Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
NOVEMBA 2-8
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | KUTOKA 39-40
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-2 884 ¶3-4
Ngozi ya sili
Jinsi Waisraeli Walivyozipata. Ikiwa neno la Kiebrania taʹchash katika Biblia linatumiwa kumaanisha aina fulani ya sili, huenda swali likatokea kwamba Waisraeli waliwezaje kupata ngozi za sili. Ingawa sili hupatikana hasa katika maeneo ya Aktiki na Antaktiki, baadhi ya sili wanapendelea maeneo yenye joto. Leo, sili wasio na masikio bado wanapatikana katika maeneo fulani ya Bahari ya Mediterania, na maeneo mengine yenye maji yenye joto. Kwa karne nyingi, mwanadamu amepunguza idadi ya sili, na huenda katika nyakati za Biblia wanyama hao walikuwa wengi sana katika Bahari ya Mediterania na Bahari Nyekundu. Katika mwaka wa 1832 kamusi ya Kiingereza ya Calmet inayoitwa Dictionary of the Holy Bible (uku. 139) ilisema hivi: “Sili wanapatikana katika visiwa vingi vya bahari Nyekundu, kuzunguka rasi ya Sinai.”—Ona pia Kitabu The Tabernacle’s Typical Teaching, kilichoandikwa na A. J. Pollock, London, uku. 47.
Wamisri wa kale walifanya biashara kwenye Bahari Nyekundu na bila shaka, walipokea bidhaa kutoka katika maeneo mengi ya Mediterania. Kwa hiyo, Wamisri walikuwa na uwezo wa kupata ngozi za sili. Hivyo, Waisraeli walipotoka Misri, huenda waliondoka na ngozi za sili walizomiliki, na nyingine ambazo Wamisri waliwakabidhi walipowapa vitu vingi vilivyo na thamani.—Kut 12:35, 36.
NOVEMBA 9-15
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MAMBO YA WALAWI 1-3
“Kusudi la Dhabihu”
it-2 525
Dhabihu
Dhabihu za kuteketezwa. Sehemu zote za dhabihu za kuteketezwa zilitolewa kwa Mungu; mwabudu hakubaki na sehemu yoyote. (Linganisha Amu 11:30, 31, 39, 40) Dhabihu hizo zilitia ndani kumwomba Yehova akubali, au aonyeshe kwamba amekubali dhabihu ya dhambi ambayo wakati mwingine ilitolewa pamoja na dhabihu ya kuteketezwa. Kwa kuwa Yesu Kristo anafananishwa na dhabihu ya kutekezwa alijitoa kikamili.
it-2 528 ¶4
Dhabihu
Matoleo ya nafaka. Matoleo ya nafaka yalitolewa pamoja na dhabihu za ushirika, dhabihu za kuteketezwa, na dhabihu za dhambi, na pia mazao ya kwanza; nyakati nyingine yalitolewa yenyewe tu. (Kut 29:40-42; Law 23:10-13, 15-18; Hes 15:8, 9, 22-24; 28:9, 10, 20, 26-28; sura ya 29) Dhabihu hizo zilitolewa ili kumshukuru Mungu kwa ukarimu na baraka zake. Mara nyingi zilitolewa pamoja na mafuta na ubani. Matoleo ya nafaka yalitia ndani unga laini, nafaka zilizokaangwa, au mikate ya mviringo, au mikate myembamba iliyookwa, kuchomwa, au kukaangwa. Baadhi ya matoleo ya nafaka yaliwekwa katika madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa, mengine yaliliwa na makuhani, na pia katika dhabihu za ushirika ambazo mwabudu angeshiriki kula. (Law 6:14-23; 7:11-13; Hes 18:8-11) Matoleo yoyote ya nafaka yaliyotolewa katika madhabahu hayakupaswa kuwa na chachu au “asali” (ambayo inaonekana ilikuwa umajimaji wa tini au rojo ya matunda) inayoweza kuchacha.—Law 2:1-16.
it-2 526 ¶1
Dhabihu
Dhabihu za ushirika (au matoleo ya amani). Dhabihu za ushirika zilizokubaliwa na Yehova zilithibitisha kwamba aliyetoa ana amani na Yehova. Aliyetoa dhabihu hiyo pamoja na familia yake walikula dhabihu hiyo (katika ua wa hema la ibada; kulingana na mapokeo ya Wayahudi, vibanda vilijengwa ndani ya pazia lililozunguka ua; katika hekalu, kulikuwa na vyumba vya kulia chakula). Kuhani aliyehudumu na makuhani waliokuwa na zamu walikula sehemu nyingine. Na ni kana kwamba Yehova alipokea moshi unaopendeza wa mafuta yaliyokuwa yakiteketea. Mungu alipewa pia damu ambayo huwakilisha uhai. Kwa hiyo, makuhani, Mwisraeli aliyetoa dhabihu, na Yehova walishiriki kula pamoja, kuonyesha kwamba walikuwa na uhusiano wenye amani. Mtu aliyekula akiwa mchafu (uchafu wowote uliotajwa katika Sheria) au aliyekula nyama iliyokuwa imekaa zaidi ya wakati uliotajwa (katika maeneo yenye joto nyama ilianza kuharibika) alipaswa kuuawa. Alinajisi mlo huo, kwa sababu ya kuwa mchafu au kula dhabihu inayochukiza mbele za Yehova Mungu, na hivyo kuonyesha kwamba hakuheshimu mambo matakatifu.—Law 7:16-21; 19:5-8.
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-1 813
Mafuta
Kwa nini sheria hiyo iliwekwa. Kulingana na Agano la Sheria, damu na mafuta yalitolewa kwa Yehova tu. Uhai umo katika damu, na ni Yehova tu anayeweza kuumba; basi uhai ni mali yake. (Law 17:11, 14) Mafuta yalionwa kuwa sehemu bora zaidi katika mwili wa mnyama. Kutoa mafuta ya mnyama kuwa dhabihu kulithibitisha kwamba sehemu bora zaidi ilikuwa mali ya Yehova, anayetuandalia kwa wingi, na kufanya hivyo kungeonyesha tamaa ya mwabudu kumpa Mungu kilicho bora. Kwa kuwa kufanya hivyo kulionyesha kwamba Waisraeli walikuwa tayari kumpa Yehova kilicho bora, vitu hivyo vilipoteketezwa kwenye madhabahu vilikuwa kama “chakula” na ‘harufu inayompendeza.’ (Law 3:11, 16) Hivyo, kula mafuta kulikuwa kuvunja sheria kwa kula kitu kilichotengwa kwa ajili ya Mungu, na hivyo kuingilia haki za Yehova. Mtu angeadhibiwa kifo ikiwa angekula mafuta. Hata hivyo, tofauti na damu, iliruhusiwa kutumia mafuta kwa makusudi mengine, hasa ikiwa mnyama alikufa mwenyewe au aliuawa na mnyama mwingine.—Law 7:23-25.
NOVEMBA 16-22
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MAMBO YA WALAWI 4-5
“Mpe Yehova Kilicho Bora”
it-2 527 ¶9
Dhabihu
Dhabihu za hatia. Dhabihu za hatia zilitolewa pia kwa ajili ya dhambi, kwa sababu hatia ya aina yoyote inahusisha dhambi. Zilitolewa kwa ajili ya dhambi hususa ambazo mtu alikuwa amejipatia hatia, na zilitofautiana kidogo na dhabihu nyingine za dhambi kwa kuwa inaonekana zilitumiwa kutosheleza au kurudisha haki fulani. Huenda mtu alikuwa amevunja haki ambayo Yehova anastahili au haki fulani ya taifa lake takatifu. Dhabihu za hatia zilitolewa ili kumtuliza Yehova ambaye haki yake ilikuwa imevunjwa. Zilitolewa pia ili kurudisha au kupata tena haki fulani za agano kwa ajili ya mtenda-dhambi aliyetubu na ili asiadhibiwe kwa dhambi aliyotenda.—Linganisha Isa 53:10.
it-1 1130 ¶2
Utakatifu
Wanyama na Mazao. Wazaliwa wa kwanza wa kiume wa ng’ombe, kondoo, na mbuzi walikuwa watakatifu machoni pa Yehova na hawakupaswa kukombolewa. Walipaswa kutolewa dhabihu, na makuhani waliotakaswa walipewa sehemu ya nyama hiyo. (Hes 18:17-19) Matunda ya kwanza yalikuwa matakatifu kutia ndani fungu la kumi. Dhabihu na zawadi zote zilizotakaswa kwa ajili ya utumishi wa patakatifu zilikuwa takatifu vilevile. (Kut 28:38) Vitu vyote vilivyokuwa vitakatifu kwa Yehova vilipaswa kuheshimiwa na havikupaswa kutumiwa kwa shughuli za kawaida, au kwa njia iliyovitia unajisi. Mfano mmoja ni sheria kuhusu kutoa sehemu ya kumi. Ikiwa mtu angetenga sehemu ya kumi ya zao fulani, kwa mfano, ngano, kisha yeye au mtu katika nyumba yake achukue kiasi fulani bila kukusudia kutokana na kilichotengwa na kukitumia kwa ajili ya matumizi ya nyumbani kama vile kupika, mtu huyo angekuwa na hatia ya kuvunja sheria ya Mungu kuhusu vitu vitakatifu. Sheria ilimtaka arudishe kiasi alichochukua na aongeze asilimia 20. Mbali na hilo, alipaswa pia kutoa kondoo dume asiye na kasoro kutoka kundini ili awe dhabihu. Hivyo, watu wangeendelea kuheshimu sana vitu vitakatifu vya Yehova.—Law 5:14-16.
NOVEMBA 23-29
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MAMBO YA WALAWI 6-7
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-1 833 ¶1
Moto
Matumizi kwenye hema la ibada na hekalu. Moto ulitumiwa katika ibada kwenye hema la ibada na kisha baadaye katika hekalu. Kila asubuhi na jioni kabla ya giza kuingia, kuhani mkuu alipaswa kufukiza uvumba katika madhabahu ya uvumba. (Kut 30:7, 8) Sheria ya Mungu ilisema kwamba moto katika madhabahu ya dhabihu ya kuteketezwa ulipaswa kuendelea kuwaka daima. (Law 6:12, 13) Mapokeo ya Kiyahudi yanadai kwamba moto huo katika madhabahu mwanzoni uliwashwa kimuujiza na Mungu, na ingawa jambo hilo linakubaliwa na wengi, Maandiko hayaungi mkono jambo hilo. Kulingana na mwongozo ambao Yehova alimpa Musa mwanzoni, wana wa Haruni walipaswa ‘kuweka moto kwenye madhabahu na kupanga kuni kwenye moto huo’ kabla ya kuweka dhabihu juu ya madhabahu. (Law 1:7, 8) Ilikuwa baada ya Haruni na wanawe kuwekwa rasmi kuwa makuhani, na baada ya kutolewa kwa dhabihu za kuwaweka rasmi, ndipo moto kutoka kwa Yehova, huenda kutoka kwenye wingu lililokuwa juu ya hema la ibada, ulipoteketeza dhabihu iliyokuwa juu ya madhabahu. Hivyo basi, moto uliotokea kimuujiza, haukuteketeza kuni zilizokuwa juu ya madhabahu, bali ‘uliteketeza ile dhabihu ya kuteketezwa na vile vipande vyenye mafuta vilivyokuwa kwenye madhabahu.’ Moto ulioendelea kuwaka katika madhabahu, bila shaka ulikuwa ni moto kutoka kwa Mungu uliochanganyika na moto uliokuwa tayari katika madhabahu. (Law 8:14–9:24) Pia, moto wa kimuujiza kutoka kwa Yehova uliteketeza dhabihu baada ya Sulemani kutoa sala wakati wa kuwekwa wakfu kwa hekalu.—2Nya 7:1; ona pia Amu 6:21; 1Fa 18:21-39; 1Nya 21:26 ili kupata mifano mingine ya jinsi Yehova alivyotumia moto kimuujiza kukubali dhabihu za watumishi wake.
NOVEMBA 30–DESEMBA 6
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MAMBO YA WALAWI 8-9
“Uthibitisho wa Baraka za Yehova”
it-1 1207
Kuwekwa rasmi
Musa alimwosha Haruni na wana wa Haruni, Nadabu, Abihu, Eleazari, na Ithamari (au, aliwaamuru wajioshe) katika beseni la shaba lililokuwa katika ua na kumvisha Haruni mavazi bora sana ya kuhani mkuu. (Hes 3:2, 3) Mavazi hayo maridadi ambayo Haruni alivishwa yaliwakilisha sifa na majukumu ya cheo chake. Kisha Musa akalitia mafuta hema la ibada, vyombo vyake vyote, na madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa, pamoja na beseni na vyombo vingine vyote. Kufanya hivyo kulivitakasa na kuviweka kando kwa ajili tu ya matumizi na utumishi wa Mungu. Mwishowe, Musa akamtia mafuta Haruni kwa kumimina mafuta juu ya kichwa chake.—Law 8:6-12; Kut 30:22-33; Zb 133:2.
it-1 1208 ¶8
Kuwekwa rasmi
Katika siku ya nane, kwa mara ya kwanza makuhani, wakiwa na vifaa kamili na wakiwa wamewekwa rasmi, walisimamia (bila kusaidiwa na Musa) shughuli ya kufunika dhambi za taifa la Israeli, ambalo lilihitaji sana kutakaswa si tu kwa sababu ya dhambi ya asili bali pia kwa sababu muda mfupi kabla ya hapo walikuwa wamemwasi Yehova kwa kuabudu ndama wa dhahabu, na hivyo kumkasirisha. (Law 9:1-7; Kut 32:1-10) Walipokuwa wakimalizia shughuli yao ya kwanza baada ya kuwekwa rasmi, Yehova alithibitisha kwamba alikubali na kutambua ukuhani wao kwa kushusha moto kimuujiza, bila shaka kutoka kwenye nguzo ya wingu iliyokuwa juu ya hema la ibada, na kuteketeza dhabihu yote iliyokuwa imebaki juu ya madhabahu.—Law 9:23, 24.
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-2 437 ¶3
Musa
Mungu alimweka rasmi Musa kuwa mpatanishi wa agano la Sheria alilofanya na Israeli, uhusiano wa karibu sana na Mungu ambao hakuna mtu mwingine aliwahi kuwa nao isipokuwa Yesu Kristo, Mpatanishi wa agano jipya. Musa alinyunyiza damu ya dhabihu za wanyama juu ya kitabu cha agano, ili kuwakilisha Yehova kuwa ‘sehemu’ moja, na akainyunyiza juu ya watu (bila shaka wanaume wazee waliowawakilisha) kuwa ‘sehemu’ ya pili. Baada ya kuwasomea watu kitabu cha agano, walijibu, “Mambo yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya, nasi tutatii.” (Kut 24:3-8; Ebr 9:19) Akiwa mpatanishi, Musa alikuwa na pendeleo la kusimamia ujenzi wa hema la ibada na vyombo vyake kwa kufuata maagizo aliyopewa na Mungu, na pia kuweka rasmi ukuhani kwa kutia mafuta hema la ibada na Haruni kuhani mkuu akitumia mafuta yaliyokuwa na mchanganyiko wa pekee. Kisha akawa wa kwanza kusimamia shughuli rasmi za kikuhani.—Kut sura 25-29; Law sura 8, 9.