Majibu Kwa Maulizo Yenu
◼ Kwa nini tungepaswa kuwa waangalifu kuhusu mvalio wetu na kujipamba kwetu tunapotembelea makao ya Sosaiti Brooklyn, Patterson na Wallkill (New York), vilevile katika matawi kuzunguka ulimwengu?
Wakristo wanapaswa kwa ukawaida kutii utaratibu. Kila wakati, mvalio wetu na kujipamba kwetu vinapaswa kuonyesha adabu na heshima inayostahili watumishi wa Yehova Mungu. Hilo ni kweli zaidi tunapotembelea makao ya Sosaiti New York na katika matawi kuzunguka ulimwengu.
Katika 1998 yatafanyika makusanyiko ya wilaya na ya kimataifa. Maelfu mengi ya ndugu zetu watatembelea makao makuu ya Sosaiti New York, vilevile matawi ya nchi nyinginezo. Tunapotembelea makao hayo, si wakati huo tu, lakini kwa wakati mwingine wowote, tunapaswa ‘katika kila njia kujipendekeza wenyewe kuwa wahudumu wa Mungu,’ kutia ndani jambo la kuwa na mvalio na kujipamba kwa ajili ya matukio ya pekee.—2 Kor. 6:3, 4.
Kinapozungumza juu ya umaana wa kuvaa na kujipamba ifaavyo, kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu kinataja ulazima wa kuwa safi, vilevile kuvaa kwa kiasi na kujipamba vizuri tunapohubiri au kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Kisha, kwenye ukurasa 131, kwenye fungu 2, kinajulisha: “Jambo ilo hilo lingehusu wakati wa kutembelea makao ya Betheli katika Brooklyn au katika yo yote ya afisi za tawi za Sosaiti. Kumbuka, jina Betheli maana yake ni ‘Nyumba ya Mungu,’ hivyo mavazi yetu, kujipamba kwetu na mwenendo wetu umepasa uwe namna ile ile tunayotazamiwa kuwa tunapohudhuria mikutano ya ibada kwenye Jumba la Ufalme.” Viwango hivyo hivyo vya juu vinapaswa kufuatwa na wahubiri wa Ufalme wanaoishi kando kando na wale wanaotoka mbali ili kuona washiriki wa familia ya Betheli au kuangalia makao ya tawi.
Mvalio wetu ungepaswa kutoa kwa wengine maoni mazuri juu ya ibada ya kweli ya Yehova. Hata hivyo, imeonwa kwamba ndugu na dada fulani wanaotembelea makao ya Sosaiti huwa na mvalio wa ovyo ovyo sana. Mvalio wa namna hiyo haufai tunapotembelea Betheli. Kwa upande huo kama vile katika pande zote za maisha yetu ya Kikristo, tunatamani kuheshimu viwango vya juu vile vile, viwango ambavyo vinafanya watumishi wa Mungu kuwa tofauti na ulimwengu katika maana ya kwamba wanafanya yote kwa utukufu wa Mungu. (Rom. 12:2; 1 Kor. 10:31) Ni jambo zuri vilevile kukumbusha watu wanaojifunza Biblia pamoja nasi au wengine ambao watatembelea Betheli kwa mara ya kwanza umaana wa kuwa waangalifu kwa mvalio wao na kujipamba kwao.
Hivyo, unapotembelea makao ya Sosaiti, jiulize mwenyewe: ‘Je! mavazi yangu na kujipamba kwangu ni vya kiasi?’ (Ona Mika 6:8.) ‘Je! vinawakilisha vizuri Mungu ninayemwabudu? Je! wengine watakengeushwa fikira au kufadhaishwa na mwendo wangu? Je! mimi ninatoa mfano kwa wale wanaotembelea Betheli kwa mara ya kwanza?’ Sikuzote, kupitia mvalio wetu na kujipamba kwetu, na tuendelee “kuremba fundisho la Mwokozi wetu, Mungu, katika mambo yote”!— Tito 2:10.