Mvalio Unaostahili, Ni Alama ya Usafi wa Kiadili
1 “Mashahidi wa Yehova ni watu wazuri kabisa! Watu wenu ni wenye fadhili na wanaovaa vizuri, wanaonyesha heshima sana.” Hivyo ndivyo alivyosema mwakilishi mmoja wa hoteli kuhusu ndugu na dada kwenye mkusanyiko mmoja wa wilaya mwaka uliopita. Kwenye mkusanyiko mwingine, mfanyakazi mmoja wa hoteli alieleza: “Inaonekana wazi kwamba watu wenu wanavaa ili kumfurahisha Mungu.” Ndiyo, wahudhuriaji wa mkusanyiko wanatambuliwa na wengine. Kwa hiyo, tunataka kuvaa “kwa namna inayostahili habari njema,” na hilo linachochea wale wasio Mashahidi kutupongeza na linaonyesha wazi kwamba sisi ni wahudumu wa Mungu. (Flp. 1:27) Tunapojitayarisha kwa ajili ya mkusanyiko wa wilaya, ni jambo linalofaa kufikiri mbele ya wakati kuhusu mvalio wetu.
2 Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili.” (Yak. 3:17) Kuonyesha usafi wa kiadili katika kuvaa kwetu kunaweza kuwa tatizo. Ulimwengu wa Shetani wenye ukosefu wa adili unavutia watu kukubali mitindo isiyo ya kiasi, yenye kuamsha tamaa za mwili, na isiyofaa. (1 Yo. 2:15-17) Kwa sababu hiyo, tunapofanya maamuzi kuhusu mavazi na kujipamba, tunahitaji kusikiliza shauri la Biblia linalotuomba “kukataa kabisa kutomwogopa Mungu na tamaa za kilimwengu na tuishi kwa utimamu wa akili . . . katikati ya mfumo wa mambo wa sasa.” (Tito 2:12) Hatutataka kamwe mvalio wetu uwasumbue wengine, iwe ndugu zetu, wafanyakazi wa hoteli na mkahawa (restaurant), au watu wengine wanaotutazama.—1 Kor. 10:32, 33.
3 Mavazi Yenye Mpangilio Mzuri Pamoja na Kiasi: Unapojitayarisha kwa ajili ya mkusanyiko, jiulize: ‘Je, mavazi yangu ni yenye kiasi, au yanavutia uangalifu usiofaa kwangu? Je, yanaonyesha heshima kwa hisia za wengine? Je, blauzi (blouse) zangu ni zenye kuacha wazi kifua au tumbo? Je, mavazi yangu ni yenye kuonyesha uchi au kubana sana? Je, ni safi na yasiyotoa harufu mbaya? Ninapotumia chakula kwenye hoteli au kujiburudisha baada ya mkusanyiko, je, mvalio wangu utakuwa mzuri, na safi kama wa mhudumu, au mavazi yangu yatakuwa ya ovyoovyo, yanayopita kiasi, yasiyopatana na hali na yasiyofaa mhudhuriaji wa mkusanyiko anayevaa kadi ya utambulisho? Mavazi ninayotumia wakati wa kujiburudisha yananifanya nisikiye haya ya kutoa ushahidi wa vivi hivi?’—Rom. 15:2, 3; 1 Tim. 2:9.
4 Tunaweza kufaidika na mapendekezo ya Wakristo waliokomaa. Wake wanapaswa kuuliza waume wao jinsi wengine wanavyoweza kuona mavazi yao. Wazazi walio watumishi wa Yehova wanaweza kusaidia watoto wao kuhusu jambo hilo. Zaidi ya hayo, dada wenye umri mkubwa, wenye kumwogopa Mungu, wanaweza “kuziamsha akili za wanawake vijana . . . wawe na utimamu wa akili, safi kiadili” katika kuvaa kwao “ili neno la Mungu lisitukanwe.” (Tito 2:3-5) Vichapo vyetu vinatoa picha zenye kusaidia zinazoonyesha mavazi yenye mpangilio mzuri pamoja na kiasi.
5 Tumletee Yehova Sifa: Mikusanyiko ya wilaya inatutolea sisi sote nafasi bora kabisa ya kumsifu Yehova, wala si wale tu wanaopewa migawo. Bila shaka, mwenendo na usemi wetu wa Kikristo utamheshimu yeye. Lakini jambo la kwanza ambalo watazamaji wengi wanatambua kutuhusu sisi ni mavazi na kujipamba kwetu. Sisi sote na tumletee Yehova sifa kupitia mvalio wetu unaostahili, alama ya usafi wa kiadili.—Zab. 148:12, 13.
[Maulizo ya Funzo]
1. Katika kujitayarisha kuhusu mkusanyiko wa wilaya, kwa nini tunapaswa kufikiria mvalio wetu?
2. Kwa nini ni tatizo kuvaa na kujipamba kwa namna iliyo safi kiadili?
3. Ni maulizo gani yatakayotusaidia kuchunguza mvalio wetu?
4. Wengine wanawezaje kutusaidia kuwa na mvalio uliyo safi kiadili?
5. Sisi sote tunawezaje kumletea Yehova sifa wakati wa mkusanyiko?
[Kisanduku Kwenye Ukurasa wa 6]
Mambo Yanayoweza Kutusaidia Kuwa na Mvalio Unaostahili
◼ Neno la Mungu
◼ Uchunguzi wa kibinafsi
◼ Mapendekezo ya wengine
◼ Vichapo vya Kikristo