Sanduku la Swali
◼ Je, inafaa Mashahidi wa Yehova wasambaze rekodi zao au maandishi yao ya hotuba mbalimbali?
Tunatiwa moyo na kuimarishwa kwa kusikiliza hotuba za Biblia. (Mdo. 15:32) Kwa hiyo, si ajabu kwamba ndugu wanataka kuwaandalia wale ambao hawakuweza kuhudhuria mkutano fulani habari zenye kutia moyo zilizozungumziwa. Leo kuna vifaa vingi vinavyoweza kutumiwa kurekodi hotuba, na kuzisambaza ni rahisi sana. Baadhi ya ndugu wamehifadhi rekodi za hotuba nyingi, hata hotuba zilizotolewa miaka mingi iliyopita, na kwa nia nzuri wanawaazima marafiki wao hotuba hizo au kuwatengenezea nakala. Wengine wamefungua vituo (tovuti) vya Intaneti na kuweka hotuba hizo kwenye vituo hivyo ili mtu yeyote aweze kuzipata hapo.
Ni wazi kwamba si vibaya kurekodi hotuba kwa ajili yetu wenyewe au kwa ajili ya watu wa familia yetu. Pia, wazee wa kutaniko wanaweza kupanga ili hotuba zirekodiwe kwa ajili ya ndugu wagonjwa ambao hawawezi kuhudhuria mikutano. Hata hivyo, kuna sababu nzuri za kutosambaza hotuba zilizorekodiwa au maandishi ya mtu binafsi ya hotuba mbalimbali.
Hotuba nyingi hutayarishwa kwa ajili ya wasikilizaji katika eneo fulani hususa, kwa hiyo, huenda tukaelewa vibaya habari fulani katika rekodi inayosambazwa, kwa sababu hatujui jinsi hali zilivyo katika eneo hilo. Isitoshe, hatuwezi kuwa na hakika kwamba habari hizo ni sahihi na za karibuni zaidi kwa sababu hatumjui msemaji, au wakati ambapo hotuba hiyo ilitolewa. (Luka 1:1-4) Na pia, huenda ndugu wakashawishika kupokea heshima isivyofaa au kumheshimu mtu mwingine kupita kiasi kwa sababu ya rekodi au maandishi ya hotuba yanayosambazwa.—1 Kor. 3:5-7.
Jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara inafanya kazi kwa bidii ili kuandaa chakula cha kiroho kwa “kipimo” kinachofaa na “katika wakati unaofaa.” (Luka 12:42) Chakula hicho huandaliwa kwa njia tofauti-tofauti kama vile hotuba zinazotolewa kwenye makutaniko ya Mashahidi wa Yehova katika maeneo mbalimbali, na kupitia rekodi za sauti zinazopatikana katika kituo chetu rasmi cha Intaneti, yaani, jw.org. Bila shaka, Baraza Linaloongoza la jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara litaendelea kutuandalia yote tunayohitaji ili tuwe imara katika imani.—Mdo. 16:4, 5.