Wengine Wanajifunza Nini Wanapokutazama?
1. Wanafunzi wa Yesu walijifunza nini walipomtazama?
1 Yesu alisema: “Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu.” (Mt. 11:29) Kwa kweli, aliwafundisha wengine kwa kuwaonyesha mfano mzuri, hakuwafundisha kwa maneno tu. Fikiria yale ambayo wanafunzi walijifunza walipomtazama Yesu. Alikuwa mpole, mwema, na mwenye upendo. (Mt. 8:1-3; Marko 6:30-34) Alikuwa na unyenyekevu wa kweli. (Yoh. 13:2-5) Walipokuwa naye katika kazi ya kuhubiri, wanafunzi waliona kwamba alikuwa mhubiri mwenye bidii aliyekuwa na matokeo mazuri katika kuwafundisha wengine kweli. (Luka 8:1; 21:37, 38) Wengine wanajifunza nini wanapotutazama katika kazi ya kuhubiri?
2. Namna gani mvalio na mwenendo wetu mzuri katika mahubiri unaweza kuwavutia wasikilizaji wetu?
2 Wasikilizaji Wetu: Mvalio wetu wa kiasi, kuonyesha adabu, na kupendezwa kabisa na wengine kunaweza kuwavutia sana wasikilizaji wetu. (2 Kor. 6:3; Flp. 1:27) Wanatambua kwamba tunatumia Biblia mara nyingi. Wengine wanavutiwa tunapowasikiliza kwa heshima wanapozungumza. Kumbuka kabisa kwamba kuonyesha mfano mzuri katika njia hizo kunaweza kuwachochea wengine wasikilize ujumbe wa Ufalme.
3. Namna gani tunaweza kuwachochea ndugu zetu kwa njia nzuri?
3 Ndugu Zetu: Tufikirie pia jinsi tunavyoweza kuwachochea ndugu zetu kwa njia nzuri. Bidii yetu katika mahubiri inaweza kuwachochea wengine wawe pia na bidii. Kama vile chuma kinavyonoa chuma, wengine wanapotuona tukitolea watu ushahidi kwa njia nzuri, hilo litawachochea wafanye ufundi wao wa kuhubiri uwe mzuri zaidi. (Met. 27:17) Ikiwa tunajikaza kuandika mambo fulani kuhusu watu wanaopendezwa na kuwarudilia bila kukawia, hilo litachochea wengine wafuate mfano wetu. Kwa kutimiza kwa ukamili utumishi wetu, tutawachochea kwa njia nzuri ndugu na dada zetu.—2 Tim. 4:5.
4. Kwa nini tunapaswa kuchunguza mara kwa mara mfano wetu?
4 Kwa nini usichunguze mara kwa mara yale unayofanya na kusema, na kuona jinsi unavyowachochea wengine kupitia mfano wako? Mfano wetu mzuri utampendeza Yehova na kutuwezesha kuwa na maoni kama ya mtume Paulo aliposema hivi: “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.”—1 Kor. 11:1.