Linda Dhidi Porojo Zenye Kudhuru!
“Katika wengi wa maneno hapakosi kuwa na maovu; bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili.”—MITHALI 10:19
1. Porojo zenye nia ya kuumiza, au uchongezi, zina uharibifu wa kadiri gani?
HAKUNA kiwezacho kubadili sumu yenye kuua iwe kinywaji chenye afya. Porojo zenye nia ya kuumiza, au uchongezi, zimefananishwa vizuri na sumu, ambayo yaweza pia kunyang’anya mtu mnyoofu jina lake zuri. Juvenal Mshairi Mroma aliuita uchongezi “ile sumu mbaya kuliko zote.” Na William Shakespeare mwanatamthilia Mwingereza alimtaja mmoja wa wahusika wa tamthilia (drama) yake kuwa akisema hivi: “Apokonyaye jina langu zuri, japo yeye hapati utajiri, anifanya maskini fakiri.”
2. Ni maswali gani yastahili ufikirio?
2 Lakini porojo ni nini hasa? Zatofautianaje na uchongezi? Kwa nini kulinda dhidi ya porojo? Na hilo laweza kufanywaje?
Jinsi Zatofautiana
3. Kuna tofauti gani kati ya porojo na uchongezi?
3 Porojo ni “maongeo ya kipuuzi, ambayo si sikuzote huwa ni ya kweli, kuhusu watu wengine na mambo yao.” Ni “maneno au maandishi mepesi, ya kutaja-taja mambo bila kujizuia sana.” Kwa kuwa sisi sote hupendezwa na watu, nyakati fulani sisi husema mambo mema, yenye kujenga kuhusu wengine. Uchongezi ni tofauti. Ni “ripoti bandia yenye kukusudiwa kudhuru jina na sifa nzuri ya mwingine.” Kwa ujumla maongeo ya jinsi hiyo huwa yenye nia ya kuumiza nayo si ya Kikristo.
4. Kulingana na mwandikaji mmoja, uchongezi waweza kuanzaje, nao hutokana na nini?
4 Huenda porojo zisizodhuru zikageuka kuwa uchongezi wenye nia mbovu. Alisema hivi mwandikaji Arthur Mee: “Mara nyingi uchongezi wenye kudhuru mtu, na labda kumletea uharibifu, huanza na porojo ambazo labda hapo kwanza huwa za kawaida tu. Ni moja la maovu makubwa zaidi ulimwenguni, lakini kwa kawaida hutokana na kutokuwa na maarifa mengi. Twazipata sana-sana miongoni mwa wasio na shughuli nyingi, wasio na lengo hususa maishani.”
5. Ni nini maana hasa ya shauri la Paulo kwenye 1 Timotheo 5:11-15?
5 Kwa kuwa maongeo ya kipuuzi huenda yakaongoza kwenye uchongezi, mtume Paulo alinena wazi dhidi ya wapiga-porojo fulani. Baada ya kutaja wajane waliostahili kupata usaidizi wa kundi, aliandika hivi: “Wakatalie wajane wachanga zaidi, kwa maana wakati misisimuko yao ya nyege iwapo imekuja kati yao na Kristo, . . . Wakati ule ule wao hujifunza pia kutokuwa na shughuli, wakitanga-tanga kwenye zile nyumba; ndiyo, si kwa kutokuwa na shughuli tu, bali pia wakiwa wenye porojo na wenye kujiingiza-ingiza katika mambo ya watu wengine, wakiongea juu ya mambo wasiyopaswa. Kwa hiyo mimi natamani wajane wachanga zaidi wafunge ndoa, wazae watoto, wawe na nyumba ya kusimamia, wasitoe kichochezi chochote cha kufanya mpinzani atukane. Kwa uhakika, tayari baadhi yao wamegeuziwa kando kumfuata Shetani.” — 1 Timotheo 5:11-15, NW.
6. Ni jambo gani lapasa kufanywa ili kushinda udhaifu wa kibinafsi wa porojo za namna iwezayo kuongoza kwenye uchongezi?
6 Kwa kuwa Paulo aliandika chini ya uvuvio wa kimungu, hakuwa akisema maneno yasiyofaa kuhusu wanawake hao. Hata hivyo, aliyosema yafaa kufikiriwa kwa uzito. Hakuna mwanamke yeyote mwenye kuhofu Mungu ataka ‘kugeukia kando amfuate Shetani.’ Hata hivyo, namna gani ikiwa mwanamke Mkristo apata kwamba ana udhaifu wa maongeo ya aina ile ambayo ingeweza kumfanya awe na hatia ya uchongezi? Hapo apaswa kutii kwa unyenyekevu shauri hili la Paulo: “Wanawake wapaswa . . . kuwa wenye uzito, si wachongezi.” Pia alisema hivi: “Acha wanawake wenye umri wawe wenye kicho katika kujiendesha, si wachongezi.” (1 Timotheo 3:11; Tito 2:3, NW) Akina ndugu pia wapaswa kulitumia shauri hilo la hekima kwa fikira timamu.
7. Kimaandiko, kwa nini wewe ungesema kwamba sisi sote twapaswa kudhibiti tusemayo?
7 Bila shaka, nyakati fulani sisi sote huongea kuhusu watu wengine, mambo waliyoona katika huduma, na kadhalika. Hata hivyo, tusipate kamwe ‘kuketi na kunena dhidi ya ndugu yetu.’ (Zaburi 50:19, 20, NW) Kweli kweli, ni jambo la hekima kutoongea mengi mno kwa sababu “katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na maovu; bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili.” (Mithali 10:19) Kwa hiyo yatupasa tulinde dhidi ya kupiga porojo, hata ikiwa hazionekani kuwa zenye kudhuru. Kwa uhakika, hatuna uhitaji wa kuongea kuhusu watu wakati wote, kwa kuwa tuna vichwa vya mambo mengi tuwezayo kuzungumza ikiwa twafikiria mambo ya uadilifu, yaliyo safi, yenye kupendeka, yenye nguvu za wema, na yenye kustahiki sifa.—Wafilipi 4:8.
Jinsi Porojo Huja Kuwa Uchongezi
8. Kwa nini si sikuzote liwapo ni kosa kuongea kuhusu Wakristo wenzetu?
8 Hakuna dhara katika kuongea kuhusu huduma ya shambani na utendaji mwingine wa kuhofu Mungu ufanywao na waamini wenzetu ikiwa tuna usahihi na ikiwa dhara halitokani na yale ambayo twasema. Kwa uhakika, maneno ya mwelekeo mzuri namna hiyo huenda yakawatia wengine moyo mkuu. (Linganisha Matendo 15:30-33.) Wakristo fulani waliongea kuhusu Gayo yule mwanamume mzee mwenye imani, ambaye mtume Yohana alimwandikia hivi: “Mpendwa, wewe unafanya kazi ya imani katika lolote lile ambalo wewe wafanyia akina ndugu, tena watu usiowajua, ambao wametoa ushuhuda kuhusu upendo wako mbele ya lile kundi.” (3 Yohana 5, 6, NW) Kwa hiyo si sikuzote liwapo ni kosa kuongea kuhusu Wakristo wenzetu.
9. (a) Ni jinsi gani maongeo mepesi yaweza kugeuka yakawa uchongezi juu ya walio wanyoofu? (b) Ni maswali gani ambayo kwa kufaa tungeweza kuuliza juu yetu wenyewe?
9 Hata hivyo, maongeo mepesi yaweza kugeuka kuwa uchongezi juu ya walio wanyoofu ikiwa sisi twapekua-pekua kindani kuhusu mambo yao ya faraghani, kutia, mashaka juu ya makusudio yao, au kuamsha shuku kuhusu mwenendo wao. Tungeweza kufanya liwe zoea letu kujiuliza maswali, kama haya: Je! uneni wangu ungeharibu sifa ya mtu mwingine? Je! nisemalo ni kweli? (Ufunuo 21:8) Je! ningesema jambo ilo hilo yeye akiwapo? Je! lingepanda fitina katika kundi? Je! taarifa zangu zingeweza kusababisha apoteze mapendeleo ya utumishi? Je! ingeweza kuwa kwamba nina husuda moyoni mwangu? (Wagalatia 5:25, 26; Tito 3:3) Je! matunda ya maneno yangu yangekuwa mema au maovu? (Mathayo 7:17-20) Je! ningalisema mambo yenye kufanana na hayo kuhusu mitume? (2 Wakorintho 10:10-12; 3 Yohana 9, 10) Je! maongeo hayo yawafaa wale ambao wana kicho kwa Yehova?
10, 11. Kulingana na Zaburi 15:1, 3, ni jambo gani ambalo sisi hatutafanya ikiwa twatamani kuwa mgeni wa Mungu?
10 Ikidokeza juu ya wale wenye kumcha Mungu, Zaburi 15:1 yasema hivi: “0 Yehova, nani atakuwa mgeni katika hema lako? Nani atakaa katika mlima wako matakatifu?” Kwa habari ya mtu huyo, mtunga zaburi Daudi alisema hivi: “Yeye hajachongea kwa ulimi wake. Hajamtenda mwandamani wake jambo lolote baya, na hajaanzisha suto dhidi ya mzoeani wake wa kindani.” (Zaburi 15:3, NW) Hapa neno ‘kuchongea’ limetoka kwenye kitenzi cha Kiebrania kinachomaanisha “kuweka jambo nyayoni” na hivyo “kwenda huku na huku.” Waisraeli waliamriwa hivi: “Usienda huku na huku ukieneza uchongezi miongoni mwa watu wako.” (Walawi 19:16, New International Version) Mtu yeyote ambaye ‘huenda huku na huku akieneza uchongezi’ si mgeni wala rafiki ya Mungu.
11 Rafiki za Mungu hawawatendi waandamani wao ubaya wowote na hawataanzisha, wala kuzipokea kuwa za kweli, hekaya zozote zenye kusuta wazoeani wanyoofu. Badala ya kueneza hadithi za bandia kuhusu waamini wenzetu na kuongezea masuto maovu ambayo tayari wao wayavumilia kwa kuletewa na wasiomhofu Mungu, yatupasa tunene vizuri juu yao. Hatungetaka kamwe kuongezea mizigo ya ndugu na dada zetu wenye imani kwa kusema mambo yenye suto kuwahusu.
Wakati Magumu Yatokeapo
12. Matendo 15:36-41 yaweza kutusaidiaje tukishawishwa kupiga porojo kuhusu mtu ambaye twakosa kukubaliana naye?
12 Kwa kuwa sisi ni wasiokamilika, huenda tukashawishwa kunena dhidi ya mtu ambaye tumekosa kukubaliana naye kwa njia nzito. Lakini fikiria lililotukia wakati mtume Paulo alipokuwa karibu kufunga safari yake ya pili ya kimisionari. Ingawa Barnaba alikuwa ameazimia Marko aandamane nao, Paulo hakukubali, “kwa kuona kwamba [Marko] alikuwa amewaondoka kutoka Pamfilia na hakuwa ameenda pamoja nao kwenye kazi.” Basi ikawa kwamba, “mfoko mkali wa kasirani” ulifuata, nao wakatengana. Barnaba alimchukua Marko akaenda pamoja naye Saiprasi, hali Paulo alifanya Sila akaenda pamoja naye kupitia Siria na Kilikia. (Matendo 15:36-41) Baadaye, ushuhuda waonyesha kwamba lile pengo la mtengano kati ya Paulo, Barnaba, na Marko lilizibwa, kwa maana Marko alikuwa pamoja na mtume katika Roma, na Paulo alinena mazuri juu yake. (Wakolosai 4:10) Hata ingawa kulikuwa kumekuwa na kutokubaliana, hakuna ushuhuda wa kwamba Wakristo hao walizunguka-zunguka wakichongeana miongoni mwa waamini wenzao.
13. Ni chini ya hali gani zenye kumhusisha Petro kwamba Paulo alikinza kile ambacho kingaliwezekana kuwa kishawishi cha kupiga porojo kuhusu Mkristo mwenzake?
13 Pia Paulo alikinza kile ambacho kingaliwezekana kuwa kishawishi cha kugeukia porojo alipomkaripia Kefa (Petro), ambaye alikuwa ameona aibu juu ya kula pamoja na waamini Wasio Wayahudi na juu ya kushirikiana nao kwa sababu ya kuwapo kwa Wakristo fulani Wayahudi wa kutoka Yerusalemu. Badala ya kuongea kuhusu Petro nyuma ya mgongo wake, Paulo “alimkinza uso kwa uso,” akinena wazi “mbele yao wote.” (Wagalatia 2:11-14, NW) Wala Petro hakupiga porojo juu ya mwenye kumkaripia. Kwa uhakika, baadaye alimrejezea kuwa “ndugu yetu mpenzi Paulo.” (2 Petro 3:15) Kwa hiyo hata ikiwa mwamini mwenzetu ahitaji kusahihishwa, hiyo haiandai udhuru wowote wa kupiga porojo kuhusu yeye. Kuna sababu nzuri sana za kulinda dhidi ya uneni wa jinsi hiyo na kukinza kishawishi cha kueneza porojo zenye kudhuru.
Kwa Nini Kulinda?
14. Ni nini sababu kubwa ya kutosikiliza au kutoeneza porojo zenye kudhuru?
14 Sababu kuu ipasayo kutufanya tusisikilize porojo zenye kudhuru au tusishiriki kuzieneza ni kwamba twataka kufurahisha Yehova, ambaye hulaani vikali uchongezi. Kama ilivyoonwa, maoni ya Mungu juu ya uneni wa jinsi hiyo yalionyeshwa wazi Waisraeli walipoamriwa hivi: “Usiende huko na huko katikati ya watu wako, kama mchongezi; wala usisimame kinyume cha damu ya jirani yako; mimi ndimi Bwana [Yehova, NW].” (Walawi 19:16) Ikiwa tutaona shangwe ya kuwa na upendeleo wa kimungu, hapo basi ni lazima sisi tusichongee mtu yeyote ambaye huenda tukamtaja katika maongeo yetu.
15. Ni nani aliye mchongezi mkubwa kupita wote, na kupiga porojo zenye kudhuru kwaweza kuwa na athari gani juu ya uhusiano wetu pamoja na Mungu?
15 Sababu nyingine ya kutojitia katika porojo zenye kudhuru ni kwamba zingeweza kuongoza kwenye kumwiga Shetani, yule mchongezi wa Yehova aliye mkubwa kupita wote. Huyu adui mkuu wa Mungu kwa kufaa alipewa jina “Ibilisi” (Kigiriki, di·aʹbo·los), ambalo lamaanisha “mchongezi.” Hawa aliposikiliza maongeo ya uchongezi wa Shetani dhidi ya Mungu na kuchukua kitendo cha kuutegemea, wanadamu wawili wa kwanza walitenganishwa na Rafiki yao aliye bora zaidi. (Mwanzo 3:1-24) Sisi tusijiachilie kamwe tukubali kufuata mbinu za Shetani na kuhusika katika uneni wenye kudhuru ambao wastahili kukosa kibali cha kimungu na ambao, kwa njia hiyo, waweza kututenganisha na Rafiki yetu aliye bora zaidi, Yehova Mungu.
16. Mchongezi ‘atenganishaje walio wazoeani’?
16 Haitupasi kuwasikiliza wenye kupiga porojo zenye nia ya kuumiza, kwa kuwa wao hutenganisha marafiki. Mara nyingi, wachongezi hutia chumvi, husingizia, husema uwongo, na hurundika milima ya maneno yenye kuwasha migogoro. Badala ya kunena na mtu uso kwa uso, wao hunong’oneza nyuma ya mgongo wake. Mara nyingi shuku zisizo na msingi huamshwa. Hivyo, “mchongezi anatenganisha wale ambao wamezoeana.”—Mithali 16:28, NW.
17. Kwa nini tulinde dhidi ya kuhusika kwa kina kirefu katika porojo nyepesi-nyepesi?
17 Yatupasa tulinde dhidi ya kuhusika kwa kina kirefu hata katika porojo nyepesi-nyepesi. Kwa nini? Kwa sababu huenda tamko lisilokusudiwa kuumiza mtu yeyote likawa na maumizo lirudiwapo. Huenda likapakwa-pakwa madoido au kupindwa mpaka liharibu sifa ya mtu mwenye kuhofu Mungu, likimnyang’anya jina lake zuri. Jambo hilo Likitukia, ungehisije ikiwa wewe ndiwe ulianzisha hadithi ile au hata ukaipitisha-pitisha? Watu wangeweza kukuona wewe kuwa mtu mwenye kuelekea kuleta jeraha, na kwa hiyo huenda wasitafute tena ushirika wako.—Linganisha Mithali 20:19.
18. Ni jinsi gani kupiga porojo kwaweza kufanya mtu awe mwongo?
18 Sababu nyingine ya kulinda ni kwamba porojo zenye kudhuru huenda zikakufanya wewe mwongo. “Maneno ya mchongezi ni kama vitoweo [vitu vya kumezwa kwa pupa, NW]. Nayo hushukia pande za ndani za tumbo.” (Mithali 26:22) Namna gani ukimeza mawongo na kurudia kuyasema? Ni kwamba, hata ikiwa wewe wafikiri mawongo hayo ni kweli, uyaenezapo unakuwa ukisema uwongo. Yatakapofunuliwa kuwa ya ubandia, huenda wewe ukaonwa kuwa mwongo. Je! wataka hilo litukie? Je! Mungu hawapasishi walimu bandia daraka la kujibu kwa mawongo yao ya kidini? Ndiyo, na pia yeye apasisha wajibu wa kutoa hesabu kwa wachongezi wanaosema uwongo. Yesu alionya hivi: “Kila neno la kipuuzi ambalo watu watanena watalitolea hesabu kwenye siku ya hukumu; kwa maana wewe utaachwa huru bila hatia kwa kutegemea maneno yako mwenyewe na kushutumiwa kwa kutegemea maneno yako mwenyewe.” (Mathayo 12:36, 37, Byington) Kwa kuwa “kila mmoja wetu atamtolea Mungu hesabu kwa ajili yake mwenyewe,” je! ungemtaka akulaani wewe vikali kuwa mchongezi anayesema uwongo? —Warumi 14:12, NW.
19. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba porojo zenye kudhuru zaweza kuua?
19 Bado sababu nyingine ya kutoeneza porojo zenye kudhuru ni kwamba zaweza kuua. Ndiyo, zaweza kuleta hatari ya kifo, zikiharibu sifa njema ya mtu asiye na hatia. Ndimi fulani ni ‘panga kali,’ na maneno machungu ni kama mishale yenye kufyatuliwa kutoka maoteoni kuwaelekea wasio na lawama. Daudi alisali hivi: “Wewe [Yehova] unifiche kutoka kwenye maongeo ya usiri wa watenda maovu, kutoka kwenye fujo za wazoeaji wa uumivu, ambao wamenoa ulimi wao sawasawa na upanga, ambao wameulenga shabaha mshale wao, uneni mchungu, ili wafyatulie mtu fulani asiye na lawama wakiwa kwenye maficho.” (Zaburi 64:2-4, NW) Je! wewe ungetaka uwe mwenye daraka la kusema maovu hayo kuhusu mwanadamu mwenzako mpaka ahisi akilazimika kumpelekea Mungu sala ndiyo apate kitulizo, kama mtunga zaburi alivyofanya? Je! wataka uwe na hatia ya kitu ambacho ni kama kuua?
20. (a) Kwa kadiri ambavyo kundi la Mungu lahusika, ni jambo gani laweza kupata mchongezi asiyetubu? (b) Ni lazima wazee wajizoeze tahadhari gani kwa habari ya porojo na uchongezi?
20 Uchongezi waweza kufanya mtu aondoshwe katika tengenezo la Mungu; mchongezi aweza kutengwa na ushirika, labda akiwa mwongo asiyetubu. Hata hivyo, kitendo hicho hakipasi kuchukuliwa kiwe cha kupigia porojo nyepesi-nyepesi. Wazee wapaswa kupima uzito wa mambo kwa sala, wakipambanua wazi sana tofauti iliyopo kati ya porojo tu na uchongezi mwovu. Ili atengwe na ushirika, ingekuwa lazima mtenda makosa awe ni mchongezi asiyetubu mwenye nia ya kuumiza. Wazee hawapewi mamlaka ya kutenga na ushirika mtu yeyote kwa sababu ya porojo ndogo-ndogo ambazo zaongozwa na hali ya kupendezwa na wanadamu lakini ambazo si za bandia wala zenye nia ya kuumiza. Ni lazima mambo yasikuzwe mno yauzidi ukubwa wayo, na ni lazima kuwe na mashahidi wenye ushuhuda hakika wa kuthibitisha kwamba pasipo shaka uchongezi wahusika. (1 Timotheo 5:19) Sababu ya msingi ambayo yafanya wachongezi wasiotubu waondoshwe nje ni ili hasa porojo zenye nia ya kuumiza zizimishwe, na kundi liepushwe kutiwa chachu ya dhambi. (1 Wakorintho 5:6-8, 13) Lakini wazee hawapaswi kamwe kuwa wenye haraka-haraka sana hata wamwondoshe nje mtu yeyote kwa sababu zisizo za Kimaandiko. Kwa njia ya sala na mashauri, mara nyingi wataweza kusaidia mtu atubu, aombe radhi au afanye marekebisho mengineyo, na kuzidi kufanya maendeleo katika kufuga ulimi.
Je! Ni Uchongezi?
21. Badala ya kupiga porojo kuhusu mtenda kosa, yakupasa wewe ufanye nini?
21 Mithali yenye hekima yasema hivi: “Mwenye kutembea huku na huku akiwa mchongezi anafunua maongeo ya usiri, lakini aliye mwaminifu katika roho anafunika jambo.” (Mithali 11:13, NW) Je! hiyo yamaanisha kwamba ukijua kwamba mtu fulani anajitia kwa siri katika dhambi nzito, ungekuwa uchongezi kusema lolote kuihusu? Sivyo. Bila shaka, haikupasi upige porojo kuhusu jambo hilo. Yakupasa unene na mtenda kosa huyo, ukimhimiza atafute msaada wa wazee. (Yakobo 5:13-18) Asipofanya hivyo baada ya muda wa kutosha, hangaikio la usafi wa kundi lapasa likusukume uripoti jambo hilo kwa wazee.—Walawi 5:1.
22. Kwa nini twaweza kusema kwamba 1 Wakorintho 1:11 haitoi mamlaka ya kupiga porojo?
22 Huenda tokeo la ripoti hiyo likawa ni kutiwa nidhamu kwa mtenda kosa huyo, na hilo halingeelekea kuwa jambo lenye shangwe. Hata hivyo, mtu mwenye kuzoezwa na nidhamu huvuna tunda la uadilifu. (Waebrania 12:11) Kosa lapasa kufunuliwa kwa wale waliowekwa rasmi kushughulikia mambo hayo, si kwa wapiga-porojo ambao waweza kupayuka-payuka ovyo kulihusu. Paulo aliwaambia hivi Wakristo katika Korintho: “Ndugu zangu, nimearifiwa habari zenu na wale walio wa nyumbani mwa Kloe, ya kwamba iko fitina kwenu.” (1 Wakorintho 1:11) Je! washiriki wa nyumba hiyo walikuwa wakipiga porojo kuhusu waamini wenzao? Sivyo, bali ripoti ilipelekwa kwa mzee mwenye daraka ambaye angeweza kuchukua hatua za kusaidia wenye kuhitaji msaada ili warudishe nyayo zao katika kijia cha uhai.
23. Ni swali gani limebakia kufikiriwa?
23 Tukisaidia mtu alinde dhidi ya kuhusika katika porojo mbovu zenye kudhuru, tunamtendea jambo la kumfaidi. Mithali yenye hekima yasema hivi: “Yeye alindaye kinywa chake huilinda nafsi yake; bali afunuaye midomo yake atapata uharibifu.” (Mithali 13:3) Basi, kwa uwazi kuna sababu njema za kulinda dhidi ya porojo zenye kudhuru na uchongezi mwovu. Hata hivyo, porojo zenye kudhuru zaweza kukandamizwaje kabisa? Makala inayofuata itaeleza.
Majibu Yako Ni Nini?
◻ Tofauti ni nini kati ya porojo nyepesi-nyepesi na uchongezi?
◻ Ni jinsi gani porojo zaweza kuwa uchongezi?
◻ Ni nini baadhi ya sababu za kulinda dhidi ya porojo zenye kudhuru?
◻ Kwa nini uchongezi hauhusiki wakati tutoapo ripoti kuhusu kosa zito la mtu mwingine?
[Picha katika ukurasa wa 14]
Hakikisha kwamba huwi kamwe na hatia ya kufyatua mtu mgongoni kwa kupiga porojo kuhusu yeye