Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Amri iliyo kwenye andiko la Mambo ya Walawi 19:16 ya ‘kutohatarisha uhai wa’ mwenzako inamaanisha nini, na inatufundisha somo gani?
Yehova aliwahimiza Waisraeli wawe watu watakatifu. Ili kuwasaidia wafanye hivyo aliwaambia hivi: “Usizungukezunguke kati ya watu wako ukieneza uchongezi. Usihatarishe uhai wa mwenzako. Mimi ni Yehova.”—Law. 19:2, 16.
Neno “usihatarishe” limetumiwa kutafsiri neno la awali la Kiebrania, lakini linamaanisha nini? Kitabu cha marejeo cha Kiyahudi kuhusu Mambo ya Walawi kinasema: ‘Si rahisi kufafanua sehemu ya mstari huo kwa sababu ni vigumu kuelewa maana ya msemo huo wa Kiebrania unaopatikana hapa, msemo ambao kihalisi unamaanisha “usisimame juu, kando, au karibu.”’
Baadhi ya wasomi wanauhusianisha msemo huo na mstari uliotangulia, unaosema: “Usitoe hukumu isiyo ya haki. Usiwabague maskini au kuwapendelea matajiri. Unapaswa kumhukumu mwenzako kwa haki.” (Law. 19:15) Kwa sababu hiyo, amri iliyo kwenye mstari wa 16, ya ‘kutohatarisha’ uhai wa mtu inaweza kumaanisha kwamba watu hawakupaswa kumtendea bila haki mfanyakazi mwenzao mahakamani, kwenye biashara, au masuala ya familia na hawakupaswa kusema uwongo ili kujinufaisha. Ni kweli kwamba hatupaswi kufanya mambo hayo, lakini kuna njia inayopatana zaidi na akili ya kuelewa msemo huo kwenye mstari wa 16.
Fikiria sehemu ya kwanza ya mstari huo. Mungu aliwaamuru watu wake wasizungukezunguke wakieneza uchongezi. Kumbuka kwamba uchongezi ni zaidi ya kupiga porojo tu, ingawa porojo hiyo inaweza kusababisha pia matatizo. (Met. 10:19; Mhu. 10:12-14; 1 Tim. 5:11-15; Yak. 3:6) Mara nyingi mchongezi husema uwongo kimakusudi ili kumharibia sifa mtu mwingine. Mchongezi anaweza kutoa ushahidi wa uwongo dhidi ya mtu mwingine, hata ikiwa kufanya hivyo kunahatarisha uhai wa mtu huyo. Kumbuka kwamba wachongezi walitoa ushahidi wa uwongo dhidi ya Nabothi, na hivyo kusababisha Nabothi apigwe mawe isivyo haki. (1 Fal. 21:8-13) Naam, mchongezi anaweza kuhatarisha uhai wa mtu mwingine kama inavyotajwa kwenye sehemu ya pili ya Mambo ya Walawi 19:16.
Zaidi ya hayo, mtu anaweza kumchongea mtu mwingine kwa sababu anamchukia. Kwenye 1 Yohana 3:15, tunasoma hivi: “Kila mtu anayemchukia ndugu yake ni muuaji, nanyi mnajua kwamba hakuna muuaji aliye na uzima wa milele ndani yake.” Inapendeza kuona kwamba baada ya maneno yaliyo kwenye mstari wa 16, Mungu alisema: “Usimchukie ndugu yako moyoni mwako.”—Law. 19:17.
Hivyo, maneno yaliyo kwenye Mambo ya Walawi 19:16 yanatoa himizo zito kwa Wakristo. Tunapaswa kuepuka mawazo mabaya na hatupaswi kamwe kumchongea mtu mwingine. Kwa ufupi, ‘tunahatarisha’ uhai wa mtu mwingine ikiwa tunaruhusu chuki au wivu utusukume kumchongea mtu huyo, na huenda hilo likathibitisha kwamba tunamchukia. Wakristo hawapaswi kumchukia mtu yeyote.—Mt. 12:36, 37.