“Endeleeni Kufanya Hivi”
Ukumbusho Utaadhimishwa Aprili 5
1. Kwa nini maadhimisho ya Ukumbusho ni muhimu?
1 “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19) Kwa kusema hivyo, Yesu aliwaagiza wafuasi wake wakumbuke kifo chake cha kidhabihu. Kwa kuwa fidia au dhabihu ya Yesu ilitimiza mambo mengi muhimu, siku ya Ukumbusho ya kila mwaka ni siku ya maana kuliko siku nyingine yoyote kwa Wakristo. Mwaka huu Ukumbusho utaadhimishwa Aprili 5. Siku hiyo inapokaribia tunawezaje kuonyesha shukrani kwa Yehova?—Kol. 3:15.
2. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunathamini Ukumbusho kwa kujifunza na kutafakari?
2 Jitayarishe: Kwa kawaida tunajitayarisha kwa mambo tunayoyaona kuwa muhimu. Watu wa familia wanaweza kutayarisha mioyo yao kabla ya Ukumbusho kwa kujifunza na kutafakari matukio ya siku za mwisho ya maisha ya Yesu duniani. (Ezra 7:10) Orodha ya maandiko kadhaa inapatikana katika kalenda na kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku, na orodha ya maandiko mengi zaidi na sura zinazozungumzia maandiko hayo katika kitabu Mtu Mkuu, inapatikana katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Februari 1, 2011, ukurasa wa 23-24.
3. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunathamini Ukumbusho kwa kuongeza utendaji wetu katika huduma?
3 Wahubirie Watu: Njia nyingine tunayoweza kuonyesha uthamini wetu, ni kwa kushiriki kikamili katika huduma. (Luka 6:45) Kampeni ya ulimwenguni pote ya kuwaalika watu kwenye Ukumbusho itaanza Jumamosi, Machi 17. Je, unaweza kupanga ratiba yako ili utumie wakati mwingi zaidi katika huduma, au hata kuwa painia msaidizi? Zungumzieni jambo hili katika kipindi chenu cha Ibada ya Familia kinachofuata.
4. Tutanufaika jinsi gani kwa kuhudhuria Ukumbusho?
4 Tunanufaika sana kwa kuhudhuria kila mwaka maadhimisho ya Ukumbusho! Shangwe yetu na upendo wetu kwa Mungu unaongezeka tunapotafakari kuhusu ukarimu wa Yehova wa kumtoa kama fidia mwana wake mzaliwa-pekee. (Yoh. 3:16; 1 Yoh. 4:9, 10) Jambo hilo linatutia moyo tusiishi kwa ajili yetu wenyewe. (2 Kor. 5:14, 15) Pia, linachochea tamaa yetu ya kumtukuza Yehova hadharani. (Zab. 102:19-21) Bila shaka, watumishi wa Yehova wenye shukrani wanatazamia kwa hamu fursa ya “kukitangaza kifo cha Bwana” wakati wa maadhimisho ya Ukumbusho, Aprili 5.—1 Kor. 11:26.