Wahubiri Wakristo Wanahitaji Kusali
1. Ni jambo gani lililo la lazima ili kutimiza kazi yetu ya kuhubiri?
1 Hatuwezi kutimiza kazi ya kuhubiri kwa nguvu yetu wenyewe. Yehova anatupa nguvu ya kufanya kazi hiyo. (Flp. 4:13) Anatumia malaika zake ili kutusaidia kupata watu walio mfano wa kondoo. (Ufu. 14:6, 7) Ni Yehova anayekomalisha mbegu za kweli tunazopanda na kutilia maji. (1 Kor. 3:6, 9) Ni jambo la lazima sana wahubiri Wakristo wamtegemee Baba yetu wa mbinguni katika sala!
2. Tunaweza kusali kwa ajili ya mambo fulani gani?
2 Kwa Ajili yao Wenyewe: Tunapaswa kusali kila mara tunapohubiri. (Efe. 6:18) Tunaweza kusali kwa ajili ya mambo fulani gani? Tunaweza kumwomba Mungu atusaidie tuwe na maoni mazuri kuhusu eneo letu na kutupa ujasiri. (Mdo. 4:29) Tunaweza kumwomba Yehova atuongoze kwenye watu wenye mioyo ya haki ambao tunaweza kujifunza nao Biblia. Ikiwa msikilizaji anatuuliza ulizo, tunaweza kufanya sala fupi ya moyoni ili kumwomba Yehova atusaidie kutoa jibu linalofaa. (Neh. 2:4) Tunaweza pia kumwomba atupe hekima ili tutie kazi ya kuhubiri pa nafasi ya kwanza maishani mwetu. (Yak. 1:5) Pia, Yehova anafurahi tunapotia katika sala zetu maneno ya shukrani kwa ajili ya pendeleo la kuwa watumishi wake.—Kol. 3:15.
3. Namna gani kusali kwa ajili ya wengine kunafanya kazi ya kuhubiri iendelee mbele?
3 Kwa Ajili ya Wengine: Tunapaswa pia “kusali kwa ajili ya mutu na mwenzake,” na hata kutaja majina ya wahubiri wenzetu katika sala inapofaa. (Yak. 5:16; Mdo. 12:5) Je, afya mbaya inakuzuia kufanya mengi katika kazi ya kuhubiri? Kwa hiyo, sali kwa ajili ya wahubiri wenzako walio na afya nzuri. Usiwazie kwamba sala zako haziwezi kuwasaidia wengine! Ni vizuri pia kusali kwa ajili ya wenye mamlaka ili wawe na mwelekeo unaofaa kuhusu kazi ya kuhubiri, ili ndugu zetu ‘waendelee kuishi maisha shwari na matulivu.’—1 Tim. 2:1, 2.
4. Kwa nini tudumu katika sala?
4 Kutangaza habari njema katika dunia yote inayokaliwa ni mgawo ambao hatuwezi kutimiza kwa nguvu yetu wenyewe. Ikiwa ‘tunadumu katika sala’ Yehova atatusaidia kutimiza kazi hiyo.—Rom. 12:12.