Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani ilianza lini kuwa mfalme wa saba kulingana na unabii wa Biblia?
▪ Ile sanamu kubwa yenye madini mbalimbali ambayo Mfalme Nebukadneza aliona haifananishi serikali zote kuu za ulimwengu. (Dan. 2:31-45) Inaonyesha wafalme watano tu ambao walitawala kuanzia wakati wa Danieli na kuendelea, na ambao waliwatesa sana watu wa Mungu.
Ufafanuzi wa Danieli kuhusu sanamu hiyo yenye madini mbalimbali hutoa wazo la kwamba Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani ingeibuka kutokana na Roma lakini si kwamba ingeishinda serikali ya Roma. Katika sanamu hiyo, Danieli anaona chuma kikianzia kwenye miguu mpaka kwenye nyayo na vidole. (Katika nyayo na vidole, chuma hicho kimechanganywa na udongo.)a Ufafanuzi huo unaonyesha kwamba Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani ingeibuka kutoka katika ile miguu ya chuma. Historia inaonyesha usahihi wa ufafanuzi huo. Uingereza, ambayo zamani ilikuwa sehemu ya Milki ya Roma, ilianza kupata umaarufu mwishoni mwa miaka ya 1700. Baadaye, nchi ya Marekani ikawa taifa lenye nguvu. Hata hivyo, serikali kuu ya saba ya ulimwengu inayotajwa katika unabii wa Biblia bado haikuwa imetokea. Kwa nini? Bado Uingereza na Marekani hazikuwa zimeanza kutenda pamoja kwa njia iliyo wazi zaidi. Jambo hilo lilitokea wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu.
Kufikia wakati huo, “wana wa ufalme” walikuwa watendaji wenye bidii sana hasa huko Marekani, ambako makao yao makuu ya ulimwenguni pote yanapatikana katika mji wa Brooklyn, New York. (Mt. 13:36-43) Washiriki wa jamii ya watiwa-mafuta waliendelea kuhubiri kwa bidii katika nchi zilizokuwa chini ya Milki ya Uingereza. Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, serikali ya Uingereza na Marekani zilianzisha uhusiano wa pekee ili kupigana na maadui wao wa kisiasa. Pia, kwa sababu ya vita, roho ya uzalendo iliongezeka nao wakaonyesha uadui kuelekea wale waliokuwa sehemu ya ule uzao wa “mwanamke” wa Mungu, wakapiga marufuku machapisho yao na kuwafunga gerezani wale waliokuwa wakiongoza katika kazi ya kuhubiri.—Ufu. 12:17.
Hivyo, kulingana na unabii wa Biblia, serikali kuu ya saba ya ulimwengu haikutokea mwishoni mwa miaka ya 1700 wakati Uingereza ilipoanza kupata umaarufu. Badala yake, ilipata mamlaka hayo mwanzoni mwa siku ya Bwana.b
[Maelezo ya Chini]
a Udongo uliochanganywa na chuma unafananisha vitu fulani ndani ya Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani inayofananishwa na chuma. Baada ya muda kupita, udongo huo umefanya iwe vigumu kwa serikali hiyo kuwa na nguvu ambazo ingependa kuwa nazo.
b Ufafanuzi huu unarekebisha habari inayozungumziwa kwenye ukurasa wa 57, fungu la 24 katika kitabu Unabii wa Danieli na chati zilizo kwenye ukurasa wa 56 na 139.
[Picha katika ukurasa wa 19]
Ndugu wanane kutoka makao makuu ya Watchtower walifungwa gerezani mwezi wa Juni 1918