Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
SEPTEMBA 3-9
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | YOHANA 1-2
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Yoh 1:1
Neno: “Au” “Logos.” Kigiriki, ho loʹgos. Hapa limetumiwa kama jina la cheo, linatumiwa pia kwenye Yoh 1:14 na Ufu 19:13. Yohana alimtambulisha mmiliki wa jina hilo la cheo, yaani, Yesu. Jina hilo la cheo lilitumiwa kumhusu Yesu akiwa kiumbe wa roho kabla ya kuwa mwanadamu, wakati wa huduma yake duniani akiwa mwanadamu mkamilifu, na baada ya kuinuliwa kwenda mbinguni. Yesu alikuwa Neno la Mungu, au Msemaji, akiwasilisha habari na maagizo kwa wana wengine wa roho na kwa wanadamu. Kwa hiyo, inapatana na akili kufikiri kwamba kabla ya Yesu kuja duniani, Yehova aliwasiliana na wanadamu kupitia Neno, malaika aliyekuwa msemaji Wake.—Mwa 16:7-11; 22:11; 31:11; Kut 3:2-5; Amu 2:1-4; 6:11, 12; 13:3.
pamoja na: Tnn., “kuelekea.” Katika muktadha huu, kihusishi cha Kigiriki pros kinarejelea ukaribu na ushirika. Pia kinarejelea kuwa hawa ni watu wawili tofauti, yaani katika kisa hiki, Neno na Mungu wa kweli.
Neno alikuwa mungu: Au “Neno alikuwa wa kimungu.” Maneno hayo ya Yohana yanafafanua sifa fulani ya “Neno” (Kigiriki, ho loʹgos; tazama habari za utafiti kuhusu Neno katika mstari huu), yaani, Yesu Kristo. Cheo kikubwa cha Neno akiwa Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu ambaye Mungu aliumba vitu vingine vyote kupitia yeye ni msingi wa kumfafanua kuwa “mungu; wa kimungu.” Watafsiri wengi wanapendelea kusema “Neno alikuwa Mungu,” na hivyo kumlinganisha na Mungu Mweza-Yote. Hata hivyo, kuna sababu nzuri za kusema kwamba Yohana hakumaanisha “Neno” ndiye Mungu Mweza-Yote. Kwanza, fungu la kwanza la maneno na la pili yanaonyesha waziwazi kwamba “Neno” alikuwa “pamoja na Mungu.” Pia, neno la Kigiriki the·osʹ linapatikana mara tatu katika mstari wa 1 na wa 2. Mara ya kwanza na ya tatu linapoonekana, the·osʹ linatanguliwa na kibainishi wazi; mara ya pili linapoonekana halina kibainishi wazi. Wasomi wengi wanakubaliana kwamba kukosekana kwa kibainishi wazi kabla ya the·osʹ ya pili ni muhimu. Kibainishi wazi kinapotumiwa katika muktadha huu, neno the·osʹ linamrejelea Mungu Mweza-Yote. Kwa upande mwingine, kukosekana kwa kibainishi hicho katika muundo huu wa kisarufi kunafanya neno the·osʹ liwe sifa na linafafanua sifa fulani ya “Neno.” Hivyo, Biblia fulani za Kiingereza, Kifaransa, na Kijerumani zinatafsiri mstari huo kama Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, kuonyesha wazo kwamba “Neno” alikuwa “mungu; wa kimungu; kama mungu.” Wazo hilo linaungwa mkono na tafsiri za kale za Injili ya Yohana katika lahaja za Kisahidi na Kibohairi za lugha ya Kikoptiki, ambazo huenda zilitokezwa katika karne ya tatu na ya nne W.K. Zinatafsiri neno the·osʹ kwa njia tofauti linapoonekana kwa mara ya kwanza kwenye Yoh 1:1 na linapoonekana kwa mara ya pili. Maneno hayo yanakazia sifa fulani ya “Neno,” kwamba alikuwa kama Mungu, lakini hazimwonyeshi kuwa sawa na Baba yake, Mungu Mweza-Yote. Kupatana na mstari huo, Kol 2:9 inamfafanua Kristo kuwa ana “ujazo wote wa sifa ya Mungu.” Na kulingana na 2Pe 1:4, hata warithi pamoja na Kristo watakuwa “washiriki katika asili ya kimungu.” Isitoshe, katika tafsiri ya Septuajinti, neno la Kigiriki the·osʹ ndilo neno lilorejelewa, Mungu, katika Kiebrania ʼel na ʼelo·himʹ, ambazo inasemekana zinawasilisha maana ya msingi “Mwenye Uwezo; Mwenye Nguvu.” Maneno hayo ya Kiebrania yanatumiwa kumrejelea Mungu Mweza-Yote, miungu wengine, na wanadamu. (Ona pia habari za utafiti—Yoh 10:34.) Kumwita Neno “mungu,” au “mwenye nguvu,” kunapatana na unabii kwenye Isa 9:6, unaotabiri kwamba Masihi angeitwa “Mungu mwenye nguvu” (si “Mungu Mweza-Yote”) na kwamba atakuwa “Baba wa Milele” kwa wale watakaopata pendeleo la kuishi wakiwa raia wake. Bidii ya Baba yake, “Yehova wa majeshi” ingetimiza hilo.—Isa 9:7.
nwtsty habari za utafiti—Yoh 1:29
Mwanakondoo wa Mungu: Baada ya Yesu kubatizwa na kushawishiwa na Ibilisi, Yohana Mbatizaji alimtambulisha kuwa “Mwanakondoo wa Mungu.” Maneno hayo yanapatikana hapa na kwenye Yoh 1:36 peke yake. (Ona Nyongeza A7.) Inafaa kumlinganisha Yesu na mwanakondoo. Kotekote katika Biblia, kondoo walitolewa ili kuonyesha kwamba mtu alitambua dhambi yake na kufungua njia ya kumfikia Mungu. Hilo lilitangulia kuonyesha dhabihu ambayo Yesu angetoa alipotoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kwa ajili ya wanadamu. Maneno “Mwanakondoo wa Mungu” yangeweza kupatana na masimulizi kadhaa katika Maandiko yaliyoongozwa na roho. Tukizingatia kwamba Yohana Mbatizaji alifahamu Maandiko ya Kiebrania vizuri, huenda maneno yake yalimaanisha jambo moja au zaidi kati ya yafuatayo: kondoo dume ambaye Abrahamu alimtoa badala ya mwana wake Isaka (Mwa 22:13), mwanakondoo wa Pasaka aliyechinjwa nchini Misri ili kuwakomboa Waisraeli waliokuwa watumwa (Kut 12:1-13), au mwanakondoo dume aliyetolewa juu ya madhabahu ya Mungu kule Yerusalemu kila siku asubuhi na jioni (Kut 29:38-42). Pia, huenda Yohana alikuwa akifikiria unabii wa Isaya, ambapo yule ambaye Yehova anamwita “mtumishi wangu” anasemekana kuwa “aliletwa kama kondoo machinjioni.” (Isa 52:13; 53:5, 7, 11) Mtume Paulo alipoandika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho, alimrejelea Yesu kuwa “mwanakondoo wetu wa Pasaka.” (1Ko 5:7) Mtume Petro alizungumza kuhusu “damu yenye thamani, kama ile ya mwanakondoo asiye na dosari na asiye na doa.” (1Pe 1:19) Na zaidi ya mara 25 katika kitabu cha Ufunuo, kwa njia ya mfano Yesu aliyetukuzwa anaitwa “Mwanakondoo.”—Mifano kadhaa ni: Ufu 5:8; 6:1; 7:9; 12:11; 13:8; 14:1; 15:3; 17:14; 19:7; 21:9; 22:1.
SEPTEMBA 10-16
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | YOHANA 3-4
nwtsty habari za utafiti—Yoh 4:6
kwa kuwa alikuwa amechoka: Katika Maandiko yote ni hapa tu ambapo Yesu anasemekana “alikuwa amechoka.” Ilikuwa saa 6:00 mchana, na huenda asubuhi hiyo Yesu alikuwa amesafiri kutoka kwenye Bonde la Yordani kule Yudea hadi Sikari iliyoko Samaria, mwinuko mkali wa mita 900 au zaidi.—Yoh 4:3-5; ona Nyongeza A7.
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Yoh 3:29
rafiki ya bwana harusi: Katika nyakati za Biblia, rafiki wa karibu wa bwana harusi alitenda akiwa mwakilishi wake wa kisheria na kutimiza fungu muhimu katika kufanya mipango ya ndoa. Alionwa kuwa ndiye aliyewakutanisha bwana na bibi harusi. Siku ya harusi, msafara wa bibi harusi ungefika ama kwenye nyumba ya bwana harusi au ya baba yake, ambako karamu ya harusi ingefanywa. Wakati wa karamu hiyo, rafiki ya bwana harusi angefurahi kusikia sauti ya bwana harusi anapozungumza na bibi harusi wake, kwa kuwa rafiki huyo angehisi alikuwa amefaulu kutimiza wajibu wake. Yohana Mbatizaji alijilinganisha na “rafiki ya bwana harusi.” Katika kisa hiki, Yesu ndiye aliyekuwa bwana harusi na wanafunzi wakiwa kikundi walifanyiza bibi harusi wake wa mfano. Akitayarisha njia kwa ajili ya Masihi, Yohana Mbatizaji aliwafikisha washiriki wa kwanza wa “bibi harusi” kwa Yesu Kristo. (Yoh 1:29, 35; 2Ko 11:2; Efe 5:22-27; Ufu 21:2, 9) “Rafiki ya bwana harusi” alitimiza lengo lake kwa kufaulu kuwatambulisha; baada ya hapo hakuwa tena mhusika mkuu. Vivyo hivyo, Yohana mwenyewe alisema hivi kumhusu Yesu: “Huyo lazima aendelee kuongezeka, lakini mimi lazima niendelee kupungua.”—Yoh 3:30.
nwtsty habari za utafiti—Yoh 4:10
maji yaliyo hai: Katika Kigiriki maneno hayo yanatumiwa kihalisi kurejelea maji yanayotiririka, maji ya chemchemi, au maji safi kutoka kwenye kisima kinachopata maji ya chemchemi. Ni tofauti na maji yaliyosimama mahali pamoja. Kwenye Law 14:5, maneno ya Kiebrania yanayotafsiriwa “maji ya kijito” kihalisi ni “maji yaliyo hai.” Kwenye Yer 2:13 na 17:13 Yehova anafafanuliwa kuwa “chemchemi ya maji yaliyo hai,” yaani, maji ya mfano yanayotokeza uhai. Alipokuwa akizungumza na mwanamke Msamaria, Yesu alitumia maneno “maji yaliyo hai” kwa njia ya mfano, lakini inaonekana kwamba mwanzoni alielewa maneno hayo kihalisi.—Yoh 4:11; ona habari za utafiti—Yoh 4:14.
SEPTEMBA 17-23
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | YOHANA 5-6
nwtsty habari za utafiti—Yoh 6:10
watu wakaketi, karibu wanaume 5,000: Mathayo peke yake ndiye anayeongezea maneno “na pia wanawake na watoto wadogo” anaporipoti muujiza huu. (Mt 14:21) Inawezekana kwamba jumla ya wale waliolishwa kimuujiza ilikuwa zaidi ya 15,000.
nwtsty habari za utafiti—Yoh 6:14
Nabii: Wayahudi wengi katika karne ya kwanza W.K. walitarajia kwamba nabii kama Musa anayetajwa kwenye Kum 18:15, 18, angekuwa Masihi. Katika muktadha huu, maneno kuja ulimwenguni yanaonekana kuwa yanarejelea kutokea kwa Masihi kulikotarajiwa.Ni Yohana peke yake aliyeandika matukio yaliyotajwa katika mstari huu.
nwtsty habari za utafiti—Yoh 6:27, 54
chakula kinachoharibika . . . chakula kinachodumu kufikia uzima wa milele: Yesu alielewa kwamba watu fulani walikuwa wakishirikiana naye na wanafunzi wake ili tu wapate faida za kimwili. Ingawa chakula cha kimwili huwategemeza watu siku baada ya siku, “chakula” cha Neno la Mungu kitawawezesha wanadamu kuendelea kuwa hai milele. Yesu anawasihi watu katika umati huo wafanye kazi kwa ajili ya “chakula kinachodumu kufikia uzima wa milele,” yaani, wafanye jitihada kutosheleza uhitaji wao wa kiroho na kudhihirisha imani katika mambo wanayojifunza.—Mt 4:4; 5:3; Yoh 6:28-39.
akila mwili wangu na kunywa damu yangu: Muktadha unaonyesha kwamba wale wanaokula na kunywa wanafanya hivyo kwa njia ya mfano kwa kudhihirisha imani katika Yesu Kristo. (Yoh 6:35, 40) Yesu alisema maneno hayo katika mwaka wa 32 W.K., kwa hiyo hakuwa akizungumzia Mlo wa Jioni wa Bwana, ambao angeanzisha mwaka mmoja baadaye. Alisema maneno hayo kabla tu ya “Pasaka, ile Sherehe ya Wayahudi” (Yoh 6:4), kwa hiyo, wasikilizaji wake wangeweza kukumbuka sherehe ilikuwa ikikaribia na umuhimu wa damu ya mwanakondoo katika kuokoa uhai usiku ambao Waisraeli walitoka Misri (Kut 12:24-27). Yesu alikuwa akikazia kwamba damu yake ingetimiza fungu muhimu katika kuwawezesha wanafunzi wake kupata uzima wa milele.
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Yoh 6:44
amvute: Ingawa kitenzi cha Kigiriki “kuvuta” kinatumiwa kurejelea kuvuta wavu wa samaki (Yoh 21:6, 11), hakimaanishi kwamba Mungu anawavuta watu kinyume na mapenzi yao. Kitenzi hicho kinaweza pia kumaanisha “kuvutia,” na maneno ya Yesu huenda yakawa yanarejelea Yer 31:3, ambapo Yehova aliwaambia hivi watu wake wa kale: “Nimekuvuta kwangu kwa upendo mshikamanifu.” (Septuajinti inatumia kitenzi kilekile cha Kigiriki hapa.) Yoh 12:32 inaonyesha kwamba katika njia kama hiyo, Yesu anawavuta watu wa aina zote kwake. Maandiko yanaonyesha kwamba Yehova amewapa wanadamu uhuru wa kuchagua. Kila mtu anaweza kuchagua ikiwa atamtumikia au la. (Kum 30:19, 20) Mungu anawavuta kwa wororo wale ambao mioyo yao ina mwelekeo unaofaa. (Zb 11:5; Met 21:2; Mdo 13:48) Yehova anafanya hivyo kupitia ujumbe wa Biblia na kupitia roho yake takatifu. Unabii ulio katika Isa 54:13, unaonukuliwa kwenye Yoh 6:45, unawahusu wale ambao wamevutwa na Baba.—Linganisha Yoh 6:65.
nwtsty habari za utafiti—Yoh 6:64
Yesu [alijua] . . . yule ambaye angemsaliti: Yesu alikuwa akizungumza kumhusu Yuda Iskariote. Yesu alisali usiku mzima kwa Baba yake kabla ya kuwateua mitume 12. (Lu 6:12-16) Kwa hiyo, mwanzoni Yuda alikuwa mwaminifu kwa Mungu. Hata hivyo, Yesu alijua unabii ulio katika Maandiko ya Kiebrania kwamba angesalitiwa na mshiriki wa karibu. (Zb 41:9; 109:8; Yoh 13:18, 19) Yuda alipoanza kupotoka, Yesu, ambaye angeweza kusoma mioyo na mawazo, alitambua badiliko hilo. (Mt 9:4) Kwa kutumia uwezo wake wa kuona mambo mapema, Mungu alijua kwamba mwandamani wa Yesu mwenye kuaminika angekuwa msaliti. Lakini haipatani na sifa za Mungu wala na matendo yake ya wakati uliopita kufikiri kwamba Yuda ndiye tu angeanguka, kana kwamba kuanguka kwake kulikuwa kumepangwa mapema.
tangu mwanzo: Maneno hayo hayarejelei kuzaliwa kwa Yuda wala kuchaguliwa kwake kuwa mtume, ambako kulitokea baada ya Yesu kusali usiku mzima. (Lu 6:12-16) Badala yake, yanarejelea wakati ambapo Yuda alianza kutenda kwa hila, jambo ambalo Yesu alitambua mara moja. (Yoh 2:24, 25; Ufu 1:1; 2:23; ona habari za utafiti—Yoh 6:70; 13:11.) Hilo pia linaonyesha kwamba Yuda alifikiria mapema na alipanga matendo hayo, hayakutokea eti kwa sababu alibadilika ghafla. Maana ya maneno “mwanzo” (Kigiriki, ar·kheʹ) katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo inaweza kubadilika, kwa kutegemea muktadha. Kwa mfano, kwenye 2Pe 3:4, “mwanzo” unarejelea mwanzo wa uumbaji. Lakini katika visa vingi, neno hilo linatumiwa kwa njia hususa zaidi. Kwa mfano, Petro alisema kwamba roho takatifu ilikuja juu ya Watu wa Mataifa “kama ilivyokuja juu yetu mwanzoni.” (Mdo 11:15) Petro hakuwa akirejelea wakati wa kuzaliwa kwake au wakati ambapo aliitwa kuwa mtume. Badala yake, alikuwa akirejelea siku ya Pentekoste 33 W.K., yaani, “mwanzoni” mwa kumwagwa kwa roho takatifu kwa kusudi hususa. (Mdo 2:1-4) Mifano mingine ya jinsi muktadha unavyoathiri maana ya neno “mwanzo” inaweza kupatikana kwenye Lu 1:2; Yoh 15:27; na 1Yo 2:7.
SEPTEMBA 24-30
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | YOHANA 7-8
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Yoh 8:58
Nimekuwapo: Wayahudi waliokuwa wakipinga walitaka kumpiga Yesu mawe kwa kudai kwamba alikuwa ‘amemwona Abrahamu,’ ingawa, kama walivyosema, Yesu hakuwa ‘amefika umri wa miaka 50.’ (Yoh 8:57) Yesu alijibu kwa kuwaeleza kuhusu maisha yake kabla ya kuwa mwanadamu akiwa kiumbe mwenye nguvu wa roho mbinguni, kabla ya Abrahamu kuzaliwa. Wengine wanadai kwamba mstari huu unamtambulisha Yesu kuwa Mungu. Wanadai kwamba neno la Kigiriki linalotumiwa hapa, e·goʹ ei·miʹ (linalotafsiriwa “nipo” katika Biblia fulani), linarejelea maneno yaliyo kwenye Kut 3:14 katika Septuajinti na kwamba mistari yote miwili inapaswa kutafsiriwa kwa njia ileile. (Ona habari za utafiti—Yoh 4:26.) Hata hivyo, katika muktadha huu, tendo linalorejelewa na kitenzi cha Kigiriki ei·miʹ lilianza “kabla Abrahamu hajakuwapo” na bado lilikuwa likiendelea. Kwa hiyo, inafaa kwamba linatafsiriwa “nimekuwapo” badala ya “nipo,” na tafsiri kadhaa za kale na za kisasa zinatumia maneno yanayofanana na “nimekuwapo.” Kwa kweli, kwenye Yoh 14:9, aina ileile ya kitenzi cha Kigiriki ei·miʹ inatumiwa kutafsiri maneno haya ya Yesu: “Je, hata baada ya kuwa pamoja nanyi kwa muda mrefu hivyo, bado Filipo hujanijua?” Tafsiri nyingi zinatumia maneno kama hayo kuonyesha kwamba kwa kutegemea muktadha hakuna msingi unaofaa wa kisarufi kupinga matumizi ya ei·miʹ kuwa “nimekuwapo.” (Mifano mingine ya kutumia njeo ya hali timilifu kuwakilisha kitenzi cha Kigiriki cha njeo ya wakati uliopo yanapatikana kwenye Lu 2:48; 13:7; 15:29; Yoh 1:9; 5:6; 15:27; Mdo 15:21; 2Ko 12:19; 1Yo 3:8.) Pia, maneno ya Yesu kwenye Yoh 8:54, 55 yanaonyesha kwamba hakuwa akijaribu kuonyesha kwamba yeye na Baba yake ni mtu yuleyule.