Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
© 2023 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
MACHI 4-10
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | ZABURI 16-17
Hazina za Kiroho
it-2 714
Mboni ya Jicho
Neno la Kiebrania ʼi·shohnʹ (Kum 32:10; Met 7:2), linapounganishwa na neno ʽaʹyin (jicho), linamaanisha kihalisi “mtu mdogo wa jicho”; vivyo hivyo, bath (binti) linatumiwa kwenye Maombolezo 2:18 katika maana ya “binti ya jicho.” Katika visa vyote viwili maneno hayo yanarejelea mboni ya jicho. Maneno hayo mawili yanatumiwa pamoja ili kukazia maana kwenye Zaburi 17:8 (ʼi·shohnʹ bath-ʽaʹyin), kihalisi, “mtu mdogo, binti ya jicho” (“mboni ya jicho,” NW). Ni wazi kwamba hilo linarejelea picha ndogo ya umbo letu tunapojitazama katika mboni ya jicho la mtu mwingine.
Jicho ni kiungo nyeti sana; tunatambua upesi hata unywele mdogo au vumbi kidogo linapogusa mboni ya jicho. Utando wa jicho (konea) unaofunika mboni ya jicho unapaswa kulindwa na kutunzwa, kwa sababu sehemu hiyo inapojeruhiwa au kufanyiza mawingu kwa sababu ya ugonjwa, mtu hawezi kuona vizuri au anaweza kupofuka. Biblia inatumia maneno “mboni ya jicho” kwa njia yenye kupendeza ili kuonyesha kitu kinachopaswa kulindwa kwa makini. Sheria ya Mungu inapaswa kushughulikiwa hivyo. (Met 7:2) Andiko la Kumbukumbu la Torati 32:10 linapozungumzia jinsi Mungu alivyotunza taifa la Israeli kama baba, linasema alilinda taifa hilo “kama mboni ya jicho lake.” Daudi alisali kwamba Mungu amlinde na kumtunza kama “mboni ya jicho.” (Zb 17:8) Alitaka Yehova atende upesi kwa niaba yake aliposhambuliwa na maadui. (Linganisha Zek 2:8; neno la Kiebrania ba·vathʹ ʽaʹyin, “mboni ya jicho,” linatumiwa.)—Ona JICHO.
MACHI 11-17
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | ZABURI 18
“Yehova Ni . . . Mwokozi Wangu”
it-2 1161 ¶7
Sauti
Mungu husikiliza sauti ya watumishi wake. Wale wanaomtumikia Mungu kwa roho na kweli wanaweza kuwa na uhakika kwamba wanapomwita atasikia sauti yao, bila kujali wanatumia lugha gani. Isitoshe, hata ikiwa ombi litatolewa kimyakimya kwa Mungu, bila kutumia sauti halisi, Mungu, anayejua mioyo ya wanadamu, husikiliza au kuwakazia uangalifu. (Zb 66:19; 86:6; 116:1; 1Sa 1:13; Ne 2:4) Mungu husikia sauti za wanaoteseka wanapomwomba msaada. Pia anasikia sauti za wale wanaompinga na wanaopanga uovu dhidi ya watumishi wake na anajua nia yao.—Mwa 21:17; Zb 55:18, 19; 69:33; 94:9-11; Yer 23:25.
Hazina za Kiroho
it-1 432 ¶2
Makerubi
Hawakuwa na umbo lenye kutisha kama ile ya michongo ya majitu iliyo na mabawa ambayo iliabudiwa na mataifa ya kipagani iliyowazunguka, kama wengine wanavyodai. Waandishi wote Wayahudi wa kale wanasema kwa upatano kwamba makerubi hao walikuwa na umbo kama la mwanadamu [Biblia haisemi lolote kuhusu jambo hili]. Walikuwa kazi bora ya usanii, wakiwakilisha malaika wenye utukufu, na walitengenezwa kwa ‘kufuata kikamili kielelezo’ ambacho Musa alipokea kutoka kwa Yehova mwenyewe. (Kut 25:9) Mtume Paulo aliwafafanua kuwa “makerubi wenye utukufu waliokifunika kile kifuniko cha upatanisho.” (Ebr 9:5) Makerubi hao walihusianishwa na kuwepo kwa Yehova: “Nitakutokea hapo na kuzungumza nawe kutoka juu ya kifuniko hicho. Kutoka katikati ya hao makerubi wawili walio juu ya sanduku la Ushahidi.” (Kut 25:22; Hes 7:89) Kwa sababu hiyo, ilisemekana kwamba Yehova ‘anaketi juu ya makerubi.’ (1Sa 4:4; 2Sa 6:2; 2Fa 19:15; 1Nya 13:6; Zb 80:1; 99:1; Isa 37:16) Kwa njia ya mfano, makerubi hao walikuwa “mfano wa lile gari” ambalo Yehova alipanda (1Nya 28:18), na mabawa ya makerubi hao yaliwakilisha ulinzi na mwendo wa kasi wa gari hilo liliposafiri. Kwa msingi huo, Daudi alitunga wimbo wa kishairi uliofafanua mwendo wa kasi ambao Yehova alikuja kumsaidia kwa kusema “alipanda juu ya kerubi, akaja akiruka” “juu ya mabawa ya kiumbe wa roho.”—2Sa 22:11; Zb 18:10.
APRIL 15-21
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | ZABURI 29-31
Nidhamu Inaonyesha Kwamba Mungu Anatupenda
it-1 802 ¶3
Uso
‘Kuficha uso’ kunamaanisha mambo mbalimbali, kwa kutegemea hali. Yehova Mungu anapoficha uso wake mara nyingi hilo humaanisha ameondoa kibali chake au nguvu zake za kumtegemeza mtu. Huenda hilo likawa kwa sababu mtu au watu wamekosa kumtii, kama vile katika kisa cha taifa la Israeli. (Ayu 34:29; Zb 30:5-8; Isa 54:8; 59:2) Katika visa fulani, huenda ikamaanisha Yehova amekataa kujifunua kupitia matendo au kumjibu mtu, akisubiri wakati wake wa kufanya hivyo. (Zb 13:1-3) Daudi alipoomba, “ugeuze uso wako mbali na dhambi zangu,” alikuwa akimsihi Mungu asamehe au aweke mbali makosa hayo.—Zb 51:9; linganisha Zb 10:11.