Sanduku la Swali
◼ Kwa nini tunapaswa kutumia kwa busara mpango wa kusikiliza mikutano ya kutaniko kupitia simu?
Makutaniko mengi yamefanya mpango ili watu ambao nyakati nyingine hawawezi kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme kwa sababu ya ugonjwa au hali nyingine zisizoepukika, wasikilize kupitia simu wakiwa nyumbani. Wazee wanaosimamia mpango huu wanahitaji kutumia busara na kupanga mambo kwa uangalifu ili kuhakikisha kwamba unatumiwa tu na wale walio na sababu nzuri ya kutohudhuria mikutano. Kwa hiyo, wazee hao wanapaswa kuhakikisha kwamba mpango huu wa upendo unatumiwa vizuri ili ‘mambo yote yatendeke kwa adabu na kwa mpango.’—1 Kor. 14:40.
Wazee watahakikisha kwamba wahubiri walio na magonjwa ya kudumu, wasiojiweza, au wasioweza kuondoka nyumbani, wanafikiriwa kwanza. Mhubiri ambaye amekuwa mgonjwa au asiyejiweza kwa muda mfupi, au mwanafunzi wa Biblia mwenye maendeleo asiyeweza kuondoka nyumbani, anaweza pia kunufaika na mpango huu na kuhesabiwa pamoja na waliohudhuria mkutano. Mahali ambapo wote walio na sababu nzuri ya kutohudhuria mikutano hawawezi kuunganishwa kwenye mfumo wa simu wa Jumba la Ufalme kwa wakati mmoja, yamkini mipango mingine inaweza kufanywa, kama kurekodi mikutano kwa ajili yao.
Bila shaka, mtu ananufaika zaidi anapokuwa kwenye mikutano. Kushirikiana na ndugu zetu kwenye Jumba la Ufalme hutupa nafasi ya ‘kutiana moyo’ na huwasaidia wapya kuona umuhimu wa kuhudhuria mikutano. Tunapokuwa mikutanoni, tunajifunza mambo mengi zaidi kutokana na maonyesho, tunaweza kusaidiwa kibinafsi na wazee, na tunafurahia moja kwa moja ushirika wenye upendo pamoja na akina ndugu. Maneno ambayo dada mmoja mzee alisema baada ya kukumbatiwa alipokuwa akiondoka kwenye Jumba la Ufalme, ni ya kweli kabisa. Alisema: “Huwezi kukumbatiwa kwenye simu!”—Rom. 1:11, 12.
Kama Ana “ambaye alikuwa hakosi kamwe kuwa katika hekalu,” leo, wengi wa ndugu zetu wenye umri mkubwa wanahudhuria mikutano kwa ukawaida kadiri afya na hali zao zinavyowaruhusu. (Luka 2:36, 37) Ingawa wanatumia simu kusikilizia mikutano inapohitajika, hawatumii mpango huu kama udhuru wa kutohudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Tuige mfano wao mzuri, na kuendelea kujitahidi kuwapo kwenye mikutano yetu ambapo tunamwabudu Mungu wetu mkuu, Yehova.—Zab. 95:1-3, 6; 122:1.