Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yi kur. 2-6
  • Vijana—Mtatumiaje Maisha Yenu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Vijana—Mtatumiaje Maisha Yenu?
  • Vijana—Mtatumiaje Maisha Yenu?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kustahili Kuwa Shahidi wa Yehova
  • Njia za Kumtumikia Mungu Wakati Wote
  • Mtumikie Yehova kwa Nafsi Yote
  • Je, Waweza Kujitolea?
    Huduma Yetu ya Ufalme—2001
  • Njia za Kupanua Huduma Yako
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Je, Hii Yaweza Kuwa Kazi-Maisha Inayokufaa Zaidi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Wakumbuke Watumishi wa Wakati Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
Pata Habari Zaidi
Vijana—Mtatumiaje Maisha Yenu?
yi kur. 2-6

Vijana​—Mtatumiaje Maisha Yenu?

“NINATAKA nifanikiwe maishani.” Ndivyo alivyosema msichana mmoja. Inaelekea wewe pia unataka kufanikiwa. Lakini unawezaje kufanikiwa maishani? Huenda vyombo vya habari, marika wako, hata labda walimu wako, wakasema kwamba mtu mwenye mafanikio ni yule ambaye amechuma pesa nyingi na ana kazi nzuri.

Hata hivyo, Biblia huwaonya vijana kwamba kutafuta mali ni “kujilisha upepo” tu. (Mhubiri 4:4) Sababu moja ni kwamba, ni vijana wachache tu wanaofanikiwa kuwa matajiri na mashuhuri. Mara nyingi, wale wanaofanikiwa huvunjika moyo sana. Kijana mmoja Mwingereza aliyepata kazi nzuri alisema kwamba kufanikiwa kupata mali ni kazi bure. ‘Unapofikiria matokeo yake unakatishwa tamaa.’ Naam, nyakati nyingine huenda kazi ikamwezesha mtu kupata mali na umashuhuri. Lakini haiwezi kutosheleza ‘uhitaji wako wa kiroho.’ (Mathayo 5:3) Isitoshe, 1 Yohana 2:17 huonya kwamba “ulimwengu unapitilia mbali.” Hata ukifanikiwa katika ulimwengu huu, mafanikio hayo hayatadumu.

Hivyo, Mhubiri 12:1 huwasihi vijana hivi: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako.” Naam, kumtumikia Yehova Mungu ndiyo njia bora ya kutumia maisha yako. Lakini kwanza, ni lazima ustahili kumtumikia Mungu. Unawezaje kustahili? Na kumtumikia Mungu huhusisha nini?

Kustahili Kuwa Shahidi wa Yehova

Kwanza kabisa, unapaswa kukuza tamaa ya kumtumikia Mungu​—na tamaa hiyo haitokei tu bila jitihada yoyote, hata kama wazazi wako ni Wakristo. Ni lazima wewe mwenyewe uwe na uhusiano pamoja na Yehova. Msichana mmoja asema hivi: “Kusali humsaidia mtu kuwa na uhusiano pamoja na Yehova.”​—Zaburi 62:8; Yakobo 4:8.

Andiko la Waroma 12:2 linaonyesha hatua nyingine unayopaswa kuchukua. Linasema hivi: ‘Jithibitishieni wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.’ Je, umewahi kutilia shaka mambo fulani ambayo umefundishwa? Basi tii shauri la Biblia, na ‘ujithibitishie mwenyewe’ kwamba mambo hayo ni ya kweli! Fanya utafiti. Soma Biblia na vichapo vyenye habari za Biblia. Hata hivyo, kujifunza juu ya Mungu si jambo la kutumia akili tu. Tumia wakati kutafakari yale unayosoma ili yaingie kabisa moyoni. Ukifanya hivyo, upendo wako kwa Mungu utazidi.​—Zaburi 1:2, 3.

Kisha, jaribu kuwaeleza wengine yale unayojifunza, labda wanafunzi wenzako shuleni. Hatua inayofuata ni kuhubiri nyumba hadi nyumba. Mara kwa mara unapohubiri, unaweza kukutana na mwanafunzi mwenzako, na huenda jambo hilo likakubabaisha. Lakini Biblia inatusihi ‘tusiaibikie habari njema.’ (Waroma 1:16) Unapeleka ujumbe unaowapa watu uhai na tumaini! Basi, ya nini uaibike?

Iwapo wazazi wako ni Wakristo, huenda tayari umehubiri nao. Lakini je, unaweza kufanya mengi zaidi badala ya kunyamaza kimya mlangoni au kugawa tu magazeti na trakti? Je, wewe mwenyewe unaweza kumhubiria mwenye nyumba, ukimfundisha kupitia Biblia? Iwapo huwezi, basi waombe wazazi wako au mtu mwingine mkomavu katika kutaniko akusaidie. Weka mradi wa kustahili kuwa mhubiri asiyebatizwa wa habari njema!

Muda si muda, utachochewa kujiweka wakfu, yaani kuweka nadhiri ya kumtumikia Mungu toka wakati huo na kuendelea. (Waroma 12:1) Hata hivyo, kujiweka wakfu si siri. Mungu anataka kila mtu afanye “tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu.” (Waroma 10:10) Wakati wa ubatizo, kwanza mtu hutangaza imani yake kwa maneno. Kisha, anabatizwa katika maji. (Mathayo 28:19, 20) Ni kweli kwamba ubatizo ni hatua nzito. Lakini usisite kubatizwa ukifikiri kuwa hutafaulu. Ukimtegemea Mungu akupe nguvu, atakupa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili usimame imara.​—2 Wakorintho 4:7; 1 Petro 5:10.

Unapobatizwa, unakuwa Shahidi wa Yehova. (Isaya 43:10) Jambo hilo lapasa kuathiri sana jinsi utakavyotumia maisha yako. Kujiweka wakfu hutia ndani ‘kujikana mwenyewe.’ (Mathayo 16:24) Huenda ukatupilia mbali miradi yako na mambo mengine uliyotamani kutimiza na ‘kutafuta kwanza ufalme wa Mungu.’ (Mathayo 6:33) Kujiweka wakfu na kubatizwa huandaa njia nyingi za kufanya hivyo. Ebu tuchunguze baadhi ya njia hizo.

Njia za Kumtumikia Mungu Wakati Wote

● Upainia ni njia moja. Mhubiri aliye painia ni Mkristo aliyebatizwa mwenye mfano mzuri. Yeye hupanga kutumia angalau saa 70 kila mwezi ili kuhubiri habari njema. Ukitumia muda mwingi zaidi shambani, utaweza kuboresha ustadi wako wa kuhubiri na kufundisha. Mapainia wengi wamepata shangwe kwa kuwasaidia wanafunzi wao wa Biblia wawe Mashahidi waliobatizwa. Hakuna kazi nyingine yoyote inayoweza kufurahisha na kuridhisha zaidi ya hiyo.

Mapainia wengi hufanya kazi ya muda ili wajiruzuku. Wengi wao hupangia kimbele jambo hilo kwa kujifunza ufundi fulani shuleni au kufundishwa na wazazi wao. Huenda wewe na wazazi wako mkaona kwamba itafaa upate masomo fulani ya ziada baada ya kumaliza shule ya sekondari. Ikiwa ndivyo, hakikisha kwamba mradi wako si kupata pesa nyingi, bali ni kutegemeza huduma yako na labda kuwa mhudumu wa wakati wote.

Hata hivyo, badala ya kutanguliza kazi yake ya kujiruzuku, painia hutanguliza huduma yake ya kuwasaidia wengine wapate uhai. Mbona usiweke mradi wa kuwa painia? Mara nyingi, upainia hutokeza mapendeleo mengine. Kwa mfano, baadhi ya mapainia huhamia maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Wengine hujifunza lugha ya kigeni na hutumikia katika kutaniko la lugha ya kigeni nchini kwao au hata katika nchi nyingine. Naam, kufanya upainia huleta uradhi maishani!

● Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme ni njia nyingine. Shule hii ya miezi miwili imekusudiwa kuwazoeza mapainia wenye uzoefu ambao wako tayari kuhamia kwenye maeneo mengine yenye uhitaji mkubwa zaidi. Wanamwiga Yesu Kristo, Mweneza-Injili mkuu ambaye alitumikia kikamili akiwa duniani, kwa kuwa na roho ya Mimi hapa! Nitume mimi! (Isaya 6:8; Yohana 7:29) Kuhamia eneo lingine huenda kukahusisha kuishi maisha rahisi. Huenda utamaduni, hali ya hewa na vyakula vikawa tofauti kabisa na vile ambavyo mtu amezoea. Huenda akahitaji kujifunza lugha mpya. Shule hii huwasaidia ndugu na dada waseja na wenzi wa ndoa walio na umri wa miaka 23 hadi 65, wasitawishe sifa za kiroho watakazohitaji ili kutimiza mgawo wao na ustadi ili waweze kutumiwa kwa ukamili na Yehova na tengenezo lake.

● Utumishi wa Betheli huhusisha kujitolea kutumikia katika mojawapo ya ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova. Washiriki wengine wa familia ya Betheli huhusika moja kwa moja katika utayarishaji wa vichapo vya Biblia. Wengine hupewa migawo inayotegemeza kazi hiyo, kama vile udumishaji wa majengo na vifaa au kutunza familia ya Betheli. Migawo yote ni mapendeleo matakatifu ya kumtumikia Yehova. Zaidi ya hayo, wale wanaotumikia katika Betheli wanajua kwamba lolote wanalofanya, huwafaidi ndugu zao wengi ulimwenguni pote.

Nyakati nyingine ndugu walio na ustadi maalum huitwa ili watumikie Betheli. Hata hivyo, wengi huzoezwa wanapowasili. Wanabetheli hawatumikii ili wapate mali bali wanatosheka na chakula, makao, na rudishio dogo la gharama kwa ajili ya mahitaji yao. Kijana mmoja anayetumikia katika Betheli anasema hivi kuhusu utumishi wake: “Unafurahisha sana! Ratiba ya kila siku si rahisi, lakini nimepata baraka nyingi kwa kutumikia hapa.”

● Utumishi wa Ujenzi humwezesha mtu kushiriki katika ujenzi wa ofisi za tawi na Majumba ya Ufalme. Watumishi wa ujenzi husaidia kufanya kazi hizo za ujenzi. Huo ni utumishi mtakatifu, sawa na kazi ya wale watu waliojenga hekalu la Solomoni. (1 Wafalme 8:13-18) Watumishi wa ujenzi hutunzwa kama Wanabetheli. Ndugu na dada hao wana pendeleo lililoje la kumsifu Yehova kwa njia hiyo!

Mtumikie Yehova kwa Nafsi Yote

Kumtumikia Yehova ndiyo njia bora ya kutumia maisha yako. Mbona usifikirie kuweka mradi wa kumtumikia Mungu wakati wote? Zungumza na wazazi wako, wazee wa kwenu, na mwangalizi wenu wa mzunguko kuhusu utumishi wa wakati wote. Ikiwa unataka kutumikia Betheli au kuhudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme, basi hudhuria mikutano inayozihusu inayofanywa kwenye kusanyiko la eneo.

Naam, si wote wanaoweza kustahili au kutumikia wakati wote. Nyakati nyingine matatizo ya afya, hali za kiuchumi, na majukumu ya familia huwazuia watu wasifanye mengi sana. Hata hivyo, Wakristo wote waliojiweka wakfu wanapaswa kutii amri hii ya Biblia: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:37) Yehova anataka ufanye yote uwezayo kulingana na hali zako. Hivyo basi, hata hali yako iweje, jambo kuu maishani mwako na liwe kumtumikia Yehova. Weka miradi ya kiroho unayoweza kufikia. Naam, “mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako”​—nawe utabarikiwa daima!

Isipokuwa imeonyeshwa vingine, manukuu ya Maandiko ya Kiebrania ni kutoka katika Union Version ya ­Kiswahili chapa ya 1994, na manukuu ya Maandiko ya Kigiriki ni kutoka katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki