SURA YA 8
Mungu Anapenda Watu Walio Safi
‘Kwa mutu anayebaki safi utakuwa safi.’—ZABURI 18:26.
1-3. (a) Sababu gani mama angetaka mutoto wake awe safi? (b) Sababu gani Yehova anataka watumishi wake wawe safi, na ni sababu gani zinazotusukuma kuwa safi?
MAMA mumoja anamutayarisha mutoto wake mudogo ili waende mahali fulani. Anamunawisha na anamuvalisha nguo safi. Anajua kama ni lazima mutoto awe safi ili awe na afya njema. Tena, anajua jambo hili: ikiwa mutoto anaonekana safi, wazazi wake wataheshimiwe na ikiwa sivyo watazarauliwa.
2 Baba yetu wa mbinguni, Yehova, anataka watumishi wake wawe safi. Neno lake linasema hivi: ‘Kwa mutu anayebaki safi utakuwa safi.’a (Zaburi 18:26) Yehova anatupenda; anajua kama ikiwa tuko safi ni kwa faida yetu. Tena, anataka usafi wetu sisi Mashahidi wake umuletee sifa. Kwa kweli, usafi na mwenendo wetu muzuri unamuletea Yehova sifa na unatukuza jina lake takatifu.—Ezekieli 36:22; 1 Petro 2:12.
3 Kwa sababu tunajua kama Mungu anawapenda watu walio safi, jambo hilo linatusukuma kuwa safi. Kwa sababu tunamupenda Mungu, tunataka namna yetu ya kuishi imuletee sifa. Tena tunataka tubaki katika upendo wake. Basi, tuone sababu gani tunapaswa kuwa safi, inamaanisha nini kuwa safi, na tunaweza kufanya nini ili tuendelee kuwa safi. Kuchunguza mambo hayo kunaweza kutusaidia tuone ikiwa tuna lazima ya kufanya mabadiliko katika jambo fulani.
SABABU GANI TUNAPASWA KUWA SAFI?
4, 5. (a) Tuna sababu gani kubwa ya kuendelea kuwa safi? (b) Mambo ambayo Yehova aliumba yanaonyesha namna gani kama yeye ni Mungu aliye safi?
4 Njia moja ambayo Yehova anatumia ili kutuongoza ni kwa kutuwekea yeye mwenyewe mufano muzuri. Ndio sababu Neno lake linatuomba ‘tuwe waigaji wa Mungu.’ (Waefeso 5:1) Sababu kubwa inayotusukuma kuwa safi ni hii: Yehova, Mungu tunayeabudu ni Mungu aliye safi na mutakatifu katika mambo yote.—Mambo ya Walawi 11:44, 45.
5 Usafi wa Yehova unaonekana katika uumbaji, vilevile sifa zake nyingi na njia zake. (Waroma 1:20) Mungu alikusudia dunia iwe mahali safi kwa ajili ya wanadamu. Aliumba mimea na wanyama fulani ili wawe na kazi ya kusafisha hewa na maji. Kuna vidudu vidogo-vidogo sana vinavyogeuza uchafu kuwa vitu visivyo hatari. Wanasayansi wametumia vidudu fulani ili kusafisha mafuta ao petrole iliyomwangika katika bahari mbalimbali na uchafu mwengine unaoletwa kwa sababu ya uchoyo na pupa ya wanadamu. Ni wazi kabisa, ‘Mutengenezaji wa dunia’ anapenda usafi. (Yeremia 10:12) Ni lazima tumuige.
6, 7. Sheria ya Musa ilionyesha namna gani kama Mungu aliwaomba waabudu wake wawe safi?
6 Sababu nyingine ya kuendelea kuwa watu walio safi ni hii: Yehova, Mutawala wetu anawaomba waabudu wake wawe safi. Katika Sheria ambayo Yehova aliwapatia Waisraeli, usafi na ibada vilienda pamoja. Sheria ilisema kama Siku ya Upatanisho kuhani mukubwa alipaswa kuosha mwili wake, si mara moja lakini mara mbili. (Mambo ya Walawi 16:4, 23, 24) Makuhani walipaswa kunawa mikono na miguu yao mbele ya kumutolea Yehova zabihu. (Kutoka 30:17-21; 2 Mambo ya Nyakati 4:6) Sheria ilitaja mambo 70 ambayo yalimufanya mutu awe muchafu na awe asiyestahili kushiriki katika ibada. Ikiwa Muisraeli angeshiriki katika ibada katika hali ya uchafu, angeweza kuuawa. (Mambo ya Walawi 15:31) Mutu yeyote ambaye alikataa kutimiza mipango ya kujisafisha, kama vile kusafisha mwili wake na nguo zake, alipaswa ‘kukatiliwa mbali kutoka katikati ya kutaniko.’—Hesabu 19:17-20.
7 Hata ikiwa sisi hatuongozwe tena na Sheria ya Musa, Sheria hiyo inatusaidia kujua mawazo ya Yehova juu ya usafi. Sheria inaonyesha waziwazi kama Mungu aliwaomba waabudu wake wawe safi. Yehova hajabadilika. (Malaki 3:6) Anaweza kukubali ibada yetu ikiwa tu iko “safi na isiyotiwa unajisi [uchafu].” (Yakobo 1:27) Kwa hiyo, tuna lazima ya kujua mambo ambayo anataka tufanye ili kuwa safi.
MAANA YA KUWA SAFI MACHONI PA MUNGU
8. Ni katika mambo gani Yehova anataka tuwe safi?
8 Katika Biblia, kuwa safi hakumaanishe tu usafi wa kimwili. Machoni pa Mungu, usafi unaangalia mambo yote ya maisha. Yehova anataka tuwe safi katika mambo ine ya musingi: kuwa safi kiroho, kuwa na mwenendo safi, kuwa safi kiakili, na kimwili. Basi tuone maana ya kuwa safi katika mambo hayo.
9, 10. Kuwa safi kiroho kunamaanisha nini na Wakristo wa kweli wanajiepusha na nini?
9 Kuwa safi kiroho. Kwa kifupi, kuwa safi kiroho ni kutochanganya ibada ya kweli na ya uongo. Wakati Waisraeli walitoka Babiloni na kurudia Yerusalemu, walipaswa kufuata agizo hili lililoongozwa na roho takatifu: ‘Mutoke, musiguse kitu chochote kilicho najisi [ao kichafu]; muwe safi.ʼ (Isaya 52:11) Sababu kubwa ya Waisraeli kurudia kwao ilikuwa ni kuanzisha upya ibada ya Yehova. Ibada hiyo ilipaswa kuwa safi, ni kusema, haikupaswa kuambukizwa na mafundisho yenye kumuzaraulisha Mungu, na pia mazoea na desturi za dini ya Babiloni.
10 Leo, sisi Wakristo wa kweli tunapaswa kuwa waangalifu ili tusiambukizwe na dini ya uongo. (1 Wakorintho 10:21) Ni lazima kabisa tuwe waangalifu kwa sababu uvutano wa dini ya uongo uko mahali pote. Katika inchi nyingi, mazoea na desturi mbalimbali zinatia ndani mafundisho ya dini ya uongo, kama vile fundisho la kwamba kuna kitu fulani ndani yetu kinachoendelea kuishi tunapokufa. (Mhubiri 9:5, 6, 10) Wakristo wa kweli wanajiepusha na desturi zinazotia ndani mafundisho ya dini ya uongo.b Hatutakubali watu watulazimishe kuvunja sheria za Biblia kuhusu ibada safi.—Matendo 5:29.
11. Kuwa na mwenendo safi kunamaanisha nini, na sababu gani ni jambo la maana sana kuwa na mwenendo safi?
11 Kuwa na mwenendo safi. Kuwa na mwenendo safi kunamaanisha kuepuka namna yote ya uasherati. (Waefeso 5:5) Ni jambo la maana sana kuwa na mwenendo safi. Kama tutakavyoona katika sura inayofuata, ili tubaki katika upendo wa Mungu, tunapaswa ‘kukimbia uasherati.’ Waasherati wasiotubu ‘hawatauriti ufalme wa Mungu.’ (1 Wakorintho 6:9, 10, 18) Machoni pa Mungu, watu kama hao wako kati ya “wale wenye kuchukiza katika uchafu wao.” Ikiwa hawasafishe mwenendo wao, “fungu lao litakuwa . . . kifo cha pili.”—Ufunuo 21:8.
12, 13. Kuna uhusiano gani kati ya mawazo na matendo, na namna gani tunaweza kubaki safi kiakili?
12 Kuwa safi kiakili. Ni mawazo ndio yanayomuongoza mutu kutenda. Tukiacha mawazo mabaya yaingie katika akili na moyo wetu, tutafikia kufanya mambo mabaya. (Mathayo 5:28; 15:18-20) Lakini tukijaza akili yetu na mawazo yaliyo safi, tutachochewa kuendelea kuwa na mwenendo safi. (Wafilipi 4:8) Namna gani tunaweza kubaki safi kiakili? Kwanza, tunapaswa kuepuka namna yoyote ya kujifurahisha inayoweza kuharibu akili yetu.c Tena, tunaweza kujaza mawazo safi katika akili yetu kwa kujifunza kwa ukawaida Neno la Mungu.—Zaburi 19:8, 9.
13 Ili kubaki katika upendo wa Mungu, tunapaswa kuwa safi kiroho, kiakili na kuwa na mwenendo safi. Mambo hayo yanazungumuziwa zaidi katika sura zingine za kitabu hiki. Kwa sasa, acheni tuzungumuzie jambo la ine—usafi wa kimwili.
MAANA YA KUWA SAFI KIMWIL
14. Sababu gani mutu hawezi kusema kama usafi wa kimwili ni jambo linalomuangalia yeye peke yake?
14 Kuwa safi kimwili maana yake mwili wetu unapaswa kuwa safi na vitu vyetu pia. Je, usafi wa kimwili ni jambo linalomuangalia mutu peke yake? Hapana. Waabudu wa Yehova hawapaswe kuwa na mawazo hayo. Kama tulivyoona, usafi wetu wa kimwili ni wa maana sana machoni pa Yehova; ni kwa faida yetu na pia jambo hilo linamuletea Mungu sifa. Fikiria mufano tuliozungumuzia hapo mwanzoni. Watu wanapoona mutoto ambaye ni muchafu kila mara, wanauliza, “Huyu ni mutoto wa nani?” Hatutake jambo fulani juu ya mwili ao mwenendo wetu limuchafue Baba yetu wa mbinguni ao liwafanye watu wazarau ujumbe tunaohubiri. Neno la Mungu linasema hivi: ‘Sisi hatutoe sababu yoyote ya kukwaza kwa njia yoyote, ili huduma yetu isilaumiwe; bali katika kila njia tunajipendekeza kuwa wahudumu wa Mungu.’ (2 Wakorintho 6:3, 4) Sasa namna gani tunaweza kuendelea kuwa safi kimwili?
15, 16. Kuwa safi kunamaanisha pia kuwa na tabia gani nzuri, na nguo zetu zinapaswa kuwa namna gani?
15 Usafi wa mwili wetu na mavazi yetu. Hata ikiwa desturi na hali za maisha zinatofautiana kulingana na kila inchi, mara nyingi tunaweza kupata sabuni na maji ili kuoga kwa ukawaida na kuhakikisha kama watoto wetu pia wako safi. Kuwa safi kunamaanisha pia kuwa na tabia nzuri ya kunawa mikono na sabuni mbele ya kula ao mbele ya kugusa chakula. Tunapotoka kwenye choo ao musalani, na kisha kumunawisha mutoto ao wakati mutu anamubadilisha mutoto nguo kwa sababu amefanya choo kubwa ao ndogo, tunapaswa kunawa mikono. Tabia ya kunawa mikono na sabuni inaweza kutuepusha na magonjwa na kulinda uzima wetu. Inaweza kusaidia mikrobe inayoleta magonjwa ya kuhara isisambae. Ni vizuri pia kuzika uchafu kama vile mavi; zamani Waisraeli waliombwa kufanya hivyo.—Kumbukumbu la Torati 23:12, 13.
16 Inaomba pia kusafisha nguo zetu kwa ukawaida ili ziwe safi na zenye kupendeza. Si lazima nguo za Mukristo ziwe za bei sana ao za kisasa ili awe safi, lakini zinapaswa kuwa safi na hazipaswe kupitisha kiasi. (1 Timotheo 2:9, 10) Hata tuwe wapi, tunataka mwili na mavazi yetu ‘yalipambe fundisho la Mwokozi wetu, Mungu.’—Tito 2:10.
17. Sababu gani nyumba na vitu vyetu vinapaswa kuwa safi na vyenye kupendeza?
17 Nyumba yetu na vitu vyetu. Nyumba yetu inaweza kuwa safi na yenye kupendeza kadiri iwezekanavyo hata ikiwa si ya bei sana ao ya hali ya juu. Vitu vyetu vyote vinapaswa kuwa safi, kama vile sakoshi yetu ya kubebea vitabu, zaidi sana ikiwa tunatumia sakoshi hiyo kwenye mikutano ao katika mahubiri. Ni hivyohivyo ikiwa tunatumia motokari. Tusisahau jambo hili: Ikiwa nyumba yetu na vitu vyetu ni safi, hilo litatoa ushahidi juu ya Mungu tunayemuabudu. Jambo lingine ni kwamba tunawafundisha watu kama Yehova ni Mungu aliye safi, na ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia,’ na hivi karibuni Ufalme wake utafanya dunia iwe paradiso. (Ufunuo 11:18; Luka 23:43) Kwa hiyo, inaomba vitu vyetu viwaonyeshe wengine kama hata leo tumeanza kuwa na tabia ya usafi ambao watu watakuwa nao katika dunia mupya.
Usafi wa kimwili unatia ndani kusafisha mwili wetu na mahali kwenye tunaishi
18. Namna gani tunaweza kuonyesha kama tunaheshimu Jumba letu la Ufalme?
18 Nafasi yetu ya ibada. Upendo wetu kwa Yehova unatusukuma tuheshimu Jumba letu la Ufalme, ambapo ni mahali pa ibada safi katika eneo letu. Wakati wapya wanakuja, tunataka wafurahie mahali petu pa mikutano. Ili Jumba letu la Ufalme liendelee kuwa mahali pa kupendeza na safi, inaomba lisafishwe na kutunzwa kwa ukawaida. Tunaonyesha kama tunaheshimu Jumba letu la Ufalme kwa kufanya yote tuwezayo ili kulisafisha na kulitunza. Ni pendeleo kutumia wakati wetu ili kusaidia kusafisha na “kutengeneza” mahali petu pa ibada. (2 Mambo ya Nyakati 34:10) Tunapaswa kufanya hivyo pia tunapokuwa kwenye Jumba la Mikusanyiko ao jengo lingine linalotumiwa kwa ajili ya mikusanyiko.
KUJIEPUSHA NA TABIA NA MAZOEA MACHAFU
19. Ili kuwa safi kimwili, tunapaswa kujiepusha na nini, na namna gani Biblia inatusaidia katika jambo hilo?
19 Ili kuwa safi kimwili, tunapaswa kujiepusha na tabia na mazoea machafu, kama vile kuvuta sigareti ao tumbaku, kunywa pombe kupita kiasi, na kutumia dawa za kulewesha bila ruhusa ya muganga ao kutumia dawa zinazofanya mutu asitumie akili vizuri. Bibia haitaje moja kwa moja tabia zote chafu na mazoea yote machafu ya siku zetu, lakini ina kanuni zinazotusaidia kutambua mawazo ya Yehova juu ya tabia hizo. Kwa sababu tunajua mawazo ya Yehova juu ya mambo hayo, upendo wetu kwake utatusukuma kufuatia njia inayofanya atukubali. Acheni basi tuzungumuzie kanuni tano za Biblia.
20, 21. Yehova anataka tujiepushe na mazoea ya namna gani, na ni sababu gani nzuri sana inayotuchochea kufuata shauri hilo?
20 ‘Wapendwa, kwa kuwa tuna ahadi hizi, acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi [ao uchafu] wa mwili na roho, tukiukamilisha utakatifu katika kumuogopa Mungu.’ (2 Wakorintho 7:1) Yehova anataka tujiepushe na mazoea yanayochafua mwili wetu na yanayoharibisha akili yetu. Kwa hiyo, tunapaswa kuepuka mazoea yote yanayoharibisha afya ya mwili wetu na yanayoharibisha akili yetu.
21 Biblia inatutolea sababu nzuri sana ya ‘kujisafisha wenyewe kila unajisi.’ Andiko la 2 Wakorintho 7:1 linaanza kwa kusema: “Kwa kuwa tuna ahadi hizi.” Ni ahadi gani? Mistari inayotangulia inaonyesha kama Yehova anaahidi hivi: “Nami nitawakaribisha ndani. Nami nitakuwa baba kwenu.” (2 Wakorintho 6:17, 18) Fikiria jambo hili: Yehova anaahidi kukulinda na kukupenda kama vile baba anavyopenda mutoto wake. Lakini Yehova atakutimizia ahadi hizo ikiwa tu unajiepusha na uchafu wa “mwili na roho.” Itakuwa upumbavu kabisa ikiwa mutu anaacha tabia fulani ao zoea fulani chafu limuzuie kuwa na urafiki muzuri kama huo pamoja na Yehova, sivyo?
22-25. Ni kanuni gani za Biblia zinazoweza kutusaidia kuepuka tabia na mazoea machafu?
22 ‘Lazima umupende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ (Mathayo 22:37) Yesu alisema kama hiyo ndio amri kubwa kuliko amri zote. (Mathayo 22:38) Yehova anastahili upendo wetu wote. Ili tumupende Yehova kwa moyo wetu wote, kwa nafsi yetu yote na kwa akili yetu yote, tunapaswa kujiepusha na mazoea yanayoweza kufupisha maisha yetu ao kupunguza akili ambayo Mungu alitupatia.
23 ‘[Yehova] huwapa watu wote uzima na pumuzi na vitu vyote.’ (Matendo 17:24, 25) Uzima ni zawadi ambayo Mungu alitupatia. Tunapaswa kuheshimu zawadi hiyo kwa sababu tunamupenda Mutoaji wa zawadi hiyo. Kwa hiyo, tunaepuka tabia ao mazoea yote yanayoweza kuharibisha afya yetu, kwa sababu tunatambua kwamba mutu aliye na mazoea hayo anaonyesha kama haheshimu hata kidogo zawadi ya uzima.—Zaburi 36:9.
24 ‘Mupende jirani yako kama wewe mwenyewe.’ (Mathayo 22:39) Mara nyingi, tabia na mazoea machafu yana matokeo mabaya, si kwa mutendaji tu lakini pia kwa watu walio karibu yake. Kwa mufano, moshi wa sigareti ao tumbako unaweza kuwa na matokeo mabaya juu ya wale wasiovuta na hata kuhatarisha maisha yao. Mutu anayetendea vibaya watu walio karibu yake anavunja amri ya Mungu ya kumupenda jirani. Tena, matendo yake yanaonyesha wazi kama yeye ni muongo hata ikiwa anasema, ninamupenda Mungu.—1 Yohana 4:20, 21.
25 ‘Munyenyekee wenye kutawala, na wenye mamlaka . . . , na kutii.’ (Tito 3:1, La Sainte Bible en Swahili de la R.D. Congo) Katika inchi nyingi, kuwa na dawa za kulewesha ao kuzitumia ni kuvunja sheria. Sisi Wakristo wa kweli hatuwezi kuwa na dawa za kulewesha ao kuzitumia kinyume na sheria.—Waroma 13:1.
26. (a) Ili kubaki katika upendo wa Mungu, tunapaswa kufanya nini? (b) Sababu gani kuendelea kuwa safi machoni pa Mungu ndio namna nzuri zaidi ya kuishi?
26 Ili kubaki katika upendo wa Mungu, tunapaswa kuendelea kuwa safi, si katika mambo fulani-fulani tu, lakini katika mambo yote ya maisha yetu. Inaweza kuwa vigumu kuachana kabisa na tabia na mazoea machafu, lakini inawezekana kufanya hivyo.d Hakika, kuendelea kuwa safi ndio namna nzuri zaidi ya kuishi, kwa sababu kila mara Yehova anatufundisha kwa faida yetu wenyewe. (Isaya 48:17) Jambo la maana zaidi ni hili: tukiendelea kuwa safi, tunaweza kupata furaha kwa sababu tunajua kama tunamuletea sifa Mungu tunayemupenda, na hivyo tutabaki katika upendo wake.
a Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “safi” halimaanishe tu usafi wa mwili, linamaanisha pia mwenendo safi na usafi wa kiroho.
b Soma Sura ya 13 ya kitabu hiki inayozungumuzia sikukuu fulani na desruri ambazo Wakristo wa kweli wanaepuka.
d Soma kisanduku “Je, Ninajikaza Kabisa Kufanya Yaliyo Sawa?” na kisanduku “Kwa Mungu Mambo Yote Yanawezekana” hapa juu.”
e Jina limebadilishwa.