SURA YA 11
Fasi Yetu ya Ibada
WAABUDU wa kweli wa Yehova wanapaswa kukusanyika ili wafundishwe na ili watiane moyo. (Ebr. 10:23-25) Fasi ya kwanza kwenye Waisraeli (watu wenye walichaguliwa na Mungu) walikuwa wanafanyia ibada iliitwa “tabenakulo, hema ya mukutano.” (Kut. 39:32, 40) Kisha, Sulemani mutoto wa Daudi alijenga nyumba ao hekalu, kwa utukufu wa Mungu. (1 Fa. 9:3) Kisha hekalu kuharibiwa mu mwaka wa 607 M.K.Y., Wayahudi walifanya mipango ya kukusanyikia mu majengo yenye iliitwa masinagogi ili kumuabudu Mungu. Wakati hekalu ilijengwa upya, Wayahudi walianza tena kukusanyikia mule, na njo ilikuwa kituo ya ibada ya kweli. Yesu alifundisha mu masinagogi na mu hekalu. (Lu. 4:16; Yoh. 18:20) Alikuwa anafanyia mukutano hata ku mulima.—Mt. 5:1–7:29.
2 Kisha Yesu kufa, Wakristo walianza kukusanyikia fasi ya watu wengi na mu manyumba ya watu ili kufundisha Maandiko na kufurahia kuwa pamoya na Wakristo wenzao. (Mdo. 19:8, 9; Ro. 16:3, 5; Kol. 4:15; Flm. 2) Wakati fulani, Wakristo wa kwanza waliona kama ni muzuri wakusanyikie fasi ya kufichama ili watu wenye walikuwa wanawatesa, wasiwaone. Zamani, watumishi waaminifu wa Mungu walifurahia kabisa kukusanyikia fasi mbalimbali ili kuabudu na ‘kufundishwa na Yehova.’—Isa. 54:13.
3 Na leo, Wakristo wanakusanyikia fasi ya watu wengi na mu manyumba ya Wakristo wenzao. Mara mingi, manyumba inatumiwaka ili kufanyia amo mikutano kwa ajili ya mahubiri. Wakristo wenye wanatoaka manyumba yao kwa ajili ya ile mikutano, wanaona ile kuwa pendeleo. Kufanya vile kunafanya wengine waone kama wako nabarikiwa kabisa.
JUMBA YA UFALME
4 Kwa kawaida, Mashahidi wa Yehova wanafanyiaka mikutano yao mu Jumba ya Ufalme. Wanaweza kuuza kiwanja na kujenga ndani Jumba ya Ufalme, ao wanaweza kuuza nyumba na kuitengeneza upya ili ikuwe Jumba ya Ufalme. Ili kupunguza garama (dépenses) ya kujenga Majumba ya Ufalme, wakati fulani makutaniko mingi inaweza kutumia Jumba moya ya Ufalme. Mu maeneo fulani inaomba kulipia nyumba yenye iko natumiwa kwa ajili ya mikutano. Kama Jumba ya Ufalme ya mupya inajengwa ao kuko mambo mingi sana yenye inatengenezwa upya, ni lazima kukuwe programu ya kuitoa kwa Yehova. Lakini kama kuko mambo kidogo tu yenye ilitengenezwa ku Jumba ya Ufalme, ile programu haitafanywa.
5 Jumba ya Ufalme haipaswe kuwa ya ajabu-ajabu juu ya kushangaza watu. Hata kama Majumba ya Ufalme haijengwe namna moya mu kila eneo, iko na kusudi ileile. (Mdo. 17:24) Kulingana na hali za eneo, Jumba ya Ufalme inapaswa kuwa fasi yenye kufaa kabisa kwa ajili ya mikutano ya Kikristo.
6 Makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova yenye imejengewa Jumba ya Ufalme, inasaidianaka ili kuitumia muzuri na kuitunza. Hakukuwake kuomba sadaka. Lakini kuko sanduku ya michango, na kila mutu anaweza kutoa muchango yenye itasaidia mu garama fulani za lazima ku ile jumba. Mutu mwenye kutoa, anafanya vile kwa kujipendea na kwa moyo wote.—2 Ko. 9:7.
7 Ndugu na dada wote mu kutaniko, wanaona kama ni pendeleo kabisa kutoa michango kwa ajili ya Jumba ya Ufalme, na kujitoa kufanya kazi mbalimbali ili kuitunza iendelee kuwa safi. Kwa kawaida, programu ya kazi ya usafi inafanywa na muzee ao mutumishi wa huduma. Mara mingi, vikundi vya mahubiri njo vinafanyaka usafi, na mwangalizi wa kikundi ya mahubiri ao musaidizi wake njo iko na daraka ya kuisimamia. Hali ya Jumba ya Ufalme, ikuwe inje ao ndani, inapaswa kumuwakilisha Yehova.
Ndugu na dada wote mu kutaniko, wanaona kama ni pendeleo kabisa kutoa michango kwa ajili ya Jumba ya Ufalme, na kujitoa kufanya kazi mbalimbali ili kuitunza iendelee kuwa safi
8 Kama mu jumba moya muko makutaniko mingi, wazee wa ile makutaniko wanaweka ao wanachagua wazee fulani ili wakuwe mu Halmashauri ya Utunzaji wa Jumba ya Ufalme. Kazi ya ile Halmashauri, ni kusimamia mambo ya ile jumba na vitu vyenye kuwa ndani. Mabaraza ya wazee ya ile makutaniko, inachagua muzee moya ili akuwe muratibu wa ile halmashauri. Ile halmashauri yenye kuongozwa na mabaraza ya wazee inapaswa kuhakikisha kama jumba iko nasafishwa na kutunzwa muzuri na kwamba vitu mbalimbali vya kutumia ili kufanya ile kazi viko tayari. Juu iwezekane inaomba makutaniko yote yenye kukusanyikia mu jumba moya itumike pamoya.
9 Kama makutaniko mingi iko nakusanyikia mu Jumba moya ya Ufalme, ni muzuri kukuwa nabadilisha programu ya mikutano kila mwaka. Wazee wa ile makutaniko watafanya programu kwa upendo na kwa faida ya wote. (Flp. 2:2-4; 1 Pe. 3:8) Haiko kutaniko moya njo itakamatia makutaniko ingine maamuzi. Wakati mwangalizi wa muzunguko anatembelea kutaniko moya kati ya makutaniko yenye kutumia ile Jumba moya ya Ufalme, makutaniko ingine itabadilisha programu ya mikutano yao mu ile juma, ikiwa ni lazima.
10 Jumba ya Ufalme inaweza kutumiwa kwa ajili ya hotuba ya ndoa ao ya mazishi. Ni Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko njo itaamua itumiwe ao hapana. Wazee wenye kuwa mu halmashauri watachunguza muzuri ombi na kukamata maamuzi kulingana na maagizo yenye kutolewa na biro ya tawi.
11 Wale wenye wanaruhusiwa kutumia Jumba ya Ufalme, wanaombwa kujiendesha muzuri ili kuheshimisha Wakristo wa kweli. Inaomba kuepuka kufanya jambo yoyote yenye inaweza kukwaza kutaniko ao kumuchafua Yehova na kuharibu sifa ya muzuri ya kutaniko. (Flp. 2:14, 15) Biro ya tawi inaweza kuruhusu Jumba ya Ufalme itumiwe kwa ajili ya mambo ingine ya kiroho, sawa vile Masomo ya Huduma ya Ufalme na Masomo ya Mapainia.
12 Kila mara kutaniko inapaswa kuheshimia Jumba ya Ufalme. Juu ni fasi ya kuabudia Yehova, namna tuko naipamba na vile tuko naonekana inapaswa kuwa ya heshima. (Mhu. 5:1; 1 Ti. 2:9, 10) Kama tunatumikisha ile mashauri, tutaonyesha kama tunaona mikutano ya Kikristo kuwa ya lazima.
13 Ni lazima kuwa na utaratibu wakati wa mikutano yetu. Kwa hiyo, ni muzuri wazazi waikale pamoya na watoto wao. Wazazi wenye kuwa na watoto wadogo, wanatiwa moyo kuikala fasi kwenye watoto wao hawatauzi sana wengine kama inakuwa lazima kuwapeleka haraka inje ili kuwapatia malipizi, ao kuwapatia mambo ingine yenye wako nayo lazima.
14 Ndugu wenye kustahili wanapewa kazi ya ukaribishaji ku Jumba ya Ufalme wakati wa mikutano. Wanapaswa kuwa waangalifu, wenye kufanya urafiki na wenye kutumia akili muzuri. Kazi yao inatia ndani kusalimia watu wenye wanakuya ku mikutano kwa mara ya kwanza na kuwafanya wajisikie kwamba wamekaribishwa muzuri. Tena, wanapatia fasi ya kuikala wale wenye wanachelewa, wanaandika hesabu ya watu wenye walikusanyika, na wanaangalia kama madirisha inafunguliwa muzuri ili hewa iingie (ao kuangalia kama vyombo vya kuleta hewa na kuleta kivukutu mu Jumba ya Ufalme vinatumika muzuri). Kama ni lazima, ndugu wenye kufanya kazi ya ukaribishaji wanaweza kukumbusha wazazi wachunge watoto wao muzuri ili wasikimbie-kimbie mu Jumba ya Ufalme ao kuchezea ku jukwaa, mbele na kisha mikutano. Kama mutoto fulani anafanya fujo wakati wa mikutano, ndugu mwenye kukaribisha watu anaweza kumuambia kwa upole muzazi wa ule mutoto amupeleke inje ili wengine waendelee kufuata mikutano muzuri. Kazi ya wakaribishaji inatusaidia sana tufurahie mikutano yetu. Ikiwezekana, ni muzuri wazee na watumishi wa huduma njo wafanye kazi ya ukaribishaji.
KAZI YA KUJENGA MAJUMBA YA UFALME
15 Wakati wa mitume, Wakristo fulani walikuwa matajiri kuliko wengine. Kwa hiyo, mutume Paulo aliandika hivi: “Kupitia usawazisho, mali yenu ya ziada kwa sasa ijazie mambo yenye wako nayo lazima, ili mali yao ya ziada pia ijazie upungufu wenu, ili kukuwe usawazisho.” (2 Ko. 8:14) Leo pia kuko ile “usawazisho.” Makuta yenye makutaniko ya dunia yote inatoaka, iko natumiwa ili kusaidia kujenga na kutengeneza upya Majumba ya Ufalme. Tengenezo, pamoya na makutaniko yenye kufaidika na ile majumba, inapendezwa sana na michango yenye kufanywa kwa ukarimu na ndugu na dada mu dunia yote.
16 Kisha kuangalia eneo, biro ya tawi inaamua ni mu jumba gani makutaniko fulani itakuwa nakusanyikia. Pia, mu eneo yenye inasimamia, tawi inaamua ni wakati gani Majumba ya Ufalme inaweza kujengwa ao kutengenezwa upya. Kama kunatokea mambo sawa vile upepo mukali, matetemeko ya inchi ao misiba ingine yenye inaharibisha Majumba ya Ufalme, mipango inafanywaka juu ya kuitengeneza; na kama manyumba ya ndugu na dada iliharibiwa, inaweza kutengenezwa pia.
17 Tawi njo inasimamiaka mipango ya ndugu wenye kujitolea ili kutafuta kiwanja. Inasimamia pia kazi ya kufanya plan ya Jumba ya Ufalme, kupata vikaratasi vya serikali, kujenga na kuitunza. Juu kuko lazima kubwa ya Majumba ya Ufalme mu inchi mingi, kuko pia lazima ya wafanyakazi wengi wa kujitolea. Wahubiri wote wenye kubatizwa, wenye kustahili na wenye kupenda kusaidia mu kazi ya kujenga, wanatiwa moyo kujaza ombi na kuipatia Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko yao. Hata wahubiri wenye hawayabatizwa wanaweza kusaidia mu kazi ya kujenga ao kutengeneza upya Jumba ya Ufalme ya kwao.
MAJUMBA YA MIKUSANYIKO
18 Kwa kawaida Wakristo wa kwanza walikuwa nakusanyika mu vikundi vidogo-vidogo. Lakini pia, wakati fulani walikuwa nakusanyika “watu wengi” sana. (Mdo. 11:26) Vilevile leo, watu wa Yehova wanafanyaka mikusanyiko ya muzunguko na ya eneo. Mara mingi wanalipia fasi ya kufanyia ile mikusanyiko, lakini kama ile fasi haifae, wanaweza kujenga fasi ya kufanyia ibada yenye inaitwa Jumba ya Mukusanyiko.
19 Wakati fulani, biro ya tawi inaweza kuuza jengo fulani, kuitengeneza upya, na kuitumia kuwa Jumba ya Mukusanyiko. Lakini mara mingi, wanajengaka Jumba ya Mikusanyiko mu kiwanja yenye waliuza. Majumba ya Mikusanyiko haina ukubwa sawasawa; kwa kawaida inajengwa kulingana na mahitaji ya eneo. Biro ya tawi inaamua kuuza ao kujenga Jumba ya Mukusanyiko kisha kuchunguza kwa uangalifu mambo yote na kujua kabisa ni makuta ngapi itatumiwa na ni mara ngapi ile jumba itakuwa natumiwa.
20 Biro ya tawi inaweka ndugu ili wakuwe naangalia namna Jumba ya Mukusanyiko iko natumiwa na kutunzwa. Mipango inafanywa ili mizunguko ifanye usafi kwa ukawaida, usafi wa kisha kila miezi sita, na kuendelea kuitunza muzuri. Ni jambo ya lazima ndugu na dada wajitoe ili kufanya ile kazi. Kwa hiyo, makutaniko inatiwa moyo kuunga mukono kwa moyo wote ile mipango ya usafi.—Zb. 110:3; Mal. 1:10.
21 Wakati fulani Jumba ya Mukusanyiko inaweza kutumiwa kwa ajili ya mambo ingine ya kiteokrasi, sawa vile masomo ya Biblia na mikusanyiko ya pekee ya waangalizi wa mizunguko. Jumba ya Mukusanyiko ni fasi yenye kutolewa kwa Yehova kwa ajili ya ibada, kama vile tu Jumba ya Ufalme. Wakati tunakusanyika mu Jumba ya Mukusanyiko, mwenendo wetu, namna yetu ya kuvala na kujipamba, vinapaswa kuonyesha heshima kama vile tunajiendesha wakati tunakusanyika mu Jumba ya Ufalme ili kumuabudu Yehova.
22 Mu hii kipindi ya mwisho ya siku za mwisho, watu wengi wako nafanya haraka ili kuya kujiunga na tengenezo ya Mungu. Ile inaonyesha kwamba Yehova iko nabariki tengenezo yake. (Isa. 60:8, 10, 11, 22) Kwa hiyo, tunapenda kuunga mukono mipango yenye kufanywa ili tupate fasi zetu za ibada na kuzitunza ili ziendelee kuwa safi. Kufanya vile, kunaonyesha kama tunaona ile majengo kuwa ya lazima juu iko natusaidia siye wote tutiane moyo kwa kadiri tunaona kwamba siku ya Yehova inakaribia.