Igeni Imani Yao
1. Tutajifunza kitabu gani wakati wa Funzo la Biblia la Kutaniko katika juma linaloanza Oktoba 19?
1 Katika juma la Oktoba 19, 2015, tutaanza kujifunza kitabu Igeni Imani Yao katika Funzo la Biblia la Kutaniko. Kitabu hicho kina masimulizi ya wanaume na wanawake 14 waliokuwa na imani. Kimeandikwa kwa njia inayotuwezesha kupiga picha akilini kuhusu watu hao waaminifu, na kinatusaidia kuwaona kuwa watu halisi ambao walikabili matatizo walipokuwa wakimtumikia Yehova. Pia masimulizi hayo yanatufundisha masomo tunayoweza kuyatumia katika maisha yetu.—Ebr. 6:12.
2. Eleza baadhi ya mambo yaliyomo katika kitabu Igeni Imani Yao.
2 Yaliyomo: Kitabu hicho kina mfuatano wa matukio na ramani inayotusaidia kujua wakati na mahali ambapo kila mhusika aliishi. Kwa kuongezea, kila sura ina sehemu yenye kichwa “Mambo ya Kufikiria . . . ,” ambayo itatusaidia kutafakari kuhusu masimulizi hayo na jinsi ya kutumia masomo muhimu tuliyojifunza. Pia, kitabu hicho kina picha zenye rangi zinazovutia, na zilizofanyiwa utafiti, ambazo zinatusaidia kuwazia simulizi hilo.
3. Tunaweza kufanya nini ili tufaidike tunapojifunza kitabu Igeni Imani Yao?
3 Jinsi Unavyoweza Kunufaika: Barua ya utangulizi kutoka Baraza Linaloongoza inatutia moyo kwa maneno haya: “Wazia mambo unayosoma; husisha hisia zako. Hisi kama watu wanaotajwa katika Biblia walivyohisi, ona mambo waliyoona. Linganisha jinsi walivyotenda katika hali fulani, na jinsi ambavyo huenda ungetenda.” Bila shaka kutumia uwezo wetu wa kuwazia matukio hakumaanishi kwamba tukisie mambo, badala yake, tunapaswa kupiga picha akilini kuhusu masomo tunayojifunza kupitia masimulizi hayo na kujiweka katika hali ya wahusika hao. Kufanya hivyo kunahitaji muda na kutafakari. (Neh. 8:8) Ikiwa somo linaanza katikati ya sura, anayeongoza ataanza kwa utangulizi wa sekunde 30 hadi dakika moja ili kupitia mambo makuu ya somo lililopita. Ikiwa somo hilo halina sehemu inayosema “Mambo ya Kufikiria . . . ” anayeongoza anaweza kuuliza swali moja au mawili mwishoni mwa somo hilo.
4. Kwa nini tunapaswa kujifunza kitabu Igeni Imani Yao?
4 Tunaishi katika ulimwengu unaotaka kuharibu au kudhoofisha imani yetu kila siku kwa njia mbalimbali. Kitabu hiki na mfululizo wa makala za gazeti la Mnara wa Mlinzi zinazotegemeza kitabu hicho ni zawadi kutoka kwa Yehova ambayo imekusudiwa kuimarisha imani yetu. (Yak. 1:17) Acheni sote tufaidike kikamili kwa kuhudhuria Funzo la Biblia la Kutaniko kwa ukawaida na kutoa maelezo kadiri tunavyoweza tutakapokuwa tukijifunza kitabu hicho!