Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • rs uku. 275-uku. 282
  • Sikukuu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sikukuu
  • Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Habari Zinazolingana
  • Shughuli za Baada ya Masomo
    Shule na Mashahidi wa Yehova
  • Desturi Zinazopendwa na Watu Wengi Zinazomchukiza Mungu
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Je, Tusherehekee Sikukuu?
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Asili ya Krismasi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
rs uku. 275-uku. 282

Sikukuu

Maana: Siku ambazo watu hawaendi kazini na shuleni ili kuadhimisha tukio fulani. Huenda siku hizo pia zikawa vipindi vya sherehe za familia au za jamii. Huenda washiriki wakaziona kuwa ni sikukuu za kidini au za kijamii au kilimwengu.

Je, mwadhimisho wa Krismasi unapatana na Biblia?

Tarehe ya mwadhimisho

Cyclopædia ya M’Clintock na Strong inasema: “Mungu hakuagiza Krismasi iadhimishwe, wala mwadhimisho huo hautokani na A[gano] J[ipya]. A[gano] J[ipya] wala chanzo kingine chochote, hakitaji siku ya kuzaliwa kwa Kristo.”—(New York, 1871) Buku la 2, uku. 276.

Luka 2:8-11 huonyesha kwamba wakati wa kuzaliwa kwa Yesu, wachungaji walikuwa nje usiku. Kitabu Daily Life in the Time of Jesus chaeleza: ‘Wakati wa baridi kali, makundi ya wanyama hayakutoka nje; na hilo pekee linaweza kuthibitisha kwamba tarehe ya Krismasi, ya wakati wa baridi kali, haiwezi kuwa sahihi, kwa kuwa Injili husema kwamba wachungaji walikuwa nje.’—(New York, 1962), Henri Daniel-Rops, uku. 228.

The Encyclopedia Americana husema hivi: “Sababu ya kuchagua Desemba 25 kuwa siku ya Krismasi haieleweki waziwazi, lakini inaaminiwa kwamba siku hiyo ilichaguliwa ili ilingane na sherehe za kipagani zilizotukia karibu na wakati ambapo jua huwa mbali zaidi na ikweta, wakati wa baridi kali, siku zinapoanza kurefuka, ili kusherehekea ‘kuzaliwa upya kwa jua.’ . . . Satanalia ya Kiroma (sikukuu ya zohali, mungu wa kilimo, na ya nguvu mpya za jua), pia iliadhimishwa wakati huo, na inaonekana kwamba desturi fulani za Krismasi zilianzia katika mwadhimisho huo wa kale wa kipagani.”—(1977), Buku la 6, uku. 666.

New Catholic Encyclopedia inakubali hivi: “Tarehe ya kuzaliwa kwa Kristo haijulikani. Injili hazitaji siku wala mwezi . . . Kulingana na nadharia iliyotolewa na H. Usener . . . na inayokubaliwa na wasomi wengi leo, kuzaliwa kwa Kristo kulipewa tarehe ambayo jua linakuwa mbali zaidi na ikweta, wakati wa baridi kali, (Desemba 25 katika kalenda ya Julias, Januari 6 katika kalenda ya Misri), kwa sababu siku hiyo, jua lilipoanza kurudi kwenye anga za kaskazini, waabudu wa kipagani wa Mithra walisherehekea dies natalis Solis Invicti (kuzaliwa kwa jua lisiloshindika). Katika Desemba 25, 274, Aurelian alikuwa amemtangaza mungu-jua kuwa mdhamini mkuu wa milki na kumjengea hekalu katika Uwanja wa Martius. Krismasi ilianza wakati madhehebu ya jua yalipositawi nchini Roma.”—(1967), Buku la 3, uku. 656.

Watu wenye hekima, au Mamajusi, walioongozwa na nyota

Mamajusi hao walikuwa wanajimu kutoka mashariki. (Mt. 2:1, 2) Ijapokuwa unajimu unapendwa na watu wengi leo, Biblia inapinga kabisa zoea hilo. (Ona ukurasa wa 175, 176 chini ya kichwa “Majaliwa.”) Je, Mungu angewaelekeza kwa Yesu aliyezaliwa karibuni watu wenye mazoea ambayo Yeye mwenyewe anayashutumu?

Mathayo 2:1-16 huonyesha kwamba nyota hiyo iliwaongoza wanajimu hao kwa Mfalme Herode kwanza kisha kwa Yesu na kwamba Herode alipanga Yesu auawe. Biblia haitaji mtu mwingine yeyote aliyeiona “nyota” hiyo ila wanajimu hao. Walipoondoka, malaika wa Yehova alimwagiza Yosefu akimbilie Misri ili kumlinda mtoto. Je, “nyota” hiyo ilikuwa ishara kutoka kwa Mungu au kutoka kwa mtu fulani aliyetaka kumwangamiza Mwana wa Mungu?

Ona kwamba masimulizi ya Biblia hayasemi kwamba walimkuta Yesu mchanga katika hori, kama vile ambavyo huonyeshwa katika picha za Krismasi. Wanajimu walipofika, Yesu na wazazi wake walikuwa wakiishi katika nyumba. Kuhusu umri wa Yesu wakati huo, kumbuka kwamba, ikitegemea habari ambazo Herode alikuwa amepata kutokana na wanajimu, alitoa amri kwamba wavulana wote katika wilaya ya Bethlehemu wenye umri wa miaka miwili kurudi chini waangamizwe.—Mt. 2:1, 11, 16.

Kutoa zawadi wakati wa maadhimisho hayo; hadithi za Baba Krismasi, n.k.

Zoea la kutoa zawadi za Krismasi halitokani na zawadi zilizotolewa na wale Mamajusi. Kama tulivyoona, hawakufika wakati wa kuzaliwa kwa Yesu. Isitoshe, badala ya kupeana zawadi wao kwa wao, walimpa zawadi Yesu mchanga, kulingana na desturi ya siku hizo wakati wa kutembelea watu mashuhuri.

The Encyclopedia Americana inaeleza hivi: “Wakati wa Satanalia . . . kulikuwa na karamu, na watu walipeana zawadi.” (1977, Buku la 24, uku. 299) Katika visa vingi hilo lawakilisha roho ya Krismasi—kupeana zawadi. Roho hiyo ya kutoa zawadi haileti furaha ya kweli, kwa sababu inavunja kanuni za Kikristo kama zile zinazopatikana katika Mathayo 6:3, 4 na 2 Wakorintho 9:7. Kwa kweli, upendo unaweza kumchochea Mkristo awape wengine zawadi nyakati nyingine mwakani, akifanya hivyo kwa kadiri anavyotaka.

Watoto huambiwa kwamba zawadi huletwa na Baba-Krismasi. (The World Book Encyclopedia, 1984, Buku la 3, uku. 414) Bila shaka, hadithi hizo si za kweli. Je, kusimuliwa kwa hadithi hizo huwafanya watoto waione kweli kuwa jambo muhimu? Na je, zoea hilo linamheshimu Yesu Kristo, aliyefundisha kwamba ni lazima Mungu aabudiwe kwa kweli?—Yoh. 4:23, 24.

Je, kuna ubaya wowote kusherehekea maadhimisho ambayo huenda yasiwe ya Kikristo maadamu si maadhimisho ya kidini?

Efe. 5:10, 11: “Endeleeni kuhakikisha lile linalokubalika kwa Bwana; na mwache kushirikiana pamoja nao katika matendo yasiyozaa matunda, ambayo ni ya giza, lakini badala yake muwe hata mkiyakaripia.”

2 Kor. 6:14-18: “Kuna ushirika gani kati ya uadilifu na uasi-sheria? Au nuru ina ushirika gani na giza? Na zaidi, kuna upatano gani kati ya Kristo na Beliali? Au mtu mwaminifu ana fungu gani na asiye mwamini? Na hekalu la Mungu lina upatano gani na sanamu? . . . ‘“Kwa hiyo tokeni katikati yao, na mjitenge,” asema Yehova, “na mwache kugusa kitu kilicho najisi”’; ‘“nami nitawakaribisha ndani, . . .  nanyi mtakuwa wana na mabinti kwangu,” asema Yehova Mweza-Yote.’” (Kumpenda Yehova kikweli na kutaka sana kumpendeza kutamsaidia mtu aache mazoea yasiyo ya Kikristo ambayo huenda yakauvutia moyo wake. Mtu ambaye kwa kweli anamjua na kumpenda Yehova haoni kwamba ananyimwa furaha kwa njia yoyote kwa kuacha mazoea yanayoheshimu miungu ya uwongo au yanayoendeleza uwongo. Upendo wa kweli unamfanya ashangilie kweli, wala si ukosefu wa uadilifu. Ona 1 Wakorintho 13:6.)

Linganisha na Kutoka 32:4-10. Ona kwamba Waisraeli walifuata zoea la kidini la Kimisri lakini wakalipa jina jipya, “sherehe kwa ajili ya Yehova.” Lakini Yehova aliwaadhibu vikali kwa sababu ya zoea hilo. Leo tunaona tu mazoea ya karne ya 20 yanayopatikana katika sikukuu nyingi. Huenda mazoea mengine yakaonekana kuwa hayana madhara. Lakini Yehova aliyaona mazoea ya kidini ya kipagani ambayo ndiyo chanzo cha mazoea ya leo. Je, hatupaswi kuzingatia hasa maoni yake?

Mfano: Tuseme umati wa watu umefika kwenye nyumba ya bwana mmoja wakisema wamekuja kuadhimisha sikukuu ya kuzaliwa kwake. Yeye hapendezwi na maadhimisho hayo ya sikukuu za kuzaliwa. Hapendi kuona watu wakila kupita kiasi au wakilewa au wakijihusisha katika mwenendo mpotovu. Lakini baadhi yao wanatenda mambo yote hayo, na kuwaletea zawadi wote waliopo isipokuwa yeye! Isitoshe, wanachagua tarehe ya kuzaliwa kwa mmoja kati ya adui za mtu huyo kuwa siku ya kufanya maadhimisho hayo. Mtu huyo angeonaje? Je, wewe ungependa kushirikiana nao? Hivyo ndivyo inavyofanywa katika maadhimisho ya Krismasi.

Ista na desturi zinazohusiana nayo zilianzia wapi?

The Encyclopædia Britannica inaeleza hivi: “Maadhimisho ya sikukuu ya Ista hayapatikani katika Agano Jipya, wala katika maandishi ya Mababa wa kimitume. Wakristo wa kwanza hawakuziona nyakati zozote za pekee kuwa takatifu.”—(1910), Buku la 8, uku. 828.

The Catholic Encyclopedia hutuambia hivi: “Desturi nyingi za kipagani, zilizokuwa zikisherehekea kurudi kwa majira ya kuchipua, zilipenya katika Ista. Yai hufananisha kuchipuka kwa uhai, mwanzoni mwa majira ya kuchipua . . . Sungura ni mfano wa kipagani ambao sikuzote huwakilisha uwezo wa kuzaa.”—(1913), Buku la 5, uku. 227.

Kitabu The Two Babylons, cha Alexander Hislop, kinasema hivi: “Neno Ista linamaanisha nini? Si jina la Kikristo. Jina hilo lilianzia Ukaldayo. Ista si lingine ila Astarte, moja kati ya majina ya cheo ya Beltis, malkia wa mbinguni, ambaye jina lake, . . . lililogunduliwa na Layard juu ya nguzo za ukumbusho za Ashuru, ni Ishtar. . . . Hiyo ndiyo historia ya Ista. Mazoea yanayopendwa na watu wengi ambayo hufanywa wakati wa Ista yanathibitisha ushuhuda wa historia wa kwamba mwadhimisho huo ulianzia Babiloni. Mikate yenye umbo la msalaba ya Ijumaa Kuu, pamoja na mayai ya Pasaka au Jumapili ya Ista yaliyopakwa rangi, yalitumiwa katika desturi za dini za Kikaldayo kama yanavyotumiwa sasa.”—(New York, 1943), uku. 103, 107, 108; linganisha na Yeremia 7:18.

Je, Wakristo wanaweza kuadhimisha Mwaka Mpya?

Kulingana na The World Book Encyclopedia, “Waroma walitenga Januari 1 kuwa Siku ya Mwaka Mpya katika mwaka wa 46 K.W.K. Waroma waliitenga siku hiyo kwa ajili ya Jano, mungu wa malango, milango, na mianzo. Mwezi wa Januari ulipata jina lake kutokana na Jano, aliyekuwa na nyuso mbili—uso mmoja ukitazama mbele na ule mwingine ukitazama nyuma.”—(1984), Buku la 14, uku. 237.

Tarehe na desturi zinazohusiana na maadhimisho ya Mwaka Mpya zinatofautiana katika nchi mbalimbali. Katika sehemu nyingi watu hufanya karamu za kula na kunywa kupindukia. Hata hivyo, Waroma 13:13 hushauri hivi: “Kama katika wakati wa mchana na tujiendeshe kwa adabu, si katika karamu za kupindukia na vipindi vya kulewa, si katika ngono isiyo halali na mwenendo mpotovu, si katika mizozo na wivu.” (Ona pia 1 Petro 4:3, 4; Wagalatia 5:19-21.)

Sikukuu za kukumbuka “roho za wafu” zilianzia wapi?

Chapa ya 1910 ya The Encyclopædia Britannica inaeleza hivi: “Siku ya Marehemu Wote . . . siku iliyotengwa katika Kanisa Katoliki ili kuwakumbuka waaminifu waliokufa. Maadhimisho hayo yanategemea fundisho la kwamba nafsi za waaminifu ambazo wakati wa kufa hazikuwa zimesafishwa dhambi zinazoweza kusamehewa, au hazijaondolewa makosa ya zamani, haziwezi kufikia Heri ya Kuona Mungu, na ya kwamba huenda zikasaidiwa kufanya hivyo kwa njia ya sala na kwa njia ya dhabihu ya misa. . . . Imani fulani za watu wengi zinazohusiana na Siku ya Marehemu Wote ni za kipagani na ni za zamani za kale. Wakulima wa nchi nyingi za Kikatoliki huamini kwamba wafu hurudi kwenye nyumba zao za zamani katika usiku wa Siku ya Marehemu Wote na kula chakula cha walio hai.”—Buku la 1, uku. 709.

The Encyclopedia Americana inasema: “Inaonekana kwamba mambo mbalimbali yanayohusiana na Mkesha wa Sikukuu ya Watakatifu Wote (Halloween) yalitokana na sherehe ya Druid katika nyakati za kabla ya Ukristo. Waselti walikuwa na sikukuu kwa ajili ya miungu wawili wakubwa—mungu-jua na mungu wa wafu (anayeitwa Samhain), ambaye sikukuu yake ilifanywa Novemba 1, mwanzo wa Mwaka Mpya wa Kiselti. Sikukuu ya wafu ilipenya hatua kwa hatua katika desturi ya dini ya Kikristo.”—(1977), Buku la 13, uku. 725.

Kitabu The Worship of the Dead chataja chanzo hiki: “Hadithi za mataifa yote ya kale zinahusiana na matukio ya Gharika . . . Uzito wa hoja hiyo unathibitishwa na maadhimisho ya ile sikukuu ya wafu ya kukumbuka tukio hilo, inayoadhimishwa na mataifa yaliyo karibu, hali kadhalika mataifa yaliyo mbali, yaliyotenganishwa kwa bahari kuu na pia kwa karne nyingi za wakati. Isitoshe, watu wote huadhimisha sikukuu hiyo katika au karibu na siku yenyewe ambayo, kulingana na masimulizi ya Musa, Gharika ilitukia, yaani, siku ya kumi na saba ya mwezi wa pili—mwezi unaolingana sana na mwezi wetu wa Novemba.” (London, 1904, Kanali J. Garnier, uku. 4) Kwa hiyo, kwa hakika maadhimisho hayo yalianza kwa kuwaheshimu watu ambao Mungu alikuwa amewaharibu kwa sababu ya ubaya wao katika siku za Noa.—Mwa. 6:5-7; 7:11.

Sikukuu hizo zenye kuheshimu “roho za wafu” kana kwamba ziko hai katika makao mengine ni kinyume cha maelezo ya Biblia kwamba kifo ni hali ya kutokuwa na fahamu kabisa.—Mhu. 9:5, 10; Zab. 146:4.

Kuhusu asili ya imani ya kutoweza kufa kwa nafsi ya binadamu, ona ukurasa wa 102-104, chini ya kichwa “Kifo,” na ukurasa wa 225, 226, chini ya kichwa “Nafsi.”

Siku ya Wapendanao ilianzia wapi?

The World Book Encyclopedia yaeleza hivi: “Siku ya Wapendanao (Valentine) huadhimishwa katika siku ya karamu ya Wakristo wawili walioitwa Valentine, waliouawa kwa sababu ya imani yao. Lakini desturi zinazohusiana na siku hiyo . . . huenda zilitokana na sikukuu ya kale ya Kiroma inayoitwa Lupercalia iliyoadhimishwa kila Februari 15. Sikukuu hiyo ilimheshimu Juno, mungu wa kike wa Kiroma wa wanawake na ndoa, na Pan, mungu wa mambo ya asili.”—(1973), Buku la 20, uku. 204.

Zoea la kutenga siku ya kuwaheshimu akina mama lilianzia wapi?

Encyclopædia Britannica inasema: “Sikukuu inayotokana na desturi ya ibada ya mama katika Ugiriki ya kale. Ibada rasmi ya mama, pamoja na sherehe za Sibele, au Rea, Mama Mkuu wa Miungu, zilifanywa Machi 15 katika sehemu zote za Asia Ndogo.”—(1959), Buku la 15, uku. 849.

Ni kanuni gani za Biblia zinazoonyesha maoni ya Wakristo kuhusu sherehe za kukumbuka matukio mbalimbali katika historia ya kisiasa ya taifa?

Yoh. 18:36: “Yesu akajibu [gavana Mroma]: ‘Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.’”

Yoh. 15:19: “Kama [ninyi wafuasi wa Yesu] mngekuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungependa kilicho chake. Sasa kwa sababu ninyi si sehemu ya ulimwengu, bali nimewachagua ninyi kutoka ulimwenguni, kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukia ninyi.”

1 Yoh. 5:19: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (Linganisha na Yohana 14:30; Ufunuo 13:1, 2; Danieli 2:44.)

Sikukuu nyingine za sehemu mbalimbali na za kitaifa

Kuna sikukuu nyingi. Zote haziwezi kuzungumziwa hapa. Lakini historia ambayo imetolewa, inaonyesha mambo tunayoweza kuzingatia kuhusiana na sikukuu yoyote, na kanuni za Biblia zilizozungumziwa zinatoa mwongozo wa kutosha kwa ajili ya wale wanaotamani kufanya mapenzi ya Yehova Mungu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki