-
Mashahidi wa Yehova Ni Watu wa Aina gani?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 1
Mashahidi wa Yehova Ni Watu wa Aina Gani?
Denmark
Taiwan
Venezuela
India
Unawajua Mashahidi wa Yehova wangapi? Baadhi yetu ni majirani, wafanyakazi, au hata wanafunzi wenzako. Huenda tumewahi kuzungumza nawe kuhusu Biblia. Sisi ni akina nani, na kwa nini tunawaeleza watu kuhusu imani yetu hadharani?
Sisi ni watu wa kawaida. Tumetoka katika malezi na jamii tofauti-tofauti. Baadhi yetu walikuwa wafuasi wa dini mbalimbali na hata wengine hawakuamini kuna Mungu. Hata hivyo, kabla ya kuwa Mashahidi, sote tulichunguza kwa makini mafundisho ya Biblia. (Matendo 17:11) Tuliamini mambo tuliyojifunza, kisha tukaamua sisi wenyewe kumwabudu Yehova Mungu.
Tunafaidika kwa kujifunza Biblia. Kama watu wengine, sisi pia tunakabiliana na matatizo na udhaifu wetu wenyewe. Lakini kwa kujitahidi kutumia kanuni za Biblia katika maisha yetu ya kila siku, tunajionea mabadiliko makubwa maishani. (Zaburi 128:1, 2) Hiyo ndiyo sababu moja inayofanya tuwaeleze wengine kuhusu mambo mazuri ambayo tumejifunza katika Biblia.
Tunaishi kulingana na viwango vya Mungu. Viwango hivyo tunavyojifunza katika Biblia vinatusaidia kuwa na hali njema na kuwaheshimu wengine, kutia ndani kuwa na sifa kama vile unyoofu na fadhili. Viwango hivyo vinatusaidia pia kuwa watu wazuri na wenye manufaa katika jamii. Isitoshe, vinasaidia familia kuwa na umoja na mwenendo mzuri. Kwa sababu tuna uhakika kwamba “Mungu hana ubaguzi,” sisi ni familia kubwa ya ulimwenguni pote ambayo haina ubaguzi wa kijamii wala wa kisiasa. Ingawa sisi ni watu wa kawaida tu, kuna tofauti kati yetu na vikundi vingine.—Matendo 4:13; 10:34, 35.
Ni mambo gani yanayoonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu wa kawaida tu?
Mashahidi wamejifunza viwango gani katika Biblia?
-
-
Kwa Nini Tunaitwa Mashahidi wa Yehova?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 2
Kwa Nini Tunaitwa Mashahidi wa Yehova?
Noa
Abrahamu na Sara
Musa
Yesu Kristo
Watu wengi wanafikiri kwamba Mashahidi wa Yehova ni jina la dini mpya. Hata hivyo, zaidi ya miaka 2,700 iliyopita, watumishi wa Mungu wa pekee wa kweli waliitwa “mashahidi” wake. (Isaya 43:10-12) Kabla ya mwaka wa 1931, tulikuwa tukiitwa Wanafunzi wa Biblia. Kwa nini basi tulianza kutumia jina Mashahidi wa Yehova?
Jina hilo linamtambulisha Mungu wetu. Kulingana na maandishi ya kale, jina la Mungu, Yehova, linapatikana mara elfu kadhaa katika Biblia. Katika tafsiri nyingi jina hilo limeondolewa na badala yake majina ya cheo, kama vile Bwana au Mungu, yametumiwa. Hata hivyo, Mungu alijifunua kwa Musa akitumia jina lake binafsi, Yehova, na kusema: “Hilo ndilo jina langu milele.” (Kutoka 3:15) Jina hilo linamtofautisha na miungu yote ya uwongo. Tunajivunia kuitwa kwa jina takatifu la Mungu.
Jina hilo linafafanua kazi yetu. Watu wengi katika nyakati za kale, kuanzia Abeli aliyekuwa mwadilifu, walitoa ushahidi kuhusu imani yao katika Yehova. Kwa muda mrefu, Noa, Abrahamu, Sara, Musa, Daudi, na wengineo walijiunga na hilo “wingu kubwa . . . la mashahidi.” (Waebrania 11:4–12:1) Kama vile mtu anavyoweza kutoa ushahidi mahakamani ili kumtetea mtu asiye na hatia, sisi pia tumeazimia kutangaza ukweli kumhusu Mungu.
Tunapotumia jina hilo tunamwiga Yesu. Biblia inamwita “shahidi mwaminifu na wa kweli.” (Ufunuo 3:14) Yesu mwenyewe alisema kwamba ‘alilijulisha jina la Mungu’ naye akaendelea ‘kutoa ushahidi kuhusu kweli.’ (Yohana 17:26; 18:37) Hivyo, wafuasi wa kweli wa Kristo, wanaitwa kwa jina la Yehova, nao huwajulisha watu jina hilo. Hilo ndilo jambo ambalo Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kufanya.
Kwa nini Wanafunzi wa Biblia walianza kuitwa Mashahidi wa Yehova?
Yehova amekuwa na mashahidi duniani kwa muda gani?
Ni nani aliye Shahidi mkuu wa Yehova?
-
-
Kweli za Biblia Zilifunuliwaje Tena?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 3
Kweli za Biblia Zilifunuliwaje Tena?
Wanafunzi wa Biblia wa miaka ya 1870
Toleo la kwanza la Mnara wa Mlinzi, 1879
Mnara wa Mlinzi la wakati huu
Biblia ilitabiri kwamba baada ya kifo cha Kristo, walimu wa uwongo wangetokea miongoni mwa Wakristo wa mapema na kupotosha kweli za Biblia. (Matendo 20:29, 30) Baada ya muda, jambo hilo lilitukia. Walimu hao walichanganya mafundisho ya Yesu na mafundisho ya dini za kipagani, na hivyo Ukristo bandia ukatokea. (2 Timotheo 4:3, 4) Tunawezaje kuwa na uhakika kwamba leo tunaelewa kwa usahihi yale ambayo Biblia inafundisha hasa?
Wakati ulifika wa Yehova kufunua ukweli. Alitabiri kwamba ‘wakati wa mwisho ujuzi wa kweli ungekuwa mwingi.’ (Danieli 12:4) Mnamo 1870, kikundi kidogo cha watu waliokuwa wakitafuta ukweli kilitambua kwamba mafundisho mengi ya kidini hayakupatana na Maandiko. Kwa hiyo, walianza kufanya utafiti ili kuelewa mafundisho ya kweli ya Biblia, na Yehova akawasaidia kuelewa Maandiko.
Watu wanyoofu waliichunguza Biblia kwa makini. Wanafunzi hao wa Biblia waliotutangulia, walitumia njia ya kujifunza ambayo bado tunaitumia leo. Walizungumzia Biblia kwa kuchunguza jambo moja baada ya lingine. Waliposoma sehemu ya Biblia ambayo haikueleweka kwa urahisi, walichunguza maandiko mengine ili kuielewa. Walipofikia uamuzi uliopatana na Maandiko yote, waliandika jambo hilo. Kwa kuacha Biblia ijieleze yenyewe walifanikiwa kufunua tena ukweli kuhusu jina la Mungu na Ufalme wake, kusudi lake kuelekea wanadamu na dunia, hali ya wafu, na tumaini la ufufuo. Uchunguzi wao uliwaweka huru kutokana na mafundisho na desturi nyingi za uwongo.—Yohana 8:31, 32.
Kufikia mwaka wa 1879 Wanafunzi wa Biblia walitambua kwamba wakati ulikuwa umefika wa kutangaza kweli za Biblia kotekote. Basi, mwaka huo wakaanza kuchapisha gazeti la Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova, ambalo bado tunaendelea kulichapisha. Leo, tunawatangazia watu ujumbe wa kweli za Biblia katika nchi 240, tukitumia lugha 750 hivi. Leo, ujuzi wa kweli ni mwingi kuliko wakati mwingine wowote!
Ni nini kilichotokea kuhusiana na kweli za Biblia baada ya kifo cha Kristo?
Ni nini ambacho kimetusaidia kufunua tena ukweli ulio katika Neno la Mungu?
-
-
Kwa Nini Tumechapisha Tafsiri ya Ulimwengu Mpya?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 4
Kwa Nini Tumechapisha Tafsiri ya Ulimwengu Mpya?
Kongo (Kinshasa)
Rwanda
Kisehemu cha tafsiri ya Kigiriki ya Symmachus cha karne ya tatu au ya nne kilicho na jina la Mungu kwenye Zaburi 69:31
Kwa miaka mingi, Mashahidi wa Yehova walitumia, wakachapisha, na kusambaza tafsiri mbalimbali za Biblia. Lakini tukaona uhitaji wa kuchapisha tafsiri mpya ya Biblia ambayo ingewasaidia zaidi watu wajifunze “ujuzi sahihi wa kweli,” na hayo ndiyo mapenzi ya Mungu kwa kila mtu. (1 Timotheo 2:3, 4) Hivyo, mwaka wa 1950 tukaanza hatua kwa hatua kuchapisha Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inayotumia lugha ya kisasa. Biblia hii imetafsiriwa kwa uaminifu na kwa usahihi katika lugha zaidi ya 130.
Biblia inayoeleweka kwa urahisi ilihitajiwa. Lugha hubadilika baada ya muda, na tafsiri nyingi za Biblia zina maneno ambayo hayatumiki tena au hayaeleweki kwa urahisi. Pia, maandishi ya kale ambayo ni sahihi zaidi na ambayo yaliandikwa muda mfupi baada ya nakala za kwanza kuandikwa yamepatikana na hivyo kufanya iwezekane kuelewa vizuri zaidi Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki kilichotumiwa kuandika Biblia.
Tafsiri ambayo haipotoshi neno la Mungu ilihitajiwa. Badala ya kubadili maandishi yaliyoongozwa na roho ya Mungu, watafsiri wa Biblia wanapaswa kutafsiri maandishi ya awali kwa uaminifu. Hata hivyo, katika tafsiri nyingi, jina la Mungu, Yehova, halipatikani katika Maandiko Matakatifu.
Biblia ambayo inamheshimu Mtungaji wake ilihitajiwa. (2 Samweli 23:2) Katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, jina la Yehova limerudishwa kila mahali ambapo jina hilo linapatikana mara 7,000 hivi katika maandishi ya zamani zaidi ya Biblia, kama inavyoonyeshwa katika picha iliyo hapa chini. (Zaburi 83:18) Kwa sababu ya utafiti uliofanywa kwa makini kwa miaka mingi, utafurahia kuisoma Biblia hii, kwa kuwa inaeleza mawazo ya Mungu waziwazi. Iwe una Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha yako au la, tunakutia moyo uwe na mazoea ya kusoma Neno la Yehova kila siku.—Yoshua 1:8; Zaburi 1:2, 3.
Kwa nini tuliamua kwamba tafsiri mpya ya Biblia inahitajiwa?
Kila mtu anayetaka kujifunza mapenzi ya Mungu anapaswa kuwa na mazoea ya kufanya nini kila siku?
-