Je! Wewe Sikuzote Ni Mtumwa Wa Mojawapo Ya Desturi Za Mababu?
1 Yesu Kristo alisema: “Nanyi mtajua kweli, na kweli itawaweka nyinyi huru.” (Yn. 8:32, TUM) Ndiyo, kweli inaweka huru. Inaweka huru na ushirikina mbalimbali na mafundisho ya uongo, matumaini ya bure na matendo ya haya. Hata hivyo, kama katika nyakati za kale, mikazo mingi inafanywa leo juu ya Wakristo ili warudilie desturi fulani za mababu.—Gal. 4:9.
2 Mtu anapochukua uamuzi wa kuwa Shahidi wa Yehova, ni kwa sababu ana uhakika wa kwamba Biblia kwelikweli ni Neno la Mungu. (2 Tim. 3:16) Tunatambua pia kwamba inatuomba tufanye mabadiliko makubwa ili kuweza kumpendeza Muumba wetu. (Kol. 3:9) Mabadiliko hayo tunapaswa kuyafanya sisi sote, haidhuru rangi yetu ya ngozi, nchi yetu, kabila yetu au mawazo yetu, kwani Biblia inahakikisha kwamba sisi sote tulizaliwa katika dhambi. (Rom. 3:23) Tukiwa wasiokamilika na kwa kuwa tulikomalia katika matendo, desturi na mafundisho yanayoshawishwa na dhambi na wa mungu wa mfumo huu wa mambo, tunapaswa bila kuepuka kufanya mabadiliko ndani yetu.
3 Mabadiliko hayo yanaomba kwamba tutupilie mbali matendo yote na desturi zilizo tofauti na mafundisho ya Neno la Mungu. Msimamo huo unaweza kutufanya tuchekelewe au kutuletea uadui na wale wasiyokubaliana na imani yetu. Ndivyo ilivyo hasa katika Afrika ambako kuna mila (desturi) nyingi juu ya vilio, maombolezo na mazishi. Ni desturi mojawapo gani zinazoweza kuharibu imani ya Wakristo?
4 Kulia: Kulingana na kamusi moja, “kulia” humaanisha “kumwanga machozi, kuhuzunika kwa ajili ya kifo cha, kusikitika sana.” Je! tunaweza kumlaumu yule anayetoa machozi au kuhuzunika wakati anapopatwa na msiba? Inafikia tunalia kwa sababu ya makosa yetu au tunapopatwa na msiba. Kulia ni jambo la kawaida kabisa linalotuliza wakati mwingine mtu aliyepatwa na msiba. Kulingana na Maandiko, hakuna ubaya wowote kulia, kumwanga machozi au kusikitika, hata kulia sana, kifo kinapompata mtu tumpendaye.—2 Sam. 1:11, 12; 18:33; Yn. 11:35.
5 Hata hivyo, jinsi gani watu hulia wafu kulingana na asili? Wanapopata tu habari ya kifo katika familia, wanapaswa kuondoa mavazi yao yaliyo safi na kuvaa mavazi machafu. Wanawake wanapaswa kuvuruga nywele na kuanza kulalamika ili kuonyesha huzuni yao mbele ya wote. Wakati mwingine, wanalia kwa kunongoneza nyimbo zenye kujaa mafundisho ya uongo, kama vile imani katika kutokufa kwa nafsi. Wengine wanamuomba mfu asiwasahau na aone jinsi wanavyohuzunishwa na kifo chake. Ikiwa aliacha watoto, wanamuuliza ni nani aliyekabizi kutunza familia. Kwa kuchunguza, je! maneno hayo hayaonyeshi kwamba wanamuomba mfu ili atosheleze mahitaji ya familia yake? Ole ni kwamba, ilifikia kwamba wahubiri walio wakfu na kubatizwa wanatamka maneno hayo kwa kuwa wanaona na kusikia wengine wanafanya hivyo. Ndani ya nyimbo hizohizo, wamoja wanatoa ujumbe mbalimbali kwa washiriki wengine wa familia ambao tayari wamekwisha kufariki.
6 Je! Mkristo anaweza kushiriki katika mazoea hayo na kumpendeza Yehova? Neno la Mungu halifundishi kwamba mtu anayo nafsi isiyokufa. (Ezek. 18:4) Mkristo hatasema hivyo maneno kwa mtu aliyekufa wala kuimba kwa sauti ya chini nyimbo zinazounga mkono wazo la kutokufa kwa nafsi. Hakika, ni jambo la kawaida kupatwa na huzuni na hatungeweza kuwa na haya kuionyesha. Kifo cha mtu mpendwa huwa ni hasara yenye kuogopesha, ambayo inatuumiza sana. Hata hivyo, hatudanganywi na hadithi za kuwazia tu zinazodai kwamba mtu ana nafsi isiyokufa au kwamba anaendelea kuishi katika “ulimwengu wa roho.” Tunaweza hivyo kuwa wenye kusikitika, lakini si kama wale wasio na tumaini.—1 Thes. 4:13.
7 Matanga ya Wafu: Katika mataifa mengi ulimwenguni, mazoea ya maombolezo ni mengi. Watu walio na kilio wanapitisha mara nyingi usiku mzima, huenda hata siku nyingi usiku, kwa mfu, ambako moto unachochewa kwa kuendelea. Familia, marafiki, majirani na hata watu ambao hawakumjua kamwe mtu aliyekufa alipokuwa mzima, wanakusanyika kando kando ya mfu ili kukesha juu yake mpaka asubuhi. Makusanyiko hayo yanadumu siku zote ambazo maiti itabaki yenye kutiwa hadharani, hasa ikiwa aliyekufa alikuwa mtu mkubwa. Wakati mwingine, washiriki wa familia yake wanafanya hotuba ndogo mbele ya watu wote ili kuonyesha kutokuhusika kwao katika kifo cha mtu huyo. Mazoea mengi ya kipagani yanaweza kufanyika. Wale wanayoyatenda wanayafanya mara nyingi kwa kumuogopa mtu aliyekufa, ili ‘kumuonyesha’ ni mara ngapi walimpenda na ni mara ngapi wanahuzika na kifo chake. Lakini nini inapaswa kuwa mwenendo wa yule anayetaka kumpendeza Muumba wake?
8 Neno la Mungu linafundisha kwamba wafu hawana uhai, hawawezi kuona, kusikia, kusema au kufikiri. (Muh. 9:5, 6, 10) Hawawezi hivyo kusumbua walio hai. Wafu hawasimami kando ya maiti zao, wakitazama mambo wanayofanyiwa. Tukiwa na ujuzi huo, je! hatungepaswa kujiepusha kufanya matanga ya wafu? Hakika, matanga yana kusudi la kuwezesha mfu “kuondoka kaburini” na kujiunga na wafu wengine. Kufuata desturi hizo je! haitakuwa ni kushiriki ibada ya wafu?
9 Wamoja walipenda kujua ikiwa ni vibaya kukesha bila sherehe na mazoea mengine ya kidesturi. Tuseme ikiwa mtu alifia hospitalini, je! haiwezekani kumpeleka moja kwa moja kwenye kaburi lake? Tunapata faida gani kuleta maiti yake nyumbani? Na ikiwa mtu anafariki nyumbani kwake, je! hatuwezi kumzika haraka? Ni jambo nzuri kabisa ikiwa maiti inapelekwa moja kwa moja kwenye kaburi. Si kwamba tu tunajilinda hivyo na uambukizaji iwezekanavyo, lakini tunaepuka pia kufanya matanga pamoja na sherehe zayo zote. Katika vijiji ambako hakuna kupata kwanza vyeti vya serikali ili kumzika mfu, kwa nini kutokumzika mfu mwishoni mwa mchana? Tukumbuke kwamba hata mwili wa Yesu haukufanyiwa matanga. Pia, haidhuru desturi pekee za eneo au za nchi ziweje, tunataka kumuheshimu Yehova, ambaye alituokoa kutoka giza, kwa kutupilia mbali zoea lolote linalohusiana na wafu.
10 Inafikia kwamba tunalazimika kulinda maiti nyumbani kwa sababu kifo kilitukia mwishoni mwa mchana. Katika miji mikubwa, ni vizuri na jambo lenye usafi kulinda maiti katika nyumba ya maiti hospitalini. Ikiwa hilo haliwezekani, tunaweza kutayarisha vikundi vingi vya akina ndugu watakaokomboana usiku ili kulinda maiti. Katika hali hiyo, ndugu watapaswa kuwa imara sana ili kwamba watu wa ulimwengu wasifanye desturi za kimababu juu ya maiti. Malaika mkuu Mikaeli hakumruhusu Ibilisi kucheza na mwili wa Musa.—Yuda 9.
11 Inaweza pia kutufikia kuhudhuria sherehe za mazishi za mtu wa ukoo ambaye hakuwa mwabudu wa Yehova. Ikiwa daraka la mazishi ni juu yetu, hatutaruhusu kwamba wafanyie ibada ya wafu chini ya uongozi wetu. Kinyume na hilo, ikiwa daraka si juu yetu, hatutatafuta kwamba kanuni za Biblia zitumikishwe.
12 Je! Tunapaswa Kulipa Faini? Mara nyingi, desturi inaomba tulipe faini (fedha). Zoea hilo linamaanisha kwamba yule ambaye wanamlazimisha kulipa faini anaonwa kama msababishi wa kifo cha mtu aliyekufa. Hata hivyo, Neno la Mungu linaonyesha kwamba kifo kinatokana na dhambi ya Adamu. Pia, hakuna Mkristo wa kweli atataka kukubaliana na desturi hiyo. (Rom. 5:12) Hakika, washiriki wa familia yetu wanaweza kutofurahia msimamo wetu, lakini tunapaswa kujionyesha kuwa imara na kukubali kuvumilia upinzani wowote wa familia.—Mt. 10:35-37.
13 Tunaweza kuwatembelea wale walio na kilio ili kuwafariji. Wakati mwingine, tunaweza kusaidia kununua sanduku au sanda, au kuchimba kaburi. Hilo ni jambo lenye kusifika. Hata hivyo, tunapaswa kuwa hakika kwamba mchango wetu hautumiwi kwa kulipia sherehe za kipagani. Ni kwa sababu hiyo inafaa kutoa mchango wetu kwa siri kwa ndugu au dada aliyefiwa.—Mt. 6:2-4.
14 Utakaso: Desturi fulani zinamuona mtu aliyefiwa na mwenzi wake wa ndoa kuwa mchafu. Kufuatana na desturi hizo, mtu hapaswi kuoga muda wa siku fulani, huenda hata miezi. Hapaswi kuchanua nywele na anapaswa kuvaa mavazi meusi. Kabla ya kurudi kwenye maisha ya kawaida, anapaswa kutakaswa. Siku ya utakaso, wanamnyoa kichwa na wanamvalisha mavazi meupe. Wakati mwingine, wanamuomba mjane kufanya ngono na mmoja wa mashemeji wake au mtu mwingine wa ukoo wa mume au mke aliyekufa. Ni baada tu ya sherehe hizo ndipo ataweza kuwa na ruhusa ya kuoa au kuolewa upya. Zoea hilo ambalo linahusu pia wanaume, hufikiriwa kuwa linatakasa mjane mwanamke au mwanaume na “roho” ya yule aliyekufa. Hata hivyo, kama mfalme Daudi alivyoonyesha, ni wakati mtu ni mgonjwa kwamba tunaweza kumuangaikia na si wakati amekwisha kufa. (2 Sam. 12:21-23) Pia, tunapaswa kujionyesha tofauti na ulimwengu kwa kutupilia mbali mazoea ya utakaso.—Eph. 4:17, 18. w95 15/8 pp. 28-30
15 Ujenzi wa Makaburi na Maneno Yanayotolewa kwa Wafu: Ujenzi wa makaburi unatokeza mara nyingi nafasi za sherehe nyingine za kipagani kwa kiasi fulani. Kabla ya kuzika, wanajielekeza wakati mwingine kwa mfu kwa kusema: “Angalia nyumba yako. Kwa sasa tunakuomba uichukue na kukaa ndani.” Kwa kuwa wafu hawasikii wala hawajui lolote, Wakristo wa kweli hawatafuata desturi ambayo inaomba kusema kwao. (Muh. 9:5, 6) Ikiwa Mkristo anajiingiza katika mojawapo ya desturi zinazoambatana na wafu na hatubu, anaweza kutengwa na kutaniko kwa sababu ya ibada ya sanamu.—1 Kor. 5:11; Kumb. 18:10, 11. w94 15/11 pp. 3-7
16 Tuishi katika tumaini la ufufuo wa wafu na tutupilie mbali mazoea ya ulimwengu huu wenye giza. Tukomaze chuki kwa yote isiyompendeza Yehova. (Ebr. 1:9) Hilo litatulinda katika nyakati za majaribu. Tubaki katika nafasi ya usalama wa kiroho ya Yehova kwa kuepuka kufanya desturi za mababu zilizo kinyume na Maandiko. Hivyo tutakubaliwa na Yehova, Mungu wa ukweli.—Zab. 31:5.