Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w14 1/1 kur. 6-7
  • Kifo Si Mwisho wa Mambo Yote!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kifo Si Mwisho wa Mambo Yote!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “MTU AKIFA, JE, ANAWEZA KUISHI TENA?”
  • WAFU WATAFUFULIWA LINI?
  • Ufufuo—Tumaini la Wafu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Inakuwaje Wakati wa Kufa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Tumaini Hakika kwa Wapendwa Wako Ambao Wamekufa
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Mtu Aliyekuwa Maiti Siku Nne
    Kumsikiliza Mwalimu Mkuu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
w14 1/1 kur. 6-7
Yesu alifufua Lazaro kutoka kwa kifo na kumwita kutoka kaburini.

HABARI KUU | JE KIFO NI MWISHO WA MAMBO YOTE?

Kifo Si Mwisho wa Mambo Yote!

Bethania kilikuwa kijiji kidogo kilichokuwa umbali wa kilomita tatu kutoka Yerusalemu. (Yohana 11:18) Msiba ulitokea huko majuma machache kabla ya kifo cha Yesu. Lazaro rafiki wa karibu wa Yesu, alishikwa na ugonjwa ghafula na kufa.

Yesu alipopata habari hiyo, aliwaambia wanafunzi wake kwamba Lazaro alikuwa analala usingizi na angemwamsha. (Yohana 11:11) Lakini wanafunzi wa Yesu hawakuelewa alichomaanisha, kwa hiyo Yesu akawaambia waziwazi: “Lazaro amekufa.”—Yohana 11:14.

Siku nne baada ya Lazaro kuzikwa, Yesu aliwasili Bethania na akaenda kumfariji Martha, dada ya Lazaro. “Kama ungekuwa hapa ndugu yangu hangekufa,” Martha akamwambia Yesu. (Yohana 11:17, 21) Yesu akamjibu: “Mimi ndiye ufufuo na uzima. Yule anayeniamini, hata akifa, atarudi kwenye uzima.”—Yohana 11:25.

“Lazaro, njoo huku nje!”

Ili kuonyesha kwamba maneno hayo hayakuwa ahadi ya uwongo, Yesu alilikaribia kaburi na kuita kwa sauti kubwa: “Lazaro, njoo huku nje!” (Yohana 11:43) Kwa mshangao wa watazamaji, yule mfu akatoka kaburini.

Yesu alikuwa amewafufua watu wawili kabla ya hapo. Pindi moja alimfufua msichana fulani—binti ya Yairo. Kabla tu ya kumfufua, Yesu alisema pia kwamba binti huyo alikuwa analala usingizi.—Luka 8:52.

Ona kwamba alipokuwa akizungumza kuhusu kifo cha Lazaro na binti ya Yairo, Yesu alifananisha kifo na usingizi. Huo ni ufananisho unaofaa kabisa. Kwa nini? Usingizi ni hali ya kukosa fahamu na unaleta wazo la kupumzika kutoka kwa maumivu na kuteseka. (Mhubiri 9:5; ona sanduku, “Kifo Ni Kama Usingizi Mzito.”) Katika karne ya kwanza, wanafunzi wa Yesu walielewa vizuri hali ya wafu. Kitabu kuhusu dini na maadili (Encyclopedia of Religion and Ethics) kinasema hivi: “Wafuasi wa Yesu walijua kwamba kifo ni usingizi na kaburi ni mahali pa kupumzikia . . . kwa wale waliokufa wakiwa na imani.”a

Tunafarijika kujua kwamba wafu wamelala katika makaburi na hawateseki. Hilo linatusaidia kujua kinachotupata tunapokufa na kwa hiyo hatuogopi tena kifo.

“MTU AKIFA, JE, ANAWEZA KUISHI TENA?”

Hata ingawa sisi hufurahia kupumzika vya kutosha usiku, hakuna mtu anayetaka kulala milele. Je, tunaweza kuwa na tumaini kwamba wafu waliolala katika kaburi watafufuliwa kama Lazaro na binti ya Yairo?

Ayubu aliuliza swali hilo alipohisi anakaribia kufa. Aliuliza hivi: “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena?”—Ayubu 14:14.

Akizungumza na Mungu Mweza-Yote, Ayubu alijibu swali lake mwenyewe kwa kusema: “Utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu. Kwa kuwa utaitamani sana kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:15) Ayubu alikuwa na uhakika kwamba Yehova alitarajia kwa hamu siku ambayo angemfufua mtumishi wake mwaminifu. Je, Ayubu alikuwa akitumaini jambo lisilowezekana? La, hasha!

Ufufuo aliofanya Yesu ulithibitisha wazi kwamba Mungu alimpa Yesu nguvu za kushinda kifo. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba sasa Yesu ana “funguo za kifo.” (Ufunuo 1:18) Kwa hiyo, Yesu atafungua malango ya kaburi, kama tu alivyoamuru jiwe lililokuwa kwenye kaburi la Lazaro liondolewe.

Biblia inarudia tena na tena ahadi hiyo ya ufufuo. Malaika alimhakikishia nabii Danieli hivi: “Utapumzika, lakini utasimama kwa ajili ya fungu lako mwishoni mwa zile siku.” (Danieli 12:13) Yesu aliwaambia hivi viongozi wa Kiyahudi, Masadukayo ambao hawakuamini ahadi ya ufufuo: “Ninyi mnakosea, kwa sababu hamjui Maandiko wala nguvu za Mungu.” (Mathayo 22:23, 29) Mtume Paulo alisema hivi: “Nina tumaini kwa Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:15.

WAFU WATAFUFULIWA LINI?

Ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu utatukia lini? Malaika alimwambia Danieli aliyekuwa mwadilifu kwamba angesimama “mwishoni mwa zile siku.” Pia Martha aliamini kwamba ndugu yake, Lazaro, “atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.”—Yohana 11:24.

Biblia inahusianisha “siku ya mwisho” na utawala wa Ufalme wa Kristo. Paulo aliandika hivi: “Kwa maana ni lazima [Kristo] atawale akiwa mfalme mpaka Mungu awe ameweka adui zote chini ya miguu yake. Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.” (1 Wakorintho 15:25, 26) Hiyo ni sababu yenye nguvu kwa nini tunapaswa kusali Ufalme wa Mungu uje na mapenzi ya Mungu yafanywe duniani.b

Ayubu alifahamu vizuri kwamba Mungu anakusudia kuwafufua wafu. Siku hiyo itakapofika, kifo kitaangamizwa kabisa. Na hakuna mtu yeyote atakayejiuliza, ‘Je, kifo ni mwisho wa mambo yote?’

a Neno la Kigiriki linalomaanisha makaburi na ambalo lilitumiwa na Wakristo wa mapema, linatafsiriwa kuwa “mahali pa kulala.”

b Ili kujifunza mengi kuhusu Ufalme wa Mungu, soma sura ya 8 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Kifo Ni Kama Usingizi Mzito

  • “Uyafanye macho yangu yang’ae, ili nisilale usingizi katika kifo.”—Zaburi 13:3.

  • “‘Rafiki yetu Lazaro amelala, lakini mimi nitakwenda kumwamsha.’ Wanafunzi wake wakamwambia, ‘Bwana, ikiwa amelala, basi atapona.’ . . . Kumbe Yesu alikuwa amesema juu ya kifo cha Lazaro.”—Yohana 11:11-13, Biblia Habari Njema.

  • “Daudi, kwa upande mmoja, alitumikia mapenzi kamili ya Mungu katika kizazi chake mwenyewe na kulala katika kifo.”—Matendo 13:36.

  • “Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu, matunda ya kwanza ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo.”—1 Wakorintho 15:20.

  • “Hatutaki mkose kujua kuhusu wale walalao usingizi katika kifo; ili msiwe na huzuni kama wale watu wengine wasio na tumaini.”—1 Wathesalonike 4:13.

Wafu Wataamka

  • “Wafu wako wataishi. Maiti wangu wataamka. Amkeni, pigeni vigelegele kwa shangwe!”—Isaya 26:19.

  • “Kutakuwa na wengi kati ya wale waliolala katika mavumbi ya nchi ambao wataamka.”—Danieli 12:2.

  • “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.”—Yohana 5:28, 29.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki