Utasema nini kwa Mhindu?
1 Kama unavyojua labda, kuna Wahindu wengi wanaoishi katika nchi mbalimbali, kutia ndani nchi hii. Hilo lamaanisha kwamba huenda wakati fulani ukakutana na Mhindu unapokuwa ukiendesha huduma yako. Utakapokutana naye, utashughulikaje na ziara hiyo?
2 Kumbuka mambo haya: Wamishonari ambao, kwa matokeo, wametoa ushahidi kwa Wahindu wamesema kwamba si lazima kujifunza Uhindu kwa kina kirefu ili kutoa ushahidi wenye matokeo. Mara nyingi, utoaji wa kweli ulio rahisi na wenye busara huleta itikio lenye kufaa. Omba upewe nafasi ya kusema kwanza na kichwa cha familia. Ikiwa itikio lake ni lenye kufaa, itakuwa rahisi zaidi kutoa ushahidi kwa washiriki wengine wa familia. Mwanzoni, epuka kutokeza wazo la kwamba unaleta ujumbe ulio wa juu kuliko yale ambayo mwenye-nyumba anaamini au kwamba unataka kuzungumza juu ya Mungu pekee wa kweli au maandishi matakatifu ya zamani zaidi. Kwa kuwa Wahindu wengi huona Biblia kuwa kitabu ya Magharibi, unaweza kuvunja ubaguzi kwa kufasiria kwamba hiyo haiendelezi ukoloni au ukuu wa rangi fulani ya mwili kuliko rangi nyinginezo.
3 Tumia vifaa vyenye kufaa: Broshua mbili zimetayarishwa kwa kufikiria Wahindu. Hizo ni Pourquoi adorer Dieu en amour et en vérité ? na Nos problèmes — Qui nous aidera à les résoudre ? Zote mbili zinapatikana katika Kifaransa. Broshua “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya” na Je! Kweli Mungu Anatujali? zimeonekana pia kuwa zenye matokeo wakati wa kutoa ushahidi kwa wale walio na malezi ya Kihindu. Broshua Anataka na kitabu Ujuzi vinaweza kutumiwa kwa matokeo ili kuongoza mafunzo ya Biblia.
4 Sitawisha uwanja wa makubaliano: Si vigumu kupata uwanja wa makubaliano na Mhindu. Wanaamini kwamba tunaishi wakati ambapo uovu umefikia kilele chake na kwamba Mungu ataondolea ulimwengu matatizo yake kupitia msiba mkubwa utakaofuatwa na kipindi cha wakati cha kweli. Unaweza kuona jinsi imani hizo zinavyoweza kwa urahisi kuhusianishwa na mafundisho ya Biblia kuhusu siku za mwisho, dhiki kubwa, na ulimwengu mpya wenye kuja. Kwa kuwa Wahindu wengi huona maisha kuwa mfuatano wa matatizo yasiyokuwa na utatuzi, wao hupendezwa na habari kuhusu maisha ya familia, uhalifu na usalama, na kile kinachotukia wakati wa kifo. Zifuatazo ni utoaji mbili ambazo unaweza kujaribu:
5 Huu unaweza kupendeza mume wa familia:
◼ “Mimi ni mwenye kutembelea watu wanaohangaishwa na hali ya familia katika nchi nyingi leo. Unafikiri ni nini kitakachosaidia kudumisha umoja wa familia? [Acha mtu ajibu.] Watu fulani wanajua kile ambacho maandiko ya Kihindu husema juu ya maisha ya familia, lakini hawajapata kamwe nafasi ya kulinganisha hilo na kile ambacho Biblia inasema juu ya jambo hilo. Ningependa kushiriki nawe wazo hili kwenye Wakolosai 3:12-14.” Baada ya kusoma andiko, onyesha mwenye-nyumba sura 15 ya kitabu Ujuzi na useme: “Ningefurahi kupitisha wakati kidogo nikisoma sura hii pamoja nawe.”
6 Kijana anaweza kuitikia utoaji ufuatao:
◼ “Bila shaka unaamini Mungu. Unafikiri kusudi la Mungu ni nini kutuelekea sisi? Acha mtu ajibu. Kisha soma Mwanzo 1:28, na useme: “Mahali pengi duniani kuna watu wengi kupita kiasi na kuna matatizo mengi. Je! unafikiri Muumba angekuwa mwenye kutaka kutusaidia kutatua matatizo yetu?” Baada ya kusikiliza jibu, vuta uangalifu juu ya kichapo chenye kufaa.
7 Furahia matokeo mazuri: Mwanamume mmoja Mhindu mwenye umri wa miaka 22 alimkaribia dada mmoja aliyekuwa akitoa ushahidi sokoni na akaomba funzo la Biblia. Alimfasiria kwamba, miaka minane mapema, alisikiliza mazungumzo ya Biblia kati ya dada huyo na mama wa mwanamume huyo. Ijapokuwa mwanamume huyo aliguswa na majibu yenye mafaa ambayo Biblia hutoa kwa matatizo ya wanadamu, mama yake hakupendezwa, na mwanamume huyo alijiona kuwa mtoto sana ili kufuata kweli yeye mwenyewe. Sasa, akiwa mwenye umri mkubwa, yeye alitaka kujifunza mengi zaidi. Mwanamume huyo kijana hakupoteza wakati. Baada ya siku 23 tu, yeye alimaliza kitabu Ujuzi, na akaomba kubatizwa miezi minne tu baada ya kukutana na dada sokoni!
8 Ndugu mmoja alianzisha funzo pamoja na mwanamume Mhindu aliyekutana naye katika gari-moshi. Mwanamume huyo alikuwa na matatizo katika familia yake. Yeye alikuwa pia na tatizo la kulewa pombe. Mwanamume huyo alikubali Shahidi yule amtembelee na kushiriki shauri la Biblia juu ya maisha ya familia. Fundisho la kiadili la Biblia lilimpendeza, na akakubali funzo la Biblia. Yeye na familia yake wakaanza kuhudhuria mikutano pamoja. Baadaye, walishiriki kweli pamoja na marafiki na watu wa familia. Hadi sasa, sita kati ya watu hao wamekubali kweli!
9 Mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4) Hilo latia ndani wanaume na wanawake wanaoamini dini zisizo za Kikristo, kama vile Uhindu. Ikiwa kuna Wahindu katika eneo lenu, kwa nini usiwatembelee mapema na kutumia baadhi ya madokezo yanayotolewa katika makala hii?