Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
SEPTEMBA 7-13
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUTOKA 23-24
“Usiufuate Umati”
it-1 11
Haruni
Ni muhimu kutambua kwamba katika pindi zote tatu alizokengeuka, haionekani kwamba Haruni ndiye aliyekuwa wa kwanza kuanzisha kitendo kiovu, badala yake, inaonekana alikubali kushinikizwa na hali au watu wengine kutoka kwenye njia inayofaa. Hasa kuhusu kosa la kwanza, angeweza kutumia kanuni inayopatikana kwenye amri hii: “Usiufuate umati ili kutenda maovu.” (Kut 23:2) Hata hivyo, baadaye jina lake linatajwa kwa njia yenye kuheshimika katika Maandiko. Vilevile, Mwana wa Mungu alipokuwa duniani, alitambua uhalali wa ukuhani wa Haruni.—Zb 115:10, 12; 118:3; 133:1, 2; 135:19; Mt 5:17-19; 8:4.
it-1 343 ¶5
Upofu
Ukosefu wa haki kupitia upotoshwaji wa kesi ulifananishwa na upofu, na mara nyingi sana Sheria ilikataza waamuzi kupokea rushwa, zawadi, au kuwa na ubaguzi, kwa sababu mambo hayo yangewapofusha na kuwafanya wasitekeleze haki bila ubaguzi. “Rushwa huwapofusha watu wanaoona vizuri.” (Kut 23:8) “Rushwa hupofusha macho ya wenye hekima.” (Kum 16:19) Hata ikiwa mwamuzi alikuwa mwadilifu na mwenye busara sana, angeweza kuathiriwa kwa kujua au bila kujua ikiwa angepokea zawadi kutoka kwa watu waliohusika katika kesi. Sheria ya Mungu ilifunua kwamba si zawadi tu iliyokuwa na uwezo wa kupofusha bali pia hisia. Ilisema: “Usiwabague maskini au kuwapendelea matajiri.” (Law 19:15) Basi, mwamuzi hakupaswa kufanya uamuzi kwa sababu tu ya hisia au ili tu apendwe na umati na hivyo kutoa uamuzi uliowaonea matajiri kwa sababu tu ya utajiri wao.—Kut 23:2, 3.
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-2 393
Mikaeli
1. Mbali na Gabrieli, ni yeye tu kati ya malaika wengine wote katika Biblia anayetajwa kwa jina, na ndiye peke yake anayeitwa “malaika mkuu.” (Yud 9) Jina lake linapatikana kwa mara ya kwanza kwenye sura ya kumi ya kitabu cha Danieli, ambapo Mikaeli anafafanuliwa kuwa “mmoja wa wakuu wenye vyeo vya juu zaidi”; alikuja kumsaidia malaika wa cheo cha chini ambaye alipingwa na “mkuu wa ufalme wa Uajemi.” Mikaeli aliitwa “mkuu anayesimama kwa ajili ya watu [wa Danieli].” (Da 10:13, 20, 21; 12:1) Hilo linaonyesha kwamba Mikaeli ndiye malaika aliyewaongoza Waisraeli nyikani. (Kut 23:20, 21, 23; 32:34; 33:2) Mkataa huo unaweza kuungwa mkono na uhakika wa kwamba “Mikaeli, yule malaika mkuu [alipingana] na Ibilisi na kubishana naye kuhusu mwili wa Musa.”—Yud 9.
SEPTEMBA 14-20
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUTOKA 25-26
“Kitu Muhimu Zaidi Katika Hema la Ibada”
it-1 165
Sanduku la Agano
Kielelezo na Muundo. Jambo la kwanza ambalo Yehova alimpa Musa alipokuwa akimwagiza atengeneze hema la ibada, ni kielelezo na muundo wa Sanduku la Agano, kwa sababu kilikuwa ndicho kitu muhimu zaidi katika hema la ibada na kambi yote ya Waisraeli. Sanduku hilo lilikuwa na urefu wa mikono miwili na nusu, upana wa mkono mmoja na nusu, na kimo cha mkono mmoja na nusu (karibu sentimita 111 × 67 × 67; inchi 44 × 26 × 26). Lilitengenezwa kwa mbao za mshita, na upande wa nje na wa ndani ulifunikwa kwa dhahabu safi. Lilipambwa kwa “ukingo wa dhahabu kulizunguka.” Sehemu ya pili ya Sanduku hilo, yaani, kifuniko chake, kilitengenezwa kwa dhahabu halisi, si mbao iliyofunikwa kwa dhahabu, na urefu na upana wake ulikuwa sawa na wa sanduku hilo. Juu ya kifuniko hicho kulikuwa na makerubi wawili wa dhahabu waliotengenezwa kwa kutumia nyundo, kila kerubi akiwa upande mmoja wa kifuniko hicho wakiangaliana, wakiwa wameinamisha vichwa vyao na mabawa yao yakiwa yameinuliwa juu kufunika Sanduku la Agano. (Kut 25:10, 11, 17-22; 37:6-9) Kifuniko hicho pia kiliitwa “kiti cha rehema” au “kifuniko cha upatanisho.”—Kut 25:17; Ebr 9:5, maelezo ya chini; pia ona KIFUNIKO CHA UPATANISHO.
it-1 166 ¶2
Sanduku la Agano
Sanduku la Agano lilitumiwa kama hifadhi takatifu ya kuweka kumbukumbu au shuhuda takatifu, na jambo kuu lililohifadhiwa humo ni yale mabamba mawili ya ushuhuda, yaani, zile Amri Kumi. (Kut 25:16) “Mtungi wa dhahabu wenye mana, [na] fimbo ya Haruni iliyochipuka” viliongezwa katika Sanduku la Agano lakini baadaye vikaondolewa wakati fulani kabla ya kujengwa kwa hekalu la Sulemani. (Ebr 9:4; Kut 16:32-34; Hes 17:10; 1Fa 8:9; 2Nya 5:10) Muda mfupi kabla ya Musa kufa, aliwapa makuhani Walawi nakala ya “kitabu cha sheria” na kuwaagiza kwamba kiwekwe, si ndani, bali “kando ya sanduku la agano la Yehova Mungu wenu, . . . [kuwa] ushahidi dhidi yenu.”—Kum 31:24-26.
it-1 166 ¶3
Sanduku la Agano
Lilihusianishwa na kuwapo kwa Mungu. Katika historia yake yote, Sanduku la Agano lilihusianishwa na kuwapo kwa Mungu. Yehova aliahidi kwamba: “Nitakutokea hapo na kuzungumza nawe kutoka juu ya kifuniko hicho. Kutoka katikati ya hao makerubi wawili walio juu ya sanduku la Ushahidi.” “Nitatokea katika wingu juu ya kifuniko hicho.” (Kut 25:22; Law 16:2) Samweli aliandika kwamba Yehova “[anaketi] akiwa mfalme juu ya makerubi” (1Sa 4:4); basi makerubi walikuwa “mfano wa lile gari” la Yehova. (1Nya 28:18) Vilevile, “kila mara Musa alipoingia katika hema la mkutano kuongea na [Yehova], alisikia sauti ikizungumza naye kutoka juu ya kifuniko cha sanduku la Ushahidi, kutoka katikati ya wale makerubi wawili; Mungu aliongea naye.” (Hes 7:89) Baadaye, Yoshua na Kuhani Mkuu Finehasi waliongea pia na Yehova mbele ya Sanduku la Agano. (Yos 7:6-10; Amu 20:27, 28) Hata hivyo, kuhani mkuu peke yake ndiye aliyeingia Patakatifu Zaidi na kuona Sanduku la Agano, siku moja kila mwaka, si ili azungumze na Yehova bali kuhusiana na sherehe ya Siku ya Kufunika Dhambi.—Law 16:2, 3, 13, 15, 17; Ebr 9:7.
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-1 432 ¶1
Kerubi
Vitu vyenye umbo la makerubi vilikuwa katika hema la ibada lililotumiwa nyikani. Kulikuwa na makerubi wawili kwenye kifuniko cha Sanduku la Agano mmoja kila upande. Walikuwa wametengenezwa kwa dhahabu kwa kutumia nyundo. Walikuwa wakiangaliana wakiwa wameinama kuelekea kifuniko kana kwamba wanaabudu. Kila mmoja alikuwa na mabawa mawili yaliyonyooshwa kuelekea juu na kufunika kifuniko kana kwamba wanatoa ulinzi. (Kut 25:10-21; 37:7-9) Vilevile, kulikuwa na michoro ya makerubi upande wa ndani wa vitambaa vya hema la ibada na kwenye pazia lililotenganisha Patakatifu na Patakatifu Zaidi.—Kut 26:1, 31; 36:8, 35.
it-2 936
Mikate ya Wonyesho
Mikate kumi na miwili iliyowekwa kwenye sehemu ya Patakatifu katika hema la ibada au hekaluni na kila siku ya Sabato mikate ya zamani iliondolewa na mikate mipya ikawekwa. (Kut 35:13; 39:36; 1Fa 7:48; 2Nya 13:11; Ne 10:32, 33) Kihalisi maneno ya Kiebrania yanayotumiwa kuhusu mikate ya wonyesho ni “mikate ya uso.” Neno “uso” nyakati nyingine humaanisha “uwepo” (2Fa 13:23), hivyo basi mikate ya wonyesho ilikuwa mbele za uso wa Yehova kama toleo la kudumu mbele zake. (Kut 25:30) Mikate ya wonyesho pia inaitwa “mikate ya tabaka” (2Nya 2:4), “mikate ya toleo” (Mk 2:26), na pia “mikate” (Ebr 9:2).
SEPTEMBA 21-27
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUTOKA 27-28
“Tunajifunza Nini Kutokana na Mavazi ya Makuhani?”
it-2 1143
Urimu na Thumimu
Baadhi ya wasomi wa Biblia wanaamini kwamba Urimu na Thumimu zilikuwa kura. Kwenye andiko la Kutoka 28:30 tafsiri ya James Moffatt inaziita “kura takatifu.” Baadhi yao wanaamini kwamba ilikuwa na vipande vitatu, kimoja kilikuwa na neno “ndiyo,” cha pili “hapana,” na cha tatu hakikuwa na maandishi yoyote. Kipande kimoja kati ya vipande hivyo kilichukuliwa ili kupata jibu la swali lililoulizwa, lakini kama kipande kisicho na maandishi ndicho kilichochukuliwa, basi ilimaanisha kwamba hakukuwa na jibu. Wengine hufikiri kwamba yalikuwa mawe madogo yenye pande mbili, upande mmoja ulikuwa mweupe na upande wa pili ulikuwa mweusi. Yalipoangushwa chini, pande mbili nyeupe zingemaanisha “ndiyo,” pande mbili nyeusi zingemaanisha “hapana,” na upande mweusi na mweupe ulimaanisha hakuna jibu. Pindi fulani, Sauli alipouliza kupitia kuhani kama anapaswa kuwashambulia tena Wafilisti, jibu lilikuwa hapana. Akihisi kwamba mmoja kati ya wanaume wake alikuwa ametenda dhambi, alisali hivi: “Ee Mungu wa Israeli, jibu kwa Thumimu! ” Sauli na Yonathani walichukuliwa kati ya wale waliokuwepo; baada ya hapo, kura ilipigwa ili kuamua ni nani kati yao wawili. Katika simulizi hili, ombi hilo “Jibu kwa Thumimu,” linaonekana halikuhusiana na kupiga kura, ingawa inaonekana kwamba kulikuwa na uhusiano fulani kati ya mambo hayo mawili.—1Sa 14:36-42.
it-1 849 ¶3
Paji la Uso
Kuhani Mkuu wa Israeli. Upande wa mbele wa kilemba cha kuhani mkuu katika Israeli, juu ya paji la uso wake, kulikuwa na bamba la dhahabu, “ile ishara takatifu ya wakfu,” ambalo lilikuwa limechongwa maneno, “Utakatifu ni wa Yehova.” (Kut 28:36-38; 39:30) Akiwa mwakilishi mkuu wa Israeli katika ibada ya Yehova, ilifaa kwamba kuhani mkuu adumishe utakatifu katika cheo chake, na maandishi hayo yangewakumbusha pia Waisraeli wote umuhimu wa kudumisha utakatifu katika utumishi wa Yehova. Vilevile, bamba hilo la dhahabu lilikuwa mfano unaofaa wa Kuhani Mkuu zaidi, Yesu Kristo, na kuwekwa wakfu kwake na Yehova kwenye utumishi huo wa kikuhani unaoendeleza utakatifu wa Mungu.—Ebr 7:26.
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-1 1130 ¶2
Utakatifu
Wanyama na Mazao. Wazaliwa wa kwanza wa kiume wa ng’ombe, kondoo, na mbuzi walionwa kuwa watakatifu machoni pa Yehova na hawakupaswa kukombolewa. Walipaswa kutolewa dhabihu, na makuhani waliotakaswa walipewa sehemu ya nyama hiyo. (Hes 18:17-19) Matunda ya kwanza yalikuwa matakatifu kutia ndani sehemu ya kumi. Dhabihu na zawadi zote zilizotakaswa kwa ajili ya utumishi wa patakatifu zilikuwa takatifu vilevile. (Kut 28:38) Vitu vyote ambavyo Yehova aliviona kuwa vitakatifu vilipaswa kuheshimiwa na havikupaswa kutumiwa kwa shughuli za kawaida, au kwa njia iliyovitia unajisi. Mfano mmoja ni sheria kuhusu kutoa sehemu ya kumi. Ikiwa mtu angetenga sehemu ya kumi ya zao fulani, kwa mfano, ngano, kisha yeye au mtu katika nyumba yake achukue kiasi fulani bila kukusudia kutokana na kilichotengwa na kukitumia kwa ajili ya matumizi ya nyumbani, kama vile kupika, mtu huyo angekuwa na hatia ya kuvunja sheria ya Mungu kuhusu vitu vitakatifu. Sheria ilimtaka arudishe kiasi alichochukua na aongeze asilimia 20. Mbali na hilo, alipaswa pia kutoa kondoo dume asiye na kasoro kutoka kundini ili awe dhabihu. Hivyo, watu wangeendelea kuheshimu sana vitu vitakatifu vya Yehova.—Law 5:14-16.
SEPTEMBA 28–OKTOBA 4
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUTOKA 29-30
“Mchango wa Yehova”
it-2 764-765
Uandikishaji
Huko Sinai. Kutokana na agizo la Yehova uandikishaji wa kwanza ulifanywa Waisraeli walipokuwa wamepiga kambi huko Sinai mwezi wa pili katika mwaka wa pili baada ya kutoka Misri. Ili kumsaidia Musa kufanya kazi hiyo, mkuu mmoja alichaguliwa katika kila kabila ili kuongoza na kusimamia uandikishaji katika kabila lake. Mbali na kuwaorodhesha wanaume wote waliokuwa na zaidi ya umri wa miaka 20—ambao wangestahili kujiunga na jeshi—Sheria pia iliwapa wajibu wale walioandikishwa kulipa kodi ya kichwa ya nusu ya shekeli (dola 1 na senti 10 za Marekani) kwa ajili utumishi wa hema la ibada. (Kut 30:11-16; Hes 1:1-16, 18, 19) Jumla ya wale walioorodheshwa ilikuwa 603,550, bila kuhesabu Walawi, ambao hawangepokea urithi katika nchi. Hawakulipa kodi ya hema la ibada na hawakupaswa kwenda jeshini.—Hes 1:44-47; 2:32, 33; 18:20, 24.
it-1 502
Mchango
Baadhi ya michango ilikuwa takwa kulingana na Sheria. Musa alipowahesabu Waisraeli, kila mwanamume kuanzia umri wa miaka 20 na kuendelea alipaswa kutoa dhabihu kwa ajili ya nafsi yake, “nusu ya shekeli [karibu dola 1 na senti 10 za Marekani] kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu.” Ulikuwa “mchango wa Yehova” ili kufunika dhambi kwa ajili ya nafsi zao na “ili zitumiwe katika utumishi wa hema la mkutano.” (Kut 30:11-16) Kulingana na mwanahistoria Myahudi Yosefo (The Jewish War, VII, 218 [vi, 6]), baadaye ‘mchango huo mtakatifu’ ulilipwa kila mwaka.—2Nya 24:6-10; Mt 17:24; ona KODI.
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-1 1029 ¶4
Mkono
Kuweka Mikono. Mbali na kushika, mikono iliwekwa juu ya mtu au kitu kwa sababu mbalimbali. Hata hivyo, kimsingi kitendo hicho kilimaanisha kuweka rasmi, kuonyesha kwamba mtu au kitu kilikuwa kimekubalika, au kutambuliwa, kwa njia fulani. Katika sherehe ya kuanzishwa kwa ukuhani, Haruni na wanawe waliweka mikono yao juu ya kichwa cha ng’ombe dume na kondoo dume wawili ambao wangetolewa dhabihu, hivyo kuonyesha wanakubali kwamba wanyama hao watolewe dhabihu kwa ajili yao ili wawe makuhani wa Yehova Mungu. (Kut 29:10, 15, 19; Law 8:14, 18, 22) Alipokuwa akimweka rasmi Yoshua achukue mahali pake kufuatia amri ya Mungu, Musa aliweka mikono yake juu ya Yoshua, ambaye baada ya hapo ‘alijaa roho ya hekima’ na hivyo angeweza kuwaongoza Waisraeli kwa njia nzuri. (Kum 34:9) Mikono iliwekwa juu ya mtu ili kuonyesha kwamba angepokea baraka fulani. (Mwa 48:14; Mk 10:16) Yesu Kristo aligusa, au kuweka mikono juu ya watu fulani aliowaponya. (Mt 8:3; Mk 6:5; Lu 13:13) Pindi fulani watu walipokea zawadi ya roho takatifu mitume walipoweka mikono juu yao.—Mdo 8:14-20; 19:6.
it-1 114 ¶1
Kutiwa Mafuta
Katika Sheria ambayo Yehova alimpa Musa, alitaja hatua za kutengeneza mafuta yaliyotumiwa kumtia mtu mafuta. Yalitengenezwa kwa mchanganyiko wa pekee kwa kutumia viungo bora—manemane, mdalasini wenye harufu nzuri, kane, kida, na mafuta ya zeituni. (Kut 30:22-25) Lilikuwa kosa lililostahili adhabu ya kifo kwa mtu kutengeneza mchanganyiko huo kwa ajili ya matumizi ya kawaida au kwa makusudi ambayo hayakuwa yameidhinishwa. (Kut 30:31-33) Kwa njia ya mfano, hilo lilionyesha umuhimu na utakatifu wa kuwekwa rasmi kwenye cheo fulani ambako kulithibitishwa kupitia kutiwa mafuta kwa kutumia mafuta matakatifu.