SURA YA 16
Pinga Ibilisi na Njia Zake za Kudanganya
‘Mumupinge Ibilisi, naye atawakimbia.’—YAKOBO 4:7.
1, 2. Ni nani wanaofurahi wanapoona maelfu ya watu wanabatizwa?
IKIWA umekwisha kumutumikia Yehova kwa miaka mingi, umekwisha kusikia hotuba nyingi za ubatizo kwenye mikusanyiko yetu. Hata ikiwa umehuzuria mikusanyiko hiyo mara nyingi, bila shaka, unakuwa na furaha sana kila mara unapowaona wale wanaokaa kwenye viti vya mbele wanaposimama ili kuonyesha kama wamejitoa kwa Yehova katika sala na kama wanataka kubatizwa. Wakati huo, wahuzuriaji wote wanakuwa wenye furaha sana na kisha unawasikia wanapiga mikono kwa uchangamufu. Unaweza hata kutoa machozi unapowaona ndugu na dada hao wapya kuchukua musimamo upande wa Yehova. Bila shaka, wakati kama huo unatufurahisha kabisa!
2 Sisi tunaweza kuona watu wanabatizwa labda mara tatu tu katika mwaka; lakini malaika wana pendeleo la kuona jambo hilo mara nyingi zaidi. Sasa wazia furaha inayokuwa mbinguni, kila juma wanapoona maelfu ya watu duniani wanajiunga na sehemu inayoonekana ya tengenezo la Yehova? (Luka 15:7, 10) Hakika, wanapoona ongezeko hilo, wanakuwa wenye furaha sana!—Hagai 2:7.
IBILISI “ANATEMBEA HUKU NA HUKU KAMA SIMBA ANAYENGURUMA”
3. Sababu gani Shetani anatembea huku na huku “kama simba anayenguruma,” na ana kusudi gani?
3 Hata hivyo, wakati watu wanabatizwa kuna viumbe wengine wa kiroho ambao wanawakasirikia sana watu hao. Shetani na mashetani wake ni wenye kukasirika sana wanapoona maelfu ya watu wanakataa kabisa ulimwengu huu muovu. Shetani anapaswa kuwa hivyo, kwa sababu yeye alisema kwa kiburi kama hakuna mwanadamu anayeweza kumutumikia Yehova kwa sababu ya upendo wa kweli, na kama hakuna mutu anayeweza kubaki mwaminifu kwa Mungu ikiwa anajaribiwa vikali. (Ayubu 2:4, 5) Kwa hiyo, kila mara mutu anapojitoa kwa Yehova katika sala na kubatizwa, hilo linaonyesha kama Shetani ni muongo. Ni kama vile kila juma Shetani anapigwa maelfu ya makofi kwenye mashavu. Basi haishangaze ikiwa ‘anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kumumeza mutu’! (1 Petro 5:8) “Simba” huyo anatamani sana kuturarua kiroho, ni kusema, kuharibu ao kuvunja urafiki wetu pamoja na Mungu.—Zaburi 7:1, 2; 2 Timotheo 3:12.
Kila wakati mutu fulani anajitoa kwa Yehova na kubatizwa, Shetani anaonekana kuwa muongo
4, 5. (a) Ni mambo gani mawili ambayo Shetani hana uwezo wa kufanya? (b) Na kila Mukristo anapaswa kufanya nini ili kumushinda?
4 Kwa kweli, tunapambana na adui mukali, hata hivyo, hatupaswe kuogopa. Sababu gani? Kwa sababu kuna mambo mawili ambayo Yehova amefanya ili kutuhakikishia kwamba ‘simba huyo anayenguruma’ hatakuwa na uwezo wa kutuangamiza. Ni mambo gani? Jambo la kwanza: Yehova ametabiri kwamba ‘umati ao mukutano mukubwa,’ wa Wakristo wa kweli, utaokoka ile ‘ziki kubwa’ inayokuja. (Ufunuo 7:9, 14) Unabii wa Mungu hauwezi kukosa kutimia hata kidogo. Kwa hiyo, Shetani mwenyewe anajua vizuri kama hana uwezo wa kuharibu watumishi wote wa Mungu kwa ujumla.
5 Jambo la pili, ni maneno ambayo nabii Azaria alimuambia Mufalme Asa. Alimuambia hivi: ‘Yehova iko pamoja nanyi ikiwa ninyi muko pamoja naye.’ (2 Mambo ya Nyakati 15:2; 1 Wakorintho 10:13) Mifano mingi ya zamani iliyoandikwa inaonyesha kama hakuna wakati ambapo Shetani alifikia kuangamiza mutumishi fulani wa Mungu ambaye alibaki karibu na Mungu. (Waebrania 11:4-40) Leo pia, ikiwa Mukristo anaendelea kubaki karibu na Mungu, anaweza kumupinga Ibilisi na hata kumushinda. Tunapata uhakika wa jambo hilo katika Neno la Mungu, kwa sababu linasema hivi: ‘Mumupinge Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.’—Yakobo 4:7.
TUNASHINDANA MUELEKA NA MAJESHI YA ROHO WAOVU
6. Shetani anamupiganisha kila Mukristo namna gani?
6 Katika vita hiyo ya mufano, Shetani hawezi kuwashinda watu wote wa Mungu kwa ujumla, hata hivyo, sisi mutu mumoja mumoja tunaweza kushindwa ikiwa hatufungue macho. Shetani anajua kama anaweza kuturarua ikiwa anafikia kuregeza urafiki wetu pamoja na Yehova. Shetani anatumia njia gani ili kuturegeza? Anatuletea magumu mengi, anatushambulia moja kwa moja, na anatumia njia mbalimbali za kudanganya. Acha sasa tuzungumuzie njia hizo kubwa ambazo Shetani anatumia.
7. Sababu gani Shetani anashambulia sana watu wa Yehova?
7 Magumu mengi. Mutume Yohana aliandika hivi: ‘Ulimwengu muzima unakaa katika nguvu za yule muovu.’ (1 Yohana 5:19) Maneno hayo ni onyo kwa Wakristo wote wa kweli. Kwa sababu Shetani amekwisha kupotosha wanadamu wote wasiomuogopa Mungu, sasa uangalifu wake ni juu ya wale ambao wameponyoka, ni kusema, watu wa Yehova, na ndio sababu anafanya wawe na magumu mengi. (Mika 4:1; Yohana 15:19; Ufunuo 12:12, 17) Ana hasira kali kwa sababu anajua kama wakati wake ni mufupi. Kwa hiyo, anafanya magumu hayo yaongezeke. Leo, anaonyesha meno yake yote na makucha yake ili atuangamize kabisa bila huruma. Basi, sasa tunapaswa ‘kutambua nyakati ili kujua yale ambayo tunapaswa kufanya.’—1 Mambo ya Nyakati 12:32.
8. Mutume Paulo alipenda kusema nini aliposema kwamba tunakushindana ‘mueleka’ na roho waovu?
8 Mashambulizi ya moja kwa moja. Mutume Paulo aliwaonya Wakristo wenzake hivi: ‘Tuna kushindana mueleka na majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.’ (Waefeso 6:12) Sababu gani mutume Paulo alitumia neno ‘mueleka’? Kwa sababu neno hilo lina wazo la watu wawili ambao wanapigana kwa kukamatana mukono kwa mukono na mwili. Kwa hiyo, Paulo alitumia neno hilo ili kuonyesha kwamba kila mumoja wetu anapigana kabisa na mashetani. Hata ikiwa tunaishi katika inchi ambamo watu wengi wanaamini kama kuna roho waovu ao hapana, tunapaswa kujua kwamba wakati tulijitoa kwa Yehova katika sala, ni kama vile tuliingia katika uwanja wa kushindana mueleka. Kila Mukristo, kuanzia siku alipojitoa, ameingia katika vita hiyo. Kwa hiyo, haishangaze kwamba mutume Paulo aliona lazima ya kuwashauri mara tatu Wakristo wenzake wa Efeso kwamba ‘wasimame imara’!—Waefeso 6:11, 13, 14.
9. (a) Sababu gani Shetani na mashetani wake wanatumia njia mbalimbali za kudanganya? (b) Sababu gani Shetani anajaribu kuharibu mawazo yetu, na namna gani tunaweza kumupinga? (Soma kisanduku “Angalisho na Njia za Kudanganya za Shetani”) (c) Ni njia gani ya kudanganya ya Shetani ambayo sasa tutazungumuzia?
9 Njia za kudanganya. Paulo anawashauri Wakristo wasimame imara ili kuzipinga “hila” ao njia za kudanganya za Shetani. (Waefeso 6:11) Unaona kwamba mutume Paulo haseme “hila ya” lakini “hila za.” Roho hao waovu wana hila ao njia mbalimbali za kudanganya, na kuna sababu. Kwa mufano, wakati fulani Wakristo walisimama imara na kupinga jaribu la aina fulani lilipotokea, lakini walishindwa walipojaribiwa kwa njia nyingine. Ndio sababu, Ibilisi na mashetani wake wanatazama sana mazoea ya kila mumoja wetu ili kujua uzaifu wake mukubwa zaidi. Wakiisha kujua uzaifu wa kiroho alio nao, wanautumia ili kumuangusha. Lakini, jambo la kupendeza ni kwamba tunaweza kujua njia mbalimbali za kudanganya ambazo Ibilisi anatumia, kwa sababu zinatajwa wazi katika Biblia. (2 Wakorintho 2:11) Katika kitabu hiki, tumekwisha kuzungumuzia mambo kama vile tamaa ya vitu vya kimwili, marafiki wabaya, mambo ya uasherati. Acha tuzungumuzie njia nyingine ya kudanganya ambayo Shetani anatumia: kuzungumuza na pepo ao mashetani.
KUZUNGUMUZA NA MASHETANI NI KUKOSA UAMINIFU KWA MUNGU
10. (a) Kuzungumuza na mashetani ni nini? (b) Yehova anaona jambo hilo namna gani, na wewe unaliona namna gani?
10 Mutu anapozungumuza na mashetani ao pepo anakuwa rafiki yao. Uaguzi, ulozi, uchawi, na kuuliza mambo kutoka kwa watu waliokufa ni njia mbalimbali za kuzungumuza na mashetani. Kama tunavyojua, kuzungumuza na mashetani ni “chukizo” machoni pa Yehova. (Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Ufunuo 21:8) Kwa sababu sisi pia tunapaswa ‘kuchukia maovu,’ hatupaswe hata kidogo kujaribu kushirikiana na roho waovu. (Waroma 12:9) Kufanya hivyo ni kukosa kabisa uaminifu kwa Baba yetu wa mbinguni, Yehova! Tunapaswa kulichukia kabisa jambo hilo.
11. Shetani akiweza kutushawishi na kutuingiza katika mambo ya kuzungumuza na mashetani, sababu gani huo unaweza kuwa ushindi mukubwa kwake? Toa mufano.
11 Kwa sababu kuzungumuza na mashetani ni kukosa uaminifu kwa Yehova, Shetani anafanya yake yote ili wengine kati yetu wajiingize katika mazoea hayo. Kila wakati Shetani anamuvuta Mukristo kuingia katika mambo ya kuzungumuza na mashetani, huo ni ushindi mukubwa sana kwake. Sababu gani? Fikiria mufano huu: Ikiwa maadui wanamushawishi askari fulani, naye anajiunga nao na kukimbia wenzake, mukubwa wa jeshi adui atafurahi sana, sivyo? Anaweza hata kumusimamisha mbele ya wengine na kujivuna, na kumuchekelea mukubwa wa jeshi lile lingine, upande ambao askari huyo alitoka. Vivyo hivyo, ikiwa Mukristo anashirikiana na mashetani, anaonyesha kama anamukana Yehova kimakusudi, na kwa kufanya hivyo, anakubali aongozwe na Shetani. Fikiria furaha ya kiburi ambayo Shetani anaweza kuwa nayo ili kuonyesha kama ameshinda! Je, wewe utataka Ibilisi ajivune hivyo? Hapana! Sisi hatutake kumukana Mungu wetu, sivyo?
ANAPENDA KUTOKEZA MASHAKA KATIKA MIOYO YETU
12. Shetani anatumia njia gani ili kubadilisha namna yetu ya kufikiri kuhusu mambo ya kuzungumuza na mashetani?
12 Ikiwa tunachukia kabisa tendo la kushirikiana na mashetani, Shetani hataweza kutushinda kwa kutumia njia hiyo. Kwa hiyo, atapenda kwanza abadilishe namna yetu ya kufikiri. Namna gani? Atatafuta njia za kuvuruga akili za Wakristo ili wengine kati yao wafikiri kwamba “wema ni ubaya na ubaya ni wema.” (Isaya 5:20) Ili kufikia kusudi hilo, Shetani anatumia moja kati ya njia zake ambazo ametumia kwa muda murefu: kutokeza mashaka katika mioyo yetu.
13. Namna gani Shetani anatumia njia ya kutokeza mashaka katika mioyo yetu?
13 Ona namna alitumia ufundi huo katika Edeni. Alimuuliza Eva hivi: ‘Je, ni kweli kwamba Mungu alisema musikule matunda ya kila muti wa bustani?’ Katika siku za Ayubu, mbinguni kulikuwa na mukutano wa malaika, Shetani aliuliza hivi: ‘Je, Ayubu anamuogopa Mungu bure?’ Na wakati Yesu alianza kazi yake hapa duniani, Shetani alimujaribu kwa kusema: ‘Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, uambie mawe haya yawe mikate.’ Unaona kama Shetani alikuwa anamuchekelea kabisa Yehova; majuma sita tu mbele ya hapo Yehova alikuwa ametumia maneno hayo: ‘Huyu ni Mwana wangu, mupendwa, ambaye nimemukubali’!—Mwanzo 3:1; Ayubu 1:9; Mathayo 3:17; 4:3.
14. (a) Namna gani Shetani anatumia njia hiyohiyo ili kuamusha mashaka juu ya mambo ya kushirikiana na mashetani? (b) Tutazungumuzia nini sasa?
14 Leo, Ibilisi anatumia njia hiyohiyo ili kufanya watu wafikiri kama hakuna hatari yoyote ya kushirikiana na mashetani. Ni sikitiko kujua kwamba amefikia kutokeza mashaka katika akili za watumishi fulani wa Yehova. Wameanza kujiuliza ikiwa namna fulani za kushirikiana na pepo ni mbaya kabisa. Ni kama vile wameanza kujiuliza hivi: ‘Je, ni kweli?’ (2 Wakorintho 11:3) Namna gani tunaweza kuwasaidia ndugu hao wabadilishe mawazo yao? Tunaweza kufanya nini ili Shetani asiharibishe akili zetu? Ili kupata jibu, acha tuzungumuzie mambo mawili ya kawaida katika maisha, ambayo kwa ujanja Shetani amefanya iwe njia ya kushirikiana na mashetani. Ni mambo ya kujifurahisha na matunzo.
SHETANI ANAWEZA KUTUMIA TAMAA ZETU NA MAHITAJI YETU
15. (a) Watu wengi katika inchi za Ulaya na Amerika wanaona mambo ya uchawi ao kuamusha mashetani namna gani? (b) Namna gani Wakristo fulani wamevutiwa na mawazo ya ulimwengu kuhusu mambo ya kushirikiana ao kuzungumuza na mashetani?
15 Zaidi sana katika inchi za Ulaya na Amerika, watu wengi wanaona mambo ya uchawi, mambo ya kuita ao kuamusha mashetani na njia zingine za kushikirana na mashetani kuwa mambo ya muchezo tu. Filme, vitabu, vipindi kwenye televizyo, na michezo ya ordinatere inazidi kufanya mazoea hayo yaonekane kuwa jambo lenye kufurahisha, lisilokuwa na hatari yoyote. Watu wengi sana wanapendezwa na filme na vitabu fulani vinavyoonyesha mambo ya uchawi, na mambo ya kuita ao kuamusha mashetani, na wanaanza sasa kufanya vikundi vya watu wanaopendezwa na mambo hayo. Ni wazi, roho waovu wamefikia kuwafunga watu macho ili wasione hatari ya mambo hayo. Je, inawezekana Wakristo fulani waanze kuona mambo hayo kuwa ni muchezo tu? Wengine wamenaswa kabisa. Namna gani? Kwa mufano, Mukristo mumoja alipoangalia filme ya mambo ya uchawi, alisema hivi: “Niliangalia tu filme hiyo, lakini mimi sikushirikiana na roho waovu.” Sababu gani kufikiri hivyo ni hatari kabisa?
16. Sababu gani ni hatari kuangalia mambo ya uchawi ili kujifurahisha?
16 Hata ikiwa ni kweli kwamba kuna tofauti kati ya kufanya uchawi na kuangalia mambo ya uchawi kwenye televizyo, lakini hiyo haimaanishe kwamba hakuna hatari yoyote ya kuangalia mambo hayo. Sababu gani? Fikiria jambo hili: Neno la Mungu linaonyesha kwamba Shetani na mashetani wake hawana uwezo wa kusoma yaliyo katika mawazo yetu.a Kwa hiyo, kama tulivyosema mwanzoni, ili kujua yaliyo katika mawazo yetu na uzaifu wetu wa kiroho, mashetani wanachunguza kwa uangalifu matendo yetu na yale tunayopenda ili kujifurahisha. Mukristo anapoonyesha kwamba anafurahia filme, na vitabu vinavyoonyesha mambo ya ufumu (medium), ya kuloga, ya mashetani kumuingia mutu, ao mambo mengine ya mashetani, anawajulisha mashetani jambo fulani. Mukristo huyo anawaambia mashetani hivi: “Uzaifu wangu ndio huu”! Hivyo, wanaweza kumushambulia zaidi Mukristo huyo, wanaweza kutumia uzaifu wake, mupaka watakapomupiga mueleka na kumuangusha chini. Kwa kweli, wale walioanza kuvutiwa na mazoea hayo, mwanzoni waliwaza ni muchezo wa kujifurahisha tu, lakini, mwishowe walijikuta wameingia kabisa katika mazoea hayo ya kushirikiana na mashetani.—Wagalatia 6:7.
Faidika na musaada wa Yehova wakati unagonjwa
17. Shetani anaweza kutumia njia gani ya kudanganya ili kushawishi ndugu ao dada walio wagonjwa?
17 Shetani hatumie tu tamaa yetu ya kujifurahisha ili kutuangusha, lakini anaweza pia kutumia tamaa tuliyo nayo ya kujitunzisha. Namna gani? Mukristo ambaye hali ya afya yake inazidi kuharibika hata kisha kujaribu matunzo ya kila namna anaweza kuvunjika moyo. (Marko 5:25, 26) Shetani na mashetani wake wanaweza kutumia hali hiyo ili kumuangusha. Wanajua vizuri kama Neno la Mungu linatushauria tusitafute ‘usaidizi wa wale wanaozoea kufanya mambo yenye kuzuru.’ (Isaya 31:2) Ili kumufanya Mukristo apuuze shauri hilo, roho waovu wanaweza kumushawishi ndugu ao dada huyo, kwa sababu hana tena tumaini, akubali matunzo ao ufundi wa kutunza unaoomba matumizi ya “nguvu za uchawi,” ao kushirikiana na mashetani: jambo ambalo ni lenye kuzuru kabisa. Ufundi huo wenye kudanganya wa mashetani ukifanikiwa, unaweza kuharibisha uhusiano wa ndugu ao dada huyo pamoja na Mungu. Namna gani?
18. Ni matunzo ya namna gani ambayo Mukristo anapaswa kukataa, na sababu gani?
18 Yehova aliwashauri Waisraeli walioanza kutumia “nguvu za uchawi,” hivi: ‘Munaponyoosha mikono yenu, mimi ninaficha macho yangu kutoka kwenu. Hata munapotoa sala nyingi, mimi sisikilize.’ (Isaya 1:13, 15) Kwa kweli, tunapaswa kuepuka kila jambo linaloweza kufanya sala zetu zisisikilizwe na kutufanya tukose musaada wa Yehova; zaidi sana wakati tuko wagonjwa. (Zaburi 41:3) Kwa hiyo, ikiwa matunzo fulani ao njia fulani ya kupimwa inagusia kidogo tu mazoea fulani ya kushirikiana na mashetani, Mukristo wa kweli anapaswa kuikataa.b (Mathayo 6:13) Kwa kufanya hivyo, anaweza kutumaini kupata musaada wa Yehova.—Soma kisanduku “Je, Ni Kushirikiana kabisa na Mashetani?””
WAKATI WATU WANAZUNGUMUZIA HADISI ZA MAMBO YA MASHETANI
19. (a) Ibilisi amewafanya watu wengi waamini nini juu ya nguvu zake? (b) Ni hadisi gani Wakristo wa kweli hawapaswe kusikiliza ao kusambaza?
19 Tumeona kama watu wa Ulaya na Amerika hawaone hatari ya nguvu za Shetani, lakini katika sehemu zingine za dunia watu wana mawazo tofauti. Katika sehemu zingine za dunia Ibilisi amewadanganya watu wengi na kuwafanya waamini kama ana nguvu nyingi kuliko zile ambazo kwa kweli anazo. Watu wengine wanaogopa mashetani katika kila jambo wanalofanya: iwe wanapokula, wanapotumika, wanapolala na hata maisha yao yote. Mazungumuzo ya watu hao ni hadisi ya nguvu za ajabu ambazo mashetani wanazo. Wanasimulia hadisi hizo kwa njia yenye kupendeza sana; na wanavutiwa sana nazo. Je, sisi pia tunapaswa kuzungumuzia hadisi kama hizo? Hapana. Kuna sababu mbili za lazima zinazowakataza watumishi wa Mungu wa kweli kufanya hivyo.
20. Namna gani Mukristo anaweza kuwa muhubiri wa Shetani bila kujua?
20 Ya kwanza: Mutu anapoeneza hadisi hizo zenye kuzungumuzia nguvu za mashetani, anamusaidia Shetani kuendeleza kazi yake. Namna gani hivyo? Neno la Mungu linaonyesha kwamba Shetani anaweza kufanya kazi zenye nguvu, lakini pia linatushauri kama Shetani anatumia ‘ishara za uongo’ na “udanganyifu.” (2 Wathesalonike 2:9, 10) Kwa kuwa Shetani ndiye fundi mukubwa wa kudanganya, anajua nini anaweza kufanya ili kuharibisha mawazo ya wale wanaopenda mambo ya kuzungumuza na mashetani na kuwafanya waamini mambo yasiyo ya kweli. Watu hao wanaweza kuamini kabisa kama waliona na kusikia mambo fulani na kisha wanaweza kuanza kuhadisia wengine mambo hayo kama kwamba ni mambo ya kweli. Kisha, hadisi hizo zinapoendelea kuzungumuziwa zinatiwa chumvi. Mukristo akisambaza hadisi hizo, anafanya kabisa mapenzi ya Ibilisi, ‘baba wa uongo.’ Mukristo huyo anakuwa muhubiri wa Shetani.—Yohana 8:44; 2 Timotheo 2:16.
21. Tunapaswa kuzungumuzia mambo gani?
21 Ya pili: Hata ikiwa wakati wa zamani Mukristo alifanya mambo hayo ya mashetani, hapaswe kuwafurahisha ndugu wengine kwa kuwaelezea hadisi za mambo hayo. Sababu gani? Biblia inatushauri tumutazame sana Wakili Mukubwa na Mukamilishaji wa imani yetu, Yesu. (Waebrania 12:2) Ndiyo, tunapaswa kumukazia Kristo fikira, wala si Shetani. Wazia jambo hili: Yesu alipokuwa duniani, hakuwafurahisha wanafunzi wake kwa kuwahadisia mambo ya mashetani, ijapokuwa yeye alijua mambo mengi ambayo Shetani anaweza ao hawezi kufanya. Lakini, Yesu alikazia fikira habari ya Ufalme. Kwa hiyo, tumuige Yesu na mitume wake, tuzungumuzie ‘mambo makubwa ya Mungu.’—Matendo 2:11; Luka 8:1; Waroma 1:11, 12.
22. Tunaweza kufanya nini ili mbinguni kuendelee kuwa na furaha?
22 Ni kweli kwamba Shetani anatumia njia nyingi za kudanganya, kutia ndani kuzungumuza na mashetani, ili kutuangusha na kuharibisha urafiki wetu na Yehova. Hata hivyo, tukichukia maovu na kushikamana na yaliyo mema, Ibilisi hataweza kuregeza azimio letu la kukataa kabisa namna zote za kushirikiana na mashetani. (Waefeso 4:27) Wazia furaha kubwa itakayokuwa mbinguni tukiendelea kusimama imara na kupinga njia za kudanganya za Ibilisi mupaka wakati hatakuwa tena!—Waefeso 6:11.
a Majina ya Shetani, (Mupinzani, Musingiziaji, Mudanganyifu, Mujaribu ao Mushawishi, Muongo) yanaonyesha kwamba hana uwezo wa kusoma katika mioyo na mawazo yetu. Lakini, Yehova yeye anasemwa kuwa ‘muchunguzi wa mioyo,’ na Yesu pia anasemwa kuwa yule ‘anayechunguza figo na mioyo.’—Methali 17:3; Ufunuo 2:23.
b Ili kupata habari zaidi, soma Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 12, 1994, ukurasa wa 19-22, kwenye kichwa “Mtihani wa Afya Kwako?” na pia Amkeni! ya tarehe 8 Mwezi wa 1, 2001, kwenye kichwa “Maoni ya Biblia: Uchaguzi Wako wa Matibabu—Je, Ni Muhimu?”