SOMO LA 50
Jitahidi Kugusa Moyo
MBALI na kuwahubiria watu, jitahidi kugusa mioyo yao. Katika Biblia, moyo huonyeshwa kuwa tofauti na jinsi mtu anavyoonekana kwa nje. Moyo wa mfano huonyesha jinsi mtu alivyo kwa ndani, yaani hisia zake, mambo anayofikiria sana, kwa nini anayafikiria, na jinsi mawazo hayo yanavyoongoza matendo yake. Basi, mbegu ya kweli hupandwa katika moyo huo wa mfano. (Mt. 13:19) Na mtu humtii Mungu kutokana na moyo huo.—Mit. 3:1; Rom. 6:17.
Ili ufundishaji wako uguse moyo, kazia fikira mambo haya: (1) Fahamu jambo ambalo tayari limemfanya msikilizaji awe na maoni fulani moyoni. (2) Kazia sifa nzuri kama upendo na kumhofu Mungu. (3) Mtie moyo msikilizaji achunguze yaliyo moyoni mwake ili ampendeze Yehova kabisa.
Kutumia Ufahamu. Sababu zinazofanya watu wengi wasikubali kweli zatofautiana. Unapoongoza funzo la Biblia la nyumbani, huenda ukahitaji kuondoa maoni mabaya na kutaja mambo ya hakika, au kumthibitishia mambo unayosema. Jiulize: ‘Je, mtu huyu anajua kwamba akiwa binadamu ana mahitaji ya kiroho? Tayari anaamini nini? Na haamini nini? Kwa nini ana maoni hayo? Je, anahitaji msaada wa kushinda tamaa ambazo zinaweza kumfanya akatae wajibu unaotokana na kujua kweli?’
Nyakati nyingine si rahisi kujua sababu zinazofanya watu waamini mambo fulani. Mithali 20:5 inasema: “Mashauri ya moyoni ni kama kilindi; lakini mtu mwenye ufahamu atayateka.” Ufahamu ni uwezo wa kutambua jambo ambalo halionekani wazi. Unahitaji kuwa makini sana na mwenye kujali ili kufaulu.
Mawasiliano si kuzungumza tu. Jambo fulani linaweza kubadili uso wa mwanafunzi au sauti yake. Ikiwa wewe ni mzazi, unatambua kwamba tabia ya mtoto wako ikibadilika inawezekana kuna mambo mapya yanayoathiri maisha yake. Usipuuze dalili hizo. Hizo zinaonyesha hali ya moyo wake.
Maswali mazuri yanaweza kufunua yaliyo moyoni mwa mtu. Unaweza kuuliza: “Unaonaje . . . ?” “Kwa nini unaamini kwamba . . . ?” “Ungefanyaje ikiwa . . . ?” Lakini tahadhari usiulize watu maswali mengi mno. Unaweza kutumia busara na kuanza maswali yako kwa kuuliza, “Ni sawa nikikuuliza hivi . . . ?” Unahitaji kujitahidi sana kugundua yaliyo moyoni mwa mtu na si jambo la kufanya haraka-haraka. Kwa kawaida unahitaji kwanza kujenga hali ya kutumainiana na mtu kwa muda fulani kabla hajafunua yaliyo moyoni mwake. Hata hivyo, ni lazima tutahadhari asifikiri tunauliza mambo ambayo hayatuhusu.—1 Pet. 4:15.
Unahitaji kutumia ufahamu pia kuhusiana na jinsi unavyoitikia mambo unayosikia. Kumbuka kwamba kusudi lako ni kuwaelewa watu ili ujue habari ya Biblia inayoweza kuwachochea. Jidhibiti usikosoe maoni yao yenye makosa. Badala yake uwe macho kufahamu hisia zao wanapozungumza. Ndipo utakapojua jinsi ya kujibu, na kwa sababu mwanafunzi wako ataona unamwelewa, inaelekea atafikiria kwa uzito mambo unayosema.—Mit. 16:23.
Unaweza kuwachochea watu kwa kadiri fulani hata kama unahutubia watu wengi. Ikiwa unawatazama wasikilizaji, na uko macho kuona ishara za nyuso zao, na unauliza maswali yanayofanya wafikiri, labda utaona jinsi wasikilizaji wanavyohisi kuhusu mambo unayosema. Ikiwa unafahamu wasikilizaji vizuri, fikiria hali zao. Fikiria mtazamo wa ujumla wa kutaniko unaposababu nao kwa kutumia Neno la Mungu.—Gal. 6:18.
Kuchochea Hisia Zinazofaa. Baada ya kufahamu mambo ambayo mtu anaamini, yale ambayo haamini, na kwa nini, utaweza kujenga mazungumzo yako kwenye msingi huo. Yesu aligusa mioyo ya wanafunzi wake baada ya kufufuliwa kwa ‘kuwafungulia kabisa yale Maandiko’ kuhusiana na matukio ya karibuni. (Luka 24:32) Wewe pia jaribu kuhusianisha mambo ambayo mtu amepitia, kile anachotamani, na kile anachoona katika Neno la Mungu. Utagusa moyo wa mwanafunzi kwa njia yenye kumfaidi anapotambua wazi kwamba “hii ndiyo KWELI!”
Unapokazia wema wa Yehova, upendo wake, fadhili zake zisizostahiliwa, na matendo yake ya haki, unawasaidia wanafunzi wampende Mungu. Unapowaonyesha wasikilizaji kwa saburi sifa nzuri ambazo Mungu anaona ndani yao wakiwa mtu mmoja-mmoja, unawapa sababu ya kuamini kwamba wanaweza kuwa na uhusiano mzuri na Mungu. Unaweza kufanya hivyo kwa kufikiria maandiko kama Zaburi 139:1-3, Luka 21:1-4, na Yohana 6:44 na kwa kuwasaidia wasikilizaji watambue kadiri Yehova anavyowapenda sana watumishi wake waaminifu. (Rom. 8:38, 39) Eleza kwamba Yehova hatazami tu makosa yetu, bali anatazama maisha yetu yote, bidii yetu kwa ajili ya ibada safi, na jinsi tunavyopenda jina lake. (2 Nya. 19:2, 3; Ebr. 6:10) Hata anakumbuka kila jambo dogo kutuhusu, na kwa njia ya kutokeza atafufua “wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho.” (Yn. 5:28, 29; Luka 12:6, 7) Kwa kuwa wanadamu wameumbwa kwa mfano wa Mungu, kuzungumzia sifa zake hugusa moyo.—Mwa. 1:27.
Pia unaweza kugusa moyo wa mtu anapojifunza kuwaona wengine jinsi Yehova anavyowaona. Ni wazi kwamba ikiwa Mungu anatupenda sisi binafsi, basi anawapenda wengine pia, bila kujali malezi, taifa, au jamii yao. (Mdo. 10:34, 35) Mtu akielewa jambo hilo, anakuwa na msingi mzuri wa Kimaandiko wa kuondoa chuki na ubaguzi moyoni mwake. Hiyo itamsaidia kuwa na amani na wengine anapojifunza kufanya mapenzi ya Mungu.
Hofu ya Mungu ni hisia nyingine ambayo tunaweza kuwasaidia wengine wakuze. (Zab. 111:10; Ufu. 14:6, 7) Hofu hiyo ya Mungu inaweza kumchochea mtu atimize jambo ambalo huenda lisiwezekane kwa nguvu zake mwenyewe. Kwa kuzungumzia matendo makuu ya Yehova na fadhili zake zenye upendo zinazostaajabisha, unaweza kuwasaidia wengine wakuze hofu nzuri ya kutomkasirisha.—Zab. 66:5; Yer. 32:40.
Hakikisha wasikilizaji wanaelewa kwamba Yehova anachukulia mwenendo wao kwa uzito. Yeye ana hisia, na jinsi tunavyoitikia mwelekezo wake humhuzunisha ama humfurahisha. (Zab. 78:40-42) Onyesha watu jinsi mwenendo wao unavyoweza kujibu shtaka ambalo Shetani anamwelekezea Mungu.—Mit. 27:11.
Wasaidie wasikilizaji waone kwamba wanafaidika wanapotimiza matakwa ya Mungu. (Isa. 48:17) Njia moja ya kufanya hivyo ni kuonyesha matokeo halisi na ya kihisia-moyo ya kukataa hekima ya Mungu, hata kwa muda mfupi tu. Eleza jinsi dhambi inavyotutenganisha na Mungu, jinsi inavyowafanya wengine wakatae kweli tunayowafunza, na jinsi inavyowanyang’anya haki zao. (1 The. 4:6) Wasaidie wasikilizaji wathamini baraka ambazo wanapata sasa kwa sababu ya kufuata sheria za Mungu. Wasaidie wathamini zaidi kwamba tunapofuata njia za uadilifu za Yehova tunaepuka misiba. Mtu anaposadiki kwamba njia za Mungu ni zenye hekima, atachukia kabisa mwenendo wowote unaopinga hekima hiyo. (Zab. 119:104) Atafahamu kwamba utii si mzigo, bali ni njia ya kushikamana na Yehova kwa upendo.
Kuwasaidia Wengine Kujichunguza. Ili kuendelea kukua kiroho ni lazima watu wajue yaliyo mioyoni mwao. Eleza jinsi Biblia inavyoweza kuwasaidia.
Wasaidie kutambua kwamba Biblia si kitabu tu chenye orodha ya sheria, mashauri, matukio ya zamani, na unabii. Bali pia inafunua mawazo ya Mungu. Katika Yakobo 1:22-25, Neno la Mungu linalinganishwa na kioo. Yaliyo moyoni mwetu huonyeshwa na jinsi tunavyoitikia ujumbe wa Biblia na tunavyoitikia jinsi Yehova anavyotimiza kusudi lake. Kwa hiyo, inafunua jinsi ambavyo Mungu, ambaye “huijaribu mioyo,” anatuona. (Mit. 17:3) Watie moyo wasikilizaji wakumbuke jambo hilo. Wahimize watafakari mambo ambayo Mungu amehifadhi katika Biblia na marekebisho ambayo wanaweza kufanya maishani mwao ili kumpendeza zaidi. Wasaidie kuona usomaji wa Biblia kuwa njia ya kujua jinsi Yehova anavyopima “fikira na makusudio ya moyo,” ili waweze kufanya marekebisho yoyote ambayo Mungu anataka.—Ebr. 4:12; Rom. 15:4.
Wanafunzi wengine wa Biblia wanaweza kufuata yale wanayojifunza, lakini wao hubabaika eti wengine watawaonaje. Huenda wanapambana na tamaa fulani za kimwili zenye nguvu. Au huenda wanawaza-waza jinsi ya kumtumikia Mungu huku wakishikilia matendo ya ulimwengu. Waonyeshe hatari ya kufanya hivyo. (1 Fal. 18:21) Wahimize wasali kwa Mungu ili aichunguze mioyo yao na kuisafisha.—Zab. 26:2; 139:23, 24.
Waonyeshe kwamba Yehova anaelewa jinsi wanavyojitahidi na kwamba Biblia inaeleza juu ya jitihada hiyo. (Rom. 7:22, 23) Wasaidie wajihadhari ili wasitawalwe na mielekeo ya moyo usio mkamilifu.—Mit. 3:5, 6; 28:26; Yer. 17:9, 10.
Mtie moyo kila mmoja achunguze kusudi lake la kufanya mambo. Mfundishe kujiuliza hivi: ‘Kwa nini nataka kufanya jambo hili? Je, litamwonyesha Yehova kwamba kwa kweli nathamini yote ambayo amenifanyia?’ Jaribu kuimarisha usadikisho wa kwamba kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova ndilo jambo muhimu zaidi kwa mtu yeyote.
Wasaidie wasikilizaji wafahamu umuhimu wa kumtumikia Yehova kwa ‘moyo wote.’ (Luka 10:27) Hiyo inamaanisha kwamba hisia zao zote, tamaa, na kusudi lao la kufanya mambo ni lazima zipatane na njia za Yehova. Basi wafundishe wasikilizaji wachanganue si tu mambo wanayofanya bali pia jinsi wanavyohisi kuhusu matakwa ya Mungu na makusudi yao ya kumtumikia. (Zab. 37:4) Wanafunzi wanapotambua sehemu ambazo wanahitaji kufanyia maendeleo, watie moyo wasali kwa Yehova: “Moyo wangu na ufurahi kulicha jina lako.”—Zab. 86:11.
Mwanafunzi anapokuwa na uhusiano wa karibu na Yehova, atamtii Mungu kwa sababu ya imani yake wala si kwa sababu unamsukuma-sukuma. Ndipo kwa hiari yake mwenyewe, ‘atafuliza kuhakikisha ni nini lililo lenye kukubalika kwa Bwana.’ (Efe. 5:10; Flp. 2:12) Yehova hufurahia sana utii kama huo unaotoka moyoni.—Mit. 23:15.
Kumbuka kwamba ni Yehova ambaye hupima mioyo na kuvuta watu kwake ili wawe na uhusiano na yeye. (Mit. 21:2; Yn. 6:44) Fungu letu ni kushirikiana naye. (1 Kor. 3:9) Ni ‘kama kwamba Mungu anasihi sana kupitia sisi.’ (2 Kor. 5:20; Mdo. 16:14) Yehova hamlazimishi mtu yeyote kukubali kweli, lakini tunapotumia Maandiko, anaweza kufanya wasikilizaji watambue kwamba mambo wanayosikia yanajibu maswali yao, au sala zao. Kila wakati unapopata nafasi ya kufundisha, kumbuka jambo hilo, na umwombe Yehova akuongoze na kukusaidia.—1 Nya. 29:18, 19; Efe. 1:16-18.