-
Wazee Hulitumikia Kutaniko Jinsi Gani?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 15
Wazee Hulitumikia Kutaniko Jinsi Gani?
Finland
Kufundisha
Uchungaji
Kuhubiri
Hatuna makasisi wanaolipwa. Badala yake, kama ilivyokuwa kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa, waangalizi wanaostahili huwekwa rasmi ili ‘walichunge kutaniko la Mungu.’ (Matendo 20:28) Wazee ni wanaume wakomavu kiroho ambao wanaongoza katika kutaniko na kulichunga, “si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari mbele za Mungu; si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu.” (1 Petro 5:1-3) Wazee hufanya kazi gani kwa faida yetu?
Wanatuhangaikia na kutulinda. Wazee huongoza na kulinda kutaniko kiroho. Kwa kuwa wanatambua kwamba Mungu amewakabidhi jukumu zito, wazee hawapigi ubwana, badala yake, wanachangia hali nzuri na shangwe kati ya washiriki wa kutaniko. (2 Wakorintho 1:24) Kama vile mchungaji anavyomtunza kila kondoo kwa bidii, wazee hujitahidi kumjua kila mmoja katika kutaniko.—Methali 27:23.
Wanatufundisha jinsi ya kufanya mapenzi ya Mungu. Kila juma, wazee huongoza mikutano ya kutaniko ili kuimarisha imani yetu. (Matendo 15:32) Wanaume hao ambao wamejitoa kwa moyo wote huongoza katika kazi ya kutangaza habari njema, wakihubiri pamoja nasi na kutuzoeza aina mbalimbali za huduma.
Wanatutia moyo. Ili kututunza kiroho, wazee hututembelea nyumbani kwetu au kuzungumza nasi kwenye Jumba la Ufalme ili kutusaidia na kutufariji kwa kutumia Maandiko.—Yakobo 5:14, 15.
Mbali na majukumu yao katika kutaniko, wazee wengi hufanya kazi ili kujiruzuku na wanahitaji kushughulikia familia zao. Ndugu hao wenye bidii wanastahili heshima kutoka kwetu.—1 Wathesalonike 5:12, 13.
Wazee wa kutaniko hufanya kazi gani?
Wazee huonyesha jinsi gani kwamba wanapendezwa na kila mmoja wetu?
-
-
Watumishi wa Huduma Wana Majukumu Gani?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 16
Watumishi wa Huduma Wana Majukumu Gani?
Myanmar
Mkutano
Kikundi cha utumishi
Udumishaji wa Jumba la Ufalme
Biblia hutaja vikundi viwili vya wanaume Wakristo ambao hushughulikia majukumu ya kutaniko, yaani, “waangalizi na watumishi wa huduma.” (Wafilipi 1:1) Kwa kawaida, katika kila kutaniko kuna wazee na watumishi wa huduma kadhaa. Watumishi wa huduma wanafanya kazi gani kwa faida yetu?
Wanalisaidia baraza la wazee kutanikoni. Watumishi wa huduma ni wanaume wa kiroho, wenye kutegemeka, na wenye bidii. Baadhi yao ni vijana na wengine wana umri mkubwa. Wanafanya kazi za kawaida lakini ambazo ni muhimu kutanikoni. Utumishi wao huwawezesha wazee kupata wakati wa kukazia fikira ufundishaji na uchungaji.
Wanatimiza huduma muhimu. Baadhi ya watumishi wa huduma hupewa mgawo wa kuwakaribisha wote wanaofika mikutanoni. Wengine hushughulikia mfumo wa sauti, vitabu na magazeti, hesabu za kutaniko, na migawo ya maeneo kutanikoni. Pia, wao husaidia katika kudumisha Jumba la Ufalme. Wazee wanaweza kuwaomba wawasaidie ndugu na dada waliozeeka. Hata iwe wana migawo gani, wanastahili kuheshimiwa na wote kutanikoni kwa sababu ya roho yao ya kutumikia.—1 Timotheo 3:13.
Wanaweka mfano mzuri. Watumishi wa huduma huwekwa rasmi kwa sababu ya sifa zao nzuri za kiroho. Wanaposhughulikia migawo yao katika mikutano, wanaimarisha imani yetu. Wanapoongoza katika kazi ya kuhubiri, wanatuchochea kuwa wenye bidii. Roho yao ya ushirikiano huchangia shangwe na umoja. (Waefeso 4:16) Baada ya muda, huenda wao pia wakastahili kutumikia wakiwa wazee.
Watumishi wa huduma ni watu wa aina gani?
Watumishi wa huduma wanalisaidiaje kutaniko?
-
-
Waangalizi wa Mzunguko Wanatusaidiaje?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 17
Waangalizi wa Mzunguko Wanatusaidiaje?
Malawi
Kikundi cha utumishi
Huduma ya shambani
Mkutano wa wazee
Biblia huwataja mara kadhaa Barnaba na mtume Paulo. Wanaume hao walikuwa waangalizi wanaosafiri, wakiyatembelea makutaniko ya karne ya kwanza. Kwa nini? Walihangaikia kikweli hali ya ndugu zao wa kiroho. Paulo alisema kwamba alitaka ‘kurudi akawatembelee akina ndugu’ ili aone jinsi wanavyoendelea. Alikuwa tayari kusafiri mamia ya kilometa kwenda kuwaimarisha. (Matendo 15:36) Hiyo ndiyo tamaa ya waangalizi wa mzunguko leo.
Wanakuja kututia moyo. Kila mwangalizi wa mzunguko hutembelea makutaniko 20 hivi. Yeye hukaa katika kila kutaniko kwa muda wa juma moja, mara mbili kila mwaka. Tunaweza kufaidika sana kutokana na uzoefu wa ndugu hao na wake zao pia, ikiwa wameoa. Wanajitahidi kuwafahamu vizuri vijana kwa wazee, nao wana hamu ya kuandamana pamoja nasi katika huduma ya shambani na kwa wale tunaojifunza nao Biblia. Waangalizi hao huandamana pamoja na wazee kufanya ziara za uchungaji. Ili kutuimarisha, wao hutoa hotuba zenye kutia moyo katika mikutano na makusanyiko.—Matendo 15:35.
Wanapendezwa na wote kutanikoni. Waangalizi wa mzunguko wanapendezwa sana na hali ya kiroho ya makutaniko. Wao hufanya mkutano pamoja na wazee na watumishi wa huduma ili kuzungumzia maendeleo ambayo yamefanywa na kuwapa mapendekezo kuhusu jinsi ya kushughulikia majukumu yao. Wanawasaidia mapainia kupata mafanikio katika huduma yao, nao hufurahia kuwajua wapya na kusikia kuhusu maendeleo yao ya kiroho. Kila mmoja wa ndugu hao hujitoa kwa hiari akiwa “mfanyakazi mwenzi kwa ajili ya faida [yetu].” (2 Wakorintho 8:23) Tunapaswa kuiga imani yao na roho yao ya kujitoa kufanya mapenzi ya Mungu.—Waebrania 13:7.
Kwa nini waangalizi wa mzunguko hutembelea makutaniko?
Unaweza kufaidika jinsi gani kutokana na ziara zao?
-
-
Tunawasaidiaje Ndugu Zetu Wakati wa Taabu?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 18
Tunawasaidiaje Ndugu Zetu Wakati wa Taabu?
Jamhuri ya Dominika
Japani
Haiti
Janga linapotokea, mara moja Mashahidi wa Yehova hupanga kuwasaidia ndugu zao ambao wanahitaji msaada. Jitihada hizo huonyesha upendo wa kweli tulio nao. (Yohana 13:34, 35; 1 Yohana 3:17, 18) Tunatoa msaada katika njia zipi?
Tunatoa msaada wa kifedha. Njaa kali ilipotokea Yudea, Wakristo wa karne ya kwanza huko Antiokia waliwatumia ndugu zao wa kiroho msaada wa kifedha. (Matendo 11:27-30) Vivyo hivyo, tunaposikia kwamba ndugu zetu katika sehemu nyingine za dunia wanakabili hali ngumu, tunatuma fedha kupitia kutaniko letu ili kuwasaidia.—2 Wakorintho 8:13-15.
Tunatoa huduma zinazohitajika. Wazee wanaotumikia katika eneo lililokumbwa na janga hujitahidi kuwasiliana na kila mshiriki wa kutaniko na kuhakikisha wote wako salama. Halmashauri ya kutoa misaada inaweza kuratibu kugawanywa kwa chakula, maji safi ya kunywa, nguo, makao, na matibabu. Mashahidi wengi wenye ujuzi hujitolea kusafiri kwa gharama zao wenyewe ili kushiriki katika kazi hiyo ya kutoa misaada au kurekebisha nyumba na Majumba ya Ufalme yaliyoharibiwa. Umoja tunaofurahia tukiwa tengenezo na uzoefu ambao tumepata kwa kufanya kazi pamoja, hutuwezesha kupanga mambo haraka uhitaji unapotokea. Ijapokuwa sisi huwasaidia “wale ambao ni ndugu zetu katika imani,” tunawasaidia wengine pia iwezekanapo, haidhuru dini yao.—Wagalatia 6:10.
Tunatoa msaada wa kiroho na faraja. Waliokumbwa na janga mara nyingi huhitaji faraja. Katika nyakati hizo, tunatiwa nguvu na Yehova, “Mungu wa faraja yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Tunafurahia kuzungumza pamoja na wale walio katika hali hizo kuhusu ahadi za Biblia zinazowahakikishia kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utakomesha majanga yote yanayosababisha uchungu na kuteseka.—Ufunuo 21:4.
Kwa nini Mashahidi huitikia haraka majanga yanapotokea?
Ni ujumbe gani wa kiroho wenye kufariji tunaoweza kuzungumzia na watu waliokabili hali ngumu?
-
-
Mtumwa Mwaminifu na Mwenye Busara Ni Nani?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 19
Mtumwa Mwaminifu na Mwenye Busara Ni Nani?
Sote tunafaidika na chakula chetu cha kiroho
Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alifanya mazungumzo ya faragha pamoja na wanafunzi wake wanne—Petro, Yakobo, Yohana, na Andrea. Yesu alipokuwa akitabiri ishara ya kuwapo kwake katika siku za mwisho, aliuliza swali muhimu: “Kwa kweli ni nani mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi asimamie watumishi wake wa nyumbani na kuwapa chakula chao kwa wakati unaofaa?” (Mathayo 24:3, 45; Marko 13:3, 4) Yesu alikuwa akiwahakikishia wanafunzi wake kwamba akiwa “bwana” wao, angewaweka rasmi wale ambao wangekuwa wakiwaandalia wafuasi wake chakula cha kiroho katika siku za mwisho. Watu hao wangekuwa akina nani?
Ni kikundi kidogo cha wafuasi wa Yesu waliotiwa mafuta. “Mtumwa” huyo huhusianishwa hasa na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Anawaandalia waabudu wenzake chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. Tunamtegemea mtumwa huyo mwaminifu aendelee kutuandalia “kipimo [chetu] cha chakula kwa wakati unaofaa.”—Luka 12:42.
Anasimamia nyumba ya Mungu. (1 Timotheo 3:15) Yesu alimpa mtumwa jukumu zito la kusimamia kazi ya sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova. Kazi hiyo inatia ndani kutunza mali zake, kuelekeza utendaji wa kuhubiri, na kutufundisha kupitia makutaniko. Kwa hiyo, ili kutuandalia kile tunachohitaji wakati tunapokihitaji, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anatuandalia chakula cha kiroho kupitia machapisho tunayotumia katika huduma, na pia kupitia mikutano na makusanyiko.
Mtumwa huyo ni mwaminifu kwa kushikamana na kweli za Biblia na utume wa kuhubiri habari njema, naye ni mwenye busara katika kutunza kwa hekima mali za Kristo duniani. (Matendo 10:42) Yehova anabariki kazi ya mtumwa huyo kwa maandalizi mengi ya kiroho na ongezeko.—Isaya 60:22; 65:13.
Ni nani aliyewekwa na Yesu kuwalisha wanafunzi wake kiroho?
Ni katika njia gani mtumwa huyo ni mwaminifu na mwenye busara?
-
-
Baraza Linaloongoza Hufanyaje Kazi Leo?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 20
Baraza Linaloongoza Hufanyaje Kazi Leo?
Baraza linaloongoza la karne ya kwanza
Kusomwa kwa barua ya baraza linaloongoza
Katika karne ya kwanza, kikundi kidogo, yaani, “mitume na wazee huko Yerusalemu,” kilitumikia kikiwa baraza linaloongoza lililofanya maamuzi muhimu kwa niaba ya kutaniko zima la Wakristo watiwa mafuta. (Matendo 15:2) Kuzungumzia Maandiko na kukubali mwongozo wa roho ya Mungu kuliwawezesha kufanya uamuzi kwa kauli moja. (Matendo 15:25) Ndivyo ilivyo leo pia.
Linatumiwa na Mungu kufanya mapenzi yake. Ndugu waliotiwa mafuta walio katika Baraza Linaloongoza wanapendezwa sana na Neno la Mungu nao wana uzoefu mwingi wa kutoa mwongozo kuhusu jinsi kazi inavyopaswa kufanywa, na pia kujibu maswali yanayohusiana na mambo ya kiroho. Wao hufanya mkutano kila juma ili kufikiria mahitaji ya ushirika wa akina ndugu ulimwenguni pote. Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, maagizo yanayotegemea Biblia huandaliwa kupitia barua, waangalizi wanaosafiri, au vinginevyo. Jambo hili huwasaidia watu wa Mungu wawe na umoja. (Matendo 16:4, 5) Baraza Linaloongoza husimamia kuandaliwa kwa chakula cha kiroho, huwatia moyo wote washiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme, nalo husimamia kuwekwa kwa akina ndugu katika majukumu ya usimamizi.
Linafuata mwelekezo wa roho ya Mungu. Baraza Linaloongoza humtegemea Mwenye Enzi Kuu, Yehova, na pia Kichwa cha kutaniko, Yesu, ili kupata mwongozo. (1 Wakorintho 11:3; Waefeso 5:23) Ndugu walio katika baraza hilo hawajioni kuwa viongozi wa watu wa Mungu. Wao, pamoja na Wakristo wote watiwa-mafuta, wanaendelea “kumfuata Mwanakondoo [Yesu] popote anapoenda.” (Ufunuo 14:4) Baraza Linaloongoza huthamini sala zetu kwa niaba yao.
Ni nani waliokuwa katika baraza linaloongoza katika karne ya kwanza?
Baraza Linaloongoza hutafuta mwongozo wa Mungu jinsi gani leo?
-
-
Betheli Ni Nini?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 21
Betheli Ni Nini?
Idara ya Uchoraji, Marekani
Ujerumani
Kenya
Kolombia
Betheli ni neno la Kiebrania linalomaanisha “Nyumba ya Mungu.” (Mwanzo 28:17, 19, maelezo ya chini) Ni jina linalofaa ambalo Mashahidi wa Yehova hutumia kurejelea majengo yaliyoko katika nchi mbalimbali ambapo mwongozo na msaada kuhusiana na kazi ya kuhubiri unatolewa. Baraza Linaloongoza linafanya kazi likiwa katika makao makuu katika Jimbo la New York, Marekani, na kutoka huko linasimamia kazi inayofanywa na ofisi za tawi katika nchi mbalimbali. Wakiwa pamoja, wote wanaofanya kazi katika ofisi hizo wanaitwa familia ya Betheli. Kama familia, wanaishi na kufanya kazi pamoja, na wanakula na kujifunza Biblia pamoja kwa umoja.—Zaburi 133:1.
Mahali pa pekee ambapo washiriki wanajitolea kwa hiari. Katika kila ofisi ya Betheli kuna wanaume na wanawake Wakristo ambao wamejitolea kufanya mapenzi ya Mungu na kuendeleza masilahi ya Ufalme kwa wakati wote. (Mathayo 6:33) Hakuna yeyote kati yao anayepokea mshahara. Wote wanapewa mahali pa kulala, chakula, na pesa kidogo kwa ajili ya matumizi ya kibinafsi. Kila Mwanabetheli ana mgawo wake, huenda ikawa ni ofisini, jikoni, au katika chumba cha kulia chakula. Wengine wanafanya kazi ya kuchapisha vitabu, kutunza vyumba, kufua nguo, kudumisha majengo, au kazi nyingine.
Sehemu yenye shughuli nyingi inayosaidia kazi ya kuhubiri Ufalme. Kusudi kuu la Betheli ni kufanya ujumbe wa kweli wa Biblia uwafikie watu wengi iwezekanavyo. Mfano mmoja ni broshua hii. Iliandikwa chini ya usimamizi wa Baraza Linaloongoza, ikatumwa kwa mamia ya vikundi vya watafsiri ulimwenguni pote, ikachapishwa katika mashine zenye uwezo mkubwa zinazopatikana katika Betheli kadhaa, na hatimaye ikatumwa katika makutaniko zaidi ya 110,000. Katika kila hatua ya kazi hii, familia za Betheli zinatekeleza huduma za lazima ili kutegemeza kazi muhimu kuliko zote, kazi ya kuhubiri habari njema.—Marko 13:10.
Ni nani wanaofanya kazi Betheli, na wanatunzwa jinsi gani?
Ni kazi gani muhimu inayotegemezwa na huduma zinazotekelezwa Betheli?
-
-
Ni Kazi Gani Zinazofanywa Katika Ofisi ya Tawi?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 22
Ni Kazi Gani Zinazofanywa Katika Ofisi ya Tawi?
Visiwa vya Solomon
Kanada
Afrika Kusini
Wanabetheli wanafanya kazi katika idara mbalimbali zinazosimamia kazi ya kuhubiri katika nchi moja au kadhaa. Huenda baadhi yao wanafanya kazi katika idara ya kutafsiri, kuchapisha magazeti, kutengeneza vitabu, sauti au video, au idara nyingine zinazoshughulikia mambo yanayohusu eneo linalosimamiwa na ofisi ya tawi.
Halmashauri ya Tawi husimamia utendaji. Baraza Linaloongoza limeikabidhi Halmashauri ya Tawi jukumu la kusimamia utendaji wa ofisi ya tawi. Kwa kawaida halmashauri hiyo huwa na wazee watatu au zaidi wanaostahili. Halmashauri ya tawi hulijulisha Baraza Linaloongoza maendeleo ya utendaji mbalimbali katika eneo lililo chini ya usimamizi wake na pia kuhusu matatizo yoyote yanayoweza kutokea. Ripoti hizo hulisaidia Baraza Linaloongoza kuamua habari zinazohitaji kuandikwa katika machapisho na zinazohitaji kuzungumziwa katika mikutano na makusanyiko. Wawakilishi wa Baraza Linaloongoza hutumwa kwa ukawaida kwenye ofisi za tawi ili kuzipatia mwongozo Halmashauri za Tawi kuhusu jinsi ya kufanya kazi zao. (Methali 11:14) Programu ya pekee inayotia ndani hotuba ambayo hutolewa na mwakilishi wa makao makuu huandaliwa ili kuwatia moyo wale wanaoishi katika eneo lililo chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi.
Makutaniko yanapata utegemezo. Ndugu waliowekwa katika ofisi ya tawi huidhinisha kuanzishwa kwa makutaniko mapya. Akina ndugu hutoa mwongozo kuhusu utendaji wa mapainia, wamishonari, na waangalizi wa mzunguko ambao wanatumikia katika eneo lililo chini ya ofisi ya tawi. Wanapanga makusanyiko, wanaratibu ujenzi wa Majumba ya Ufalme, na kuhakikisha kwamba machapisho yamefika kwenye makutaniko. Kazi zote zinazofanywa katika ofisi ya tawi huchangia umoja na upatano katika kutimiza kazi ya kuhubiri.—1 Wakorintho 14:33, 40.
Halmashauri za Tawi hulisaidiaje Baraza Linaloongoza?
Ni majukumu gani yanayotimizwa katika ofisi ya tawi?
-
-
Jinsi Machapisho Yetu Yanavyoandikwa na KutafsiriwaNi Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 23
Jinsi Machapisho Yetu Yanavyoandikwa na Kutafsiriwa
Idara ya Uandikaji, Marekani
Korea Kusini
Armenia
Burundi
Sri Lanka
Ili tufanikiwe kutangaza “habari njema” katika “kila taifa na kabila na lugha na watu,” tunachapisha vitabu na magazeti katika lugha zaidi ya 750. (Ufunuo 14:6) Kazi hiyo yote inafanywaje? Tuna waandishi katika nchi mbalimbali na vilevile vikundi vya watafsiri. Wote hao ni Mashahidi wa Yehova.
Makala ya kwanza huandikwa katika Kiingereza. Baraza Linaloongoza husimamia kazi ya Halmashauri ya Uandikaji katika makao yetu makuu. Halmashauri hii huratibu kazi za waandikaji wanaoishi katika makao makuu na pia wale walio katika baadhi ya ofisi za tawi. Kwa sababu Halmashauri ya Uandikaji inatumia waandikaji wa nchi mbalimbali, machapisho yetu huwapendeza watu wa mataifa yote.
Makala hutumwa kwa watafsiri. Baada ya kuandikwa na kuidhinishwa, makala hutumwa kwa vikundi vya watafsiri duniani kote. Watafsiri hao hujitahidi kuchagua “maneno sahihi ya kweli” yanayotafsiri maana kamili katika lugha yao.—Mhubiri 12:10.
Kompyuta huharakisha kazi. Kompyuta haiwezi kufanya kazi zinazofanywa na waandikaji na watafsiri. Hata hivyo, kazi hiyo inaweza kuharakishwa kwa kutumia kamusi zilizo kwenye kompyuta, pamoja na vifaa vingine vya kufanyia utafiti. Mashahidi wa Yehova walibuni programu ya kompyuta inayoitwa Multilanguage Electronic Publishing System (MEPS). Programu hiyo huwezesha maandishi yaliyotafsiriwa katika mamia ya lugha kuunganishwa pamoja na picha, na kuyatayarisha kwa ajili ya uchapishaji.
Kwa nini tunafanya kazi yote hiyo ya uchapishaji, hata katika lugha zinazozungumzwa na watu wachache tu? Kwa sababu ni mapenzi ya Mungu kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:3, 4.
Machapisho yetu huandikwa jinsi gani?
Kwa nini tunatafsiri machapisho yetu katika lugha nyingi sana?
-
-
Kazi Yetu ya Ulimwenguni Pote Inagharimiwaje?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 24
Kazi Yetu ya Ulimwenguni Pote Inagharimiwaje?
Nepal
Togo
Uingereza
Tengenezo letu linachapisha na kusambaza mamia ya mamilioni ya Biblia na machapisho mengine kila mwaka bila malipo. Tunajenga na kurekebisha Majumba ya Ufalme na ofisi za tawi. Tunatunza maelfu ya Wanabetheli na wamishonari, na pia kutoa msaada wakati wa majanga. Kwa hiyo, huenda ukajiuliza, ‘Kazi yote hii inagharimiwaje?’
Hatukusanyi sadaka wala fungu la kumi. Ingawa gharama za kutegemeza kazi ya kuhubiri habari njema ni kubwa, hatuombi-ombi fedha. Zaidi ya miaka 100 iliyopita, toleo la pili la Mnara wa Mlinzi lilisema kwamba tunaamini Yehova ndiye anayetusaidia na kwamba ‘hatutawaomba-omba watu au kuwasihi watutegemeze,’ nasi hatujawahi kufanya hivyo!—Mathayo 10:8.
Kazi yetu inategemezwa kwa michango ya hiari. Watu wengi wanathamini kazi yetu ya kufundisha Biblia, nao hutoa michango ili kuiunga mkono. Mashahidi wenyewe wanatumia wakati, nguvu, fedha, na rasilimali zao nyingine ili kutimiza mapenzi ya Mungu duniani kote. (1 Mambo ya Nyakati 29:9) Kuna masanduku ya michango katika Majumba ya Ufalme na makusanyikoni, na wote wanaopenda wanaweza kutoa michango ya hiari. Pia, michango inaweza kutolewa kupitia tovuti yetu ya jw.org. Sehemu kubwa ya fedha tunazopokea ni michango ya watu wa kawaida ambao si matajiri, kama yule mjane maskini ambaye Yesu alimsifu. Mjane huyo alitumbukiza sarafu mbili ndogo kwenye sanduku la hazina la hekalu. (Luka 21:1-4) Kwa hiyo mtu yeyote anaweza “kuweka kando kitu fulani” kwa ukawaida ili atoe mchango “kama alivyoazimia moyoni mwake.”—1 Wakorintho 16:2; 2 Wakorintho 9:7.
Tuna hakika kwamba Yehova ataendelea kuchochea mioyo ya wale wanaotaka ‘kumheshimu kwa vitu vyao vyenye thamani,’ kwa kuunga mkono kazi ya Ufalme, ili mapenzi yake yatendeke.—Methali 3:9.
Ni nini kinachofanya tengenezo letu liwe tofauti na dini nyinginezo?
Michango inatumika jinsi gani?
-
-
Majumba ya Ufalme Yanajengwa Jinsi Gani na Kwa Nini?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 25
Majumba ya Ufalme Yanajengwa Jinsi Gani na Kwa Nini?
Bolivia
Nigeria, kabla na baada
Tahiti
Kama jina lenyewe linavyoonyesha, fundisho kuu la Biblia katika majumba yetu ni Ufalme wa Mungu. Hicho ndicho kilichokuwa kichwa kikuu cha mahubiri ya Yesu.—Luka 8:1.
Ni mahali pa ibada ya kweli katika eneo. Hapo ndipo kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme huratibiwa. (Mathayo 24:14) Majumba ya Ufalme yanatofautiana kwa ukubwa na muundo, na hayana madoido. Majumba mengi hutumiwa na zaidi ya kutaniko moja. Ili kwenda sambamba na ongezeko la idadi ya makutaniko, katika miaka ya karibuni tumejenga makumi ya maelfu ya Majumba ya Ufalme (wastani wa majumba matano kila siku). Jambo hilo limewezekanaje?—Mathayo 19:26.
Yanajengwa kwa kutegemea michango. Michango hutumwa kwenye ofisi ya tawi ili makutaniko yanayohitaji kujenga au kukarabati Jumba la Ufalme yaweze kuitumia.
Hujengwa na wajitoleaji wa matabaka mbalimbali ambao hawalipwi mshahara. Katika nchi nyingi Vikundi vya Ujenzi wa Majumba ya Ufalme vimeanzishwa. Vikundi vya watumishi na wajitoleaji wa ujenzi husafiri kutoka kutaniko moja hadi jingine na wakati mwingine kwenda kwenye maeneo ambayo ni vigumu kuyafikia, ili kusaidia makutaniko kujenga Majumba ya Ufalme. Katika nchi nyingine, Mashahidi wanaostahili husimamia ujenzi na ukarabati wa Majumba ya Ufalme katika eneo walilogawiwa. Ingawa wajitoleaji wengi wenye ustadi husaidia wakati wa ujenzi, washiriki wa kutaniko hujitolea kwa wingi. Roho ya Yehova pamoja na jitihada za nafsi yote za watu wake hufanikisha kazi hiyo.—Zaburi 127:1; Wakolosai 3:23.
Kwa nini mahali petu pa ibada panaitwa Jumba la Ufalme?
Inawezekanaje kujenga Majumba ya Ufalme Ulimwenguni pote?
-
-
Tunaweza Kusaidiaje Kudumisha Jumba Letu la Ufalme?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 26
Tunaweza Kusaidiaje Kudumisha Jumba Letu la Ufalme?
Estonia
Zimbabwe
Mongolia
Puerto Riko
Kila Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova linawakilisha jina takatifu la Mungu. Kwa hiyo, ni pendeleo na ni sehemu muhimu ya ibada yetu takatifu kushiriki kulidumisha likiwa safi, nadhifu, na katika hali nzuri. Wote wanaweza kushiriki.
Jitolee kufanya usafi baada ya mikutano. Kila baada ya mkutano, ndugu na dada hujitolea kwa furaha kufanya usafi kwenye Jumba la Ufalme. Mara moja kila juma, usafi wa kina hufanywa. Mzee au mtumishi wa huduma hutoa maelekezo, kwa kawaida akifuata orodha ya mambo yanayopaswa kufanywa. Ikitegemea uhitaji, watu hujitolea kufagia, kusafisha sakafu, kupangusa vumbi, kupanga viti, kusafisha vyoo, kusafisha madirisha na vioo, kutupa takataka, au kufanya usafi wa nje. Angalau mara moja kwa mwaka, siku maalumu hutengwa ya kufanya usafi mkubwa. Tunapowahusisha watoto wetu kufanya usafi, tunawafundisha kuheshimu mahali petu pa ibada.—Mhubiri 5:1.
Jitolee kufanya marekebisho yanapohitajika. Kila mwaka Majumba ya Ufalme hukaguliwa nje na ndani. Kwa kutegemea ukaguzi huo marekebisho hufanywa ili kuepuka gharama zisizo za lazima baadaye. (2 Mambo ya Nyakati 24:13; 34:10) Jumba la Ufalme safi na lililotunzwa vizuri ni mahali panapofaa pa kumwabudia Mungu wetu. Tunaposhiriki katika kazi hii, tunaonyesha tunampenda Yehova na pia mahali petu pa ibada. (Zaburi 122:1) Jambo hilo linawavutia watu wengine pia katika eneo.—2 Wakorintho 6:3.
Kwa nini hatupaswi kupuuza mahali petu pa ibada?
Ni mipango gani ambayo hufanywa ili kudumisha usafi katika Jumba la Ufalme?
-
-
Maktaba ya Jumba la Ufalme Inaweza Kutunufaisha Jinsi Gani?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 27
Maktaba ya Jumba la Ufalme Inaweza Kutunufaisha Jinsi Gani?
Israeli
Jamhuri ya Cheki
Benin
Visiwa vya Cayman
Je, ungependa kufanya utafiti ili uielewe Biblia vizuri zaidi? Je, ungependa kujua mengi zaidi kuhusu andiko, mtu, eneo, au jambo lolote katika Biblia? Au, je, ungependa kujua ikiwa Neno la Mungu linaweza kukusaidia kushughulikia jambo fulani linalokuhangaisha? Ikiwa ndivyo, unaweza kutumia maktaba ya Jumba la Ufalme.
Kuna vifaa vya utafiti. Labda huna machapisho yote ya Biblia ya Mashahidi wa Yehova katika lugha yako. Hata hivyo, maktaba ya Jumba la Ufalme ina machapisho mengi ya karibuni. Huenda pia kukawa na tafsiri mbalimbali za Biblia, kamusi, na vitabu vya marejeo. Unaweza kutumia maktaba hiyo kabla au baada ya mikutano. Ikiwa kuna kompyuta huenda ikawa na programu ya Watchtower Library. Programu hiyo ina machapisho mengi na ni rahisi kuitumia kufanya utafiti kuhusu jambo lolote, neno, au hata andiko la Biblia.
Inasaidia wanafunzi katika Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo. Unaweza kutumia maktaba ya Jumba la Ufalme unapotayarisha migawo yako. Mwangalizi wa Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ndiye msimamizi wa maktaba. Yeye ana jukumu la kuhakikisha machapisho mapya yanawekwa na kupangwa vizuri. Yeye au yule anayejifunza Biblia pamoja nawe anaweza kukuonyesha namna ya kutafuta habari unayohitaji. Hata hivyo, hatupaswi kuchukua vitabu vya maktaba ya Jumba la Ufalme na kwenda navyo. Pia, tunapaswa kutunza vitabu hivyo na kuepuka kuvichora au kuvitia alama yoyote.
Biblia inaeleza kwamba ili “[tupate] ujuzi kumhusu Mungu” ni lazima tuutafute kama tunavyotafuta “hazina zilizofichika.” (Methali 2:1-5) Maktaba ya Jumba la Ufalme inaweza kukusaidia kutimiza jambo hilo.
Ni vifaa gani vya utafiti vinavyopatikana katika maktaba ya Jumba la Ufalme?
Ni nani anayeweza kukusaidia kutumia maktaba hiyo vizuri?
-
-
Ni Habari Gani Zinazopatikana Kwenye Tovuti Yetu?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 28
Ni Habari Gani Zinazopatikana Kwenye Tovuti Yetu?
Ufaransa
Poland
Urusi
Yesu Kristo aliwaambia wafuasi wake hivi: “Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili waone matendo yenu mema na kumtukuza Baba yenu aliye mbinguni.” (Mathayo 5:16) Hiyo ndiyo sababu tunatumia teknolojia ya kisasa, kutia ndani Intaneti. Tovuti yetu, jw.org, ni kituo rasmi chenye taarifa kuhusu imani na utendaji wa Mashahidi wa Yehova. Mambo hayo yanatia ndani nini?
Majibu ya Biblia ya maswali ambayo huulizwa kwa ukawaida. Unaweza kupata majibu ya maswali muhimu ambayo watu hujiuliza. Kwa mfano trakti, Je, Kuteseka Kutaisha? na Je, Kweli Wafu Wataishi Tena? zinapatikana kwenye mtandao katika lugha zaidi ya 600. Pia unaweza kupata Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha zaidi ya 130 pamoja na vifaa vya kukusaidia kujifunza Biblia, kutia ndani kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? na matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Machapisho mengi yanaweza kusikilizwa au kusomwa kwenye mtandao au hata kupakuliwa kama MP3, PDF, au EPUB. Hata unaweza kuchapisha kurasa kadhaa za kusoma na mtu anayependezwa katika lugha yake! Video zinapatikana katika lugha nyingi za ishara. Pia, unaweza kupakua drama za Biblia na muziki mtamu unaoweza kusikiliza unapopumzika.
Habari za kweli kuhusu Mashahidi wa Yehova. Pia kwenye tovuti kuna habari za karibuni kuhusu kazi yetu ya ulimwenguni pote, matukio yanayowahusu Mashahidi wa Yehova, na jitihada zetu za kutoa misaada. Unaweza kupata taarifa kuhusu makusanyiko yajayo na anwani za ofisi zetu za tawi.
Kupitia njia hizi tunaangaza nuru ya kweli kwa mapana na marefu. Watu wa kila bara, kutia ndani Antaktika, wanafaidika. Tunasali “neno la Yehova lizidi kuenea upesi” duniani kote kwa utukufu wa Mungu.—2 Wathesalonike 3:1.
Tovuti ya jw.org inawasaidiaje watu wengi kujifunza Biblia?
Ungependa kuchunguza nini katika tovuti yetu?
-