Tuunge Mkono Maoni ya Biblia Kuhusu Mazishi — Sehemu ya 2
Mavazi ya Kilio
1. (a) Mavazi ya kilio ni nini? (b) Ni nini kinachoyatofautisha na mavazi ambayo watu wanavaa kwa kawaida?
Mara nyingi watu wa jamaa na marafiki wanaombwa kuvaa mavazi ya kilio. Ni jambo la maana kuelewa kwamba mavazi ya kilio ambayo tunazungumzia hapa si nguo za kawaida ambazo watu wanavaa wakati mwingine, na pia wakati wa mazishi. Mavazi ya kilio yanavaliwa tu mutu anapokufa. Kwa mfano, katika kila luga ya Ghana mavazi hayo yanaitwa kwa jina la pekee linaloyatofautisha na mavazi ambayo watu wanavaa kwa kawaida.
2. (a) Nguo za magunia ni nini, na zilivaliwa kwa kusudi gani katika nyakati za Biblia? (b) Nguo za magunia hazikuvaliwa hata kidogo kwa kusudi gani?
2 Watu fulani wanafikiri kwamba mavazi ya kilio yanavaliwa katika inchi nyingi za Afrika kama vile watu wa nyakati za Biblia walivyovaa nguo za magunia. Ni kweli kwamba wakati fulani watu waliofiwa walivaa nguo za magunia; hata hivyo nguo hizo zilivaliwa pia wakati mwingine usio wa kilio. Zilitengenezwa na manyoya ya mbuzi, na zilitumiwa zaidi sana kwa kutengeneza saki, kwa mfano saki za kuwekea mbegu. Wakati wa zamani wachungaji wa nyama walivaa nguo hizo za saki kwa kuwa zilikuwa bei chini na hazikuwa zikiharibika mbio. Pia, watu walivaa nguo za magunia ili kuonyesha kwamba wanatubu. (1 Fal. 21:27; Yona 3:6-8) Mbele ya kumtolea Yehova sala ya bidii, Danieli alijifunika nguo ya gunia. (Dan. 9:3) Nyakati nyingine, manabii Waebrania walivaa nguo za magunia kwa kuwa walipewa kazi ya kutoa ujumbe wa kuonya watu. (Isa. 20:2) Watu walivaa nguo za magunia kwa kusudi mbalimbali, lakini watumishi wa Mungu hawakuvaa nguo hizo wakiwa na wazo la kwamba wafu wanaweza kuwasaidia ao kuwatendea vibaya. Je, mawazo ya watu leo yanalingana na hayo ya watumishi wa Mungu wanapovaa mavazi ya kilio?
3. (a) Kwa kawaida, mavazi ya kilio yana rangi gani katika eneo lenu? (b) Mavazi hayo yanategemea mafundisho gani ambayo watu wameamini? (c) Mara nyingi mavazi ya rangi nyeusi, nyeupe, ao rangi nyingine yanavaliwa kwa kusudi gani?
3 Watu wanavaa mavazi ya kilio ili kuonyesha hali ya huzuni. Maana ya rangi ya mavazi hayo na mapambo yayo vinategemea desturi na mahali. Vinategemea pia mafundisho ya kidini ya zamani ambayo watu wameamini kuhusiana na hali ya wafu, na uhusiano wa kifamilia ambao mutu aliyekufa alikuwa nao pamoja na walio hai. Kwa mfano, katika maeneo fulani, watu wa jamaa wa karibu wa yule aliyekufa wanavaa mavazi ya kilio ya pekee. Kwa kufanya hivyo wanaamini kwamba wanajilinda na hatari yoyote inayoweza kuwapata kwa sababu ya uhusiano wa kijamaa ambao walikuwa nao pamoja na yule aliyekufa. Watu fulani wanavaa mavazi ya rangi nyeusi. Katika mahali pengi, watu wanafikiri kwamba kwa kufanya hivyo wanajilinda na roho waovu na kwamba ni jambo la maana ili yule aliyekufa aweze kuingia katika ulimwengu wa roho mahali ambapo mababu wanapatikana. Mavazi ya kilio yenye rangi nyeupe pia yana maana fulani. Kwa watu wengi mavazi hayo yanamaanisha ushindi juu ya kifo na yanaonyesha nia ya wale wanaoyavaa kwamba roho ya yule aliyekufa iingie kwa amani katika ulimwengu mwingine. Katika makabila fulani, watu wanafunga kichwani sehemu ya nguo ya rangi nyeupe ya yule aliyekufa ili kuonyesha kwamba si wao waliomwua. Zaidi ya hiyo, nywele zinakatwa ili kuonyesha kwamba wanamlia yule aliyekufa, na wanawake ambao ni watu wa jamaa ao marafiki wa yule aliyekufa wanapaswa kulia wakiwa vifua wazi na miguu isiyo na viatu. Watu fulani wanavaa mavazi yasiyo safi wakati huu.
4. (a) Katika eneo lenu, watu wanavaa mavazi ya kilio kwa muda gani? (b) Kwa nini watu fulani wanabadilisha mavazi mara nyingi wakati wa kilio na kuvaa mavazi ya rangi tofauti?
4 Watu wanavaa mavazi ya kilio kwa muda wa siku moja, majuma, miezi, hata mwaka mmoja ao zaidi kisha mazishi, ikitegemea uhusiano wa kijamaa na yule aliyekufa. Katika maeneo fulani, wakati wa kilio, watu wanabadilisha mavazi mara nyingi na kuvaa mavazi ya kilio ya rangi tofauti. Wanafanya hivyo ili kuonyesha hali ya uhusiano wao pamoja na yule aliyekufa. Kwa mfano, mjane anavaa mavazi ya rangi fulani ili kujilinda na roho ya mume wake. Kadiri wakati unavyopita anabadilisha mavazi ili kuonyesha kwamba uwezekano wa kupata hatari unapunguka. Anaendelea kubadilisha mavazi mpaka atakapoona kwamba kifo cha mume wake hakiwezi kumtokezea tena hatari yoyote. Mwishowe, anaachana na mavazi hayo ili kukata kabisa uhusiano wowote pamoja na mume wake aliyekufa.
5. (a) Namna gani tunaweza kutumia andiko la Isaya 52:11 kuhusiana na matumizi ya alama hizo? (b) Kwa nini wale ambao hawamwabudu Yehova wanaweza kuhuzunishwa ikiwa mutu havae mavazi ya kilio?
5 Nyakati nyingine mavazi ya kilio yana alama na maneno yenye maana ya pekee, kama vile “kwa heri”. Alama na maneno hayo yanatiwa kwenye nguo kama vile tricot. Kwa kuwa nyingi kati ya alama hizo zinaunga mkono mafundisho kuhusu roho za mababu na uhusiano wao pamoja na walio hai, inaomba kuziepuka. (Isa. 52:11) Kwa kawaida ni watu wenye umri mkubwa katika jamaa ndio wanaoamua aina ya mavazi yatakayovaliwa, na wakati fulani, alama na maneno yatakayotumiwa. Kisha, watu wa jamaa wote wanalazimishwa kuvaa hivyo. Wale ambao si Mashahidi wanaona mavazi ya kilio kuwa ya maana sana hivi kwamba ikiwa mutu hayavae inakuwa kama anamtukana yule aliyekufa na anakosa heshima kwa jamaa yake. Namna gani habari hizo zinaweza kutusaidia ili kujua jambo la kufanya kuhusu mavazi ya kilio? Tufikirie kanuni tatu za maana.
6. (a) Soma 1 Wathesalonike 4:13. Namna gani kanuni hii inaweza kutusaidia kuhusiana na maoni tuliyo nayo juu ya mavazi ya kilio? (b) Soma 2 Wakorintho 6:3. Ni maulizo gani tunayopaswa kujiuliza kuhusiana na mavazi ya kilio?
6 Kanuni za Kufikiria: Kwanza, sisi watumishi wa Yehova, hatuonyeshe huzuni yetu kupita kiasi kama ilivyo desturi ya wale “wasio na tumaini.” (1 The. 4:13) Pili, hatutaki kufanya jambo lolote linaloweza kuwa ‘sababu ya kuwakwaza’ wengine. (2 Kor. 6:3) Kuhusiana na kanuni hiyo, tujiulize hivi: ‘Ikiwa ninavaa mavazi ya kilio, je watu hawatafikiri kwamba ninakubali mafundisho na mazoea yasiyopatana na Maandiko? Je, hilo linaweza kuwakwaza wale wanaojua mafundisho ya Mashahidi wa Yehova kuhusu watu waliokufa? Je, kufanya hivyo hakutasumbua zamiri ya Wakristo wengine wa Congo ao wa inchi nyingine? Je, hilo halitawavunja moyo ndugu ambao waliteswa kwa kuwa walikataa kuvaa mavazi hayo?’ —Ona Mnara wa Mlinzi wa tarehe 15 mwezi wa 7, 1998, ukurasa 22-23.
7. (a) Soma Methali 27:11 na Wakolosai 1:9, 10. Ni kanuni gani za maana zilizo katika maandiko hayo, na namna gani tunaweza kuzitumia kuhusiana na mavazi ya kilio? (b) Kulingana na 1 Wakorintho 10:21, 22, je, kuvaa mavazi ya kilio kunaweza kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova? Kwa nini?
7 Kanuni ya maana sana kuliko kanuni zote tunazopaswa kufikiria ni hii: Haiwezekani hata kidogo kwetu kufanya jambo linalomchukiza Yehova. (Met. 27:11; Kol. 1:9, 10) Tunajua maana ya mavazi ya kilio na jinsi yanavyohusiana na mafundisho ya kwamba wafu wanaendelea kujua mambo yanayotendeka. Kwa hiyo, tunapaswa kufikiri kwa uangalifu jinsi kufuata desturi hiyo kunavyoweza kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova. Sisi ‘hatuwezi kuwa tukishiriki meza ya Yehova na meza ya roho waovu.’ — 1 Kor. 10:21, 22.
8. Ikiwa mpaka sasa hatukujua uhusiano ulio kati ya mavazi ya kilio na roho waovu, ni nini linalotusaidia sasa tuelewe kwa nini wakristo wa kweli hawapaswi kuvaa mavazi kama hayo? (Rudilia kanuni kubwa tatu zinazotajwa katika fungu la 6 na 7.)
8 Ni kweli kwamba watu fulani hawajui maana ya mavazi hayo. Lakini hawawezi pia kufasiria kwa nini wanatamani sana kuvaa mavazi hayo tu wakati wa kilio. Ijapokuwa wengi wanavaa mavazi hayo bila kuelewa vizuri maana yake, hilo halimaanishe kwamba tunapaswa kuwaiga. Tunapofikiri sana juu ya kanuni hizo katika sala, tutaelewa kwa nini hatupaswi kufuata desturi ya kuvaa mavazi ya pekee kama alama ya kilio.
9. Kuliko kuvaa mavazi ya kilio, namna gani Wakristo wa kweli wanaweza kuvalia wakati wa kilio bila kuwakwaza wengine?
9 Jinsi ya Kuvaa Wakati wa Mazishi: Watu wanaweza kuvalia namna gani wakati wa mazishi? Vichapo vya mtumwa mwaminifu na mwenye busara vimezungumzia ulizo hilo kwa miaka mingi.a Tumetiwa moyo kuonyesha usawaziko kwa kuchagua mavazi ya kawaida na yanayofaa. Mavazi hayo yanaweza kuwa ya rangi yenye kufifia yanayohusiana na hali ya huzuni; mavazi ambayo watu wanavaa wanapoenda “katika nyumba ya maombolezo.” (Mhu. 7:2) Kwa hiyo, hatutajisikia kuwa wenye kulazimishwa kuvaa “mavazi yenye kufanana” (uniforme) ambayo watu wa jamaa na marafiki wa yule aliyekufa wanaombwa wavae. Iwe tunaamua kuvaa mavazi fulani, kuelewa vizuri hali ya wafu kutatusaidia tuonyeshe heshima, hata ikiwa hatuvae mavazi ya kilio ambayo watu wanavaa kwa sababu ya desturi.
Kutayarisha Mazishi
10. Namna gani kanuni zinazopatikana katika Waefeso 5:7-11 na 1 Wakorintho 10:32 zinatuongoza tunapotayarisha mazishi?
10 Mazishi ya Kikristo yanapaswa kufanywa kwa njia yenye heshima na kwa kufuata sheria zote za inchi na za usafi. Ili sherehe ya mazishi iwafariji watu kweli kweli kwa kufuata kanuni za Biblia na kuonyesha ukweli kuhusu hali ya wafu, hatuwezi kuruhusu desturi ao mazoea yoyote inayopingana na Maandiko. (Efe. 5:7-11) Mambo yanayotendeka wakati wa sherehe ya mazishi hayapaswi kusumbua zamiri ya Wakristo wenzetu. (1 Kor. 10:32) Namna gani tunaweza kutumia kanuni hizo za Biblia tunapotayarisha mazishi ya Kikristo?
11. (a) Ikiwa kuna mpango wa kuandika mambo fulani kwenye kijitabu kwa ajili ya mazishi, ni nini ambalo hatutaruhusu wale wasio Mashahidi wafanye? (b) Ni maneno gani ambayo Wakristo wa kweli hawatatumia, na kwa nini?
11 Kumsifu Aliyekufa: Watu wanaweza kuamua kuandika mambo fulani kwenye kijitabu kuhusu matendo ya uaminifu ya yule aliyekufa; lakini inaomba kuwa mwangalifu kuhusu mambo ya kuandika. Kwa mfano, labda watu wa jamaa na marafiki ambao si Mashahidi watapenda waongeze maneno ya kusifu yanayoelekezwa moja kwa moja kwa yule aliyekufa. Hatari ni kwamba wanaweza kutumia maneno yanayoweza kufanya watu wafikiri kwamba Mungu alimwita mbinguni yule aliyekufa ao kwamba yuko njiani akijielekeza mahali pengine. Mara nyingi wanatumia maneno kama vile “pumziko njema,” “ulale vizuri,” na “safari njema.” Kwa wengi, maneno hayo ni alama ya kumwonyesha yule aliyekufa heshima kwa mara ya mwisho. Hata hivyo, tunajua kwamba mutu anapokufa hajui kwamba watu wanamsifu. Jambo la maana zaidi ni kwamba Wakristo wa kweli hawapaswi kutumia maneno hayo kwa kuwa yanaunga mkono fundisho la kutokufa kwa nafsi. — Isa. 52:11.
12. (a) Kulingana na Maandiko, ni nani aliye na haki ya kuamua jinsi mazishi yatafanywa, na kwa nini hilo linapingana na desturi ya asili? (b) Kulingana na 2 Wakorintho 6:14-17, kwa nini si jambo la hekima kuruhusu wale ambao si Mashahidi, iwe wazazi, watu wa jamaa ao watu wengine wachukue maamuzi kuhusu mipango ya mazishi?
12 Ni Nani Ataamua? Katika maeneo mengi, watu wa jamaa ambao si Mashahidi wanakubali kwamba jamaa nzima inaruhusiwa kutoa uamuzi kuhusu namna na wakati wa kufanya mazishi. Hata hivyo, katika ndoa ya Kikristo, mume na muke wana haki ya kuchukua maamuzi fulani ya maana kuhusu maisha yao na ya watoto wao. Wazazi, watu wa jamaa, na hata ndugu na dada katika kutaniko wanapaswa kuheshimu haki hiyo inayopatana na Maandiko. (Mat. 19:5, 6) Haki hiyo inapaswa pia kuheshimiwa na watu wa jamaa yetu. (Mwa. 23:19; 35:29) Ili kuepuka ‘kufungwa nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini,’ Mkristo ataeleza waziwazi kwamba mambo yote yatafanywa kulingana na kanuni za Biblia. (2 Kor. 6:14-17) Ni hatua gani tunazopaswa kuchukua ili kuwa hakika kwamba kanuni hizo zitaheshimiwa?
13. (a) Kwa nini ni jambo la maana sana mutu aandike maagizo kuhusu jinsi ya kuendesha kilio na mazishi yake? (b) Ni nini iliyo njia nzuri zaidi ya kufanya hivyo, na ni mambo gani anayopaswa kuandika kwenye kikaratasi hicho?
13 Onyesha Waziwazi Msimamo Wako: Ikiwa mutu anaandika kwenye kikaratasi jinsi mazishi yake yatafanywa, itakuwa vyepesi kufikiri pamoja na watu wa jamaa, ambao mara nyingi wanaheshimu maamuzi ya mwisho ya yule aliyekufa. (Mwa. 50:5) Itakuwa vizuri zaidi mutu aandike maamuzi yake kwenye karatasi na kuomba itiwe sahihi na mwenzi wa ndoa, na watu wa jamaa wanaume ambao ni Mashahidi pia na wanaokubali kabisa maamuzi yake. Anaweza hata kuweka karatasi hiyo mbali na karatasi zinazoonyesha maamuzi yake ya mwisho kuhusu jinsi ya kugawanya vitu vyake. Wale ambao wanafikiria wakati ujao kwa hekima wanajua kwamba hawangojee wawe wazee ao wagonjwa ili kuchukua maamuzi kama hayo. (Mhu. 9:11) Wakati mutu angali na afya nzuri ni jambo la maana ajulishe maoni yake kuhusu mambo yafuatayo: Kilio kitaendeshwa namna gani, mazishi yatafanywa wakati gani na wapi; na ni nani peke yake anapaswa kuongoza sherehe zote za kilio na mazishi. Ni vema kumpa mzee mmoja wa kutaniko kopi moja ya karatasi hiyo kwa kuwa ile ya kwanza inaweza kupotea. Njia nyingine ambayo mutu anaweza kutumia ili kujulisha maamuzi yake ni kuyarekodi kwa kutumia chombo cha kunasa sauti ao kaseti na kumpatia mutu mwenye kutumainika.
14. (a) Kwa nini watu fulani hawapendezwe na wazo la kuandika mbele ya wakati maagizo kuhusiana na mazishi yao? (b) Soma Wafilipi 2:4 na Waefeso 5:28, 33. Namna gani kanuni hizo zinaweza kutusaidia kuhusiana na maoni tuliyo nayo juu ya jambo hili la maana?
14 Watu fulani hawapendezwe na wazo la kuandika mbele ya wakati maagizo kuhusiana na kilio na mazishi yao. Lakini kufanya hivyo kunaonyesha kwamba mutu amekomaa kiroho na ni mwenye upendo kabisa. Wale ambao wana ujuzi sahihi wa Biblia wanajua kwamba jambo hilo halitawafanya wakufe mbio wala nyuma zaidi. Ni kweli kwamba watu wa jamaa wasio Mashahidi wanaweza kukasirika ao kuona kwamba wanakosewa heshima mutu anapoandika maagizo yanayoonyesha waziwazi kwamba hawapaswi kubadilisha yale ambayo yamepangwa kuhusiana na mazishi. Lakini ni vizuri mutu amalize jambo hilo wakati angali hai kuliko kuliachia watu wa jamaa waliofiwa, ambao labda watachochewa ao kulazimishwa kufuata mazoea yasiyo safi yasiyokubaliwa. (Flp. 2:4) Mutu akipanga mambo mbele ya wakati kwa kufikiria wengine anaonyesha kwamba anawapenda na kuwahangaikia. — Efe. 5:28, 33.
15. (a) Mara nyingi, ni kwa kusudi gani mazishi yanacheleweshwa siku fulani, na kwa nini si vizuri kufanya hivyo? (b) Namna gani tutatumia kanuni zinazopatika katika 2 Wakorintho 6:14 ikiwa watu wa jamaa wanangangania kuongoza sherehe fulani za mazishi?
15 Kushugulika na Watu wa Jamaa Wasio Mashahidi: Katika maeneo fulani, imekuwa desturi kukusanya watu muda kidogo kisha kifo cha mutu, ili kutayarisha mazishi. Wanakusanyika pamoja kwa muda wa siku 8 hivi. Kusudi lao ni kuona namna ya kupata feza na kufariji wale waliofiwa, na hivyo kuamua mazishi yatafanywa namna gani na wakati gani. Mambo yaliyoonwa yanaonyesha kwamba wakati huo Shahidi anaweza kuvutwa na maamuzi ya wale ambao si Mashahidi. Kama tulivyoona hapo juu, Maandiko yanaonyesha wazi kwamba hatuwezi kuruhusu watu wasiomtumikia Yehova wafanye sherehe fulani za mazishi na Mashahidi wafanye sherehe nyingine. (2 Kor. 6:14) Kwa hivyo, ikiwa yule aliyekufa alikuwa Mkristo mwaminifu, haitakuwa vizuri kuruhusu watu wa jamaa ambao si Mashahidi wafanye “kamati ya mazishi” ambayo itaamua jinsi mazishi yatafanywa. Ndugu na dada wa kutaniko ambao si watu wa jamaa hawatajiingiza katika mikutano hiyo ya kutayarisha mazishi ao mipango ya mazishi. Lakini Wakristo ambao walifiwa wanaweza kuomba mashauri kwa mzee mmoja ao wawili yatakayowasaidia kupanga mazishi kulingana na kanuni za Biblia.
16. (a) Familia ya Kikristo inapaswa kuwaelezea nini waziwazi watu wa jamaa wasio Mashahidi? (b) Jambo la kufanya ni gani ikiwa watu wa jamaa wanangangania kuingiza mazoea yasiyo safi? (c) Kuandika maagizo kuhusu mazishi, kunasaidia kuepuka nini?
16 Familia ya Kikristo inapaswa kuonyesha watu wa jamaa mambo ambayo yamepangwa kwa ajili ya mazishi; lakini kwa uvumilivu na wema. Ikiwa watu wa jamaa wasio Mashahidi wanakubaliana na mipango hiyo, inaweza kuwa vizuri kutumika pamoja nao. Lakini jambo la kufanya ni gani ikiwa watu wa jamaa wanangangania sana kuingiza desturi na mazoea yasiyo safi? Wakati huo, ni jambo la maana kusimama imara na kuwaelezea kwa upole na bila woga msimamo wetu wa Kikristo. Hapo pia, maagizo yaliyoandikwa yanayoonyesha wazi jinsi mutu anavyopenda mazishi yake yafanywe yatasaidia ili kuepuka mabishano.
17. (a) Tutafanya nini ikiwa wale wasio Mashahidi wanangangania kabisa kuongoza sherehe za mazishi? (b) Ikiwa ni hivyo, ni mipango gani tunayoweza kuchukua? (c) Soma 2 Wakorintho 4:7. Kwa nini tunaweza kupata faraja hata ikiwa wale wasio Mashahidi wanavuruga mipango ya mazishi?
17 Ikiwa watu wa jamaa wasio Mashahidi wanangangania tu kuongoza sherehe za mazishi, washiriki wa familia wanaomtumikia Yehova wanaweza kuona vizuri kujiondoa kabisa katika mambo ili waendelee kuwa na zamiri safi. Wanaweza kupanga hotuba fupi ya mazishi itolewe kwenye Jumba la Ufalme ao mahali pengine panapofaa. Hivyo wale ambao wamehuzunishwa kwa sababu ya kifo cha mpendwa wao watapata “faraja kutokana na Maandiko.” (Rom. 15:4; Zab. 119:50) Hata ikiwa mwili wa yule aliyekufa hauko mahali ambapo hotuba inatolewa, mpango huo unaonyesha heshima na ni wenye kukubalika kabisa. (Kum. 34:5, 6, 8) Ni kweli kwamba wakati wale ambao si Mashahidi wanapoingiza mazoea yasiyofaa, hilo linaweza kuongeza huzuni inayoletwa na kifo. Lakini tunafarijiwa kujua kwamba Mungu anaona jinsi tulivyojikaza kabisa kufuata maoni ya Maandiko kuhusu mazishi na kwamba anaweza kuwatolea watumishi wake waaminifu “nguvu zinazopita za kawaida.”—2 Kor. 4:7.
[Footnote]
a Ona Mnara wa Mlinzi wa tarehe 15 mwezi wa 7, 1998, ukurasa wa 22-23 na wa tarehe 15 mwezi wa 4, 1985 (Kifaransa), ukurasa wa 21-23, na kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu, ukurasa wa 70.