Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • wp16 Na. 2 kur. 8-10
  • Je, Wakristo Wanapaswa Kuabudu Katika Maeneo Matakatifu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Wakristo Wanapaswa Kuabudu Katika Maeneo Matakatifu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2016
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUABUDU “KWA ROHO NA KWELI”
  • MAONI YA WAKRISTO KUHUSU MAENEO MATAKATIFU
  • Walsingham—Patakatifu pa Uingereza Penye Kubishaniwa
    Amkeni!—1994
  • Je! Mungu Hujibu Sala Zako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Biblia Inabadili Maisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Ni Ibada ya Nani Anayoikubali Mungu?
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2016
wp16 Na. 2 kur. 8-10

Je, Wakristo Wanapaswa Kuabudu Katika Maeneo Matakatifu?

KILA mwaka, watu zaidi ya milioni sita husafiri mpaka kwenye eneo la mbali lenye msitu wa mizeituni katika Peninsula ya Shima huko Japani. Wanaenda kwenye Hekalu Kuu la Ise, ambapo Amaterasu Omikami mungu wa kike wa jua wa Shinto ameabudiwa kwa miaka elfu mbili hivi. Waabudu hao hujitakasa kwanza kwa kusafisha mikono na midomo yao. Kisha, wakiwa wamesimama mbele ya haiden (ukumbi wa ibada), wanaanza kufuata utaratibu wa ibada kwa kuinama, kupiga makofi, na kusali kwa mungu wao.a Dini ya Shinto inaruhusu waumini wake kufuata imani zingine, hivyo baadhi ya Wabudha, wale wanaodai kuwa Wakristo, na wafuasi wa dini nyingine hushiriki katika desturi za ibada zinazofanywa kwenye madhabahu hiyo ya dini ya Shinto.

Karibu dini zote kubwa leo zina maeneo matakatifub ambayo hutembelewa na mamilioni ya watu. Katika nchi zinazodai kuwa za Kikristo, kuna makanisa mengi na maeneo matakatifu au madhabahu yaliyotengwa kwa ajili ya Yesu, Maria, na watakatifu. Maeneo mengine kama hayo yametengwa kuwa matakatifu kwa sababu ya matukio yaliyotajwa katika Biblia au kwa kuwa tu inasemekana kwamba “miujiza” fulani ilifanyika hapo au ni sehemu ambayo ina mabaki ya vitu vya kidini. Watu wengine husali katika maeneo hayo matakatifu kwa kuwa wanaamini kwamba sala zao zitasikiwa. Wengine huona kwamba kufika katika eneo takatifu ni jambo muhimu linaloonyesha kwamba anaipenda dini yake.

Watu wakitembelea Hekalu Kuu la Ise, Japani, na Pango la Massabielle, Lourdes, Ufaransa

Watu wakitembelea Hekalu Kuu la Ise, Japani, na Pango la Massabielle, Lourdes, Ufaransa

Je, sala na maombi yanasikiwa zaidi na kujibiwa ikiwa yatatolewa katika eneo takatifu? Je, Mungu anafurahishwa na bidii ya wale wanaotembelea maeneo matakatifu? Na jambo la muhimu hata zaidi, Je, Wakristo wanapaswa kuabudu katika maeneo matakatifu? Kupata majibu ya maswali hayo kutatusaidia kujua ukweli kuhusu kuabudu katika maeneo matakatifu na pia aina ya ibada ambayo Mungu anapenda.

KUABUDU “KWA ROHO NA KWELI”

Yesu akizungumza na mwanamke Msamaria katika kisima cha maji

Yesu alimaanisha nini aliposema kwamba lazima tuabudu “kwa roho na kweli”?

Mazungumzo ya Yesu na mwanamke Msamaria yanaonyesha maoni ya Mungu kuhusu kufanya ibada katika maeneo matakatifu au madhabahu fulani. Akiwa katika safari yake huko Samaria, Yesu aliamua kupumzika karibu na kisima katika jiji la Sikari. Alianza kuzungumza na mwanamke aliyekuja kuchota maji katika kisima hicho. Walipokuwa wakiongea, mwanamke huyo alitaja tofauti kubwa ya kidini iliyokuwapo kati ya Wayahudi na Wasamaria. Alisema hivi: “Mababu zetu waliabudu katika mlima huu; lakini ninyi husema kwamba Yerusalemu ndipo mahali ambapo watu wanapaswa kuabudia.”—Yohana 4:5-9, 20.

Mwanamke huyo alikuwa akizungumzia Mlima Gerizimu, uliokuwa umbali wa kilomita 50 kaskazini mwa Yerusalemu. Wasamaria waliwahi kuwa na hekalu katika eneo hilo ambalo walitumia kwa ajili ya sherehe kama vile Pasaka. Hata hivyo, badala ya kukazia fikira tofauti hiyo kubwa kati yao, Yesu alimwambia hivi mwanamke huyo: “Niamini mimi, mwanamke, saa inakuja wakati ambapo mtamwabudu Baba si katika mlima huu wala kule Yerusalemu.” (Yohana 4:21) Maneno ya ajabu sana, hasa ukizingatia kwamba anayeyasema ni Myahudi! Kwa nini watu wangeacha kuabudu katika hekalu la Mungu huko Yerusalemu?

Yesu aliendelea kusema: “Saa inakuja, nayo ipo sasa, wakati ambapo waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana, kwa kweli, Baba anawatafuta watu wa namna hiyo wamwabudu.” (Yohana 4:23) Kwa karne nyingi, Wayahudi waliliona hekalu hilo la kifahari lililokuwa Yerusalemu kuwa kitovu cha ibada. Walisafiri kuelekea huko mara tatu kila mwaka ili kutoa dhabihu kwa Mungu wao, Yehova. (Kutoka 23:14-17) Hata hivyo, Yesu alisema yote hayo yangekwisha na kwamba “waabudu wa kweli” watamwabudu “kwa roho na kweli.”

Hekalu la Wayahudi lilikuwa jengo halisi katika eneo hususa. Lakini, roho na kweli si vitu vinavyoweza kuonwa kwa macho au kutembelewa. Hivyo, Yesu alikuwa akimaanisha kwamba ibada ya kweli ya Kikristo haingetegemea jengo au eneo halisi, iwe ni katika Mlima Gerizimu, hekalu lililokuwa Yerusalemu, au sehemu nyingine takatifu.

Katika mazungumzo yake na mwanamke Msamaria, Yesu alisema kwamba “saa” ya badiliko hilo katika ibada ya Mungu ilikuwa “inakuja.” Saa hiyo ingekuja lini? Saa hiyo ilikuja Yesu alipokufa kifo cha kidhabihu, na hivyo kumaliza mfumo wa ibada wa Kiyahudi uliotegemea Sheria ya Musa. (Waroma 10:4) Pamoja na hayo, Yesu alisema hivi pia: “Saa . . . ipo sasa.” Kwa nini? Kwa sababu, akiwa Masihi, alikuwa akikusanya wanafunzi wake ambao wangetii amri aliyotaja katika maneno yaliyofuata: “Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu lazima wamwabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Hivyo, inamaanisha nini kuabudu kwa roho na kweli?

Yesu alipotaja kuabudu kwa roho, hakuwa akizungumzia ibada fulani hususa yenye kuchochewa na msisimko. Badala yake, alikuwa akizungumzia kuongozwa na roho takatifu ya Mungu, ambayo ni kati ya mambo yanayotusaidia kuelewa Maandiko. (1 Wakorintho 2:9-12) Pia, kweli aliyotaja Yesu ni ujuzi wa kweli wa mafundisho ya Biblia. Hivyo, badala ya kufanya ibada katika eneo fulani la pekee, ibada yetu itakubaliwa na Mungu ikiwa itapatana na kile ambacho Biblia inafundisha na ikiwa itaongozwa na roho takatifu.

MAONI YA WAKRISTO KUHUSU MAENEO MATAKATIFU

Hivyo, Wakristo wanapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kuabudu katika maeneo matakatifu? Kwa kuzingatia amri ya Yesu kwamba waabudu wa kweli wanamwabudu Mungu kwa roho na kweli, tunaona wazi kwamba ibada yoyote inayofanywa katika madhabahu au maeneo matakatifu, haikubaliwi na Baba yetu wa mbinguni. Kwa kuongezea, Biblia inatuambia maoni ya Mungu kuhusu kuabudu sanamu. Inasema: “Ikimbieni ibada ya sanamu” na “jilindeni na sanamu.” (1 Wakorintho 10:14; 1 Yohana 5:21) Hivyo, Mkristo wa kweli hatafanya ibada katika eneo linaloonwa kuwa takatifu au linalotukuza ibada ya sanamu. Kwa kuwa maeneo matakatifu yametengwa kwa kusudi hilo, Wakristo wa kweli hawatafanya ibada yao hapo.

Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba Neno la Mungu linakataza kuwa na eneo fulani hususa kwa ajili ya kusali, kujifunza, au kutafakari. Ni jambo linalofaa kuwa na eneo zuri na linaloleta heshima kwa ajili ya kujifunza na kuzungumzia mambo ya kiroho. Pia, si vibaya kuweka kumbukumbu, kama vile kujenga kaburi kwa ajili ya mpendwa wetu aliyekufa. Hilo lingeonyesha kwamba tunamkumbuka na kumpenda ndugu yetu aliyekufa. Hata hivyo, kuona eneo hilo kuwa takatifu au kuabudu sanamu au mabaki ya vitu vya kidini kungekuwa tofauti na maneno ya Yesu.

Hivyo, hauhitaji kwenda katika eneo takatifu ukiwa na matumaini kwamba Mungu atasikiliza sala yako hapo. Pia, Mungu hatapendezwa nawe na hatakubariki ikiwa utatembelea maeneo matakatifu kwa kusudi la kufanya ibada. Biblia inatuambia kwamba Yehova Mungu, “Bwana wa mbingu na dunia, hakai katika mahekalu yaliyofanywa kwa mikono.” Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba Mungu yuko mbali nasi. Tunaweza kusali kwake na akatusikia kwa kuwa “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.”—Matendo 17:24-27.

a Huenda desturi za ibada katika madhabahu za dini ya Shinto zikatofautiana.

b Tazama sanduku “Eneo Takatifu ni Nini?”

Eneo Takatifu Ni Nini?

Watu wametenga maeneo kwa ajili ya ibada ya miungu au kumtukuza “mtakatifu” fulani. Mara nyingi maeneo hayo huwekwa picha na mabaki ya vitu vya kidini yanayohusishwa na miujiza, maono, au mizuka kutoka katika makao ya roho. Leo, maeneo matakatifu yanaweza kutia ndani hekalu, kanisa, au sehemu nyingine ambazo watu huabudu. Wengine wametenga eneo takatifu katika nyumba zao. Kwa ujumla watu katika nchi za Mashariki ya Kati au nchi za Magharibi, hujenga madhabahu ndogo katika nyumba zao kwa ajili ya sala, kutafakari, au kutoa dhabihu.

Si maeneo yote matakatifu yamekusudiwa kutumika kwa ajili ya ibada. Kwa mfano, katika nchi nyingi ni jambo la kawaida kwa ndugu na marafiki waliofiwa na wapendwa wao kutokana na aksidenti za magari, kulifanya eneo la tukio kuwa takatifu kwa ajili ya kumbukumbu ya wapendwa wao waliokufa. Maeneo mengine yamefanywa kuwa matakatifu ili kukumbuka vita vilivyopiganwa au watu waliokufa katika vita au janga. Ijapokuwa kumbukumbu hizo huwapa watu nafasi ya kutafakari na kuomboleza, mara nyingi hutia ndani ibada.

Shahidi wa Yehova akijifunza Biblia na mwanamke ambaye nyumbani kwake kuna sanamu ya Maria
    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki