Tengenezo
Maana: Ushirika au jamii ya watu ambao jitihada zao zinaunganishwa ili kutimiza kazi au kusudi fulani. Washiriki wa tengenezo wanaunganishwa kwa mipango ya usimamizi na kwa viwango au matakwa. Watu ambao ni Mashahidi wa Yehova waliojiweka wakfu na kubatizwa huingia katika tengenezo la Yehova kwa sababu ya uchaguzi wa kibinafsi, si kwa kuzaliwa wala kwa kulazimishwa. Wamevutwa kuja kwenye tengenezo lake la duniani kwa sababu ya mafundisho na matendo yake na kwa sababu wanataka kushiriki kazi ambayo linafanya.
Je, kweli Yehova ana tengenezo hapa duniani?
Ili kujibu swali hilo, fikiria mambo haya:
Je, viumbe wa mbinguni wa Mungu, malaika, wamepangwa kitengenezo?
Dan. 7:9, 10: “Nikaendelea kutazama mpaka viti vya ufalme vikawekwa na Mzee wa Siku akaketi. Mavazi yake yalikuwa meupe kama theluji, na nywele za kichwa chake zilikuwa kama sufu safi. Kiti chake cha ufalme kilikuwa ni miali ya moto; magurudumu yake yalikuwa ni moto unaowaka. Kulikuwa na mto wa moto unaotiririka kutoka mbele zake. Kulikuwa na maelfu elfu walioendelea kumtumikia, na elfu kumi mara elfu kumi walioendelea kusimama mbele zake. Ile Mahakama ikaketi, na vitabu vikafunguliwa.”
Zab. 103:20, 21: “Mbarikini Yehova, enyi malaika zake, mlio na uwezo katika nguvu, mnaolitenda neno lake, kwa kuisikiliza sauti ya neno lake. Mbarikini Yehova, enyi majeshi yake yote, enyi wahudumu wake, mnaofanya mapenzi yake.” (“Jeshi” ni kikundi kilichopangwa kitengenezo.)
Mungu aliwapelekeaje maagizo watumishi wake duniani hapo zamani?
Waabudu wa Yehova walipokuwa wachache, aliwapa maagizo vichwa vya familia kama vile Noa na Abrahamu, kisha nao wakawa wasemaji wa Yehova kwa familia zao. (Mwa. 7:1, 7; 12:1-5) Wakati Yehova alipowakomboa Waisraeli kutoka Misri, aliwapa maagizo kupitia Musa. (Kut. 3:10) Kwenye Mlima Sinai, Mungu aliwapanga watu hao kitengenezo wakawa taifa, akawapa sheria na masharti ya kuelekeza ibada yao na mahusiano kati yao wenyewe. (Kut. 24:12) Aliweka ukuhani ili uongoze katika mambo ya ibada na kuwafundisha watu matakwa ya Yehova; nyakati nyingine yeye pia aliwatuma manabii ili wawape watu himizo na onyo linalohitajiwa. (Kum. 33:8, 10; Yer. 7:24, 25) Kwa hiyo, ingawa Yehova alisikiliza sala za mwabudu mmoja-mmoja, aliwafundisha kupitia mpango wa kitengenezo.
Wakati wa Yehova kuanza kuwaunganisha waabudu wa kweli pamoja naye mwenyewe kupitia Yesu Kristo ulipokaribia, Mungu alimtuma duniani ili awe msemaji Wake. (Ebr. 1:1, 2) Kisha roho takatifu ilipomiminwa siku ya Pentekoste 33 W.K., kutaniko la Kikristo lilianzishwa. Baada ya Yesu kurudi mbinguni, kutaniko hilo likawa mpango wa Yehova kwa ajili ya kufundisha na kwa ajili ya kuunganisha jitihada za Wakristo. Kulikuwako waangalizi wa kuongoza katika makutaniko, na baraza moja linaloongoza lilifanya maamuzi yaliyohitajiwa na kusaidia kupanga utendaji. Kwa wazi, Yehova alikuwa ameanzisha tengenezo duniani ambalo washiriki wake walikuwa Wakristo wa kweli.—Mdo. 14:23; 16:4, 5; Gal. 2:7-10.
Je, uumbaji wa Yehova unaoonekana unaonyesha kwamba yeye ni Mungu wa kupanga mambo kitengenezo?
Isa. 40:26: “Inueni macho yenu juu, mwone. Ni nani ameviumba vitu hivi? Ni Yeye anayelileta jeshi lake kulingana na hesabu, ambaye zote anaziita kwa jina. Kutokana na wingi wa nguvu zenye msukumo, yeye pia akiwa hodari katika nguvu, hakuna hata moja kati ya hizo inayokosekana.” (Nyota zimewekwa katika makundi ya galaksi nazo zinasonga pamoja, hata ingawa maumbile ya nyota moja hayafanani na nyingine. Sayari zinasonga kulingana na wakati barabara, katika mizunguko yake. Elektroni zilizo katika kila atomu ya kila elementi pia zina mizunguko. Na muundo wa mata zote hufuata vielelezo vya hesabu ambavyo vinapatana kabisa hivi kwamba wanasayansi waliweza kutabiri kuwako kwa elementi fulani kabla hawajazivumbua. Yote hayo yanathibitisha kwamba kuna mpango wa ajabu mno wa kitengenezo.)
Je, Biblia inaonyesha kwamba Wakristo wa kweli watakuwa watu waliopangwa kitengenezo?
Mt. 24:14; 28:19, 20: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza . . . na kuwafundisha.” (Kazi hiyo ingetimizwaje pasipo tengenezo? Yesu alipowazoeza wanafunzi wake wa kwanza kwa ajili ya kazi hiyo, Yeye hakumwambia tu kila mmoja wao aende popote alipopenda na kutangaza imani yake kwa njia yoyote ile aliyochagua. Aliwazoeza, akawapa maagizo na kuwatuma waende kwa njia iliyopangwa kitengenezo. Ona Luka 8:1; 9:1-6; 10:1-16.)
Ebr. 10:24, 25: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile kuwa inakaribia.” (Je, mtu angewaelekeza wapi wale wanaopendezwa ili wapate kutii amri hiyo kama hakungekuwa na tengenezo ambalo lina mikutano ya kawaida, mahali ambapo wangeweza kukusanyika?)
1 Kor. 14:33, 40: “Mungu si Mungu wa machafuko, bali ni wa amani. . . . Mambo yote na yatendeke kwa adabu na kwa mpango.” (Mtume Paulo hapa anazungumzia utaratibu katika mikutano ya kutaniko. Kutumia shauri hili lililoongozwa na roho ya Mungu kunataka mpango wa tengenezo uheshimiwe.)
1 Pet. 2:9, 17: “Lakini ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa kuwa mali ya pekee, ili mtangaze kotekote sifa bora’ zake yeye aliyewaita ninyi kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu. . . . Upendeni ushirika mzima wa akina ndugu.” (Ushirika wa watu ambao jitihada zao zinaelekezwa ili kutimiza kazi fulani ni tengenezo.)
Je, wale walio watumishi waaminifu wa Mungu ni watu tu waliotawanyika katika makanisa mbalimbali ya Jumuiya ya Wakristo?
2 Kor. 6:15-18: “Mtu mwaminifu ana fungu gani na asiye mwamini? . . . ‘Kwa hiyo tokeni katikati yao, na mjitenge,’ asema Yehova, ‘na mwache kugusa kitu kilicho najisi’; ‘nami nitawakaribisha ndani.’ ‘Nami nitakuwa baba kwenu, nanyi mtakuwa wana na mabinti kwangu,’ asema Yehova Mweza-Yote.” (Je, kweli mtu ni mtumishi mwaminifu wa Mungu ikiwa anaendelea kushiriki katika ibada pamoja na wale wanaoonyesha kwa njia yao ya maisha kwamba kwa kweli si waamini? Ona kichwa “Babiloni Mkubwa.”)
1 Kor. 1:10: “Sasa nawahimiza ninyi, akina ndugu, kupitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kwamba nyote mseme kwa upatano, na kwamba kusiwe na migawanyiko katikati yenu, bali kwamba muunganishwe vema katika akili ileile na katika njia ileile ya kufikiri.” (Umoja huo haumo katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo ambayo yamegawanyika.)
Yoh. 10:16: “Nina kondoo wengine, ambao si wa zizi hili; hao pia nitawaleta, nao wataisikiliza sauti yangu, nao watakuwa kundi moja, mchungaji mmoja.” (Kwa kuwa Yesu angewaleta hao katika “kundi moja,” je, si wazi kwamba hawawezi kuwa watu waliotawanyika katika dini za Jumuiya ya Wakristo?)
Tengenezo la Yehova linaloonekana linaweza kutambuliwaje leo?
(1) Linamtukuza kikweli Yehova kuwa ndiye Mungu wa pekee wa kweli, nalo hulitukuza jina lake.—Mt. 4:10; Yoh. 17:3.
(2) Linatambua kikamili daraka muhimu la Yesu Kristo katika kusudi la Yehova—akiwa mteteaji wa enzi kuu ya Yehova, Wakili Mkuu wa uzima, kichwa cha kutaniko la Kikristo, Masihi Mfalme anayetawala.—Ufu. 19:11-13; 12:10; Mdo. 5:31; Efe. 1:22, 23.
(3) Linashikamana sana na Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho yake, na msingi wa mafundisho na viwango vyake vyote vya mwenendo ni Biblia.—2 Tim. 3:16, 17.
(4) Limejitenga na ulimwengu.—Yak. 1:27; 4:4.
(5) Linadumisha kiwango cha juu cha usafi wa kiadili kati ya washiriki wake, kwa sababu Yehova mwenyewe ni mtakatifu.—1 Pet. 1:15, 16; 1 Kor. 5:9-13.
(6) Linatumia jitihada zake kuu ili kufanya kazi ambayo Biblia ilitabiri kwamba itafanywa wakati wetu, yaani, kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu katika ulimwengu wote ili kuwa ushahidi.—Mt. 24:14.
(7) Ijapokuwa kutokamilika kwa wanadamu, washiriki wake husitawisha na kuzaa matunda ya roho ya Mungu—upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia—nao hufanya hivyo kwa kadiri inayowatenga na ulimwengu kwa ujumla.—Gal. 5:22, 23; Yoh. 13:35.
Tunaweza kuonyeshaje heshima kwa tengenezo la Yehova?
1 Kor. 10:31: “Fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”
Ebr. 13:17: “Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee, kwa maana wanaendelea kuzilinda nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu.”
Yak. 1:22: “Iweni watendaji wa neno, na si wasikiaji tu.”
Tito 2:11, 12: “Fadhili zisizostahiliwa za Mungu zinazowaletea watu wa namna zote wokovu zimeonyeshwa, zikitufundisha kukataa kabisa kutomwogopa Mungu na tamaa za kilimwengu na tuishi kwa utimamu wa akili na uadilifu na ujitoaji-kimungu.”
1 Pet. 2:17: “Upendeni ushirika mzima wa akina ndugu.”