-
Yehova Ni “Mfunuaji wa Siri”Mnara wa Mlinzi—2012 | Juni 15
-
-
Yehova Ni “Mfunuaji wa Siri”
“Kwa kweli Mungu wenu ni Mungu wa miungu na Bwana wa wafalme na Mfunuaji wa siri.”—DAN. 2:47.
UNGEJIBUJE?
Yehova ametufunulia mambo gani kuhusu wakati ujao?
Vichwa sita vya kwanza vya yule mnyama-mwitu vinafananisha nini?
Kuna uhusiano gani kati ya mnyama-mwitu na ile sanamu ambayo Nebukadneza aliona?
1, 2. Yehova ametufunulia nini, na kwa nini amefanya hivyo?
NI SERIKALI gani zitakazokuwa zikiitawala dunia wakati Ufalme wa Mungu utakapoukomesha utawala wa wanadamu? Tunajua jibu la swali hilo kwa sababu tumefunuliwa na Yehova Mungu ambaye ni “Mfunuaji wa siri.” Anatuwezesha kutambua serikali hizo kupitia mambo yaliyoandikwa na nabii Danieli na mtume Yohana.
2 Yehova aliwafunulia wanaume hao mfululizo wa maono kuhusu wanyama-mwitu wanaofuatana mmoja baada ya mwingine. Pia alimwambia Danieli maana ya ndoto ya kinabii kuhusu sanamu kubwa sana yenye madini mbalimbali. Yehova alihakikisha kwamba masimulizi hayo yameandikwa na kuhifadhiwa katika Biblia kwa faida yetu. (Rom. 15:4) Alifanya hivyo ili kuimarisha tumaini letu la kwamba hivi karibuni Ufalme wake utazivunja serikali zote za wanadamu.—Dan. 2:44.
3. Ili kuelewa unabii kwa usahihi, tunahitaji kuelewa nini kwanza, na kwa nini?
3 Kwa ujumla, masimulizi ya Danieli na Yohana hayafunui tu kuhusu wafalme wanane, au serikali za wanadamu, bali pia yanaonyesha jinsi ambavyo serikali hizo zingefuatana. Hata hivyo, tunaweza kuelewa kwa usahihi unabii huo mbalimbali ikiwa tu tunaelewa maana ya unabii wa kwanza kabisa ulioandikwa katika Biblia. Kwa nini? Kwa sababu kutimizwa kwa unabii huo ndilo jambo kuu linalokaziwa katika Biblia yote. Katika njia fulani, unabii mwingine wote unategemea unabii huo wa kwanza.
UZAO WA NYOKA NA MNYAMA-MWITU
4. Uzao wa mwanamke unatia ndani nani, na uzao huo utafanya nini?
4 Mara tu baada ya uasi katika Edeni, Yehova alitoa ahadi ya kwamba “mwanamke” angetokeza “uzao.”a (Soma Mwanzo 3:15.) Mwishowe, uzao huo ungemponda nyoka kichwa, yaani, Shetani. Baadaye, Yehova alifunua kwamba uzao huo ungetokana na Abrahamu, ungetoka katika taifa la Israeli, katika kabila la Yuda, na katika ukoo wa Mfalme Daudi. (Mwa. 22:15-18; 49:10; Zab. 89:3, 4; Luka 1:30-33) Kristo Yesu ndiye aliyekuwa sehemu ya msingi ya uzao huo. (Gal. 3:16) Washiriki wa kutaniko la Kikristo waliotiwa mafuta kwa roho ndio sehemu ya pili ya uzao huo. (Gal. 3:26-29) Yesu na hao watiwa-mafuta wanaungana kufanyiza Ufalme wa Mungu ambao utatumiwa na Mungu kumponda Shetani.—Luka 12:32; Rom. 16:20.
5, 6. (a) Danieli na Yohana wanataja serikali ngapi kuu? (b) Vichwa vya yule mnyama-mwitu wa kitabu cha Ufunuo vinafananisha nini?
5 Unabii huo wa kwanza uliotolewa katika Edeni ulisema pia kwamba Shetani angetokeza “uzao.” Uzao wake ungeonyesha uadui, au chuki, kuelekea uzao wa mwanamke. Uzao wa nyoka ni nani? Ni wote wanaomwiga Shetani kwa kumchukia Mungu na kuwapinga watu wa Mungu. Katika historia yote, Shetani amepanga uzao wake katika makundi mbalimbali ya kisiasa, au falme. (Luka 4:5, 6) Hata hivyo, ni falme chache sana za wanadamu ambazo zimejitahidi sana kuwapinga watu wa Mungu, iwe ni taifa la Israeli au kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta. Kwa nini jambo hilo ni muhimu? Kwa sababu linaeleza kwa nini maono ya Danieli na Yohana yanafafanua jumla ya falme nane kuu peke yake.
6 Mwishoni mwa karne ya kwanza W.K., Yesu aliyefufuliwa alimpa mtume Yohana mfululizo wa maono yenye kustaajabisha. (Ufu. 1:1) Katika moja ya maono hayo, Yohana alimwona Ibilisi, anayefananishwa na joka mkubwa, akiwa amesimama kwenye ufuo wa bahari kubwa. (Soma Ufunuo 13:1, 2.) Yohana aliona pia mnyama-mwitu wa ajabu akipanda kutoka katika bahari hiyo, naye akapokea mamlaka kubwa kutoka kwa Ibilisi. Baadaye malaika anamwambia Yohana kwamba vichwa saba vya mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu, ambaye ni mfano wa mnyama-mwitu anayetajwa kwenye Ufunuo 13:1, vinafananisha “wafalme saba,” au serikali. (Ufu. 13:14, 15; 17:3, 9, 10) Yohana alipoandika maneno hayo, wafalme watano kati yao walikuwa tayari wameanguka, mmoja alikuwa akitawala wakati huo, na mmoja alikuwa “bado hajafika.” Falme au serikali hizo kuu za ulimwengu ni zipi? Acheni tuchunguze kila kichwa cha mnyama-mwitu huyo anayezungumziwa katika kitabu cha Ufunuo. Tutaona pia jinsi maandishi ya Danieli yalivyotaja mambo mengine ya ziada ambayo ni muhimu kuhusu nyingi kati ya falme hizo, na alitabiri baadhi ya mambo hayo karne nyingi kabla falme hizo hazijatokea.
VICHWA VIWILI VYA KWANZA —MISRI NA ASHURU
7. Kichwa cha kwanza kinafananisha nini, na kwa nini?
7 Kichwa cha kwanza cha huyo mnyama-mwitu kinafananisha Misri. Kwa nini? Kwa sababu Misri ilikuwa serikali ya kwanza kuu kuonyesha uadui dhidi ya watu wa Mungu. Wazao wa Abrahamu, ambao kupitia kwao uzao ulioahidiwa wa mwanamke ungetokea, waliongezeka na kuwa wengi huko Misri. Kisha, Misri ikaanza kuwakandamiza Waisraeli. Shetani alijaribu kuwafagilia mbali watu wa Mungu kabla ya uzao huo kutokea. Jinsi gani? Kwa kumchochea Farao awaangamize watoto wote wa kiume Waisraeli. Yehova alizuia jaribio hilo naye akawaweka huru watu wake kutoka utumwani huko Misri. (Kut. 1:15-20; 14:13) Baadaye akawawezesha Waisraeli waimiliki Nchi ya Ahadi.
8. Kichwa cha pili kinafananisha nini, na kilijaribu kufanya nini?
8 Kichwa cha pili cha yule mnyama-mwitu kinafananisha Ashuru. Ufalme huo wenye nguvu ulijaribu pia kuwafagilia mbali watu wa Mungu. Ni kweli kwamba Yehova aliutumia ufalme wa Ashuru ili kuuadhibu ufalme wa makabila kumi ya Israeli kwa sababu ya ibada ya sanamu na uasi wao. Hata hivyo, ufalme wa Ashuru ulilishambulia jiji la Yerusalemu. Huenda Shetani alikuwa na lengo la kuuangamiza kabisa ukoo wa kifalme ambao mwishowe ungetokeza Yesu. Shambulizi hilo halikuwa sehemu ya kusudi la Yehova, na kwa sababu hiyo aliwakomboa kimuujiza watu wake waaminifu kwa kuwaharibu wavamizi.—2 Fal. 19:32-35; Isa. 10:5, 6, 12-15.
KICHWA CHA TATU—BABILONI
9, 10. (a) Yehova aliwaruhusu Wababiloni wafanye nini? (b) Ili unabii utimie, ilikuwa lazima mambo gani yatukie?
9 Kichwa cha tatu cha mnyama-mwitu ambaye Yohana aliona kinafananisha ufalme wenye mji mkuu ulioitwa Babiloni. Yehova aliwaruhusu Wababiloni walishinde jiji la Yerusalemu na kuwapeleka watu wake utekwani. Hata hivyo, kabla ya kuruhusu Waisraeli waaibishwe kwa njia hiyo, Yehova aliwaonya watu hao walioasi kwamba msiba huo ungewapata. (2 Fal. 20:16-18) Alitabiri kwamba ukoo wa wafalme wa kibinadamu ambao ilisemekana kwamba wanaketi juu ya “kiti cha ufalme cha Yehova” huko Yerusalemu ungeondolewa. (1 Nya. 29:23) Hata hivyo, Yehova pia aliahidi kwamba mzao wa Mfalme Daudi, mzao ambaye alikuwa na “haki ya kisheria,” angekuja na kuchukua mamlaka hayo.—Eze. 21:25-27.
10 Unabii mwingine ulionyesha kwamba bado Wayahudi wangekuwa wakiabudu kwenye hekalu la Yerusalemu wakati wa kuja kwa Masihi au Mtiwa-Mafuta aliyeahidiwa. (Dan. 9:24-27) Unabii fulani ulioandikwa mapema kabla ya Waisraeli kupelekwa utekwani Babiloni, ulisema kwamba huyo Masihi angezaliwa Bethlehemu. (Mika 5:2) Ili unabii huo mbalimbali utimie, Wayahudi wangehitaji kuwekwa huru kutoka utekwani, warudi katika nchi yao, na kujenga upya hekalu. Lakini sheria za Wababiloni hazikuruhusu mateka waachiliwe huru. Tatizo hilo lingetatuliwaje? Yehova aliwafunulia manabii wake jibu la swali hilo.—Amo. 3:7.
11. Ni mifano gani mbalimbali inayotumiwa kufananisha Milki ya Babiloni? (Tazama maelezo ya chini.)
11 Nabii Danieli alikuwa miongoni mwa mateka waliopelekwa Babiloni. (Dan. 1:1-6) Yehova alimtumia kufunua jinsi ambavyo falme zingefuatana baada ya serikali hiyo kuu ya ulimwengu kuanguka. Yehova alifunua siri hizo akitumia mifano mbalimbali. Kwa mfano, alimletea Mfalme Nebukadneza wa Babiloni ndoto kuhusu sanamu kubwa sana ambayo ilitengenezwa kwa madini ya aina mbalimbali. (Soma Danieli 2:1, 19, 31-38.) Kupitia Danieli, Yehova alifunua kwamba kichwa cha dhahabu cha sanamu hiyo kilifananisha Milki ya Babiloni.b Serikali kuu ya ulimwengu iliyotawala baada ya Babiloni ilifananishwa na kifua na mikono ya fedha. Ingekuwa serikali gani hiyo, na ingewatendeaje watu wa Mungu?
KICHWA CHA NNE—UMEDI NA UAJEMI
12, 13. (a) Yehova alifunua nini kuhusu kushindwa kwa Babiloni? (b) Kwa nini serikali ya Umedi na Uajemi inafananishwa kwa kufaa na kichwa cha nne cha yule mnyama-mwitu?
12 Kwa zaidi ya karne moja kabla ya siku za Danieli, Yehova alifunua kupitia nabii Isaya maelezo mengi kuhusu serikali kuu ya ulimwengu ambayo ingeshinda Babiloni. Yehova hakufunua tu jinsi ambavyo jiji la Babiloni lingeshindwa bali pia alifunua jina la yule ambaye angelishinda jiji hilo. Kiongozi huyo aliitwa Koreshi Mwajemi. (Isa. 44:28–45:2) Danieli alipata maono mengine mawili kuhusu Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Umedi na Uajemi. Katika moja ya maono hayo, ufalme huo ulifananishwa na dubu ambaye ameinuliwa upande mmoja. Dubu huyo aliambiwa ‘ale nyama nyingi.’ (Dan. 7:5) Katika maono tofauti, Danieli aliona serikali hiyo pacha ya ulimwengu yenye wafalme wawili ikifananishwa na kondoo-dume mwenye pembe mbili.—Dan. 8:3, 20.
13 Yehova aliitumia Milki ya Umedi na Uajemi kutimiza unabii kwa kuishinda Babiloni na kuwarudisha Waisraeli kwenye nchi yao. (2 Nya. 36:22, 23) Hata hivyo, baadaye serikali hiyo kuu ilikuwa karibu kuwafagilia mbali watu wa Mungu. Kitabu cha Biblia cha Esta kinaeleza kuhusu njama fulani iliyopangwa na waziri mkuu wa Uajemi, aliyeitwa Hamani. Alipanga njama ili Wayahudi wote walioishi katika Milki kubwa sana ya Uajemi waangamizwe naye akapanga tarehe hususa ya kuwaangamiza Wayahudi wote. Hata hivyo, kwa mara nyingine tena Yehova aliingilia kati na kuwalinda watu Wake kutokana na chuki ya uzao wa Shetani. (Esta 1:1-3; 3:8, 9; 8:3, 9-14) Kwa hiyo, serikali ya Umedi na Uajemi inafananishwa kwa kufaa na kichwa cha nne cha mnyama-mwitu wa kitabu cha Ufunuo.
KICHWA CHA TANO—UGIRIKI
14, 15. Yehova anafunua mambo gani kuhusu Milki ya kale ya Ugiriki?
14 Kichwa cha tano cha mnyama-mwitu wa kitabu cha Ufunuo kinafananisha Ugiriki. Kama Danieli alivyokuwa amefunua mapema alipofasiri ndoto ya Nebukadneza, serikali hiyo kuu inafananishwa pia na tumbo na mapaja ya shaba ya ile sanamu. Danieli alipata pia maono mawili ambayo yanafunua mambo mengi yenye kustaajabisha kuhusu milki hiyo na kuhusu mtawala wake aliyekuwa maarufu zaidi.
15 Katika moja ya maono hayo, Danieli aliona milki ya Ugiriki ambayo ilifananishwa na chui mwenye mabawa manne, kuonyesha kwamba milki hiyo ingeshinda kwa kasi sana. (Dan. 7:6) Katika maono mengine, Danieli alieleza jinsi mbuzi mwenye pembe moja kubwa anavyomuua haraka kondoo-dume mwenye pembe mbili, yaani, Umedi na Uajemi. Yehova alimwambia Danieli kwamba mbuzi huyo alifananisha Ugiriki na ile pembe kubwa ilifananisha mmoja wa wafalme wake. Vilevile, Danieli alisema kwamba ile pembe kubwa ingevunjwa na kisha pembe nne ndogo zaidi zingekua au kutokea mahali pake. Hata ingawa unabii huo uliandikwa miaka mingi sana kabla ya Ugiriki kuanza kutawala, kila jambo lilitimia. Aleksanda Mkuu, mfalme maarufu zaidi wa Milki ya kale ya Ugiriki, aliongoza mashambulizi dhidi ya Umedi na Uajemi. Hata hivyo, pembe hiyo ilivunjika mara moja wakati mfalme huyo mkuu alipokufa akiwa katika upeo wa mamlaka yake na akiwa na umri wa miaka 32 tu. Kisha, ufalme wake uligawanyika mwishowe na kuchukuliwa na majenerali wake wanne.—Soma Danieli 8:20-22.
16. Antioko wa Nne alifanya nini?
16 Baada ya kushinda Uajemi, serikali ya Ugiriki ilitawala nchi ya watu wa Mungu. Wakati huo, Wayahudi walimiliki tena Nchi ya Ahadi na kujenga upya hekalu huko Yerusalemu. Bado walikuwa watu waliochaguliwa na Mungu, na hekalu lililojengwa upya bado lilikuwa kitovu cha ibada ya kweli. Hata hivyo, katika karne ya pili K.W.K., kichwa cha tano cha mnyama-mwitu, yaani, serikali ya Ugiriki iliwashambulia watu wa Mungu. Antioko wa Nne, mmoja wa warithi wa milki ya Aleksanda iliyogawanyika, alijenga madhabahu ya kipagani kwenye uwanja wa hekalu huko Yerusalemu na akaagiza kwamba mtu yeyote aliyefuata dini ya Kiyahudi alikuwa na hatia iliyostahili adhabu ya kifo. Uzao wa Shetani ulitenda kwa njia ya chuki kama nini! Hata hivyo, muda si muda, Ugiriki iling’olewa kuwa serikali kuu ya ulimwengu. Ni serikali gani ingekuwa kichwa cha sita cha yule mnyama-mwitu?
KICHWA CHA SITA CHENYE ‘KUOGOPESHA NA KUTISHA’—ROMA
17. Kichwa cha sita kilitimiza sehemu gani kubwa katika utimizo wa Mwanzo 3:15?
17 Roma ndiyo iliyokuwa serikali kuu ya ulimwengu wakati Yohana alipopata maono ya yule mnyama-mwitu. (Ufu. 17:10) Kichwa hicho cha sita kilitimiza sehemu kubwa katika utimizo wa unabii ulioandikwa katika Mwanzo 3:15. Shetani aliwatumia maofisa Waroma kuupiga na kuulemaza kwa muda ule uzao, kwa kuutia jeraha “kwenye kisigino.” Jinsi gani? Walimhukumu Yesu kwa mashtaka ya uwongo ya uchochezi na kuagiza auawe. (Mt. 27:26) Lakini punde si punde, jeraha hilo lilipona kwa sababu Yehova alimfufua Yesu.
18. (a) Yehova alichagua taifa gani jipya, na kwa nini? (b) Uzao wa nyoka uliendelea jinsi gani kuonyesha chuki dhidi ya uzao wa mwanamke?
18 Viongozi wa kidini katika Israeli walishirikiana na Roma kumpinga Yesu, na pia watu wengi katika taifa hilo wakamkataa. Kwa hiyo, Yehova aliwakataa Waisraeli wa asili wasiwe watu wake. (Mt. 23:38; Mdo. 2:22, 23) Kisha akachagua taifa jipya, “Israeli wa Mungu.” (Gal. 3:26-29; 6:16) Taifa hilo lilikuwa kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta ambalo lilitia ndani Wayahudi pamoja na watu wasio Wayahudi. (Efe. 2:11-18) Baada ya kifo na ufufuo wa Yesu, uzao wa nyoka uliendelea kuonyesha chuki dhidi ya uzao wa mwanamke. Mara nyingi, serikali ya Roma ilijaribu kufagilia mbali kutaniko la Kikristo, sehemu ya pili ya ule uzao.c
19. (a) Danieli anaeleza nini kuhusu serikali ya sita kuu ya ulimwengu? (b) Makala nyingine itazungumzia nini?
19 Katika ndoto ambayo Danieli alimfasiria Nebukadneza, Roma inafananishwa na miguu ya chuma. (Dan. 2:33) Danieli aliona pia maono ambayo hayafunui tu kuhusu Milki ya Roma bali pia serikali kuu ya ulimwengu inayofuata ambayo ingetokana na Roma. (Soma Danieli 7:7, 8.) Kwa karne nyingi, maadui wa serikali ya Roma waliiona serikali hiyo kuwa yenye ‘kuogopesha na kutisha na yenye nguvu isivyo kawaida.’ Hata hivyo, unabii ulitabiri kwamba zile “pembe kumi” zingekua kutokana na milki hiyo na pembe moja hasa ingepata umaarufu. Hizo pembe kumi zinafananisha nini, na ile pembe ndogo inafananisha nini? Ile pembe ndogo inalinganaje na maelezo kuhusu ile sanamu kubwa ambayo Nebukadneza aliona? Makala iliyo kwenye ukurasa wa 14 itajibu maswali hayo.
[Maelezo ya Chini]
a Mwanamke huyo anafananisha tengenezo la Yehova ambalo ni kama mke, linalofanyizwa na viumbe wa roho walio mbinguni.—Isa. 54:1; Gal. 4:26; Ufu. 12:1, 2.
b Babiloni inafananishwa na kichwa cha ile sanamu katika kitabu cha Danieli na pia kichwa cha tatu cha yule mnyama-mwitu wa kitabu cha Ufunuo. Tazama chati kwenye ukurasa wa 12-13.
c Ingawa Roma iliharibu Yerusalemu mwaka wa 70 W.K., shambulizi hilo halikuwa sehemu ya utimizo wa andiko la Mwanzo 3:15. Kufikia wakati huo, Waisraeli wa asili hawakuwa tena taifa lililochaguliwa na Mungu.
-
-
Yehova Anafunua Mambo Ambayo “Lazima Yatendeke Upesi”Mnara wa Mlinzi—2012 | Juni 15
-
-
Yehova Anafunua Mambo Ambayo “Lazima Yatendeke Upesi”
“Ufunuo kupitia Yesu Kristo, ambao Mungu alimpa, kuwaonyesha watumwa wake mambo ambayo lazima yatendeke upesi.”—UFU. 1:1.
UNGEJIBUJE?
Ni sehemu gani za ile sanamu kubwa sana zinazofananisha Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani?
Yohana anaonyeshaje uhusiano uliopo kati ya Umoja wa Mataifa na Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani?
Danieli na Yohana wanaonyeshaje mwisho wa utawala wa wanadamu?
1, 2. (a) Unabii wa Danieli na Yohana unatuwezesha kufanya nini? (b) Vichwa sita vya kwanza vya yule mnyama-mwitu vinafananisha nini?
UNABII wa Danieli na Yohana unalingana katika njia ambazo zinatuwezesha kuelewa maana ya mambo mengi yanayotukia sasa ulimwenguni na yale ambayo yatatukia wakati ujao. Tunaweza kujifunza nini tunapolinganisha maono ya Yohana kuhusu mnyama-mwitu, simulizi la Danieli kuhusu mnyama wa kutisha mwenye pembe kumi, na ufasiri wa Danieli kuhusu ile sanamu kubwa? Na uelewaji sahihi wa unabii huo mbalimbali unapaswa kutuchochea kufanya nini?
2 Acheni tuzungumzie maono ya Yohana kuhusu yule mnyama-mwitu. (Ufu., sura ya 13) Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, vichwa sita vya kwanza vya mnyama huyo vinafananisha Misri, Ashuru, Babiloni, Umedi na Uajemi, Ugiriki, na Roma. Serikali hizo zote zilionyesha chuki dhidi ya uzao wa mwanamke. (Mwa. 3:15) Kichwa cha sita, yaani, Roma, kiliendelea kuwa serikali kuu ya ulimwengu kwa karne nyingi baada ya Yohana kuandika maono yake. Mwishowe, kichwa cha saba kingechukua mahali pa Roma. Kichwa hicho kilithibitika kuwa serikali gani kuu ya ulimwengu, na kingeutendeaje uzao wa mwanamke?
UINGEREZA NA MAREKANI ZAPATA MAMLAKA
3. Yule mnyama anayetisha mwenye pembe kumi anafananisha nini, na pembe kumi zinafananisha nini?
3 Tunaweza kutambua kichwa cha saba cha yule mnyama-mwitu wa kitabu cha Ufunuo sura ya 13 kwa kulinganisha maono ya Yohana na maono ya Danieli kuhusu yule mnyama anayetisha mwenye pembe kumi.a (Soma Danieli 7:7, 8, 23, 24.) Mnyama huyo ambaye Danieli aliona anafananisha Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Roma. (Tazama chati kwenye ukurasa wa 12-13.) Katika karne ya tano W.K., Milki ya Roma ilianza kusambaratika. Pembe kumi zinazoota kwenye kichwa cha mnyama huyo mwenye kuogopesha zinafananisha falme zilizotokana na milki hiyo.
4, 5. (a) Pembe ndogo ilifanya nini? (b) Kichwa cha saba cha yule mnyama-mwitu kinafananisha nini?
4 Ni pembe nne, au falme nne tu kati ya falme zilizoota kwenye kichwa cha mnyama huyo mkali ndizo zinazozungumziwa kwa njia ya pekee. Pembe tatu zinang’olewa na pembe nyingine “ndogo.” Unabii huo ulitimia wakati Uingereza, ambayo zamani ilikuwa nchi ndogo chini ya Milki ya Roma, ilipoibuka na kuwa maarufu. Kufikia karne ya 17, Uingereza ilikuwa serikali isiyo na nguvu sana. Nchi nyingine tatu katika Milki ya kale ya Roma, yaani, Hispania, Uholanzi, na Ufaransa, zilikuwa na uvutano zaidi. Uingereza iling’oa serikali hizo moja baada ya nyingine, ikaziondoa kwenye vyeo hivyo vya kifahari. Kufikia katikati ya karne ya 18, Uingereza ilikuwa ikielekea kuwa serikali kuu ya ulimwengu. Lakini bado haikuwa kichwa cha saba cha yule mnyama-mwitu.
5 Ingawa Uingereza ilipata mamlaka, nchi zilizokuwa chini ya ukoloni wake huko Amerika Kaskazini zilijitenga. Hata hivyo, Uingereza haikuizuia Marekani kuendelea kupata nguvu, na Marekani ililindwa na jeshi la wanamaji la Uingereza. Siku ya Bwana ilipoanza mwaka wa 1914, Uingereza ilikuwa imejenga milki kubwa zaidi katika historia na Marekani ilikuwa sasa nchi iliyositawi zaidi kiviwanda duniani.b Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, Marekani ilikuwa imesitawisha uhusiano wa pekee na Uingereza. Kichwa cha saba cha yule mnyama sasa kilikuwa kimeibuka kikiwa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Kichwa hicho kiliutendeaje uzao wa mwanamke?
6. Kichwa cha saba kimewatendeaje watu wa Mungu?
6 Muda mfupi baada ya kuanza kwa siku ya Bwana, kichwa cha saba kiliwashambulia watu wa Mungu, ndugu za Kristo waliobaki duniani. (Mt. 25:40) Yesu alisema kwamba wakati wa kuwapo kwake, washiriki waliobaki wa ule uzao wangekuwa wakifanya kazi kwa bidii duniani. (Mt. 24:45-47; Gal. 3:26-29) Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani ilipigana vita na watakatifu hao. (Ufu. 13:3, 7) Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, serikali hiyo iliwakandamiza watu wa Mungu, ikapiga marufuku baadhi ya machapisho yao, na kuwatupa gerezani wawakilishi wa jamii ya mtumwa mwaminifu. Ni kana kwamba kichwa cha saba cha mnyama-mwitu kilikomesha kazi ya kuhubiri kwa kipindi fulani. Yehova aliona mapema tukio hilo la ajabu na kumfunulia Yohana. Pia, Mungu alimwambia Yohana kwamba sehemu ya pili ya ule uzao ingepewa uhai tena na kushiriki kwa bidii zaidi katika utendaji wa kiroho. (Ufu. 11:3, 7-11) Historia ya kisasa ya watumishi wa Yehova inathibitisha kwamba mambo hayo yalitukia kama ilivyotabiriwa.
SERIKALI KUU YA ULIMWENGU YA UINGEREZA NA MAREKANI NA MIGUU YA CHUMA NA UDONGO
7. Kuna uhusiano gani kati ya kichwa cha saba cha mnyama-mwitu na ile sanamu kubwa sana?
7 Kuna uhusiano gani kati ya kichwa cha saba cha mnyama-mwitu na ile sanamu kubwa sana? Uingereza, kutia ndani na Marekani, zilitokana na Milki ya Roma. Hata hivyo, namna gani miguu ya hiyo sanamu? Biblia inasema kwamba miguu hiyo ni mchanganyiko wa chuma na udongo. (Soma Danieli 2:41-43.) Maelezo hayo kuhusu miguu yanatimia kipindi kilekile ambacho kichwa cha saba, yaani, Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani inapoibuka na kupata umaarufu. Kama vile ambavyo kitu kilichotengenezwa kwa mchanganyiko wa chuma na udongo kilivyo dhaifu kuliko kitu kilichotengenezwa kwa chuma tu, vivyo hivyo pia Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani ni dhaifu kuliko serikali ambayo ilitokana nayo. Hilo lilitukia jinsi gani?
8, 9. (a) Serikali kuu ya saba ya ulimwengu ilionyesha jinsi gani nguvu kama za chuma? (b) Udongo ulio katika miguu ya ile sanamu unafananisha nini?
8 Nyakati nyingine, kichwa cha saba cha mnyama huyo kimeonyesha nguvu kama za chuma. Kwa mfano, kilithibitisha kwamba kina nguvu kiliposhinda Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Katika Vita vya Pili vya Ulimwengu, kichwa cha saba kilionyesha pia nguvu kama za chuma.c Hata baada ya vita hivyo, mara kwa mara kichwa cha saba kilionyesha nguvu kama za chuma. Hata hivyo, tangu mwanzoni, chuma hicho kimechanganyika na udongo.
9 Kwa muda mrefu watumishi wa Yehova wamekuwa wakijitahidi kuelewa kile ambacho miguu ya sanamu hiyo inafananisha. Andiko la Danieli 2:41 linasema kwamba mchanganyiko wa chuma na udongo ni “ufalme,” mmoja, si falme nyingi. Kwa hiyo, udongo unafananisha vitu fulani katika utawala wa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani, ambavyo vinaifanya iwe dhaifu zaidi kuliko Milki ya Roma iliyokuwa na nguvu kama chuma ambacho hakijachanganywa na kitu kingine chochote. Udongo unafananisha “uzao wa wanadamu,” au watu wa kawaida. (Dan. 2:43) Katika Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani, watu wameinuka na kudai haki zao kupitia kampeni za kupigania haki za raia, vyama vya wafanyakazi, na harakati za kutafuta uhuru. Watu wa kawaida wanafanya iwe vigumu kwa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani kutenda kwa nguvu kama za chuma. Pia, maoni ya kisiasa yanayopingana na matokeo ya uchaguzi yanayokaribiana na ambayo hayaonyeshi wazi mshindi yamedhoofisha uwezo wa hata viongozi maarufu, hivi kwamba hawana mamlaka ya kutekeleza sera zao. Danieli alitabiri hivi: “Sehemu moja ya ufalme huo itakuwa yenye nguvu na nyingine itakuwa dhaifu.”—Dan. 2:42; 2 Tim. 3:1-3.
10, 11. (a) Ni nini kitakachoipata “miguu” ya ile sanamu? (b) Tunaweza kukata kauli gani kuhusu idadi ya vidole vya miguu?
10 Katika karne ya 21, serikali ya Uingereza na ya Marekani zimeendelea kuwa na uhusiano wa pekee, na mara nyingi zinashirikiana katika kushughulikia masuala ya ulimwengu. Unabii mbalimbali kuhusu ile sanamu kubwa sana na yule mnyama-mwitu unathibitisha kwamba wakati ujao hapatakuwa na serikali nyingine kuu ya ulimwengu ambayo itachukua mahali pa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Huenda serikali hiyo kuu ya mwisho ya ulimwengu ya Uingereza na Marekani ikawa dhaifu zaidi kuliko serikali inayofananishwa na ile miguu ya chuma, lakini serikali hiyo haitavunjika yenyewe.
11 Je, idadi ya vidole vya miguu vya sanamu hiyo vina maana ya pekee? Fikiria jambo hili: Katika maono mengine, Danieli anataja idadi hususa, kwa mfano, idadi ya pembe zilizo kwenye vichwa vya wanyama mbalimbali. Idadi hizo zina maana. Hata hivyo, anapoeleza kuhusu ile sanamu, Danieli hataji idadi ya vidole vya miguu. Kwa hiyo, inaonekana kwamba idadi hiyo si muhimu sana kama vile ambavyo idadi ya mikono, vidole, miguu, na nyayo za sanamu hiyo si muhimu. Danieli anataja kihususa kwamba vidole vya miguu vingekuwa mchanganyiko wa chuma na udongo. Kutokana na maelezo yake, tunaweza kukata kauli kwamba Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani ndiyo itakayokuwa ikitawala wakati ambapo “jiwe” linalofananisha Ufalme wa Mungu litakapoipiga miguu ya sanamu hiyo.—Dan. 2:45.
SERIKALI YA UINGEREZA NA MAREKANI NA MNYAMA-MWITU MWENYE PEMBE MBILI
12, 13. Mnyama-mwitu mwenye pembe mbili anafananisha nini, naye anafanya nini?
12 Ingawa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani ni mchanganyiko wa chuma na udongo, maono ambayo Yesu alimpa Yohana yanaonyesha kwamba serikali hiyo ingeendelea kutimiza sehemu kubwa katika siku za mwisho. Jinsi gani? Yohana aliona maono ya mnyama-mwitu mwenye pembe mbili ambaye alisema kama joka mkubwa. Mnyama huyo wa ajabu anafananisha nini? Ana pembe mbili, kwa hiyo ni serikali pacha. Yohana anaona tena Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani lakini sasa ikitimiza daraka fulani la pekee.—Soma Ufunuo 13:11-15.
13 Mnyama-mwitu huyo anawachochea watu watengeneze sanamu ya mnyama-mwitu. Yohana aliandika kwamba sanamu ya huyo mnyama ingetokea, ingetoweka, na kisha kuinuka tena. Hivyo ndivyo ilivyotukia hasa kwa shirika lililoanzishwa na Uingereza na Marekani, lililokusudiwa kuziunganisha na kuziwakilisha falme za ulimwengu.d Shirika hilo lilitokea baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu na liliitwa Ushirika wa Mataifa. Shirika hilo likatoweka wakati Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipoanza. Wakati wa vita hivyo, watu wa Mungu walitangaza kwamba sanamu ya mnyama-mwitu ingeinuka tena kulingana na unabii wa kitabu cha Ufunuo. Na kwa kweli sanamu hiyo iliinuka tena ikiwa Umoja wa Mataifa.—Ufu. 17:8.
14. Ni katika maana gani sanamu ya yule mnyama-mwitu ni “mfalme wa nane”?
14 Yohana alieleza kwamba ile sanamu ya mnyama ni “mfalme wa nane.” Katika maana gani? Mnyama huyo haonyeshwi akiwa kichwa cha nane cha yule mnyama-mwitu wa kwanza. Yeye ni sanamu tu ya mnyama huyo. Nguvu zozote ambazo sanamu hiyo inazo zinatoka kwa mataifa ambayo ni wanachama wa shirika hilo, hasa kutoka kwa mtegemezaji wake mkubwa, Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. (Ufu. 17:10, 11) Lakini sanamu hiyo inapokea mamlaka ya kutenda kama mfalme ili kutimiza jukumu fulani hususa, jukumu ambalo litasababisha mfuatano wa matukio yatakayobadili historia ya ulimwengu.
SANAMU YA MNYAMA INAMWANGAMIZA KAHABA
15, 16. Kahaba anafananisha nini, na imekuwaje kwa watu wanaomuunga mkono leo?
15 Yohana anasema kwamba kahaba wa mfano ameketi juu ya au anamtawala mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu, yaani, sanamu ya yule mnyama-mwitu. Kahaba huyo anaitwa “Babiloni Mkubwa.” (Ufu. 17:1-6) Kwa kufaa, kahaba huyo anafananisha dini yote ya uwongo, hasa makanisa ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Mashirika ya kidini yameibariki sanamu ya yule mnyama na yamejaribu kuiongoza.
16 Hata hivyo, katika siku ya Bwana, Babiloni Mkubwa ameona maji yakikauka, yaani, watu ambao wanamuunga mkono wakipungua kabisa. (Ufu. 16:12; 17:15) Kwa mfano, sanamu ya yule mnyama-mwitu ilipotokea kwanza, sehemu ya Babiloni Mkubwa yenye uvutano mkubwa, yaani, makanisa ya dini zinazodai kuwa za Kikristo, ilitawala nchi za Magharibi. Leo, makanisa na wahudumu wake hawaheshimiwi wala kuungwa mkono na watu kwa ujumla. Ukweli ni kwamba watu wengi wanaamini kwamba dini inachangia au kusababisha vita. Kikundi fulani cha wasomi wa nchi za Magharibi wanaopinga vikali dini, kinawahimiza watu wakomeshe uvutano wa dini katika jamii.
17. Ni nini kitakachotukia kwa dini ya uwongo hivi karibuni, na kwa nini?
17 Hata hivyo, dini ya uwongo haitapoteza mamlaka yake hatua kwa hatua na kisha kutoweka tu. Kahaba huyo ataendelea kuwa na uvutano wenye nguvu na kujaribu kuwashawishi wafalme wafanye jinsi anavyotaka mpaka Mungu atakapotia wazo fulani ndani ya mioyo ya wenye mamlaka. (Soma Ufunuo 17:16, 17.) Hivi karibuni Yehova atasababisha sehemu za kisiasa za mfumo wa Shetani, ambazo zinawakilishwa na Umoja wa Mataifa, ziishambulie dini ya uwongo. Zitakomesha uvutano wa kahaba huyo na kuuharibu utajiri wake. Huenda jambo hilo lilionekana kuwa haliwezi kutukia miongo michache tu iliyopita. Leo, kahaba huyo anayumbayumba juu ya mgongo wa huyo mnyama mwenye rangi nyekundu. Hata hivyo, hataanguka polepole. Ataanguka kwa ghafla na kwa kishindo.—Ufu. 18:7, 8, 15-19.
WANYAMA-MWITU WAHARIBIWA
18. (a) Yule mnyama-mwitu atafanya nini, na matokeo yatakuwa nini? (b) Andiko la Danieli 2:44 linasema kwamba Ufalme wa Mungu utaharibu falme zipi? (Tazama sanduku kwenye ukurasa wa 17.)
18 Baada ya dini ya uwongo kuharibiwa, huyo mnyama-mwitu, yaani, mfumo wa kisiasa wa Shetani duniani, atachochewa aushambulie Ufalme wa Mungu. Kwa kuwa wafalme wa dunia hawawezi kufika mbinguni, watawamwagia ghadhabu wale wanaounga mkono Ufalme wa Mungu duniani. Jambo hilo litasababisha vita vya mwisho pamoja na Mungu. (Ufu. 16:13-16; 17:12-14) Danieli anaeleza jambo fulani kuhusu vita hivyo vya mwisho. (Soma Danieli 2:44.) Yule mnyama-mwitu anayetajwa katika andiko la Ufunuo 13:1, sanamu yake, na yule mnyama-mwitu mwenye pembe mbili wataharibiwa.
19. Tunaweza kuwa na uhakika gani, na huu ndio wakati wa kufanya nini?
19 Tunaishi katika siku ambazo kile kichwa cha saba kinatawala. Hakuna vichwa vingine vitakavyoibuka juu ya mnyama huyo kabla hajaharibiwa. Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani ndiyo itakayokuwa ikiutawala ulimwengu wakati dini ya uwongo itakapoharibiwa. Unabii wa Danieli na Yohana umetimizwa kikamili kabisa. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba hivi karibuni dini ya uwongo itaharibiwa na vita vya Har–Magedoni vitaanza. Mungu ametufunulia mambo haya mapema. Je, tutakazia uangalifu maonyo ya kinabii? (2 Pet. 1:19) Huu ndio wakati wa kuchukua msimamo upande wa Yehova na kuunga mkono Ufalme wake.—Ufu. 14:6, 7.
[Maelezo ya Chini]
a Katika Biblia, mara nyingi nambari kumi inawakilisha kikundi kamili, katika kisa hiki inawakilisha falme zote zilizotokana na Milki ya Roma.
b Ingawa nchi ya Uingereza na Marekani ambazo zinafanyiza serikali hiyo pacha ya ulimwengu zimekuwapo tangu karne ya 18, Yohana anaeleza jinsi ambavyo zingetokea mwanzoni mwa siku ya Bwana. Kwa kweli, maono yaliyoandikwa katika kitabu cha Ufunuo yanatimia katika “siku ya Bwana.” (Ufu. 1:10) Kichwa cha saba kilianza kutenda kama serikali kuu ya ulimwengu ya muungano wakati tu wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu.
c Danieli alitabiri uharibifu mbaya ambao mfalme huyo angesababisha wakati wa vita hivyo kwa kuandika hivi: “Naye atasababisha uharibifu kwa njia ya ajabu [ya kutisha].” (Dan. 8:24) Kwa mfano, Marekani ilisababisha uharibifu usio na kifani ilipoangusha mabomu mawili ya atomu juu ya maadui wa serikali hiyo pacha ya ulimwengu.
d Tazama Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, ukurasa wa 240, 241, 253.
[Sanduku katika ukurasa wa 17]
“FALME HIZI ZOTE” ZINATIA NDANI FALME GANI?
Unabii wa Danieli 2:44 unasema kwamba Ufalme wa Mungu “utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote.” Unabii huo unarejelea tu falme ambazo zinafananishwa na sehemu mbalimbali za ile sanamu.
Namna gani serikali nyingine zote za wanadamu? Unabii huohuo katika kitabu cha Ufunuo unafunua mambo mengi zaidi. Unaonyesha kwamba “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” watakusanywa pamoja ili kupambana na Yehova katika “ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” (Ufu. 16:14; 19:19-21) Hivyo, si falme tu za ile sanamu zitakazoharibiwa katika Har–Magedoni, bali pia serikali nyingine zote za wanadamu.
-
-
Wafalme Wanane WafunuliwaMnara wa Mlinzi—2012 | Juni 15
-
-
Wafalme Wanane Wafunuliwa
Kwa ujumla, vitabu vya Biblia vya Danieli na Ufunuo havifunui tu wafalme wanane, au serikali za wanadamu, bali pia vinaonyesha jinsi ambavyo serikali hizo zingefuatana. Tunaweza kuelewa maana ya unabii huo mbalimbali tukielewa unabii wa kwanza kabisa ulioandikwa katika Biblia.
Katika historia yote, Shetani amepanga uzao wake katika makundi mbalimbali ya kisiasa au falme. (Luka 4:5, 6) Hata hivyo, ni falme chache sana za wanadamu ambazo zimejitahidi sana kuwapinga watu wa Mungu, iwe ni taifa la Israeli au kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta. Maono ya Danieli na Yohana yanaeleza kuhusu jumla ya serikali kuu nane tu za aina hiyo.
[Chati/Picha katika ukurasa wa 12, 13]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
UNABII MBALIMBALI UNABII MBALIMBALI
ULIO KATIKA KITABU ULIO KATIKA KITABU
CHA DANIELI CHA UFUNUO
1. Misri
2. Ashuru
3. Babiloni
4. Umedi
na Uajemi
5. Ugiriki
6. Roma
7. Uingereza
na Marekania
8. Ushirika wa Mataifa
na Umoja wa Mataifab
WATU WA MUNGU
2000 K.W.K.
Abrahamu
1500
Taifa la Israeli
1000
Danieli 500
K.W.K./W.K.
Yohana
Israeli wa Mungu 500
1000
1500
2000 W.K.
[Maelezo ya Chini]
a Katika siku za mwisho, wafalme wote wawili wanatawala. Tazama ukurasa wa 19.
b Katika siku za mwisho, wafalme wote wawili wanatawala. Tazama ukurasa wa 19.
[Picha]
Ile sanamu kubwa sana (Dan. 2:31-45)
Wanyama wanne kutoka baharini (Dan. 7:3-8, 17, 25)
Kondoo-dume na mbuzi (Dan., sura ya 8)
Mnyama-mwitu mwenye vichwa saba (Ufu. 13:1-10, 16-18)
Mnyama-mwitu mwenye pembe mbili anachochea utengenezaji wa sanamu ya mnyama-mwitu (Ufu. 13:11-15)
[Hisani]
Photo credits: Egypt and Rome: Photograph taken by courtesy of the British Museum; Medo-Persia: Musée du Louvre, Paris
-