Kampeni ya Kuwaalika Watu Kwenye Ukumbusho Itaanza Machi 17
1. Ni kampeni gani itakayoanza Machi 17?
1 Maadhimisho ya Ukumbusho ya kila mwaka hutangaza kifo cha Yesu. (1 Kor. 11:26) Kwa hiyo, tunataka watu wengine wahudhurie pamoja nasi na kusikia kuhusu zawadi ya fidia ambayo Yehova alitoa kwa upendo. (Yoh. 3:16) Mwaka huu kampeni yetu ya kuwaalika watu kwenye Ukumbusho itaanza Jumamosi, Machi 17. Je, una hamu ya kufanya yote uwezayo katika kampeni hiyo?
2. Tunaweza kusema nini tunapompa mtu mwaliko?
2 Tunaweza Kusema Nini?: Ni bora kusema kifupi. Huenda tukasema hivi: “Habari. Tumekuja ili kuwapa watu wa familia yenu mwaliko huu wa kuhudhuria tukio muhimu litakaloadhimishwa ulimwenguni pote Aprili 5. Hotuba inayoeleza maana ya kifo cha Yesu na mambo anayofanya leo itatolewa. Hotuba hiyo itatolewa bila malipo. Mwaliko huu unaonyesha mahali na wakati wa maadhimisho hayo katika eneo letu.” Tutakaposambaza mialiko siku za Jumamosi na Jumapili, tunapaswa pia kutoa magazeti inapofaa.
3. Tunaweza kuwaalika watu wengi iwezekanavyo jinsi gani?
3 Waalike Watu Wengi Iwezekanavyo: Lengo letu ni kuwaalika watu wengi iwezekanavyo. Kwa hiyo, hakikisha kwamba umewaalika wanafunzi wako wa Biblia, watu unaowarudia kwa ukawaida, watu wa ukoo, wafanyakazi wenzako, wanafunzi wenzako, majirani, na watu wengine unaofahamiana nao. Wazee wa kutaniko lenu watafanya mpango wa kusambaza mialiko katika eneo lote. Kampeni yetu ya kila mwaka ya kuwaalika watu kwenye Ukumbusho huwa na matokeo mazuri. Mwaka uliopita, mwanamke mmoja aliingia mahali ambapo kutaniko fulani lilifanyia Ukumbusho, na mkaribishaji alimwuliza kama angehitaji msaada wa kumpata mhubiri aliyemwalika. Lakini mwanamke huyo alisema hamjui yeyote humo, na kwamba alipewa mwaliko na mtu aliyehubiri nyumba kwa nyumba mapema siku hiyo.
4. Tuna sababu gani za kushiriki kwa bidii katika kampeni hii?
4 Huenda ikawa mtu atahudhuria Ukumbusho kwa sababu ulimpa mwaliko. Lakini, iwe mtu yeyote uliyemwalika atahudhuria au la, bidii yako itatoa ushahidi. Mialiko ambayo utasambaza itatangaza kwamba Yesu ni Mfalme mwenye nguvu. Watu wote watakaoiona bidii yako ya kusambaza mialiko, yaani, watu katika eneo, wahubiri wenzako, na hasa Yehova, watajua kwamba wewe unathamini sana zawadi ya fidia.—Kol. 3:15.