote tunaoonyesha unapaswa kutoka moyoni. Watu wakitambua kwamba tunajifanya na hatuzungumzi kutoka moyoni, labda hawatachukua ujumbe wetu kwa uzito. Basi, hakikisha unazungumza kwa njia yako ya kawaida. Unaweza kuzungumza kwa sauti ya juu kuliko kawaida na kwa mkazo zaidi kulingana na idadi ya wasikilizaji. Lakini unapaswa kukusudia la kuzungumza kwa unyofu na kwa njia ya kawaida sana.

Mambo Yanayotusaidia Kuonyesha Usadikisho. Kwa kuwa usadikisho unahusu hisia zako juu ya habari unayozungumzia, njia kuu ya kufaulu ni kujitayarisha vizuri. Kutoa tu habari mahali fulani na kurudia kuitaja hakutoshi. Unahitaji kuelewa habari hiyo vizuri na kuweza kuieleza kwa maneno yako mwenyewe. Ni lazima usadiki kabisa kwamba habari hiyo ni kweli na kwamba unasema jambo ambalo linafaidi wale wanaokusikiliza. Hii inamaanisha kwamba unapotayarisha hotuba, fikiria hali za wasikilizaji na pia mambo ambayo tayari wanafahamu kuhusu habari hiyo au jinsi wanavyoiona.

Ni rahisi kwa wengine kuona usadikisho wetu tunapotoa hotuba kwa ufasaha. Basi, mbali na kutayarisha hotuba nzuri, fanya bidii uitoe vizuri. Fikiria sana sehemu za hotuba ambazo zinapaswa kukaziwa ili uzikazie bila kutazama sana maandishi. Kumbuka pia kusali ili Yehova abariki jitihada zako. Ukifanya hivyo ‘utajipa ujasiri kwa njia ya Mungu,’ ukizungumza kwa njia inayoonyesha usadikisho kuhusu ukweli na umuhimu wa ujumbe wako.—1 The. 2:2.

JINSI YA KUFAULU

  • Zungumza kwa hisia inayofaa habari hiyo.

  • Tumia semi zinazoonyesha usadikisho.

  • Chunguza hotuba yako mpaka uielewe vizuri na kuweza kuitoa kwa maneno yako mwenyewe. Ni lazima usadiki kabisa kwamba hotuba hiyo ina mambo ya kweli na itawafaidi wasikilizaji.

MAZOEZI: Soma masimulizi yafuatayo ya Biblia: Kutoka 14:10-14; 2 Wafalme 5:1-3; Danieli 3:13-18; Matendo 2:22-36. Katika masimulizi hayo, watumishi wa Mungu walionyeshaje usadikisho? Usadikisho wao ulitegemea nini? Unawezaje kuonyesha usadikisho kama huo leo?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki