Faidika Kabisa na Funzo la Kibinafsi
1. Kujifunza na kutafakari kunaweza kutunufaishaje?
1 Tunafaidika sana ‘tunapokaza uangalifu kuliko ilivyo kawaida’ wakati tunajifunza kibinafsi na kutafakari. (Ebr. 2:1) Kusoma na kutafakari mambo yaliyo katika Biblia na machapisho ya Kikristo kutatusaidia sana kukazia kweli za Neno la Mungu moyoni mwetu. Kufanya hivyo kutabadili kabisa njia yetu ya kufikiri na kutenda. Kwa kweli, kutatusaidia tupendezwe na kufanya mapenzi ya Yehova. (Zab. 1:2; 40:8) Kwa hiyo, ili tufaidike tunapojifunza, tunahitaji kukuza uwezo wetu wa kuwa makini. Ni rahisi sana kukengeushwa! Mambo madogo-madogo kama vile simu au kelele yanaweza kutukengeusha. Au huenda hatuwezi kukazia uangalifu jambo fulani kwa muda mrefu. Huenda tukaketi tukiwa na kusudi la kujilisha kiroho, lakini punde si punde akili zetu zinaanza kutangatanga. Tunaweza jinsi gani ‘kukaza uangalifu kuliko ilivyo kawaida’ tunapokuwa na funzo la kibinafsi la Neno la Mungu?
2. (a) Kwa nini ni muhimu kupanga ratiba kwa ajili ya funzo la kibinafsi? (b) Umepangaje ratiba yako ili upate wakati wa kujifunza Neno la Mungu?
2 Ni muhimu kuwa na ratiba na kuchagua mazingira bora zaidi ya kujifunza. Wengi wetu hatuna wakati wala pindi ya faragha. Tunaweza kuona kana kwamba matukio ya kila siku yanatulemea na kutupeleka mbio kama kijiti kinachopelekwa na mto unaoenda kasi. Basi, tunahitaji kupambana na hali hiyo na kutafuta nyakati zenye utulivu ili tujifunze. Tusingojee tu fursa ya kujifunza ijitokeze yenyewe. Badala yake, tunahitaji kutenga wakati wa kujifunza. (Efe. 5:15, 16) Wengine hutenga muda mfupi asubuhi wakati ambapo hakuna mambo mengi ya kuwakengeusha. Wengine hupendelea usiku. Jambo kuu ni kwamba tusipuuze kamwe umuhimu wa kupata ujuzi sahihi juu ya Mungu na Mwana wake. (Yoh. 17:3) Hivyo basi, acheni tupange ratiba kwa ajili ya funzo la kibinafsi na kushikamana na ratiba hiyo.
3. Kutafakari ni nini, na kunaweza kutunufaishaje?
3 Ni muhimu sana kutafakari, yaani, kufikiria kwa uzito mambo ambayo tumejifunza. Kufanya hivyo hutusaidia kuingiza moyoni mwetu mawazo ya Mungu ambayo tumesoma. Kutafakari hutusaidia kuona jinsi tunavyoweza kutumia mashauri ya Biblia ili tuwe “watendaji wa neno, na si wasikiaji tu.” (Yak. 1:22-25) Vilevile, kutafakari hutusaidia kumkaribia zaidi Yehova, kwa sababu kunatuwezesha kufikiria sifa zake na jinsi habari tunayosoma inavyokazia sifa hizo.
4. Ni hali gani zinazohitajika ili mtu aweze kutafakari ifaavyo?
4 Ili tufaidike kabisa na funzo na kutafakari, ni lazima tuondoe akilini mambo yanayoweza kutukengeusha. Ili tujifunze mambo mapya tunapotafakari, tunahitaji kuepuka kabisa vikengeusha fikira vya maisha ya siku hizi. Kufanya hivyo kunahitaji wakati na mahali patulivu, na inaburudisha sana kujilisha chakula cha kiroho na kunywa maji ya kweli yanayopatikana katika Neno la Mungu.
5. (a) Wengine wameongezaje muda wanaoweza kukaza uangalifu wanapokuwa na funzo la kibinafsi? (b) Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu funzo, na tunaweza kupata faida gani kutokana na kujifunza?
5 Namna gani ikiwa hatuwezi kukazia uangalifu jambo fulani kwa muda mrefu na akili zetu huanza kutangatanga baada ya kujifunza kwa muda mfupi tu? Wengine wameona kwamba wanaweza kuboresha uwezo wao wa kukaza uangalifu wakati wa funzo kwa kuanza na vipindi vifupi-vifupi kisha kurefusha vipindi hivyo hatua kwa hatua. Tunapaswa kutumia muda wa kutosha tunapojifunza badala ya kupitia habari mbiombio. Tunapaswa kupendezwa sana na habari tunayojifunza. Na tunaweza kufanya utafiti zaidi kwa kutumia vifaa vingi ambavyo vimeandaliwa na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Kuna faida kubwa sana ya kuchunguza “mambo mazito ya Mungu.” (1 Kor. 2:10) Kufanya hivyo kunatuwezesha kupata ujuzi zaidi juu ya Mungu na kukuza nguvu zetu za ufahamu. (Ebr. 5:14) Ikiwa tunajifunza Neno la Mungu kwa bidii, tutakuwa pia na “sifa za kustahili vya kutosha kufundisha wengine.”—2 Tim. 2:2.
[Ukurasa mtupu]