Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w12 4/1 kur. 18-19
  • Injili za Apokrifa—Je, Zina Ukweli Uliofichwa Kumhusu Yesu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Injili za Apokrifa—Je, Zina Ukweli Uliofichwa Kumhusu Yesu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tofauti Kati ya Injili Zinazokubalika na Injili za Apokrifa
  • Injili za Apokrifa: Masimulizi Yasiyoaminika Kumhusu Yesu
  • Injili za Apokrifa na Uasi Imani Kutoka Kwenye Ukristo
  • Ubora wa Injili Zinazokubalika
  • Kwa Nini Unaweza Kuamini Vitabu vya Injili vya Biblia?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Gospeli—Je, Ni za Kweli au Ni Hekaya Tu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Gospeli—Mjadala Wake Waendelea
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Vitabu vya Injili Vinategemeka Kadiri Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
w12 4/1 kur. 18-19

Injili za Apokrifa​—Je, Zina Ukweli Uliofichwa Kumhusu Yesu?

“HUU ni uvumbuzi mkubwa. Watu wengi watakasirika.” “Habari hii inabadili historia ya Ukristo wa mapema.” Maneno hayo yenye kuchochea fikira yalisemwa na wasomi fulani waliofurahi kupata maandishi ya “Injili ya Yuda,” yaliyodhaniwa kwamba yalikuwa yamepotea kwa zaidi ya karne 16 (yameonyeshwa hapo juu).

Leo, watu wengi wameanza kupendezwa tena na injili kama hizo za apokrifa. Watu fulani wanadai kwamba maandishi hayo yanafunua matukio makubwa na mafundisho yaliyofichwa kwa muda mrefu kuhusu maisha ya Yesu. Lakini injili za apokrifa ni nini? Je, zinaweza kutufundisha ukweli ambao hatuwezi kuupata katika Biblia kumhusu Yesu na Ukristo?

Tofauti Kati ya Injili Zinazokubalika na Injili za Apokrifa

Kati ya mwaka wa 41 na 98 W.K., Mathayo, Marko, Luka, na Yohana waliandika “historia ya Yesu Kristo.” (Mathayo 1:1) Nyakati nyingine masimulizi hayo yanaitwa injili, yaani, “habari njema” kuhusu Yesu Kristo.—Marko 1:1.

Ingawa huenda kulikuwa na mapokeo na maandishi mengine kumhusu Yesu, Injili hizo nne ndizo tu zilizoonwa kuwa zimeongozwa na roho ya Mungu na kwamba zilistahili kuwa sehemu ya Maandiko Matakatifu—ili ziwe chanzo cha “uhakika wa mambo” kuhusu maisha ya Yesu duniani na mafundisho yake. (Luka 1:1-4; Matendo 1:1, 2; 2 Timotheo 3:16, 17) Injili hizo nne zinatajwa katika orodha zote za zamani za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Hakuna msingi wa kushuku ikiwa vitabu hivyo vinakubalika, yaani, kama vinastahili kuwa sehemu ya Neno la Mungu lililoongozwa na roho takatifu.

Hata hivyo, baada ya muda, maandishi mengine ambayo pia yaliitwa injili yalianza kutokea. Maandishi hayo yaliitwa injili za apokrifa.a

Mwishoni mwa karne ya pili, Irenaeus wa Lyon aliandika kwamba wale waliokuwa wameasi imani kutoka kwenye Ukristo walikuwa na “vitabu vingi sana vya apokrifa na maandishi ya uwongo,” kutia ndani injili ambazo “wao wenyewe walikuwa wameziandika, ili kupotosha akili za watu wapumbavu.” Hivyo basi, ikawa hatari kusoma na pia kuwa na injili za apokrifa.

Hata hivyo, wakati wa enzi za kati vitabu hivyo vilihifadhiwa na watawa na watu walionakili maandishi. Katika karne ya 19, watu wengi sana walianza kupendezwa na vitabu hivyo na hilo likafanya mkusanyo wa maandishi na matoleo mbalimbali ya apokrifa yaliyokuwa yamefichwa yapatikane, kutia ndani injili mbalimbali. Leo, kuna matoleo ambayo yamechapishwa katika lugha nyingi za kisasa zinazozungumzwa na watu wengi.

Injili za Apokrifa: Masimulizi Yasiyoaminika Kumhusu Yesu

Mara nyingi injili za apokrifa zinakazia fikira watu ambao hawazungumziwi sana au ambao hawatajwi kamwe katika Injili zinazokubalika. Au zinazungumzia mambo ambayo yanadhaniwa yalitukia katika maisha ya Yesu alipokuwa mtoto. Fikiria mifano kadhaa.

◼ Injili inayodaiwa iliandikwa na Yakobo ambayo pia inaitwa “Kuzaliwa kwa Maria,” inaeleza kuhusu kuzaliwa kwa Maria na maisha yake ya utotoni na vilevile jinsi alivyoolewa na Yosefu. Kwa sababu zinazofaa, imeitwa hekaya na pia hadithi ya kubuniwa ya kidini. Inaendeleza fundisho la kwamba Maria ni bikira milele na imeandikwa hasa ili kumtukuza.—Mathayo 1:24, 25; 13:55, 56.

◼ “Injili ya Tomasi Kuhusu Maisha ya Utotoni” inakazia fikira maisha ya utotoni ya Yesu, alipokuwa na umri wa kati ya miaka 5 na 12, na inasema kwamba alifanya miujiza fulani isiyoaminika. (Ona Yohana 2:11.) Yesu anaelezwa kuwa mtoto mtukutu, mwenye hasira, na anayelipiza kisasi, ambaye anatumia nguvu zake za kufanya miujiza kujilipizia kisasi kwa walimu, majirani, na watoto wengine, huku akiwapofusha wengine wao, kuwalemaza, au hata kuwaua.

◼ Injili fulani za apokrifa, kama vile “Injili ya Petro,” zinazungumzia matukio yanayohusu kushtakiwa, kuuawa, na kufufuliwa kwa Yesu. Injili nyingine, kama vile “Matendo ya Pilato,” ambayo ni sehemu ya “Injili ya Nikodemo,” zinakazia fikira watu wanaotajwa katika matukio hayo. Maandishi hayo hayaaminiki kabisa kwa sababu yanataja matukio na watu wa kuwaziwa. “Injili ya Petro” inajaribu kuonyesha kwamba Pontio Pilato hakuwa na hatia na inaelezea ufufuo wa Yesu kwa njia ya kustaajabisha.

Injili za Apokrifa na Uasi Imani Kutoka Kwenye Ukristo

Mnamo Desemba 1945, wakulima fulani walipata bila kutazamia hati 13 za mafunjo zenye maandishi 52 karibu na mji wa Nag Hammadi, katika Eneo la Juu huko Misri. Hati hizo za karne ya nne zimehusianishwa na kikundi cha kidini na cha kifalsafa kilichoitwa Ugnostiki. Kikundi hicho kilichanganya mafumbo, upagani, falsafa za Kigiriki, mafundisho ya Dini ya Kiyahudi, na Ukristo, na hivyo kuwapotosha watu fulani waliodai kuwa Wakristo.—1 Timotheo 6:20, 21.

“Injili ya Tomasi,” “Injili ya Filipo,” na “Injili ya Ukweli,” ambazo zinapatikana katika “Maktaba ya Nag Hammadi,” zinazungumzia mafumbo fulani ya Kignosti kana kwamba yalisemwa na Yesu. “Injili ya Yuda” ambayo ilipatikana hivi karibuni inaonwa kuwa kati ya injili za Kignosti. Inamtaja Yuda kwa njia inayofaa kama mtume pekee ambaye alimjua Yesu kwa undani. Mtaalamu mmoja wa aliyechunguza injili hiyo alisema kwamba inamfafanua Yesu kuwa “mwalimu na mfunuaji wa hekima na ujuzi, bali si mwokozi aliyekufa kwa ajili ya dhambi za ulimwengu.” Injili zilizoongozwa na roho ya Mungu zinafundisha kwamba Yesu alikufa ili kuwa dhabihu kwa dhambi za ulimwengu. (Mathayo 20:28; 26:28; 1 Yohana 2:1, 2) Ni wazi kwamba injili za Kignosti zimekusudiwa kudhoofisha, bali si kuimarisha imani katika Biblia.—Matendo 20:30.

Ubora wa Injili Zinazokubalika

Tunapochunguza kwa makini injili za apokrifa tunatambua kwamba ni za uwongo. Zinapolinganishwa na Injili zinazokubalika, inaonekana wazi kwamba hazikuandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu. (2 Timotheo 1:13) Kwa kuwa ziliandikwa na watu ambao hawakumjua kamwe Yesu au mitume wake, hazifunui ukweli wowote uliofichwa kumhusu Yesu na Ukristo. Badala yake, zina masimulizi yasiyo sahihi, ya kubuniwa, na ya kustaajabisha ambayo hayawezi kutusaidia kumjua Yesu na mafundisho yake.—1 Timotheo 4:1, 2.

Kwa upande mwingine, Mathayo na Yohana walikuwa kati ya wale mitume 12; Marko alishirikiana na mtume Petro, naye Luka akashirikiana kwa ukaribu na mtume Paulo. Waliandika Injili zao chini ya mwongozo wa roho takatifu ya Mungu. (2 Timotheo 3:14-17) Kwa sababu hiyo, zile Injili nne zina habari zote zinazohitajiwa ili mtu aamini kwamba “Yesu ndiye Kristo Mwana wa Mungu.”—Yohana 20:31.

[Maelezo ya Chini]

a Neno “apokrifa” linatokana na neno la Kigiriki ambalo linamaanisha “kuficha.” Mwanzoni neno hilo lilimaanisha maandishi ambayo yalisomwa tu na kikundi fulani cha watu waliokuwa na maoni yaliyopatana na ambayo yalifichwa kutoka kwa watu ambao hawakuwa sehemu ya kikundi hicho. Hata hivyo, baadaye neno hilo likatumiwa kumaanisha maandishi ambayo hayakuonwa kuwa kati ya vitabu vya Biblia vinavyokubalika.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 18]

Kenneth Garrett/National Geographic Stock

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki