Kiasi Katika Mavazi na Kujipamba
1 “Wanaume wote, hata na wavulana wachanga, wanavaa utepe wa shingoni. Wanawake na wasichana wote, wale wenye umri wa miaka kati ya 13 na 19 na wale ambao ni wachanga zaidi, wanavaa kanzu au marinda (jupes). Hakuna suruali za jinzi (jeans) au kuvalia ovyoovyo. Kila mtu hapa ni mwenye kung’aa.” Hivyo ndivyo ilivyosema ripoti moja ya habari. Ripoti hiyo ilikuwa ikifafanua mkutano gani wa watu? Mkusanyiko wa kisiasa? Tukio la michezo? Mchezo wa miziki? Bila shaka hapana! Ilikuwa ikifafanua kikundi cha ndugu na dada kwenye mkusanyiko mkubwa wa wilaya mnamo majira ya kiangazi yaliyopita.
2 Katika mji mwingine wa mkusanyiko, mwandishi-habari wa gazeti moja alitoa ufafanuzi huu kuhusu mkutano wa Mashahidi: “Wanaume wote ni safi na wanavaa koti na suruali na utepe wa shingoni. Wanawake wanavaa kwa kiasi lakini kwa namna yenye kupendeza.” Mtazamaji wa pili, ambaye ni mlinzi wa usalama, alisema: “Nyinyi ni watu wenye kujiendesha vizuri, wenye adabu, walio safi, na wenye utaratibu. Jambo ninaloona ni zuri. Katika ulimwengu huu mchafu, mmefanikiwa kuondoa uchafu!” Ni ushuhuda mzuri kama nini kutuhusu sisi! Je, sisi si wenye shukrani kuona ndugu na dada zetu waliweza kusifiwa hivyo? Bila shaka, wote katika mkutano huo walichangia katika ripoti hizo nzuri kupitia hali yao ya nje ya kuigwa.
3 Tunajulikana ulimwenguni pote kuwa tofauti kabisa katika hali yetu ya nje. (Mal. 3:18) Kwa nini? Kwa sababu tunafuata shauri la Kimaandiko la ‘kujipamba wenyewe katika mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili, katika njia inayofaa wale wanaodai kumstahi Mungu.’—1 Tim. 2:9, 10.
4 Unaonyesha Nini Kupitia Mavazi Yako na Kujipamba Kwako? Mavazi tunayovaa na jinsi tunavyoyavaa inasema waziwazi kutuhusu sisi—imani zetu, mtazamo wetu, na nia zetu. Mitindo tunayochagua inasema sisi ni nani na kile tunachowakilisha. Hatupaswi kamwe kuendeleza mawazo yenye ufisadi na mwenendo unaofanywa upendwe na wote katika ulimwengu. Hangaiko letu si kujua ikiwa mtindo fulani ni wa kisasa kupita kiasi lakini ni kujua ikiwa unafaa kwa mtu anayesema kwamba yeye ni mhudumu wa Mungu. (Rom. 12:2) Badala ya kuchagua hali ya nje yenye kuonyesha roho ya kujitegemea au mtindo wa maisha usio wa adili, tunataka kuonyesha kwamba ‘tunatukuza Mungu’ kwelikweli.—1 Pet. 2:12.
5 Nyakati nyingine, mtu ambaye ni mpya, asiye na ujuzi, au aliye dhaifu kiroho huenda akakubali jambo lolote ambalo ulimwengu unapendekeza kuhusiana na mavazi na kujipamba bila kufikiria kwanza maoni ambayo hilo litatoa kuhusu Yehova na tengenezo lake. Sisi sote tunaweza kujichunguza ili kuona ikiwa tumechochewa na mafikiri ya ulimwengu. Tunaweza kukaribia ndugu au dada mwenye kuheshimiwa na mwenye kukomaa kiroho ili kumwomba atuambie kwa unyofu kuhusu mtindo wetu wa mavazi na kujipamba, na kisha tukadirie kwa uzito mapendekezo yanayotolewa.
6 Wengine hukubali bila kusita kwamba wanapaswa kuwa waangalifu kuhusu jinsi wanavyovaa wanapohudhuria mkusanyiko. Lakini baadaye wanapunguza kiwango chao wakati wa utendaji wa mapumziko baada ya vipindi vya mkusanyiko. Dumisha kiwango cha juu kinachofaa wahudumu Wakristo. (2 Kor. 6:3, 4) Mahali popote tunapokwenda kati ya watu, kadi za vitambulisho tunazovaa kwenye mkusanyiko na mavazi na kujipamba kwetu kwenye kufaa ni mambo yanayotutambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo, mavazi yetu yanapaswa sikuzote kuwa yenye mpangilio mzuri na yenye kiasi, yakionyesha kwamba sisi “si sehemu ya ulimwengu.”—Yn. 15:19.
7 Acheni tufanye yote tuwezayo kwenye Mkusanyiko wa Wilaya wa mwaka huu, “Watangazaji Wenye Bidii wa Ufalme,” ili kuonyesha kwamba sisi ni “taifa takatifu kwa BWANA Mungu [wetu].” Maoni mazuri yatakayotokana na jambo hilo yataongezea ‘sifa na jina na heshima’ ya Yehova.—Kum. 26:19.
[Picture on page 6]
Jinsi ya Kumtukuza Yehova:
[Picture on page 6]
■ Vaa kwa namna yenye kufaa mhudumu wa Mungu
■ Epuka mitindo inayofuata roho ya ulimwengu
■ Onyesha kiasi, ambayo ni alama ya utimamu wa akili