Wazee Je, Mutaburudisha ‘Nafsi Zilizochoka’?
Angela,a dada asiyeolewa aliye na miaka 30 hivi, ni mwenye wasiwasi kidogo. Anangojea wazee wa kutaniko. Watamuambia nini? Ni kweli kwamba alikosa mikutano fulani, lakini sasa amechoka kisha kupitisha siku nzima akiwahudumia wazee-wazee. Zaidi ya mahangaiko yake ya kila siku, ana wasiwasi sana kuhusu afya ya mama yake.
Ikiwa wewe ndiye ungemutembelea dada Angela, namna gani ungetia moyo ‘nafsi [hiyo] iliyochoka’? (Yer. 31:25) Lakini, acheni kwanza tuone namna gani wazee wa kutaniko wanaweza kujitayarisha ili kufanya ziara za uchungaji zenye kuburudisha.
MUFIKIRIE HALI ZA NDUGU NA DADA ZENU
Wakati fulani, sisi wote tunachokeshwa na kazi yetu ya kimwili ao madaraka yetu katika kutaniko. Kwa mufano, nabii Danieli ‘alichoka kabisa’ alipopata maono ambayo hakuelewa. (Dan. 8:27) Malaika Gabrieli ndiye aliyemutembelea ili kumutia moyo. Mujumbe huyo wa Mungu alimusaidia Danieli kuelewa maono hayo, na kumuhakikishia kwamba Yehova alisikia sala zake, na kwamba alikuwa angali ‘mutu mwenye kutamanika’ machoni pa Mungu. (Dan. 9:21-23) Wakati mwingine baadaye, maneno yenye kufaa yaliyosemwa na malaika mwengine yalimutia nguvu nabii huyo aliyekuwa amechoka.—Dan. 10:19.
Mbele ya kumutembelea mwamini mwenzako, chukua wakati wa kufikiria hali zake
Vivyo hivyo, mbele ya kumutembelea mwamini mwenzako ambaye labda amechoka ao amevunjika moyo, chukua wakati wa kufikiria hali zake. Anapambana na matatizo gani? Namna gani matatizo hayo yamemuchokesha? Ni sifa gani nzuri anazoonyesha? Richard, ambaye amekuwa muzee kwa miaka zaidi ya 20 anasema: “Ninakazia uangalifu sifa nzuri za ndugu na dada zangu.” Anaongeza hivi: “Kufikiria kwa uangalifu hali za ndugu na dada mbele ya kuwatembelea, kunafanya iwe rahisi kujua namna ya kuwatia moyo kulingana na mahitaji yao.” Ikiwa muzee mwengine atakusindikiza katika ziara ya uchungaji, kwa nini musifikirie pamoja hali ya ndugu ao dada yenu?
MUFANYE NDUGU NA DADA WAJISIKIE HURU
Labda utakubali kwamba si jambo rahisi mutu kueleza namna anavyojisikia. Kwa mufano, ndugu yako anaweza kushindwa kujieleza waziwazi mbele ya wazee waliokuja kumutembelea. Kwa hiyo basi, namna gani unaweza kumusaidia ajisikie huru kuongea? Kumuonyesha sura ya kicheko na kumutolea maneno fulani yenye kutia moyo kunaweza kuwa na matokeo mazuri. Kila mara Michael, ambaye amekuwa muzee kwa miaka zaidi ya 40, anaanza ziara zake kwa maelezo haya: “Unajua, kutembelea ndugu na dada nyumbani kwao na kuwajua vizuri zaidi ni moja kati ya mapendeleo mazuri sana ya muzee. Kwa hiyo nimekuwa nikingojea kwa hamu ziara ya leo.”
Unaweza kuanza mazungumuzo kwa sala. Katika sala zake, mutume Paulo alizungumuzia sifa za ndugu zake, kama vile imani, upendo, na uvumilivu. (1 Thes. 1:2, 3) Unapozungumuzia katika sala sifa za ndugu na dada unaotembelea, unatayarisha moyo wako na moyo wao kwa ajili ya mazungumuzo yenye kujenga. Maneno yako yanaweza pia kuwatia moyo. Ndugu Ray, ambaye ni muzee mwenye uzoefu alitambua jambo hili: “Wakati fulani, sisi wote tunasahau mambo mazuri ambayo tunatimiza. Kwa hiyo, wakati mutu fulani anatukumbusha mambo hayo, hilo linatuburudisha.”
MUWATOLEE ZAWADI YA KIROHO
Munaweza kuwatolea wengine “zawadi ya kiroho,” kama mutume Paulo alivyofanya, kwa kuwatolea wazo fulani la Maandiko, kupitia hata andiko moja. (Rom. 1:11) Kwa mufano, ndugu mwenye kushuka moyo anaweza kujisikia kuwa hafae, kama mutunga-zaburi aliyejilinganisha na “kiriba [mufuko wa ngozi] katika moshi” ambacho kimekunjamana. (Zab. 119:83, 176) Kisha kumufasiria kwa kifupi maneno hayo, unaweza kumuambia kwamba uko hakika kwamba ‘hajasahau’ amri za Mungu.
Vivyo hivyo, labda mufano wa sarafu ya drakma iliyopotea unaweza kumugusa moyo dada ambaye ameacha kutaniko ao ambaye ameregea kiroho. (Lu. 15:8-10) Labda sarafu hiyo iliyopotea ilikuwa sehemu ya mukufu wa shingoni uliofanyizwa na sarafu nyingi za feza. Kuzungumuzia mufano huo kunaweza kumusaidia dada huyo aone kwamba yeye ni wa maana sana katika kutaniko. Kisha kuzungumuzia jambo hilo, unaweza kuonyesha namna Yehova anamuhangaikia sana kwa kuwa yeye ni mumoja wa kondoo wake wadogo.
Kila mara ndugu zetu wanafurahia kutoa mawazo yao kuhusu maandiko ya Biblia. Kwa hiyo, usitawale mazungumuzo! Kisha kusoma andiko fulani linalohusiana na hali yao, unaweza kuwaacha watoe maelezo kuhusu maneno fulani makubwa ao mistari fulani ya andiko hilo. Kwa mufano, kisha kusoma andiko la 2 Wakorintho 4:16, muzee anaweza kuuliza hivi: “Je, umejionea namna Yehova anavyofanya upya mutu uliye kwa ndani, ni kusema, kukupatia nguvu mupya?” Kutumia njia hiyo kunaweza kufanya kuwe na “ubadilishanaji wa kitia-moyo” kinachofaa.—Rom. 1:12.
Kila mara ndugu zetu wanafurahia kutoa mawazo yao kuhusu maandiko ya Biblia
Unaweza pia kuburudisha ndugu ao dada kwa kuzungumuzia mutu fulani anayetajwa katika Biblia aliyepatwa na hali kama zao. Labda hali ya ndugu ao dada mwenye kuvunjika moyo inafanana na ile ya Hana ao Epafrodito, ambao walivunjika moyo wakati fulani lakini waliendelea kuwa watu wa maana sana mbele ya Mungu. (1 Sam. 1:9-11, 20; Flp. 2:25-30) Kwa nini usizungumuzie mifano fulani mizuri ya Biblia ikiwa hali zinaruhusu?
MUENDELEE KUWAHANGAIKIA
Munaweza kuonyesha kama munahangaikia kabisa ndugu na dada zenu kwa kuendelea kupendezwa nao kisha ziara muliyowafanyia. (Mdo. 15:36) Mwishoni mwa ziara ya uchungaji, munaweza kufanya mupango ili kuhubiri pamoja nao siku fulani. Ndugu Bernard, muzee mwenye uzoefu, anapokutana tena na ndugu ao dada ambaye alitembelea hivi karibuni, anamuuliza hivi kwa siri: “Je, mambo ni sawa sasa?” Kwa kuonyesha kupendezwa hivyo na wale ambao tumetembelea, tunaweza kujua ikiwa wana lazima tena ya musaada.
Huu ndio wakati ambao ndugu na dada zetu wana lazima sana ya kujikisia kuwa tunawahangaikia, tunaelewa hali zao, na kuwapenda. (1 Thes. 5:11) Kwa hiyo, mbele ya kufanya ziara ya uchungaji, muchukue wakati wa kufikiria hali za ndugu na dada zenu. Musali kwa ajili ya jambo hilo. Mutafute maandiko yanayolingana na mahitaji yao. Mukifanya hivyo, mutapata maneno yanayofaa ili kuburudisha ‘nafsi zilichoka’!
a Majina yamebadilishwa.