Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Mei kur. 8-13
  • Yehova Hutupatia Faraja

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Hutupatia Faraja
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YEHOVA ANATUSAMEHE KWA REHEMA
  • YEHOVA ANATUPATIA TUMAINI
  • YEHOVA ANATULIZA WOGA WETU
  • Yehova “Huwaponya Waliovunjika Moyo”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Uwe Mwenye Kiasi Inapohusu Mambo Usiyoyajua
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Kamwe Hatuko Peke Yetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Maamuzi Yanayoonyesha Unamtegemea Yehova
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2023
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Mei kur. 8-13

MAKALA YA 20

WIMBO 7 Yehova, Nguvu Yetu

Yehova Hutupatia Faraja

“Asifiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.”—2 KOR. 1:3.

JAMBO KUU

Mambo tunayojifunza kutokana na jinsi Yehova alivyowafariji Wayahudi waliokuwa uhamishoni.

1. Eleza jinsi hali ya Wayahudi waliokuwa uhamishoni ilivyokuwa.

WAZIA jinsi ambavyo Wayahudi waliokuwa uhamishoni Babiloni walivyohisi. Walikuwa wameona nchi yao ikiharibiwa. Kwa sababu ya dhambi zao na za mababu zao, walikuwa wamechukuliwa kutoka kwenye nyumba zao na kupelekwa katika nchi ya kigeni. (2 Nya. 36:​15, 16, 20, 21) Ni kweli kwamba wakiwa Babiloni walikuwa na uhuru wa kadiri fulani wa kufanya shughuli zao za kila siku. (Yer. 29:​4-7) Hata hivyo, maisha hayakuwa rahisi, na hapakuwa mahali ambapo walitaka kuishi. Walihisije kuhusu hali yao? Hivi ndivyo mmoja wao alivyosema: “Kando ya mito ya Babiloni, hapo ndipo tulipoketi. Tulilia tulipokumbuka Sayuni.” (Zab. 137:1) Wahamishwa hao waliovunjika moyo walihitaji kufarijiwa, lakini wangepata wapi faraja?

2-3. (a) Yehova aliwafanyia nini Wayahudi waliokuwa uhamishoni? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

2 Yehova ni “Mungu wa faraja yote.” (2 Kor. 1:3) Akiwa Mungu mwenye upendo, anafurahia kuwafariji wale wote wanaomkaribia. Yehova alijua kwamba baadhi ya wahamishwa wangekubali nidhamu yake na kumrudia. (Isa. 59:20) Zaidi ya miaka 100 kabla ya kupelekwa uhamishoni, Yehova alimwongoza nabii Isaya aandike kitabu kinachoitwa kwa jina lake. Kwa kusudi gani? Isaya anaeleza hivi: “‘Wafarijini, wafarijini watu wangu,’ asema Mungu wenu.” (Isa. 40:1) Naam, kupitia kitabu cha Isaya, Yehova aliwapatia Wayahudi hao walio uhamishoni faraja waliyohitaji.

3 Kama Wayahudi hao waliokuwa uhamishoni, sisi pia tunahitaji faraja pindi fulani. Katika makala hii, tutachunguza njia tatu ambazo Yehova aliwafariji watu hao waliokuwa uhamishoni: (1) Aliahidi kuwasamehe wale waliotubu, (2) aliwapa watu wake tumaini, na (3) aliwasaidia wasiwe na woga. Tunapochunguza mambo hayo, ona jinsi tunavyoweza kunufaika na maneno ya Yehova yenye kufariji.

YEHOVA ANATUSAMEHE KWA REHEMA

4. Yehova alionyeshaje kwamba yeye ni Mungu mwenye rehema? (Isaya 55:7)

4 Yehova ni “Baba wa rehema nyororo.” (2 Kor. 1:3) Alionyesha sifa hiyo alipoahidi kuwasamehe wahamishwa waliotubu. (Soma Isaya 55:7.) Alisema hivi: “Nitakuonyesha rehema kwa upendo mshikamanifu wa milele.” (Isa. 54:8) Yehova angewaonyeshaje rehema? Ingawa bado Wayahudi wangehitaji kukabiliana na matokeo ya matendo yao, Yehova aliahidi kwamba hawangeendelea kubaki Babiloni milele. Wangekuwa uhamishoni kwa kipindi fulani cha wakati. (Isa. 40:2) Ni lazima maneno hayo yaliwafariji Wayahudi waliotubu!

5. Kwa nini tuna sababu kubwa zaidi ya kuthamini rehema za Yehova kuliko Wayahudi waliokuwa uhamishoni?

5 Tunajifunza nini? Yehova yuko tayari kuwasamehe watumishi wake kwa njia kubwa. Leo, tunaweza kuwa na uhakika zaidi kuliko Wayahudi waliokuwa Babiloni kwamba Yehova anasamehe dhambi zetu. Jinsi gani? Tunaelewa msingi wa msamaha wa Yehova. Mamia ya miaka baada ya Isaya kutoa unabii, Yehova alimtuma Mwana wake mpendwa aje duniani ili kutoa dhabihu kwa ajili ya watenda dhambi wote wanaotubu. Dhabihu hiyo inatoa msingi ili dhambi zetu “zifutwe,” yaani, ziondolewe kabisa. (Mdo. 3:19; Isa. 1:18; Efe. 1:7) Tunamtumikia Mungu mwenye rehema sana!

6. Tunanufaikaje tunapokazia fikira rehema za Yehova? (Tazama pia picha.)

6 Maneno ya Yehova yanayopatikana kwenye Isaya 55:7 yanaweza kutufariji ikiwa tumelemewa na hisia za hatia. Huenda baadhi yetu tunaendelea kuhisi hatia kwa sababu ya makosa ya zamani hata baada ya kutubu. Inaweza kuwa hivyo, hasa ikiwa bado tunateseka kwa sababu ya matokeo ya makosa yetu. Hata hivyo, ikiwa tumetubu dhambi zetu na kurekebisha mwenendo wetu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ametusamehe. Na Yehova anapotusamehe, anachagua kutokumbuka dhambi zetu. (Linganisha Yeremia 31:34.) Hivyo, ikiwa Yehova hakazii fikira dhambi zetu za zamani, sisi pia hatupaswi kufanya hivyo. Jambo muhimu kwa Yehova ni mambo tunayofanya sasa, si makosa tuliyofanya zamani. (Eze. 33:​14-16) Na hivi karibuni, Baba yetu wa rehema nyororo atatuweka huru milele kutokana na matokeo mabaya ya dhambi zetu.

Ndugu akitembea kwa uhakika. Mkusanyo wa picha: Picha zinaonyesha mambo aliyokuwa akifanya zamani na mambo anayofanya sasa. Makosa aliyofanya zamani: 1. Alicheza michezo ya video inayoonyesha jeuri. 2. Alikunywa kupita kiasi na kuvuta sigara. 3. Alitazama picha zisizofaa kwenye kompyuta yake. Mambo anayofanya sasa: 1. Akisafisha Jumba la Ufalme. 2. Akizungumza na dada mwenye umri mkubwa. 3. Akishiriki katika huduma.

Jambo muhimu kwa Yehova si makosa tuliyofanya zamani, bali ni mambo tunayofanya sasa (Tazama fungu la 6)


7. Ni jambo gani linaloweza kutuchochea kutafuta msaada ikiwa tumekuwa tukificha dhambi?

7 Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunasumbuliwa na dhamiri yenye hatia kwa sababu ya kuficha dhambi nzito? Biblia inatutia moyo tuwaombe msaada wazee wa kutaniko. (Yak. 5:​14, 15) Hata hivyo, huenda isiwe rahisi kwetu kuwaeleza dhambi tuliyofanya. Lakini tutachochewa kuwaendea wanaume hao waaminifu ikiwa tumetubu na kukumbuka kwamba Yehova na wanaume hao aliowaweka rasmi ili kutusaidia, watatuonyesha rehema kwa upendo. Fikiria jinsi rehema za Yehova zilivyomfariji ndugu anayeitwa Arthur,a ambaye dhamiri yake ilikuwa ikimsumbua sana. Anasema hivi: “Nilitazama ponografia kwa mwaka mmoja hivi. Lakini baada ya kusikiliza hotuba kuhusu dhamiri, nilimweleza mke wangu na wazee kuhusu dhambi yangu. Baada ya hapo, hatimaye nilipata kitulizo, lakini bado nililemewa na hisia za huzuni kwa sababu ya jambo nililofanya. Wazee walinikumbusha kwamba Yehova hajanikataa. Anatutia nidhamu kwa sababu anatupenda. Maneno yao ya fadhili yaligusa moyo wangu na kunisaidia kurekebisha njia yangu ya kufikiri.” Leo, Arthur anatumikia akiwa painia na mtumishi wa huduma. Inafariji sana kujua kwamba Yehova anatuonyesha rehema ikiwa tunatubu!

YEHOVA ANATUPATIA TUMAINI

8. (a) Yehova aliwapatia Wayahudi waliohamishwa tumaini gani? (b) Kulingana na Isaya 40:​29-31, tumaini hilo lingekuwa na matokeo gani kwa Wayahudi waliotubu?

8 Kwa maoni ya wanadamu, Wayahudi waliotekwa hawakuwa na tumaini lolote. Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Babiloni ilijulikana kwa kutowaachilia mateka. (Isa. 14:17) Hata hivyo, Yehova aliwapatia watu wake tumaini. Aliahidi kuwaweka huru watu wake, na hakuna jambo lolote ambalo lingeweza kumzuia. (Isa. 44:26; 55:12) Machoni pa Yehova, Babiloni ilikuwa kama mavumbi membamba. (Isa. 40:15) Mavumbi ambayo yakipulizwa kidogo tu, hayapo tena. Tumaini hilo lingekuwa na matokeo gani kwa Wayahudi waliohamishwa? Lingewafariji. Lakini pia lingeweza kufanya mengi zaidi. Isaya aliandika hivi: “Wale wanaomtumaini Yehova watapata nguvu tena.” (Soma Isaya 40:​29-31.) Naam, tumaini hilo lingewapatia nguvu tena; nao wangeweza “[kupaa] juu kwa mabawa kama tai.”

9. Ni mambo gani ambayo yangewapatia Wayahudi waliohamishwa sababu ya kutumaini ahadi za Yehova?

9 Yehova aliwapatia Wayahudi waliohamishwa sababu ya kutumaini ahadi zake. Jinsi gani? Fikiria kuhusu unabii mbalimbali ambao tayari ulikuwa umetimizwa. Walijua kwamba Waashuru walikuwa wameushinda ufalme wa kaskazini wa Israeli na kuwachukua watu kwenda uhamishoni. (Isa. 8:4) Waliwaona Wababiloni wakiliharibu jiji la Yerusalemu na kuwapeleka uhamishoni wakaaji wake. (Isa. 39:​5-7) Walikuwa hai Mfalme Sedekia alipopofushwa na kupelekwa Babiloni. (Yer. 39:7; Eze. 12:​12, 13) Kila jambo ambalo Yehova alitabiri lilitimia. (Isa. 42:9; 46:10) Bila shaka, lazima mambo hayo yote yaliimarisha imani yao kwamba ahadi ya Yehova ya kuwaweka huru ingetimia pia!

10. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuendelea kuimarisha tumaini letu katika siku hizi za mwisho?

10 Tunajifunza nini? Tunapovunjika moyo, tumaini linaweza kutufariji na kutusaidia kupata nguvu tena. Tunaishi katika nyakati za hatari na tunapingwa na maadui wa Mungu wenye nguvu. Hata hivyo, hatupaswi kuvunjika moyo. Yehova ametupatia tumaini zuri sana—uzima wa milele tukiwa na amani ya kweli na usalama. Ni lazima tuendelee kukazia fikira tumaini hilo akilini na moyoni mwetu. Tusipofanya hivyo, tumaini letu linaweza kufifia na kuwa kama mandhari maridadi ambayo hatuwezi kuiona vizuri kwa sababu tunaitazama kupitia dirisha chafu. Tunawezaje “kulisafisha dirisha hilo,” na kudumisha tumaini letu likiwa jangavu? Tunaweza kutenga wakati kwa ukawaida ili kuwazia jinsi maisha yetu yatakavyokuwa katika ulimwengu mpya. Tunaweza kusoma makala, kutazama video, na kusikiliza nyimbo zinazozungumzia tumaini letu. Na tunaweza kumweleza Yehova katika sala kuhusu ahadi ambazo tunatazamia kwa hamu kuona zikitimizwa.

11. Ni nini kinachomsaidia dada mwenye matatizo ya kudumu ya afya apate nguvu tena?

11 Fikiria jinsi ambavyo tumaini linamfariji na kumwimarisha dada anayeitwa Joy, ambaye ana matatizo ya kudumu ya afya. Anasema hivi: “Ninapolemewa na hisia, ninamweleza Yehova hisia zangu za ndani kabisa, nikijua kwamba ananielewa. Yehova amenijibu kwa kunipatia ‘nguvu zinazopita zile za kawaida.’” (2 Kor. 4:7) Pia, Joy anajiwazia akiwa kwenye ulimwengu mpya, ambapo “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isa. 33:24) Ikiwa sisi pia tutamweleza Yehova hisia zetu zote na kukazia fikira tumaini letu, tutaweza kupata nguvu tena.

12. Tuna sababu gani za kutumaini ahadi za Yehova? (Tazama pia picha.)

12 Kama alivyowafanyia Wayahudi waliohamishwa, Yehova ametupatia pia sababu nyingi za kutumaini ahadi zake. Fikiria kuhusu unabii mbalimbali ambao tunaona ukitimia leo. Kwa mfano, tunaiona serikali kuu ya ulimwengu ambayo ina “nguvu kwa sehemu na . . . dhaifu kwa sehemu.” (Dan. 2:​42, 43) Pia, tunasikia kuhusu “matetemeko ya ardhi sehemu mbalimbali,” na tunawahubiria watu kutoka katika “mataifa yote.” (Mt. 24:​7, 14) Unabii huo mbalimbali na mwingine mwingi unaimarisha imani yetu katika ahadi za Yehova zenye kufariji ambazo bado hazijatimia.

Dada akisoma na kutafakari unabii mbalimbali wa Biblia. Mkusanyo wa picha: 1. Wenzi wa ndoa wamesimama karibu na kigari cha machapisho wakizungumza na mwanamume. 2. Baba na mwana wake wakitazama uharibifu uliosababishwa na janga la asili. 3. Jiwe likiipiga miguu ya sanamu ambayo Nebukadneza aliiona kwenye ndoto kama inayoelezwa kwenye Danieli sura ya 2. 4. Watu wakifurahia maisha katika paradiso duniani.

Unabii mbalimbali ambao tunaona ukitimizwa leo, unatupatia sababu za kutumaini ahadi za Yehova (Tazama fungu la 12)


YEHOVA ANATULIZA WOGA WETU

13. (a) Wayahudi wangekabili changamoto gani wakati ambapo wangewekwa huru? (b) Kama inavyofafanuliwa kwenye Isaya 41:​10-13, Yehova aliwafariji jinsi gani Wayahudi waliohamishwa?

13 Ingawa Yehova aliwafariji Wayahudi waliohamishwa kupitia tumaini zuri sana, alijua kwamba wangekabili changamoto wakati ambapo wangewekwa huru. Yehova alikuwa ametabiri kwamba mwishoni mwa kipindi cha uhamisho wa Wayahudi, mfalme mwenye nguvu angeshambulia mataifa jirani na kutishia Milki ya Babiloni. (Isa. 41:​2-5) Je, Wayahudi wangehitaji kuogopa? Yehova aliwafariji watu wake mapema, akisema: “Usiogope, kwa maana mimi niko pamoja nawe. Usihangaike, kwa maana mimi ni Mungu wako.” (Soma Isaya 41:​10-13.) Yehova alimaanisha nini aliposema “mimi ni Mungu wako”? Hakuwa akiwakumbusha Wayahudi wamwabudu yeye—tayari walikuwa wanajua jambo hilo. Badala yake, alikuwa akiwakumbusha kwamba yeye bado yuko upande wao.—Zab. 118:6.

14. Yehova alifanya jambo gani lingine ili kuwasaidia Wayahudi wasiogope?

14 Pia, Yehova alituliza woga wa Wayahudi hao waliohamishwa kwa kuwakumbusha kuhusu nguvu zake nyingi sana na ujuzi wake mwingi. Aliwaambia Wayahudi waliohamishwa watazame juu mbinguni na kuona nyota. Aliwaambia kwamba aliumba nyota hizo na pia anazijua zote kwa majina. (Isa. 40:​25-28) Ikiwa Yehova anajua jina la kila nyota, bila shaka anajua jina la kila mtumishi wake! Na ikiwa Yehova alikuwa na nguvu za kuumba nyota, bila shaka ana nguvu za kuwasaidia watu wake. Naam, Wayahudi waliohamishwa hawakuwa na sababu ya kuhangaika au kuogopa.

15. Mungu aliwatayarishaje Wayahudi waliohamishwa kwa ajili ya matukio ya wakati ujao?

15 Pia, Yehova aliwatayarisha watu wake kwa ajili ya matukio ya wakati ujao. Katika sura zilizotangulia za kitabu cha Isaya, Mungu aliliambia hivi taifa hilo: “Ingieni katika vyumba vyenu vya ndani, na mfunge milango nyuma yenu. Jificheni kwa muda mfupi mpaka ghadhabu itakapopita.” (Isa. 26:20) Huenda andiko hilo lilitimizwa kwa mara ya kwanza Mfalme Koreshi alipolishinda jiji la Babiloni. Mwanahistoria wa Ugiriki ya kale anasema kwamba Koreshi alipoingia Babiloni, “aliwapa maagizo [wanajeshi wake] wawauwe watu wote ambao walikuwa nje ya nyumba zao.” Unaweza kuwazia jinsi wakaaji wa jiji la Babiloni walivyoogopa sana! Lakini huenda Wayahudi waliohamishwa waliepuka msiba huo kwa sababu walitii maagizo ya Yehova.

16. Kwa nini hatupaswi kuwa na wasiwasi kupita kiasi kuhusu wakati wetu ujao? (Tazama pia picha.)

16 Tunajifunza nini? Hivi karibuni tutakabili dhiki kuu zaidi katika historia ya wanadamu. Itakapoanza, watu ulimwenguni watachanganyikiwa na kuogopa. Lakini si watu wa Yehova. Tunajua kwamba Yehova ni Mungu wetu. Tutasimama wima, tukijua kwamba “ukombozi [wetu] unakaribia.” (Luka 21:28) Hata muungano wa mataifa utakapotushambulia, tutasimama imara. Yehova atatupatia ulinzi kupitia malaika na mwongozo utakaookoa uhai wetu. Atatupatiaje maagizo hayo? Tutahitaji kusubiri ili tuone. Hata hivyo, inaelekea kwamba tutapokea maagizo hayo kupitia makutaniko yetu. Kwa njia fulani, huenda makutaniko hayo yakawa ‘vyumba vyetu vya ndani,’ mahali ambapo tutapata usalama. Tunaweza kujitayarishaje kwa ajili ya matukio ya wakati ujao? Ni lazima tuwe karibu na ndugu na dada zetu, tutii kwa hiari mwongozo wa kitheokrasi, na kusadiki kabisa kwamba Yehova analiongoza tengenezo letu.—Ebr. 10:​24, 25; 13:17.

Ndugu na dada wakiwa katika chumba wakisoma Biblia pamoja wakati wa dhiki kuu. Wanatazama nje kupitia dirisha, ndugu mmoja anaponyoosha kidole kuonyesha anga la usiku.

Kwa kutafakari kuhusu nguvu na uwezo wa Yehova wa kutuokoa, hatutahitaji kuwa na wasiwasi kupita kiasi wakati wa dhiki kuu (Tazama fungu la 16)b


17. Unawezaje kutafuta faraja kutoka kwa Yehova?

17 Ingawa Wayahudi waliohamishwa wangekabili hali ngumu, Yehova aliwaandalia faraja ambayo wangehitaji. Atafanya hivyo kwetu pia. Hivyo, hata ukipatwa na nini wakati ujao, endelea kutafuta faraja kutoka kwa Yehova. Naam, uwe na imani kwamba Yehova atakuonyesha rehema zake nyingi. Dumisha tumaini lako likiwa na nguvu. Kumbuka, Yehova akiwa Mungu wako, huhitaji kuogopa chochote.

MAANDIKO YAFUATAYO YANAWEZAJE KUKUFARIJI?

  • Isaya 55:7

  • Isaya 40:​29-31

  • Isaya 41:​10-13

WIMBO 3 Tumaini, Nguvu, na Uhakika Wetu

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

b MAELEZO YA PICHA: Kikundi kidogo cha akina ndugu na dada kimekusanyika. Wana uhakika katika nguvu na uwezo wa Yehova wa kulinda watu wake popote wanapoishi duniani.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki