Asili ya Krismasi
JINA “Krismasi,” linalomaanisha “Misa ya Kristo” (au Sherehe ya Kristo), ladokeza kwamba sikukuu inayoitwa hivyo ni ya Kikristo. Watu wengi huiona kama inaadhimisha kuzaliwa kwa Yesu Kristo Desemba 25.
Lakini, ushuhuda wa Biblia waonyesha Kristo hakuzaliwa wakati wa baridi. Wakati Yesu alipozaliwa, wachungaji bado walikuwa wakiishi malishoni wakilinda makundi yao nyakati za usiku. (Luka 2:8) Wasingeweza kufanya hivyo mwezi wa Desemba, unaokuwa na barafu nyingi mara kwa mara katika eneo la Bethlehemu. Majira ya mvua yaanzapo mwishoni mwa Oktoba, wachungaji hawaishi tena malishoni.
Basi, Desemba 25 ilipataje kuwa siku ya kusherehekea “kuzaliwa kwa Kristo”? Namna gani desturi mbalimbali zinazohusiana na Krismasi? Je! asili yazo ni ya Kikristo? Angalia yanayosemwa na vitabu mbalimbali.
Kwa Sababu Gani Ikawa Desemba 25?
“Washiriki wa kanisa hapo kwanza walichukuliwa kati ya wapagani, kwa hiyo ikaonekana kwamba sikukuu fulani ikianzwa wakati huo, waongofu hao wangekaza fikira zao juu ya sikukuu ya Kikristo.” Funk & Wagnalls Standard Dictionary of Folklore, Mythology, and Legend, Vol. 1, uku. 229.
Je! Kweli Ni Sikukuu ya Kikristo?
“Sherehe hiyo haikuadhimishwa katika karne za mwanzo-mwanzo wa kanisa la Kikristo . . . Katika karne ya 5 kanisa la Magharibi liliagiza sikukuu hiyo isherehekewe siku ambayo Waajemi walikuwa na desturi za kuabudu kuzaliwa kwa jua na mwishoni mwa sikukuu ya mungu Saturn, kwa maana siku ya kuzaliwa kwa Kristo haikujulikana. Kati ya makabila ya Kijeremani na ya mchanganyiko wa Wahindi na Wazungu, majira ya baridi wakati jua linapokuwa mbali na ikweta yalifikiriwa kuwa wakati bora wa mwaka, nao waliadhimisha kurudi kwa jua kwa kusherehekea sikukuu yao kubwa zaidi ya yule, ambayo iligeuzwa kama sherehe nyingine za kipagani ikawa Krismasi.”—The Encyclopedia Americana, chapa ya 1959, Vol. 6, uku. 622.
“Desturi nyingi ambazo sasa zahusiana na Krismasi hazikuwa desturi za Krismasi bali zilikuwako kabla ya Ukristo na hivyo hazikuwa za Kikristo, zikachukuliwa na kanisa la Kikristo. Saturnalia, sikukuu ya Kirumi iliyosherehekewa katikati ya Desemba, ndiyo iliyoigwa ili kuingiza desturi nyingi za shangwe katika sikukuu ya Krismasi. Kwa mfano, karamu yenye mapambo mengi, utoaji wa zawadi, na kuwasha mishumaa ni mambo yaliyotolewa katika sherehe hiyo.”—The Encyclopedia Americana, chapa ya 1959, Vol. 6, uku. 622.
“Desturi ya kupamba nyumba na makanisa kwa kutumia miti yenye majani mabichi nyakati zote ilianza nyakati za kale. Warumi walibadilishana matawi ya kijani kibichi wawe na bahati nzuri wakati wa calends (siku ya kwanza) ya Januari.” (The World Book Encyclopedia, 1973, Vol. 3, uku. 415) Kwa habari ya wimbo wa Krismasi unaoitwa “Holly and the Ivy,” Funk & Wagnalls Standard Dictionary of Folklore, Mythology, and Legend chasema: “Ni mmoja wa nyimbo kadha zinazotaja mimea holly na ivy ikiwa na maana ile ile ya nyakati zilizotangulia Ukristo, ya kufananisha hali za waume na wake.”
Je! Krismasi ni Nzuri kwa Wakristo?
“Katika Kanisa, malawama yalitolewa juu ya mwadhimisho huo kwa sababu unafanana na desturi za ibada za kipagani, kwa sababu ni ibada ya jua (Waarmenia waliwaita wanakanisa wa Kanisa Katoliki waabudu sanamu pia, kwa sababu Krismasi yasherehekewa siku ambayo jua lilizaliwa), na baadaye mwaka 1644, wakati wa kutokea Waprotestanti wasiotaka sherehe fulani za kanisa, Bunge la Uingereza lilikataza sikukuu hiyo isisherehekewe.”—Funk & Wagnalls Standard Dictionary of Folklore, Mythology, and Legend, Vol. 1, uku. 229.
Biblia yauliza ulizo: “Pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza?” (2 Kor. 6:14) Mambo hayo hayana uhusiano wo wote. Lakini je sherehe ya Krismasi haijaribu kushirikisha upagani wa kale na Kristo?