Mashahidi wa Yehova
Maana: Jamii ya Wakristo ulimwenguni pote wanaotoa ushahidi kwa bidii kuhusu Yehova Mungu na makusudi yake kwa wanadamu. Imani zao zote zinategemea Biblia.
Ni imani gani za Mashahidi wa Yehova zinazowatofautisha na dini nyingine?
(1) Biblia: Mashahidi wa Yehova huamini kwamba Biblia nzima ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake, na badala ya kushikilia kanuni za mapokeo ya wanadamu, wanashikamana na Biblia kuwa kiwango cha imani zao zote.
(2) Mungu: Wanamwabudu Yehova, Mungu pekee wa kweli na huwaambia wengine waziwazi kumhusu Yehova na makusudi yake ya upendo kwa wanadamu. Mtu yeyote anayewatolea wengine ushahidi kumhusu Yehova kwa kawaida anatambuliwa kuwa mmoja wa “Mashahidi wa Yehova.”
(3) Yesu Kristo: Hawaamini kwamba Yesu Kristo ni sehemu ya Utatu, bali, kama vile Biblia inavyosema, ni Mwana wa Mungu, wa kwanza kati ya viumbe wa Mungu; kwamba alikuwako kabla ya kuwa binadamu na kwamba uhai wake ulihamishwa kutoka mbinguni ukaingizwa katika tumbo la uzazi la bikira, Maria; kwamba uhai wake mkamilifu wa kibinadamu uliotolewa ukiwa dhabihu unawawezesha wale wanaoamini wapate wokovu na kuishi milele; kwamba Kristo anatawala dunia yote akiwa Mfalme, akiwa na mamlaka aliyopewa na Mungu tangu mwaka wa 1914.
(4) Ufalme wa Mungu: Wanaamini kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini la pekee la wanadamu; ni serikali halisi; hivi karibuni utaharibu mfumo mbovu wa mambo uliopo, kutia ndani serikali zote za wanadamu, na utafanyiza mfumo mpya ambamo uadilifu utakaa.
(5) Kuishi mbinguni: Wanaamini kwamba Wakristo 144,000 waliotiwa mafuta watashiriki pamoja na Kristo katika Ufalme wake wa mbinguni, watatawala wakiwa wafalme pamoja naye. Hawaamini kwamba kila mtu “mwema” ataenda mbinguni.
(6) Dunia: Wanaamini kwamba kusudi la Mungu la kwanza kwa ajili ya dunia litatimizwa; dunia itajawa kabisa na waabudu wa Yehova nao wataishi milele wakiwa wanadamu wakamilifu; hata wafu watafufuliwa wapate nafasi ya kushiriki baraka hizo.
(7) Kifo: Wanaamini kwamba wafu hawajui lolote kamwe; hawana maumivu wala furaha katika ulimwengu fulani wa roho; hawaendelei kuishi isipokuwa wanakumbukwa na Mungu, kwa hiyo wanaweza kuishi tena wakati ujao kupitia ufufuo kutoka kwa wafu.
(8) Siku za mwisho: Wanaamini kwamba sasa, tangu 1914, tunaishi katika siku za mwisho za mfumo huu mbovu wa mambo; wanaopenda uadilifu wataokoka na kuingia katika dunia safi.
(9) Kutokuwa sehemu ya ulimwengu: Wanajitahidi kutokuwa sehemu ya ulimwengu, kama Yesu alivyosema kuhusu wafuasi wake. Wanawaonyesha jirani zao upendo wa kweli wa Kikristo, lakini hawashiriki katika siasa wala vita vya taifa lolote. Wanaandalia familia zao mahitaji ya kimwili lakini wanaepuka kufuatia kupita kiasi ulimwengu na vitu vya kimwili na umashuhuri na kujiingiza katika anasa kupita kiasi.
(10) Wanatumia shauri la Biblia: Wanaamini kwamba ni muhimu kutumia shauri la Neno la Mungu katika maisha ya kila siku sasa—nyumbani, shuleni, kazini, katika kutaniko lao. Haidhuru jinsi mtu alivyokuwa akiishi zamani, anaweza kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova akiacha mazoea yanayoshutumiwa na Neno la Mungu na kutumia shauri la Mungu lililomo. Lakini baada ya hapo mtu yeyote akianza mazoea ya kufanya uzinzi, kufanya uasherati, kufanya ngono kati ya watu wa jinsia moja, kutumia vibaya dawa za kulevya, kulewa, kusema uwongo, au kuiba, atatengwa na ushirika wa tengenezo.
(Mambo hayo yaliyoorodheshwa yanaeleza kifupi imani fulani kuu za Mashahidi wa Yehova lakini hayaelezi mambo yote yanayofanya imani zao zitofautiane na zile za dini nyingine. Msingi wa Kimaandiko wa imani hizo zilizotajwa unapatikana katika Fahirisi ya kitabu hiki.)
Je, Mashahidi wa Yehova ni dini ya Marekani?
Wanautetea Ufalme wa Mungu, wala si mfumo wa kisiasa, wa kiuchumi, au wa kijamii wa taifa lolote la ulimwengu huu wa kale.
Ni kweli kwamba katika nyakati zetu, Mashahidi wa Yehova walianzia Marekani. Kuwa na makao yao makuu ya ulimwengu huko kumefanya iwezekane kuchapisha na kutuma vitabu vya Biblia sehemu nyingi ulimwenguni. Lakini Mashahidi hawapendelei taifa moja kuliko lingine; wanapatikana karibu katika kila taifa, nao wana ofisi katika sehemu nyingi za dunia ili kusimamia utendaji wao katika maeneo hayo.
Hebu fikiria: Yesu, aliyekuwa Myahudi alizaliwa nchini Palestina, lakini Ukristo si dini ya Palestina, sivyo? Mahali alipozaliwa Yesu akiwa mwanadamu silo jambo muhimu zaidi. Mambo ambayo Yesu alifundisha yalitoka kwa Baba yake, Yehova Mungu, anayewatendea watu wa mataifa yote bila ubaguzi.—Yoh. 14:10; Mdo. 10:34, 35.
Gharama ya kazi ya Mashahidi wa Yehova hulipiwaje?
Kupitia michango ya hiari, kama walivyofanya Wakristo wa kwanza. (2 Kor. 8:12; 9:7) Hakuna sadaka zinazokusanywa wakati wowote kwenye mikutano yao; hawaombi-ombi kamwe pesa kutoka kwa watu. Michango yoyote inayotolewa na watu wanaopendezwa hutumiwa kuendeleza kazi ya elimu ya Biblia inayofanywa na Mashahidi wa Yehova.
Mashahidi hawalipwi ili kwenda nyumba kwa nyumba au kuwapa watu vichapo vya Biblia barabarani. Wao huhubiri kuhusu maandalizi ya upendo ya Mungu kwa wanadamu kwa sababu wanampenda Mungu na jirani zao.
Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, shirika halali la kidini linalotumiwa na Mashahidi wa Yehova, lilianzishwa kisheria mwaka wa 1884 kulingana na Nonprofit Corporation Law of the Commonwealth of Pennsylvania, U.S.A. Hivyo, kisheria haliwezi kuwa, wala si shirika lenye kupata faida. Watu mmoja-mmoja hawapati faida kupitia Sosaiti hii. Katiba ya Sosaiti inasema hivi: “[Sosaiti] haipangi kupata mapato wala faida ya kifedha, moja kwa moja au kwa njia nyingine, kwa ajili ya washiriki, wakurugenzi wala maofisa wake.”
Je, Mashahidi wa Yehova ni farakano (sect) au madhehebu (cult)?
Watu fulani hufafanua farakano kuwa kikundi ambacho kimejitenga na dini fulani iliyostawi. Wengine hutumia neno hilo kurejezea kikundi kinachofuata mwanadamu fulani akiwa kiongozi au mwalimu wake. Mara nyingi neno hilo hutumiwa kuonyesha dharau. Mashahidi wa Yehova hawakutokana na kanisa fulani bali ni watu wa tabaka mbalimbali za maisha na waliokuwa washiriki wa dini mbalimbali. Hawamtegemei mwanadamu yeyote, bali wanamtegemea Yesu Kristo, kuwa kiongozi wao.
Madhehebu ni dini fulani inayosemekana kuwa haifuati kawaida zinazokubaliwa na watu wote au inayokazia kujitoa kulingana na desturi inayopendekezwa. Madhehebu nyingi humfuata mwanadamu aliye hai akiwa kiongozi wake, na mara nyingi wafuasi wake huishi vikundi-vikundi mbali na watu wengine. Hata hivyo, Neno la Mungu ndilo linalopaswa kuamua kawaida zinazokubaliwa na watu wote, nao Mashahidi wa Yehova huifuata sana Biblia. Ibada yao ni njia ya maisha, wala hawajitoi kidesturi. Hawamfuati mwanadamu yeyote wala hawajitengi na watu wengine. Wanaishi na kufanya kazi pamoja na watu wengine.
Dini ya Mashahidi wa Yehova ilianza wakati gani?
Kulingana na Biblia, Mashahidi wa Yehova walianzia kwa Abeli mwaminifu. Waebrania 11:4–12:1 husema hivi: “Kwa imani Abeli alimtolea Mungu dhabihu ya thamani kubwa zaidi kuliko Kaini . . . Kwa imani Noa, baada ya kupewa onyo la kimungu la mambo ambayo yalikuwa bado hayajaonekana, alionyesha woga wa kimungu . . . Kwa imani Abrahamu, alipoitwa, alitii kwa kutoka akaenda na kuingia mahali alipokusudiwa kupokea kuwa urithi . . . Kwa imani Musa, alipokuwa mtu mzima, alikataa kuitwa mwana wa binti ya Farao, akachagua kutendewa vibaya pamoja na watu wa Mungu badala ya kufurahia dhambi kwa muda . . . Kwa hiyo, basi, kwa sababu tuna wingu kubwa hivyo la mashahidi linalotuzunguka, acheni sisi pia tuondoe kila uzito na dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi, na acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.”
Kuhusu Yesu Kristo, Biblia inaeleza hivi, “Haya ndiyo mambo anayosema Amina, shahidi mwaminifu na wa kweli, mwanzo wa uumbaji wa Mungu.” Alikuwa shahidi wa nani? Yeye mwenyewe alisema kwamba alilifunua jina la Baba yake. Yeye ndiye aliyekuwa shahidi mkuu wa Yehova.—Ufu. 3:14; Yoh. 17:6.
Kwa kupendeza, baadhi ya Wayahudi waliuliza kama utendaji wa Yesu Kristo ulikuwa “fundisho jipya.” (Marko 1:27) Baadaye, Wagiriki fulani walidhani kwamba mtume Paulo alikuwa akianzisha ‘fundisho jipya.’ (Mdo. 17:19, 20) Lilikuwa jipya masikioni mwa wale waliokuwa wakilisikia, lakini jambo muhimu ni kwamba, ulikuwa ukweli, unaopatana kabisa na Neno la Mungu.
Siku zetu, Mashahidi wa Yehova walianza kwa kikundi cha kujifunza Biblia huko Allegheny, Pennsylvania, Marekani, mapema katika miaka ya 1870. Kwanza walikuwa wakiitwa Wanafunzi wa Biblia, lakini mwaka wa 1931 walikubali kuitwa Mashahidi wa Yehova, jina linalotokana na Maandiko. (Isa. 43:10-12) Imani zao na mazoea yao si mapya bali ni kurudishwa kwa Ukristo wa karne ya kwanza.
Je, Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba dini yao tu ndiyo ya kweli?
Biblia haikubaliani na maoni ya kisasa ya kwamba kuna njia nyingi zinazokubalika za kumwabudu Mungu. Waefeso 4:5 husema kuna “Bwana mmoja, imani moja.” Yesu alisema hivi: “Barabara inayoongoza kwenye uzima ina nafasi ndogo, na wachache ndio wanaoipata. . . . Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni ndiye atakayeingia.”—Mt. 7:13, 14, 21; ona pia 1 Wakorintho 1:10.
Maandiko huyaita mafundisho ya kweli ya Kikristo kuwa “kweli,” na Ukristo unasemwa kuwa “njia ya kweli.” (1 Tim. 3:15; 2 Yoh. 1; 2 Pet. 2:2) Kwa kuwa Mashahidi wa Yehova wanategemeza imani zao zote, viwango vyao vya mwenendo, na taratibu za kitengenezo juu ya Biblia, imani yao katika Biblia yenyewe kuwa Neno la Mungu inawasadikisha kwamba wana kweli kabisa. Kwa hiyo msimamo wao si wa kujisifu bali unaonyesha uhakika wao kwamba Biblia ndiyo kiwango sahihi cha kupimia dini ya mtu. Wao si wenye ubinafsi bali wanatamani sana kushiriki imani zao pamoja na wengine.
Je, dini nyingine pia hazifuati Biblia?
Nyingi huitumia kwa kadiri fulani. Lakini je, kweli zinafundisha na kufuata yaliyomo? Hebu fikiria: (1) Zimeondoa jina la Mungu wa kweli kutoka katika tafsiri zao za Biblia. (2) Fundisho la Utatu, maoni yao kumhusu Mungu mwenyewe, lina vyanzo vya kipagani nalo lilisitawi na kuwa lilivyo leo, karne nyingi baada ya Biblia kuandikwa. (3) Imani yao kuhusu kutoweza kufa kwa nafsi ya wanadamu ili kuendeleza uhai, haitokani na Biblia; ilianzia Babiloni ya kale. (4) Kichwa cha mahubiri ya Yesu kilikuwa Ufalme wa Mungu, naye aliwatuma wafuasi wake wawaambie wengine juu yake; lakini makanisa yanataja Ufalme huo mara chache leo na washiriki wake hawafanyi kazi ya kuhubiri “hii habari njema ya Ufalme.” (Mt. 24:14) (5) Yesu alisema kwamba wafuasi wake wa kweli wangetambuliwa kwa urahisi kwa upendo wao wa kujidhabihu kwa ajili ya mmoja na mwenzake. Je, hivyo ndivyo dini za Jumuiya ya Wakristo zilivyo wakati mataifa yanapoenda vitani? (6) Biblia inasema kwamba wanafunzi Wakristo hawapaswi kuwa sehemu ya ulimwengu, na inaonya kwamba yeyote anayetaka kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya mwenyewe kuwa adui ya Mungu; lakini makanisa ya Jumuiya ya Wakristo pamoja na washiriki wake, yamejiingiza sana katika mambo ya kisiasa ya mataifa. (Yak. 4:4) Kwa sababu hiyo, je, kwa kweli tunaweza kusema kwa unyoofu kwamba makanisa hayo yanaifuata Biblia?
Mashahidi wa Yehova huifafanua Biblia jinsi gani?
Jambo kuu ni kwamba Mashahidi wanaamini kabisa kwamba Biblia ni Neno la Mungu na kwamba yaliyomo ni ya kutufundisha. (2 Tim. 3:16, 17; Rom. 15:4; 1 Kor. 10:11) Kwa hiyo, hawatumii hoja za kifalsafa ili kuhepa maelezo yake ya kweli yaliyo wazi au kutetea njia ya maisha ya watu ambao wameacha viwango vyake vya maadili.
Wanapoeleza maana ya mifano katika Biblia, wao huiacha Biblia ijifafanue, badala ya kutoa maoni yao wenyewe. (1 Kor. 2:13) Mara nyingi, sehemu nyingine za Biblia huonyesha maana ya mifano hiyo. (Kwa mfano, ona Ufunuo 21:1; ndipo, kuhusu maana ya “bahari,” soma Isaya 57:20. Ili kumtambua “Mwana-Kondoo” anayetajwa katika Ufunuo 14:1, ona Yohana 1:29 na 1 Petro 1:19.)
Kuhusu kutimizwa kwa unabii, wanatumia maneno ya Yesu kuhusu kuwa macho ili kuona matukio yanayolingana na mambo aliyotabiri. (Luka 21:29-31; linganisha na 2 Petro 1:16-19.) Wanataja matukio hayo kwa uangalifu na kuelekeza fikira kwenye mambo ambayo Biblia inaonyesha kuwa maana yake.
Yesu alisema kwamba hapa duniani angekuwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” (kikundi cha wafuasi wake watiwa-mafuta), ambaye angemtumia kuandaa chakula cha kiroho kwa ajili ya watu wa nyumba ya imani. (Mt. 24:45-47) Mashahidi wa Yehova wanaukubali mpango huo. Kama Wakristo wa karne ya kwanza walivyokuwa, wao wanalitegemea baraza linaloongoza la jamii hiyo ya “mtumwa” kutatua maswali magumu—si kwa kutegemea hekima ya kibinadamu, bali kwa kutumia ujuzi wao wa Neno la Mungu na anavyowatendea watumishi wake, na kwa msaada wa roho ya Mungu, ambayo wanaomba kwa bidii.—Mdo. 15:1-29; 16:4, 5.
Kwa nini mafundisho ya Mashahidi wa Yehova yamekuwa yakibadilika?
Biblia inaonyesha kwamba Yehova anawawezesha watumishi wake waelewe kusudi lake hatua kwa hatua. (Met. 4:18; Yoh. 16:12) Kwa hiyo, manabii walioongozwa na roho ya Mungu kuandika vifungu vya Biblia hawakufahamu maana ya kila jambo waliloandika. (Dan. 12:8, 9; 1 Pet. 1:10-12) Mitume wa Yesu Kristo walijua kwamba kulikuwako mengi ambayo hawakufahamu wakati huo. (Mdo. 1:6, 7; 1 Kor. 13:9-12) Biblia inaonyesha kwamba kungekuwako ongezeko kubwa la ujuzi wa ukweli katika “wakati wa mwisho.” (Dan. 12:4) Mara nyingi, mtu anapopata ujuzi zaidi anahitaji kurekebisha mawazo yake. Mashahidi wa Yehova wana nia ya kufanya marekebisho hayo kwa unyenyekevu.
Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanahubiri nyumba kwa nyumba?
Yesu alitabiri kazi hii ifanywe wakati wetu: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Tena aliwaagiza wafuasi wake: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.”—Mt. 24:14; 28:19.
Wakati Yesu alipowatuma wanafunzi wake wa kwanza, aliwaelekeza waende kwenye nyumba za watu. (Mt. 10:7, 11-13) Mtume Paulo alisema hivi kuhusu huduma yake: “Sikuepuka kuwaambia ninyi lolote kati ya mambo yenye faida wala kuwafundisha ninyi hadharani na nyumba kwa nyumba.”—Mdo. 20:20, 21; ona pia Matendo 5:42.
Ujumbe ambao Mashahidi wanatangaza unahusu maisha ya watu; wanajitahidi kumfikia kila mtu. (Sef. 2:2, 3) Wanachochewa na upendo kuwatembelea watu—kwanza upendo kwa Mungu, pia kwa jirani yao.
Mkutano wa viongozi wa kidini nchini Hispania ulisema hivi: “Labda [makanisa] yanapuuza kupita kiasi kile ambacho hasa ndiyo kazi kubwa zaidi ya Mashahidi—kuwatembelea watu nyumbani, njia ambayo mitume walitumia katika kanisa la kwanza. Huku makanisa yakijishughulisha sana na ujenzi wa mahekalu yao, kupiga kengele ili kuvutia watu na kuhubiri katika mahali pao pa ibada, [Mashahidi] wanaifuata njia ya mitume ya kwenda nyumba kwa nyumba na kutumia vizuri kila nafasi ili watoe ushahidi.”—El Catolicismo, Bogotá, Colombia, Septemba 14, 1975, uku. 14.
Lakini kwa nini Mashahidi hurudi tena na tena hata kwenye nyumba za watu wasio wa imani yao?
Wao hawalazimishi wengine wakubali ujumbe wao. Lakini wanajua kwamba watu huhamia makao mapya na hali za watu hubadilika. Leo huenda mtu akawa na shughuli nyingi mno asiweze kusikiliza; wakati mwingine huenda akatenga wakati ili asikilize kwa furaha. Huenda mshiriki mmoja wa familia asipendezwe, lakini huenda wengine wakapendezwa. Watu wenyewe hubadilika; matatizo mazito maishani huenda yakawachochea waone uhitaji wa kiroho.—Ona pia Isaya 6:8, 11, 12.
Kwa nini Mashahidi wa Yehova huteswa na kutukanwa?
Yesu alisema: “Ikiwa ulimwengu unawachukia ninyi, mnajua kwamba umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungependa kilicho chake. Sasa kwa sababu ninyi si sehemu ya ulimwengu, bali nimewachagua ninyi kutoka ulimwenguni, kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukia ninyi.” (Yoh. 15:18, 19; ona pia 1 Pet. 4:3, 4) Biblia inaonyesha kwamba ulimwengu kwa ujumla uko chini ya uongozi wa Shetani; yeye ndiye mchochezi mkuu wa mateso.—1 Yoh. 5:19; Ufu. 12:17.
Pia Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu.” (Marko 13:13) Neno hili “jina” hapa linamaanisha cheo rasmi cha Yesu, Mfalme Masihi. Mashahidi wa Yehova huteswa kwa sababu wanatanguliza amri zake kuliko zile za mtawala yeyote wa kidunia.
Mtu Akisema—
‘Kwa nini hamshiriki kufanya ulimwengu (jumuiya) kuwa mahali bora pa kuishi?’
Unaweza kujibu hivi: ‘Bila shaka hali za jumuiya ni muhimu kwako na kwangu pia. Hebu nikuulize, Unafikiri ni tatizo gani linalopaswa kutatuliwa kwanza?’ Kisha unaweza kuongezea: ‘Kwa nini unafikiri hilo limekuwa uhitaji mkubwa hivyo? . . . Bila shaka, hatua ya haraka kuhusu jambo hilo inaweza kunufaisha, lakini nina hakika utakubali kwamba tungependa kuona marekebisho ya kudumu. Hivyo ndivyo sisi Mashahidi wa Yehova tunavyoshughulikia jambo hilo. (Eleza tunayofanya ili kuwasaidia watu wafuate kanuni za Biblia katika maisha yao ili mtu binafsi afikie utatuzi wa jambo hilo; pia, jambo ambalo Ufalme wa Mungu utafanya, na kwa nini hilo litawatatulia wanadamu tatizo hilo daima.)’
Au unaweza kusema: ‘(Baada ya kuzungumzia baadhi ya mambo yaliyo katika jibu linalotangulia . . . ) Watu fulani huchangia maendeleo ya jumuiya kwa kutoa pesa; wengine hufanya hivyo kwa kujitolea kutumikia. Mashahidi wa Yehova hufanya yote hayo. Acha nikueleze.’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Ili mtu awe mmoja wa Mashahidi wa Yehova, ni lazima alipe kodi zake kwa unyoofu; kufanya hivyo husaidia serikali kupata pesa za kutoa huduma zinazohitajiwa.’ (2) ‘Sisi hufanya mengi zaidi, tunawatembelea watu nyumbani, na kuwatolea funzo la Biblia bila malipo. Wanapofahamu mambo ambayo Biblia inasema, wanajifunza kufuata kanuni za Biblia na hivyo wanakabiliana na matatizo yao.’
Pia unaweza kusema: ‘Ninafurahi kwamba umetokeza jambo hilo. Watu wengi hawajawahi kuuliza ili wajue jambo ambalo Mashahidi wanafanya katika jumuiya. Bila shaka kuna njia nyingi za kutoa msaada.’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Watu fulani hufanya hivyo kwa kuanzisha mashirika—hospitali, makao ya wazee, vituo vya kuwarekebishia waraibu wa dawa za kulevya, na kadhalika. Huenda wengine wakajitolea kwenda moja kwa moja kwenye nyumba za watu na kutoa msaada unaofaa kulingana na uwezo wao. Hivyo ndivyo Mashahidi wa Yehova wanavyofanya.’ (2) ‘Tumeona kwamba kuna jambo linaloweza kugeuza mtazamo mzima wa mtu kuhusu maisha, na jambo hilo ni kujua yale ambayo Biblia inasema kuwa ndilo kusudi halisi la maisha na yale yatakayotukia wakati ujao.’
Pendekezo lingine: ‘Asante kwa kuuliza swali hilo. Tungependa kuona hali zikiwa bora, sivyo? Hebu nikuulize, Wewe unaonaje yale ambayo Yesu Kristo mwenyewe alifanya? Je, ungesema kwamba njia aliyotumia kuwasaidia watu ilikuwa nzuri? . . . Sisi hujaribu kufuata mfano wake.’
‘Wakristo wanapaswa kuwa mashahidi wa Yesu, wala si wa Yehova’
Unaweza kujibu hivi: ‘Hilo ni jambo lenye kupendeza. Na ni kweli kwamba tunapaswa kuwa mashahidi wa Yesu. Ndiyo sababu cheo cha Yesu katika kusudi la Mungu kinakaziwa katika vichapo vyetu. (Unaweza kutumia kitabu cha sasa au gazeti ili kuonyesha jambo hilo.) Lakini hapa pana jambo fulani ambalo huenda likawa jipya kwako. (Ufu. 1:5) . . . Yesu alikuwa “Shahidi Mwaminifu” wa nani? (Yoh. 5:43; 17:6) . . . Yesu alituwekea mfano tunaopaswa kufuata, sivyo? . . . Kwa nini ni muhimu sana kumjua Yesu na Baba yake pia? (Yoh. 17:3)’