Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha
Septemba 19-25
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-1 783 ¶5
Kutoka
Kwa wonyesho mkubwa wenye nguvu, Yehova alitukuza jina lake na kulikomboa taifa la Israeli. Wakiwa salama kwenye ufuo wa Mashariki wa Bahari Nyekundu, Musa aliwaongoza wana wa Israeli kuimba wimbo, huku Miriamu ambaye alikuwa nabii na dada ya Musa, akiwa na tari mkononi mwake aliwaongoza wanawake wote wenye matari kucheza dansi na kuwaitikia wanaume waliokuwa wakiimba. (Kut 15:1, 20, 21) Waisraeli walikuwa wametenganishwa kabisa na adui zao. Walipotoka Misri, Mungu hakuruhusu wapatwe na madhara yoyote kutoka kwa mwanadamu au mnyama; hakuna hata mbwa yeyote aliyewabwekea kwa ukali au kuuchezesha ulimi wake dhidi yao. (Kut 11:7) Ingawa simulizi la kitabu cha Kutoka halielezi kihususa kwamba Farao aliangamia baharini pamoja na jeshi lake, Zaburi 136:15 inaeleza kwamba Yehova ‘alimkung’uta Farao na jeshi lake ndani ya Bahari Nyekundu.’
Septemba 26–Oktoba 2
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-2 448
Kinywa
Ni kiungo cha mwili kilichoumbwa na Mungu kwa ajili ya kupokea na kumeng’enya chakula kabla ya kufika tumboni, pia, kinywa kinatumika kwa ajili ya mazungumzo. Usemi wote unapaswa kumletea sifa Muumba. (Zb 34:1; 51:15; 71:8; 145:21) Mtunga-zaburi alitangaza kwamba kila kitu kinachopumua kitamsifu Yehova; kwa hiyo ni lazima wanadamu wafanye hivyo ikiwa wanatamani kuishi. Mtume Paulo anaeleza kwamba imani kwa Mungu na Mwana wake, haipaswi kuonyeshwa kwa moyo tu. Ni lazima imani iambatane na tangazo la hadharani ili kuleta wokovu.—Zb 150:6; Ro 10:10.
Kulingana na kusudi lake, haki yake, na nguvu zake akiwa Muumba, Yehova anaweza kuweka maneno yanayofaa kwenye kinywa cha mtumishi wake. Aliweka maneno hayo katika vinywa vya manabii kimuujiza, nao wakasema maneno yanayofaa kwa mwongozo wa roho yake. (Kut 4:11, 12, 15; Yer 1:9) Katika kisa kimoja alisababisha hata mnyama, punda, aweze kusema. (Hes 22:28, 30; 2Pe 2:15, 16) Leo, watumishi wa Mungu wanaweza kuweka maneno ya Yehova katika vinywa vyao, si kwa kuongozwa na roho kimuujiza, bali kupitia Neno lake lililoandikwa, ambalo limeongozwa na roho, linalowapatia vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema. (2Ti 3:16, 17) Sasa hawahitaji kusubiri hadi Kristo aje kuwapatia habari njema, wala hawahitaji kwenda katika chanzo kingine kupata jambo la kuhubiri. Tayari liko mbele yao, kazi yao ni kulisema tu. Maandiko yanawaambia hivi: “Lile neno liko karibu nawe, katika kinywa chako mwenyewe na katika moyo wako mwenyewe.”—Ro 10:6-9; Kum 30:11-14.
Kinaleta Uzima au Kifo. Ni jambo muhimu kutumia vizuri kinywa chetu, na hata Yehova amesema tufanye hivyo. Neno lake linasema hivi: “Kinywa cha mwadilifu ni chemchemi ya uzima.” (Met 10:11) Kwa hiyo, kinywa kinapaswa kulindwa kwa uangalifu zaidi (Zb 141:3; Met 13:3; 21:23), na mtu akikitumia vibaya, kinywa kunaweza kumsababishia uharibifu wake mwenyewe. (Met 10:14; 18:7) Mungu atamtoza hesabu mtu kutokana na mambo anayozungumza kwa kinywa chake. (Mt 12:36, 37) Mtu anaweza kuzungumza haraka haraka na kutoa ahadi bila kufikiri. (Mhu 5:4-6) Anaweza kumsifu kupita kiasi mtu mwingine, na kumfanya abadilike na kujihukumu mwenyewe. (Met 26:28) Ni muhimu kwa mtu kulinda kinywa chake anapokuwa mbele ya watu waovu, kwa sababu kuteleza kidogo na kutofuata mambo ambayo kwa hekima Mungu anawaambia watumishi wake wafanye kutaliletea suto jina la Mungu na kunaweza kumsababishia kifo mtu huyo. (Zb 39:1) Yesu anatupatia mfano mzuri wa kutii mapenzi ya Mungu bila kulalamika au kutoa matukano yoyote kwa wapinzani wake waliokuwa waovu.—Isa 53:7; Mdo 8:32; 1Pe 2:23.
Mkristo anapaswa kuwa macho kila siku, kwa sababu hajakamilika; kwa hiyo anahitaji kuchunguza moyo wake. Yesu alisema kwamba mtu hatiwi unajisi na kile kinachoingia ndani ya kinywa chake, bali na kile kinachotoka katika kinywa chake, kwa maana “kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.” (Mt 12:34; 15:11) Hivyo, mtu anahitaji kuwa mwangalifu kutoruhusu jambo lolote litoke kinywani mwake bila kufikiria matokeo ya maneno yake. Hilo linahitaji mtu atumie uwezo wake wa kufikiri kutenda kulingana na mambo mazuri aliyojifunza katika Neno la Mungu.—Met 13:3; 21:23.