Je, wewe unayo roho ya kujinyima?
1 Shukrani kwa yale ambayo Yesu Kristo alifanya bila uchoyo kwa ajili ya wanadamu inapaswa kutuchochea sisi sote tutumie uwezo wetu mbalimbali, nishati yetu, na nguvu zetu kwa namna ya kujinyima. Maandiko yanahimiza: “[Toeni] miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu.” (Rom. 12:1) Kujichunguza pindi kwa pindi kutakusaidia uone ikiwa wewe ni mwenye kuonyesha aina hiyo ya roho kikamili kadiri hali zako binafsi zinavyoruhusu.
2 Katika ufuatiaji wa ujuzi wa Biblia: Je, umeweka kando wakati kwa ajili ya usomaji wa kibinafsi na funzo la Biblia la kawaida? Je, unashikamana na programu hiyo? Je, ni kawaida yako kujitayarisha vizuri kwa ajili ya mikutano ya kutaniko? Ikiwa wewe ni kichwa cha familia, je, unalo funzo la Biblia la kawaida pamoja na watu wa nyumba yako? Huenda kufanya mambo hayo kukaomba kujinyima wakati unaopitishwa mbele ya televisheni au kwenye kompyuta au utendaji mwingine mbalimbali. Hata hivyo, ni kujinyima mambo madogo kama nini, ukijua kwamba wakati unaopitisha kwa kujifunza neno la Mungu utasaidia kukuongoza kwenye uhai udumuo milele!—Yn. 17:3.
3 Katika kuzoeza watoto wako: Wakati bora zaidi wa kuanza kujifunza maisha ya kujinyima ni katika utoto. Wafundishe watoto wako kwamba kwa kuwa kuna wakati wa kucheza, kunapaswa pia kuwa wakati wa kazi na wa utendaji mbalimbali wa kitheokrasi. (Efe. 6:4) Wape kazi fulani yenye mafaa ya kufanya kuzunguka nyumba. Panga programu ya kawaida ya kushiriki katika huduma pamoja nao. Kaza mafundisho yako kwa kutoa mfano mzuri wewe mwenyewe.
4 Katika utendaji mbalimbali wa kutaniko: Kutaniko ni lenye kutajirishwa wakati kila mmoja humo hujinyima vitu kwa ajili ya faida ya wote. (Ebr. 13:16) Je, inawezekana kwako kupitisha wakati mwingi zaidi katika kazi ya kufundisha na kufanya wanafunzi? Je, unaweza kujitoa kusaidia wagonjwa au watu wazee-wazee, labda kuwasaidia katika kuwasafirisha mpaka kwenye mikutano?
5 Kabla ya kutoa dhabihu kubwa zaidi ya uhai wake wa kibinadamu, Yesu alishauri wanafunzi wake wakaze macho yao juu ya faida za Ufalme, wakiweka mambo mengine yote pa nafasi ya pili maishani. (Mt. 6:33) Kufuatia roho hiyo ya kujinyima kutatuletea furaha kubwa zaidi kadiri tunavyoendelea kutumikia Yehova kwa shangwe.