Waamoni—Watu Waliorudisha Uhasama kwa Fadhili
JIJI la kisasa liitwalo Amman, jiji kuu la ufalme wa Hashemi wa Yordani, lahifadhi kumbukumbu la watu ambao wametoweka duniani. Wao waliitwa Waamoni. Walikuwa akina nani, nasi tunaweza kujifunza somo gani kutokana na maangamizi yao?
Waamoni walikuwa wazao wa Loti aliyekuwa mwadilifu. (Mwanzo 19:35-38) Kwa kuwa Loti alikuwa mpwa wa Abrahamu, waweza kusema kwamba Waamoni walikuwa binamu za Waisraeli. Hata hivyo, wazao wa Loti, waligeukia ibada ya miungu bandia. Na bado, Yehova Mungu aliendelea kupendezwa nao. Taifa la Israeli lilipokaribia Bara Lililoahidiwa, Mungu aliwaonya hivi: “Usiwasumbue wana wa Amoni, wala usishindane nao; kwa kuwa sitakupa katika nchi ya hao wana wa Amoni kuwa milki yako; kwa sababu nimewapa wana wa Lutu iwe milki yao.”—Kumbukumbu la Torati 2:19.
Je, Waamoni walithamini fadhili hiyo? Kwa kinyume, walikataa kwamba Yehova hakuwa amewapa kitu chochote. Wao waliorudisha uhasama wenye kuendelea kuelekea watu wa Mungu, Waisraeli, kwa upendezi wenye fadhili wa Mungu kuwaelekea. Ingawa Waisraeli waliiheshimu amri ya Yehova ya kutowashambulia, Waamoni na ndugu zao Wamoabi waliwahofu. Ni kweli, Waamoni hawakufanya shambulizi lolote la kijeshi, lakini walimwomba nabii fulani aliyeitwa Balaamu awalaani Waisraeli!—Hesabu 22:1-6; Kumbukumbu la Torati 23:3-6.
Kisha jambo lisilo la kawaida likatendeka. Biblia yaripoti kwamba Balaamu alishindwa kutamka laana yake. Aliweza tu kuwabariki, akisema: “Na abarikiwe kila akubarikiye, na alaaniwe kila akulaaniye.” (Hesabu 24:9) Wale waliohusika, kutia ndani Waamoni, walipaswa kujifunza somo lenye nguvu kutokana na jambo hilo: Wakati watu wa Mungu walipohusika, Mungu alikuwa tayari kabisa kuingilia mambo kwa niaba yao!
Ingawa hivyo, Waamoni, waliendelea kutafuta njia za kupinga Israeli. Wakati wa kipindi cha Waamuzi, Amoni lilijiunga na Moabu na Amaleki katika kulishambulia Bara Lililoahidiwa, wakifikia Yeriko. Hata hivyo, ushindi wao ukawa wa punde tu, kwa kuwa Ehudi Mwamuzi wa Israeli aliwafukuza hao washambuliaji. (Waamuzi 3:12-15, 27-30) Mapatano yasiyo thabiti yalifikia siku za Mwamuzi Yeftha. Kufikia wakati huo taifa la Israeli lilikuwa limeangukia ibada ya sanamu, hivyo Yehova akaondolea mbali ulinzi wake. Kwa miaka ipatayo 18, Mungu alikuwa ‘amewauza mikononi mwa wana wa Amoni.’ (Waamuzi 10:6-9) Kwa mara nyingine tena Waamoni walishindwa vibaya Waisraeli walipoacha ibada ya sanamu na kuunga mkono uongozi wa Yeftha.—Waamuzi 10:16–11:33.
Kipindi cha utawala wa waamuzi wa Israeli kilikwisha kwa kutawazwa kwa mfalme walo wa kwanza, Sauli. Mara tu Sauli alipoanza kutawala uhasama wa Waamoni ukatokea tena. Mfalme Nahashi akafanya shambulizi la ghafula dhidi ya jiji la Israeli la Yabesh-gileadi. Watu wa hilo jiji walipoomba amani, Nahashi Mwamoni alitoa madai haya ya kustaajabisha sana: “Kwa sharti hii mimi nitapatana nanyi, kila mtu ang’olewe jicho la kuume.” Mwanahistoria Flavio Yosefo adai kwamba sababu moja ya kufanya hivyo ilikuwa ni kujikinga, ili kwamba “jicho lao la kushoto likifunikwa na ngao zao, wawe hoi vitani.” Hata hivyo, kusudi lenyewe la mkataa huo usio na huruma lilikuwa ni kufanya Israeli kuwa kielelezo chenye kushusha hadhi.—1 Samweli 11:1, 2.
Kwa mara nyingine tena Waamoni walikuwa wamerudisha uhasama kwa fadhili za Yehova. Yehova hakupuuza shambulizi hilo lenye jeuri. “Roho ya Mungu ikamjilia Sauli kwa nguvu, hapo alipoyasikia maneno yale [ya Nahashi], na hasira yake ikawaka sana.” Chini ya mwelekezo wa roho ya Mungu, Sauli alikusanya kikosi cha watu 330,000 wenye kupigana vita ambao waliwashinda kabisa Waamoni hivi kwamba ‘hawakuachwa wawili wao pamoja.’—1 Samweli 11:6, 11.
Hali ya ubinafsi ya Waamoni ya kujitakia faida zao wenyewe, hali yao ya kukosa huruma, na pupa yao mwishowe ilifanya waharibiwe kabisa. Kama nabii wa Yehova Sefania alivyokuwa ametabiri, walikuja kuwa “kama Gomora, . . . ukiwa wa daima; . . . kwa kuwa wamewatukana watu wa BWANA wa majeshi, na kujitukuza juu yao.”—Sefania 2:9, 10.
Viongozi wa ulimwengu leo wapaswa kuona yaliyotokea kwa Amoni. Vivyo hivyo Mungu ameonyesha mataifa kiasi fulani cha fadhili kwa kuwaruhusu kuishi katika dunia, kibago chake cha miguu. Lakini badala ya kuitunza dunia, mataifa yenye ubinafsi yanaiharibu, hata yakikaribia kuiharibu kabisa kwa nyuklia. Badala ya kuonyesha fadhili kwa waabudu wa Yehova duniani, mara nyingi mataifa huonyesha uhasama, wakiwanyanyasa kikatili. Kwa hiyo somo la Waamoni ni kwamba Yehova halioni kuwa jambo dogo kuonyesha uhasama kwa fadhili yake. Na kwa wakati wake, atachukua hatua, kama alivyofanya katika nyakati za kale.—Linganisha Zaburi 2:6-12.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]
Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.
[Picha katika ukurasa wa9]
Magofu ya Waroma katika Amman, mahali pa Raba, jiji kuu la Waamoni
[Hisani]
Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.
[Picha katika ukurasa wa10]
Waamoni waliishi eneo hili
[Hisani]
Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.